Ndugu wa Mwanamke aliyedaiwa kujinyonga akiwa mahabusu Mburahati walifungulia kesi Jeshi la Polisi

Lady Whistledown

JF-Expert Member
Aug 2, 2021
1,005
1,583
Ndugu wa mwanamke anayedaiwa kujinyonga akiwa mahabusu jijini Dar es Salaam wameliburuza mahakamani Jeshi la Polisi na Hospitali ya Taifa Muhimbili wakitaka uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo.

Stella Moses (30) alifariki usiku wa Desemba 20, 2020 akiwa mahabusu katika Kituo cha Polisi Mburahati alipojisalimisha baada ya kupata taarifa kuwa alikuwa akihitajika kituoni hapo.

Ndugu hao wamefungua shauri hilo baada ya kutoridhika na upelelezi, mwendenzo wa uchunguzi wa tukio na sababu za kifo hicho, hivyo wakitaka ufanyike uchunguzi huru.

Shauri hilo limefunguliwa na shemeji wa marehemu, Emmanuel Kagongo kwa niaba ya familia ya marehemu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Dar es Salaam, Kivukoni (Kinondoni) kupitia kwa wakili Peter Madeleka.

Baada ya kifo cha Stella, Jeshi la Polisi kupitia Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kinondoni, Ramadhani Kingai lilitoa taarifa kuwa mama huyo wa watoto wawili kuwa amefariki dunia baada ya kujinyonga akiwa mahabusu kwa kutumia nguo yake.

Kingai alisema inaonekana mwanamke huyo alikuwa na madeni mengi na kwamba baada ya kuchunguza waliona kifo hicho hakikusababishwa na uzembe wa askari, kwa kuwa wakati mtuhumiwa anaingizwa mahabusu taratibu zote, ukiwemo ukaguzi, zilifuatwa.

Ingawa Kingai alidai mwanamke huyo alifariki Desemba 21, 2020, ndugu zake walipozungumza na Mwananchi walidai Stella alifariki Jumapili ya Desemba 20 jioni, siku aliyojisalimisha kituoni hapo baada ya kupata taarifa kuwa anatafutwa.

Walidai walipompelekea mtyhuhumiwa huyo chai Jumatatu saa 2 asubuhi, waliambiwa na polisi wamechelewa na wakatakiwa kurudi saa tano.

Walidai kuwa waliporudi, waliambiwa ndugu yao alijaribu kujinyonga na amepelekwa Hospitali ya Muhimbili, hivyo wamfuate huko.

Msemaji wa familia hiyo, alidai walipofika Muhimbili walielezwa mwili wa ndugu yao ulipelekwa hospitalini hapo na polisi saa 5:27 usiku ukiwa hauna uhai.

Kifo cha Stella kilizua mvutano baina ya Jeshi la Polisi na ndugu wa marehemu waliopinga maelezo ya polisi na kutaka uchunguzi huru wa chanzo cha kifo cha ndugu yao, lakini polisi walipuuza madai yao.

Mvutano huo ulisababisha mwili wa Stella kukaa katika chumba cha kuhifadhia maiti Muhimbili kwa zaidi ya wiki moja kabla ya kuchukuliwa na kwenda kuzikwa na ndugu hao.

Uchunguzi huru
Baada ya kupambana kwa zaidi ya mwaka mmoja kutaka uchunguzi huru dhidi ya kifo hicho, ndugu wa Stella sasa wamefungua kesi dhidi ya viongozi wa Jeshi la Polisi na uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili wakiomba mahakama iridhie kufanya uchunguzi huru.

Wanalituhumu Jeshi la Polisi na Muhimbili kwa madai ya kushindwa kutimiza wajibu wao.

Katika shauri hilo, Kagongo anaomba mahakama hiyo iridhie kufanya uchunguzi huru ili kujua ukweli wa mazingira ya kifo cha ndugu yao.

Wajibu maombi katika shauri hilo ni Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu Dar es Salaam na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni.

Wengine ni Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi Mburahati, Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Katika maombi hayo yaliyofunguliwa kwa hati ya dharura, Kagongo anadai endapo mahakama hiyo haitafanya uchunguzi wa kifo hicho kwa wakati, maisha ya shemeji yake yatakuwa yamepotea kikatili.

Maelezo ya Kagongo
Kagongo anadai shemeji yake alikamatwa na kuwekwa kizuizini katika Kituo cha Polisi Mburahati, katika Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam Desemba 20, 2020.

