Nchi sasa inayumba

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Nchi sasa inayumba

Mwandishi Wetu Aprili 16, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Kitendo


Lowassa, Rostam, Chenge, Mkapa ‘moto’

Kikwete, CCM, Bunge watishwa

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) na Serikali zake vinasukwasukwa kiasi kwamba kuna hofu kwamba kama hali haitabadilika nchi itafika pabaya, imeelezwa.

Watu mbalimbali waliozungumza na Raia Mwema wiki hii wanalitaja suala la kuzuiwa kwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz kujitetea kuwa dalili za mwisho za jinsi hali ilivyo mbaya ndani ya CCM, hali ambayo inaigusa pia Serikali.

Watu hao wanataja pia tukio la Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge, ambaye ana fedha nyingi za kigeni nje ya nchi kuwa ufa mwingine ndani ya CCM na Serikali ambako Chenge anaheshimiwa sana.

Yanatajwa pia matukio kama ya wizi ndani ya Benki Kuu (BoT) kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), mikataba mibaya ya uchimbaji madini na kushindwa kwa Rais Jakaya Kikwete kuchukua hatua thabiti juu ya watuhumiwa, wengine watu wa karibu naye, kuwa ambayo yanatia doa katika mchakato wa nchi kujiletea maendeleo.

Ni mambo hayo, habari zinasema, ambayo yameibua mgawanyiko kwenye CCM na serikalini katika makundi ya wanasiasa wenye nguvu upande mmoja kiasi kwamba sasa mazungumzo ya wazi yameibua mjadala wa kuanza kutafuta mrithi wa Rais Kikwete, miaka miwili kabla ya kipindi chake cha kwanza kwisha.

Anasema mwanasiasa mmoja kuhusu mjadala huo: “ Katika mfumo wa vyama vingi tulioiga kwa wenzetu kama mnakuwa na kipindi mlichojiwekea basi mnamuacha huyo aliyepo amalize kipindi hicho. Lakini mkianza kumjadili hata kabla ya kipindi chake cha kwanza kwisha, hiyo ina maana kwamba kwenye chama chenu kuna matatizo makubwa.”

Lakini vyanzo mbalimbali vya habari vinasema sababu kubwa ya kukua kwa mtikisiko huo ni jinsi Kikwete “alivyoliachia gurudumu” la kile kinachoitwa mapambano dhidi ya ufisadi, huku likiwakumba watu waliokaribu naye na hata wasaidizi wake ndani na nje ya serikali.

Matuko ya hivi karibuni yakiwamo yale yaliyotokea bungeni mjini Dodoma na baadaye katika vikao vya CCM kijijini Butiama, yamechochea moto wa mtikisiko huo ndani ya CCM na serikali yake.

Moto huo unaelezwa kuwashwa ama kuchochewa zaidi na wahusika ama watu walio karibu na waathirika wa ripoti ya Kamati Teule ya Bunge kuhusu mradi tata wa umeme wa dharura uliokabidhiwa kampuni ya Richmond ya Marekani na wale wanaoguswa na uchunguzi ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na maeneo mengine yanayonuka rushwa.

Tayari Kikwete anaelezwa kupokea maelezo, ushauri, lawama na hata vitisho baada ya kuibuka kwa tuhuma na uchunguzi wa masuala yote yanayohusishwa na ufisadi ambayo yameibuka mfululizo na yakaitikisa Serikali yake.

Mbali na kupoteza rafiki zake wa karibu, Edward Lowassa, ambaye alijiuzulu kutokana na kuguswa kwake na kashfa ya mkataba wa Richmond na Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz ambaye anatikiswa na tuhuma hizo hizo, Rais Kikwete anapata wakati mgumu kumtetea rais mstaafu, Benjamin Mkapa, ambaye anatajwa karibu katika kila kashfa inayochunguzwa ama kuanikwa hadharani.

Kuanguka kwa Lowassa, kunaelezwa kumfanya Kikwete aanze kukwama katika baadhi ya mambo ambayo yalikuwa yakisukumwa na kusimamiwa na Lowassa binafsi na watu walio karibu naye, lakini pia imeelezwa kuwapo kwa uwezekano mkubwa wa hujuma ama woga na kutojiamini kwa watu waliobakia serikalini na ndani ya CCM.

