National hospital

Glucky

Senior Member
Dec 16, 2009
123
40
HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH) imeingia katika kashfa mpya baada ya mtu mmoja kubainika akitoa huduma za kidaktari na kuwatapeli fedha wagonjwa kwenye hospitali hiyo.

Tayari mtu huyo, ambaye alikuwa akitumia ofisi za hospitali hiyo kutoa huduma hizo na kujipatia fedha, ameshakamatwa na kufikishwa kituo cha polisi cha Selander Bridge jijini Dar es salaam.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili zinasema mtu huyo amekuwa akifanya kazi ya kutibu watu katika hospitali hiyo na kuendesha utapeli wa fedha huku akihamishia wagonjwa katika zahanati moja aliyodai ni yake maeneo ya Kitunda, Ukonga jambo ambalo si kweli.

Habari za uhakika kutoka kwa baadhi ya watu waliotapeliwa na daktari huyo anayejulikana kwa jina moja la Dk Charle na baadhi ya madaktari wa MNH zinasema kuwa mtu huyo amekuwa akisumbua madaktari na wagonjwa akidai alipelekwa hospitalini hapo na mkurugenzi wa huduma ya tiba wa MNH, Profesa Andrew Swai.

Hata hivyo, Profesa Swai amekanusha kumfahamu mtu huyo na kueleza kuwa uongozi wa MNH tayari ulimwekea mtego ambao ulifanikiwa kumkamata daktari huyo na baadaye kumkabidhi kwenye vyombo vya dola.

Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi umebaini kuwa mtu huyo alikamatwa usiku wa kuamkia jana na kupelekwa kituo cha polisi cha Selander Bridge ambako anashikiliwa huku uchunguzi dhidi yake ukiendelea.

Habari za uhakika zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na uongozi wa MNH, zinasema kuwa daktari huyo alikamatwa katika mtego aliowekewa baada ya uongozi kupokea malalamiko na mmoja wa wagonjwa waliotapeliwa.

Ndugu wa karibu na mgonjwa huyo ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe kwa sababu za kiusalama, walidai kuwa mlalamikaji huyo alimpeleka mtoto wake Ashraf Sudi, 6, anayesumbuliwa na ugonjwa wa ngiri, kwa ajili ya kupata matibabu kwenye chumba namba 5 cha jengo jipya la watoto.

Aliongeza kuwa baada ya kukaa katika foleni kama wagonjwa wengine akisubiri kumuona daktari, alifanikiwa kuingia na kuzungumza na daktari huyo ambaye alimweleza kuwa mtoto huyo anatakiwa kufanyiwa upasuaji na kumtaka atoe Sh80,000 kama gharama ya tiba.

Alidai kuwa alilazimika kurudi nyumbani na kumueleza mume wake ili ampatie fedha hizo na akarudi hospitalini siku iliyofuata.

Alidai kuwa alipofika Muhimbili alimkuta Dk Charle akihudumia wagonjwa kama kawaida na ilipofika zamu aliambiwa asubiri kidogo wakati akiendelea kuhudumia wagonjwa wengine.

"Ndipo baada ya muda akatoka na kuondoka na mdogo wangu na kumpeleka zahanati moja ya jijini aliyodai ni yake," alisema mtoa habari huyo.

Alifafanua kuwa mdogo wake alienda naye hadi maeneo ya Kitunda, jirani na Moshi Bar ilipo zahanati hiyo na mtoto huyo alichomwa sindano nne na Dk Charle, zilizosababisha apoteze nguvu.

Baadaye daktari huyo alimtaka mama wa mtoto huyo ampatie fedha walizokubaliana kwa ajili ya kununua vifaa vya upasuaji ndipo amuhudumie mgonjwa.

"Kwa hiyo mdogo wangu akampatia zile fedha, yule daktari akaondoka na kumuacha yule mtoto ndani, lakini cha kushangaza zaidi ya masaa matano yule daktari hakutokea tena hivyo mdogo wangu ilibidi awaulize wauguzi wa zahanati hiyo kujua alipokwenda Dk Charle,"alisema.

Aliongeza kuwa wale wauguzi wakamjibu hawamfahamu huyo daktari, lakini mdogo wangu aliwaonyesha kadi ambayo inaonesha kwamba mtoto wake ameanza kupatiwa huduma katika zahanati hiyo, lakini wauguzi wakamwambia kwa kuwa ana kadi ya zahanati hiyo hawezi kuondoka hadi alipe Sh4,000 ambazo ni gharama ya kadi.

"Mdogo wangu akawa analia huku akijitetea, lakini walimbana hadi akawapa fedha walizohitaji," alisema ndugu huyo.

Alisema kuwa baada ya tukio hilo, mdogo wake alimweleza na kumtaka amsindikize Muhimbili ili wakamkamate Dk Charle na walipofika kwenye chumba alichomkuta awali, hakuwepo na badala yake walimkuta mtu tofauti ambaye aliwaambia kuwa hamfahamu Dk Charle na kwamba huwa wanamuona hospitalini hapo na anawasumbua.

“Huyu mtu tumekuwa tukimuona tu hapa na kila anapoulizwa anadai kuwa ameletwa na Profesa Swai,” ndugu huyo alimkariri daktari waliyemkuta.

"Baada ya hapo tuliondoka na daktari huyo hadi kwa Prof Swai ndipo tukamwelezea tukio zima, wakatushauri tukatoe taarifa kituo cha polisi kwanza, tulipoenda kituo cha Polisi cha Selander wakatushauri tumpeleke mgonjwa hospitali wakati malalamiko yetu yanashughulikiwa. Sasa mtoto amepangiwa kufanyiwa upasuaji Januari 24."

Profesa Swai, akizungumza na Mwananchi, alikiri kuwepo kwa tukio hilo akieleza kuwa uongozi wa hospitali umeshamkamata na kumpeleka katika kituo cha polisi cha Selander.

Alisema hawamfahamu mtu huyo na wala si mwajiriwa wa MNH, ndio maana baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa mgonjwa huyo waliyafanyia kazi na kufanikiwa kumnasa mtuhumiwa na kumkabidhi kwenye vyombo vya dola.

Kwenye kituo cha polisi cha Selander, Mwananchi ilithibitishiwa kukamatwa kwa daktari huyo feki na kuelezwa kuwa bado maelezo yake hayajachukuliwa.
"Walalamikaji walileta malalamiko yao siku za nyuma tukawafungulia jalada kwa hiyo tutakapochukua maelezo ndipo tutajua kama ana hatia au hana,"alisema mmoja wa maofisa wa polisi aliyeomba jina lihifadhiwe kwa kuwa si msemaji wa polisi.
 
huyu siyo charle aliyekuwa mtumishi wa hapo MNH katika idara ya Umeme.maana najiuliza inawezekana vipi mtu asiyefahamu mazingira ya MNH akaweza kutumia majengo hayo ya ofisi/ lazima anapajua vyema hapo MNH.
 
Back
Top Bottom