Anadai akiwa kituoni hapo kufuatilia tukio hilo Desemba 21, 2020, alitaarifiwa na ofisa wa polisi kwamba shemeji yake alijinyonga usiku wa Desemba 20, 2020 wakati akiwa chini ya ulinzi wa polisi.

Anadai kuwa Desemba 28, 2020 Idara ya Vizazi na Vifo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ilitoa kibali cha mazishi ya Stella kwa Eliud Ernest Kagongo, chenye namba 1097179 ili kuridhia mazishi ya ndugu yao.

Hata hivyo, haridhiki na kibali hicho kwa kuwa haki

kubainisha sababu za kifo cha shemeji yake bali kilieleza tu kuwa uchunguzi wa kimaabara ulikuwa unasubiriwa.

“Mpaka leo hakuna taarifa yoyote ya kitabibu iliyokwishatolewa kuhusu sababu ya kifo cha Stella Moses kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa familia ya marehemu.”

“Mpaka sasa sababu ya kifo cha marehemu Stella Moses bado haijulikani kwa sababu zisizofahamika na hakuna mwenendo wowote wa uchunguzi kuhusu kifo chicho ambao umeshafanyika,” anasema Kagango katika kiapo chake.

Shauri hilo linalosikilizwa na Hakimu Mkazi Aron Lyamuya liliitwa Mei 11, 2022 ili kuona kama wajibu maombi walikuwa wamewasilisha majibu dhidi ya maombi hayo.

Mpaka siku hiyo, ni wajibu maombi wawili tu, RPC Kinondoni na Mkurugenzi Mkuu MNH, ndio waliokuwa wamewasilisha majibu yao huku wengine wakiwa bado.

Wakili Madeleka aliiomba mahakama ikubali kuwa wajibu maombi waliobaki walikuwa wamepoteza haki yao ya kuhoji, isipokuwa wana haki ya kuhoji masuala ya kisheria pekee.

Wakili wa Serikali, Ester Charles alikiri wameshindwa kuwasilisha kiapo kinzani kwa ajili ya wajibu maombi wanne na kuiomba mahakama iwape tarehe nyingine ili waweze kuwasilisha viapo kinzani.

Hakimu aliahirisha kesi hiyo hadi Mei 31, 2022 kwa ajili ya kutolea uamuzi hoja hizo, lakini ilipofika tarehe hiyo mahakama iliahirisha tena kesi hiyo hadi Juni 13, 2022 kwa ajili ya uamuzi

Chanzo: Mwananchi
 
Upelelezi haujakamilika jibu hilo walitarajie ndugu wa marehemu mpka watachoka wenyewe
 
Kingai huyu huyu tuliyemfahamu kwenye kesi ya Mbowe au mwingine? Kama ndiye basi poleni wafiwa.
 
Huyo dada alikuwa na kosa gani.

Familia ushukuru Mungu tu maana hao wanasheria gharama zao kubwa sana, watachanga hadi watakimbiana
 
Najaribu kuwaza hivi kwa ubovu wetu wa kuhifadhi kumbukumbu, kifo cha mwaka 2020, leo kinaweza kuchunguzwa na matokeo yasilete utata? hasa ukizingatia wanaochunguzwa ni polisi?
 
Ni vizuri mkakubali maumivu na mkasamehe bure! Ameisha kufa, ni huzuni kwa kweli, basi na tusamehe kwa hiari.
Ukiitwa Polisi ni vizuri ukaenda na mtu wa kukuwekea dhamana aliyekamilika(unaulizia kwa wazoefu viambata).
Mahabusu ni kubaya sana kama hujawahi kuingia!! Unaweza ukafa bila hata kujinyonga!
 
Ni vizuri mkakubali maumivu na mkasamehe bure! Ameisha kufa, ni huzuni kwa kweli, basi na tusamehe kwa hiari.
Ukiitwa Polisi ni vizuri ukaenda na mtu wa kukuwekea dhamana aliyekamilika(unaulizia kwa wazoefu viambata).
Mahabusu ni kubaya sana kama hujawahi kuingia!! Unaweza ukafa bila hata kujinyonga!
Acha uongo.
Mie mbona nimekaa sana mahabufu tofauti hapa Dar es Salaam sijaona hatari za kifo
 
3 Reactions
Reply
Back
Top Bottom