Mjini Dodoma wiki hii hali haikuwa shwari kutokana na mkanganyiko wa maelezo aliyotaka kuwasilisha Rostam Aziz, akielezwa kujiandaa kikamilifu “kupasua bomu” ambalo linadaiwa lingelitikisa Bunge lakini pia lingeidhalilisha CCM na serikali na hivyo kuendelea “kumkandamiza” Rais Kikwete.

Kwa kutumia Kanuni za Bunge, Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ameyazuia maelezo ya Rostam kwa kwa kile kinachoelezwa na watoa habari wetu kwamba ni kulinda maslahi na hadhi ya Bunge, lakini pia “kulinda mshikamano ndani ya Bunge na ndani ya CCM”.

Uamuzi wa kumzuia Rostam kuwasilisha maelezo yake ulifikiwa baada ya vikao vya wabunge wa CCM wakiongozwa na Kamati ya Uongozi ya Wabunge wa chama hicho na baadaye kamati ya wabunge wote wa CCM. Rostam ni mjumbe wa vikao vyote kutokana na wadhifa wake wa kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM.

Pamoja na kutowekwa hadharani kwa maelezo ya Rostam, yeye mwenyewe amenukuliwa katika baadhi ya vyombo vya habari akisema kwamba alikuwa na maelezo yenye nguvu na ambayo yangebainisha kuwa yeye ni mtu safi ambaye hakuhusika kwa namna yoyote na mkataba wa Richmond pamoja na kuwa na uhusiano wa kibiashara na kampuni iliyorithi mkataba huo ya Dowans.

Wakati wa mjadala wa ripoti ya Kamati Teule ya Bunge iliyoongozwa na Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe, Rostam alichangia kwa maandishi akisema kwamba hakutendewa haki na ripoti hiyo na kwamba pamoja na kuwa nje ya nchi, angeweza kusikilizwa baada ya kamati hiyo kuwasilisha ripoti yake bungeni.

Katika maelezo yake hayo aliituhumu kamati hiyo kufanya vikao vyake hata baada ya kukabidhi ripoti yake kwa Spika akidai ilifanya kazi yake ikiwa na malengo maalumu, kauli ambayo alitakiwa kuifuta ama kuitolea ushahidi katika mkutano wa Bunge unaoendelea sasa kabla ya kukumbana na ‘kizingiti’ kutoka kwa Spika.

Imeelezwa kwamba Rostam alijiandaa kwa maelezo ambayo yangeibua mjadala mpya wa sakata la Richmond na pengine ingeilazimu kamati ya Mwakyembe kuomba muda wa kujibu hoja hizo, wakati Kanuni za Bunge hazitoi nafasi hiyo na kuacha hoja ya Mbunge huyo wa Igunga kuifunika ripoti nzima bila kupingwa na yeyote.

Hali hiyo pamoja na unyeti wa baadhi ya maelezo ya Mbunge huyo, ni mambo yanayotajwa na vyanzo vyetu kuwa sababu ya msingi iliyowasukuma vigogo wa CCM ndani ya Bunge kuamua kumzuia Rostam kuwasilisha hoja yake huku yakiibuka maswali mengi yasiyokuwa na majibu.

Unyeti wa maelezo ya Rostam unaelezwa pia kuhofiwa kuwachafua ama kuwaingiza hata viongozi wa juu wa CCM wa sasa na wa zamani ambao hawakuguswa kabisa katika ripoti ya Mwakyembe, jambo ambalo lingezidisha hasira na chuki miongoni mwa wana CCM.

Hata hivyo, baadhi ya wanasheria wa Bunge walielezea kusikitishwa kwao na uamuzi wa kumzuia Rostam kuwasilisha hoja yake kwa maelezo kwamba ungeandaliwa utaratibu ambao ungewezesha hoja hizo kujibiwa kwa vile Kamati Teule ilifanya kazi yake kwa umakini.

“Unajua CCM imemsaidia sana Rostam kumzuia asiwasilishe hoja yake kwani ushahidi ambao anautaja kuwa nao hauna maana yoyote kwani hana mamlaka ya kisheria ya kuthibitisha uhalali wa nyaraka hizo, lakini pia kusema kamati ilikaa baada ya kuwasilisha ripoti ni kutojua taratibu za kamati na ndiyo maana hata baada ya Lowassa kuwasilisha maelezo yake, kamati ilikutana na kumjibu,” anasema Ofisa Mwandamizi wa Bunge.

