Neno La Leo: Mtoto Wa Mkulima Na Wasomi Wa Mlimani

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
( Hii ni sehemu ya makala yangu ya Raia Mwema iliyochapwa leo Jumatano)




Ndugu Zangu,



WAKATI wa uhai wake, Profesa Abdulahaman Babu alipata kusema, kuwa ukichanja mwili wa Mwafrika, basi, kwenye damu yake utaona kuna chembe chembe za mkulima. Profesa Babu alimaanisha, kuwa kwa asili Mwafrika ni mkulima.


Waziri Mkuu wetu, Ndugu Mizengo Pinda ametamka hadharani kuwa yeye ni ’ Mtoto wa Mkulima’. Lakini, tukimrejea Profesa Abdulahaman Babu, tunaona, kuwa tulio wengi tu watoto, au tuna asili ya watoto wa wakulima. Ni bahati mbaya, kuwa watoto wengi wa wakulima wamekuwa wakiionea haya historia yao.


Majuzi hapa Mizengo Pinda alifika pale Chuo Kikuu Mlimani. Akakutana na bango la watoto wenzake wa wakulima. Walimwambia; ”Mtoto wa Mkulima, tunalala nje!” Iliwachukua dakika kadhaa kwa Pinda na Mkuu wa Chuo hicho Prof. Mukandara kujadili namna wanafunzi hao walivyofaulu kupenyeza bango hilo ndani ya ukumbi ule wa Nkrumah. Hatimaye Pinda akaweka wazi; kuwa ujumbe umefika.Kisha akajibu ujumbe ule wa watoto wenzake wa wakulima kwa kuahidi kutoa shilingi milioni kumi kila mwaka kwa kipindi cha miaka mitano.


Labda wanafunzi wale wa Chuo Kikuu walikuwa na ujumbe mzito uliojificha katika maelezo yao yale kupitia bango lile, au ndivyo walivyojipanga; kumwambia tu mtoto mwenzao wa mkulima, kuwa tunalala nje, basi. Maana, kama tatizo ni kulala nje , Mizengo Pinda hakupata tabu sana kuingiza mikono mfukoni kuitafuta milioni kumi kwa mwaka.


Lakini, kama watoto wale wa wakulima pale Mlimani wangemwuliza Waziri Mkuu wao swali lifuatalo; ”Mtoto wa Mkulima, kwanini tunalala nje? Ni dhahiri, Mizengo Pinda asingekimbilia kuingiza mikono mfukoni. Maana, hutokea kwangu nikakutana na kijana anayeniambia; ”Braza, sijala tangu asubuhi!” Jibu langu laweza kuwa; chukua elfu moja hii , nenda ukale!


Lakini, kama kijana huyo huyo ataniuliza; ”Braza , nimemaliza Chuo Kikuu, sina ajira wala hakika ya kula yangu ya kila siku. Unaweza kuniambia ni kwa nini katika nchi hii vijana wasomi wanakosa ajira na hakika ya kula yao? Swali hilo alitaukimbiza mkono wangu mfukoni kuisaka elfu moja ya kumpa kijana huyo. Litanifanya niumize kichwa.


Na katika historia tunasoma, kuwa kuna wakati, katika nchi ya Ufaransa, alitokea Malkia aliyeitwa Marie Antoinette. Malkia huyu aliamka asubuhi moja kwenye kasri yake na kukuta maandamano ya wakazi wa jiji la Paris. Waandamanaji walibeba mabango yenye kusema; Hatuna mikate. Naye Malkia aliwatazama wasaidizi wake, kisha akatamka; “ Basi, wapeni keki!” Jibu la Malkia lilikuwa jepesi sana kwa tatizo kubwa. Na hilo ni Neno La Leo.

Maggid
Kinondoni Biafra, Dar es Salaam.
Desmba 15, 2010
mjengwa
 
Bwana Mjengwa hii ndio Nchi yetu tumezoea kutoa majibu mepesi kwa maswali magumu, kwa kweli ni aibu ukilinganisha utashi wa kisiasa uliojitokeza kuijenga UDOM kwa speed ya LIGHT na kuiacha UDSM ikienda kwa speed ya 24kbs, hapo tatizo ni wanasiasa kutafuta cheap popularity tu kwani wanaamini kuwa Udom ndio itakuwa chakujidaia wakati wa kampeni zijazo,
 
Back
Top Bottom