esther mashiker
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 616
- 552
SHIRIKA la Maendeleo la Taifa (NDC) limesambaza jumla ya matrekta 442 yanayotolewa kwa mkopo nafuu katika maeneo mbalimbali nchini, ukiwamo mkoa wa Dodoma. Akizungumza baada ya kumkabidhi Spika wa Bunge, Job Ndugai trekta alilonunua, Mkurugenzi Mkuu wa NDC, Profesa Damiani Kabagambi amesema mradi huo umelenga kuchangia mapinduzi ya sekta ya kilimo.
Amesema kati ya matrekta hayo 442 waliyosambaza nchini, matrekta 28 yamesambazwa katika mkoa wa Dodoma wakati kati ya hayo 11 yamepelekwa katika wilaya ya Kongwa. Mkoa wa Manyara ndio ulioongoza kwa kuchukua matrekta 136.
“Azma ya serikali ni kukia uchumi wa kati kupitia mapinduzi ya viwanda, hivyo tukaona tuje na mradi wa matrekta, lengo ni kusaidia katika mapinduzi ya kilimo. Mradi huu si wa kiubabaishaji ni mradi nafuu na wenye unafuu kwa mkopaji.
Ni mradi uliolenga kufanya jembe la mkono kupelekwa makumbusho na kujikita kuzalisha kwa njia ya kisasa kwa trekta,” alisisitiza. Kabagambi aliongeza:
“ Nchi jirani zinatarajia kupata chakula kutoka nchini Tanzania hivyo ili kukabiliana na mahitaji hayo na mahitaji ya maligha kwa ajili ya viwanda ni lazima kuachana na jembe la mkono, kwa kuwa halina tija na linachelewesha katika uzalishaji.” Kabagambi alitumia fursa hiyo kuwasihi watanzania kujitokeza kuchangamkia fursa hiyo na kumsihi Spika kutumia nafasi yake kushuhudia umuhimu wa kukopa matrekta kutoka NDC