Ofisa huyo alisema kwa Rostam kudai kuwapo kwa ripoti mbili za Kamati Teule, angejikuta akikabiliwa na kesi ya kijinai kwa kuwa na nakala ambayo si halisi ama iliyopatikana kwa njia ya kijinai kwa kuwa kisheria ripoti inayotambulika ni ile iliyowasilishwa bungeni na mwenye mamlaka ya kuitambua ni Spika na Bunge zima.

“Utakumbuka hata ripoti ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge iliyosikiliza kesi ya Mwenyekiti wa IPP, Reginald Mengi na Mbunge wa Mkuranga, Adam Malima, ilikuwa na ripoti zaidi ya moja na baadaye iliwasilisha ripoti ya mwisho kwa Spika huku wabunge wawili wakiwasilisha ripoti mbadala kabla ya Spika kutoa uamuzi wake nje ya ripoti husika. Leo Malima hawezi kuja na zile ripoti za awali, hataeleweka,” alisema ofisa huyo.

Uchunguzi wa EPA umetikisa kutokana na kwamba umekuwa kama mchezo wa kuigiza kwa vile hakuna aliyekamatwa na badala yake imeelezwa kuwa wanakusanya fedha kutoka kwa wanaochunguzwa kwanza.

Sakata la EPA linaigusa CCM moja kwa moja, lakini hadi sasa chama hicho kimekuwa kikitangaza hadharani kutohusika kabisa na sakata hilo huku kikiagiza wahusika wachukuliwe hatua.

Sasa imesalia takriban miezi miwili kabla ya Tume ya EPA kukamilisha uchunguzi wake. Lakini tume hiyo inayoongozwa na Mwanasheria Mkuu, Johnson Mwanyika, akisaidiwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Saidi Mwema na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), imekuwa haiaminiki sana miongoni mwa umma.

Imani hiyo finyu inatokana na dhana kwamba watuhumiwa wa EPA wanabembelezwa hasa kutokana na kwamba wengi wao ni watu wazito.

Hata hivyo, baadhi ya wanasiasa wanasema pamoja na nia nzuri ya Kikwete, uamuzi wa kuanika hadharani uozo wa BoT na hata kuruhusu Waziri Mkuu wake kujiuzulu, ni mambo yatakayoisumbua sana serikali na CCM kwa muda mrefu.

Kuchunguzwa kwa kuhusika na rushwa ya ununuzi wa rada ya Sh bilioni 70, na hatimaye kupekuliwa kwa Waziri Chenge ni tatizo jingine kwa Rais Kikwete.

Chenge amekutwa na kiasi kikubwa cha fedha katika akaunti zake za nje na akaunti moja pekee katika benki moja ya kisiwa cha Jersey nchini Uingereza imekutwa na fedha zinazofikia Sh bilioni moja za Tanzania.

Imeelezwa kwamba kitendo cha Kikwete kumteua Chenge katika mabadiliko yaliyotokana na kujiuzulu kwa Lowassa, Nazir Karamagi na Ibrahim Msabaha kutokana na kashfa ya Richmond, kinazidi kumpa wakati mgumu na kuzidisha mtikisiko katika serikali yake, jambo ambalo lingeepukika kwa kumuacha kama alivyomuacha Basil Mramba.

Kikwete pia alikubali kuwapo kwa Chenge katika msafara wake wa ziara ya China, siku chache baada ya waziri huyo kupekuliwa, kuliibua maswali mengi na hata kuhoji umakini wa wasaidizi wake ambao walimuandalia safari hiyo, kama ambavyo walimshauri kumrudisha katika baraza lake la mawaziri.

Chenge anaelezwa kuwa karibu na Kikwete tokea wakiwa katika jengo moja, mmoja akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kwa miaka kumi (1995-2005), na mwingine (Kikwete) akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, chini ya rais mstaafu Benjamin Mkapa.

Hata hivyo, ukaribu wa Chenge na Kikwete, unaelezwa hauwezi kuzidi ule wa Kikwete na Lowassa, na hivyo kuendeleza kile kinachoelezwa sasa kuanza kuwageuka marafiki ambao wamekuwa pamoja katika harakati mbalimbali za kisiasa na kijamii.




