NEC yawafanyia semina wasimamizi wa chaguzi ndogo zinazotarajiwa kufanyika nchini

Singo Batan

JF-Expert Member
Apr 24, 2020
292
191
Wasimamizi wa uchaguzi mdogo wa Jimbo la Konde wametakiwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, kanuni na maelekezo ya Tume na hivyo kuepuka kufanya kazi kwa mazoea.

Akifungua mafunzo kwa wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi huo leo tarehe 08 Septemba, 2021, Kisiwani Pemba, Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji Rufaa (mst) Mbarouk Salim Mbarouk amewataka wasimamizi hao kuhakikisha kwamba taratibu zote zinafuatwa ili kuwa na uchaguzi huru na wa haki.

“Jambo muhimu mnalotakiwa kuzingatia ni kujiamini na kufanya kazi kwa weledi, na kwamba katika utendaji wa majukumu yenu mnapaswa kuzingatia Katiba ya Nchi, Sheria za Uchaguzi na Kanuni zake, Maadili ya Uchaguzi na Maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume,” amesema.

Jaji Mbarouk amesema uchaguzi ni mchakato unaojumuisha, hatua na taratibu mbalimbali za kufuatwa na kuzingatiwa ambazo zinaweka msingi wa uchaguzi kuwa bora, wenye ufanisi na usio na malalamiko au vurugu.

“Nachukua nafasi hii kuwaasa kuwa pamoja na uzoefu ambao baadhi yenu mnao katika uendeshaji wa uchaguzi, mhakikishe mnazingatia maelekezo mtakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea,” amesema.

Jaji Mbarouk amewaasa wasimamizi hao wa uchaguzi kuvishirikisha vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi katika maeneo yao juu ya masuala ya kiuchaguzi ambayo wanastahili kushirikishwa, akaongeza kwamba kwa kufanya hivyo watarahisisha utekelezaji wa majukumu yao.

Amewataka wasimamizi hao kufanya utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika kwa lengo la kuhakikisha mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanaendeshwa na Tume kwa lengo la kuwaelimisha wasimamizi hao wa uchaguzi juu ya masual mbalimbali yanayohusiana na uchaguzi ili kuwajengea uwezo na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi huo iliyotolewa na Tume, wagombea watachukua fomu za uteuzi tarehe 13 hadi 19 Septemba, 2021, uteuzi wa wagombea utafanyika tarehe 19 Septemba, 2021, kampeni za uchaguzi zitafanyika tarehe 20 Septemba hadi tarehe 08 Oktoba, 2021 na siku ya kupiga kura itakuwa tarehe 09 Oktoba, 2021.

Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Konde lililopo Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba unafanyika kufuatia kujiuzulu kwa mbunge mteule wa jimbo hilo Bw. Shekha Mpemba Faki ambaye alitangazwa kuwa mshindi wa uchaguzi mdogo uliofanyika tarehe 18 Julai, 2021.

Aidha, uchaguzi huo unafanyika sambamba na uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ushetu Mkoani Shinyanga na kata sita za Tanzania Bara.

SOURCE: NEC PRESS
 
weledi ni kufanya kitu bila ya kujulikana ,sasa wanapoambiwa wafanye kazi kwa weledi ,mmeona ?
 
Back
Top Bottom