RAIS Mstaafu Mkapa

Ugumu mwingine unaomuweka pabaya Kikwete ni kauli yake ya kwamba Mkapa kama walivyo wastaafu wengine anastahili “kuachwa apumzike kwa amani”, kutokana na karibu kila tuhuma kubwa kumgusa Rais huyo aliyeingia madarakani mwaka 1995 kwa jina la ‘Mr. Clean’.

Mkapa ambaye wasaidizi wake wakuu (akiwamo Chenge), marafiki zake na hata familia yake wameguswa na tuhuma mbalimbali za ufisadi na baadhi tayari wameanza kuchukuliwa hatua za kiuchunguzi, ambazo zimeelezwa kumgusa moja kwa moja kiongozi huyo ambaye amekuwa kimya kujibu tuhuma kadhaa dhidi yake.

Uchunguzi unaondelea dhidi ya Chenge kuhusiana na kesi ya rada na baadhi ya tuhuma nyingine na habari za kuchunguzwa kwa mawaziri wengine wawili wa zamani, bila shaka kutamgusa moja kwa moja Mkapa na hivyo kumpa Kikwete mtihani mwingine mgumu wa kuamua kuachia sheria kuchukua mkondo wake dhidi ya mtu ambaye hakupenda ashughulikiwe kupitia mikono yake.

“Huwezi kumgusa Chenge ukaacha kumgusa Mkapa wakati yeye anasema uamuzi wa kununua rada ulipitishwa na Baraza la Mawaziri, ambalo baadhi yao bado wamo serikalini hadi sasa na kwamba yeye alihusika kwa kiasi kidogo mno katika mchakato wa ununuzi wa rada hiyo. Kikwete atalazimika kuacha Mkapa achunguzwe na kuondolewa kinga yake ya kikatiba, vinginevyo atajikuta akijiharibia yeye kabla ya uchaguzi wa mwaka 2010,” anasema mwanasiasa mmoja ndani ya CCM.

Wakati hayo yakiendelea, tayari magazeti yamechokoza mjadala wa uwezekano wa wana CCM kujitokeza kugombea urais sambamba na Kikwete mwaka 2010, habari ambazo zinaelezwa kuandaliwa mahususi kuchokoza mjadala huo ambao ni dhahiri unatokana na hali mbaya ya kisiasa ndani ya CCM na serikali yake.

Mjadala huo unaelezwa kuandaliwa kukumbusha hali ya kisiasa mwaka 2000 ambao Mkapa alikuwa akiwania kipindi chake cha pili kwa Urais wa Muungano, huku Zanzibar, rais mstaafu, Dk. Salmin Amour alikuwa akimaliza muda wake kwa misukosuko kutokana na kuelezwa kutaka kubadili katiba na baadaye kumpisha mtu wake kabla ya kuzidiwa na kupita kwa Rais wa sasa Amani Karume.

Imeelezwa kwamba mwaka 2000 walijitokeza watu ndani ya Kamati Kuu ya CCM ambao walihoji uhalali wa utamaduni huo wa kumwachia Rais aliye madarakani kuwania vipindi viwili bila kupingwa kwa maelezo kwamba inapotokea kwa kiongozi huyo kutokidhi matakwa ya wana CCM na Watanzania, itakuwa na athari mbaya kwa CCM, lakini hoja hiyo “ilimalizwa kikubwa” na CCM.

Hoja hiyo inaelezwa kuweza kuibuliwa upya kumtisha Kikwete kwa nia ya kupunguza kasi yake ya “kuwageuka” wenzake ambao wanatajwa kumsaidia kwa miaka mingi kufika hapo alipo, wakiwa na malengo ya kuendelea kumsaidia hadi mwaka 2015.

Hata hivyo, baadhi ya wana CCM wamesema Kikwete hapaswi kutishika kwa kuwa mambo mengi anayoyafanya anaungwa mkono kwa kiwango cha juu na wananchi walio wengi pamoja na wanasiasa ambao wamekuwa wakiweka pembeni maslahi binafsi na hivyo kumshauri kutorudi nyuma katika mapambano dhidi ya ufisadi na maovu mengine katika jamii.
 
Wajinga ndio waliwao, Kilichotokea hapa ni kuwa muajiriwa ameonesha kuwa ana fedha kuliko muajiri.
 
Back
Top Bottom