NACTE na maamuzi ya utata kuhusu mitihani ya marudio kwa wanafunzi wa vyuo vya kati: Je, Waziri wa elimu anafahamu kilio hiki?

Travelogue_tz

JF-Expert Member
Sep 28, 2010
848
1,212
Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) ni chombo kilichoanzishwa kwa Sheria ya Bunge Sura Namba 129 ili kusimamia na kuratibu utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi katika Vyuo ambavyo si Vyuo Vikuu ama Vyuo Vikuu Vishiriki nchini. Jukumu mojawapo la Baraza ni kuhakikisha kuwa mafunzo yanayotolewa katika Vyuo vya Ufundi nchini yanakidhi vigezo na ubora unaohitajika katika soko la ajira ndani na nje ya nchi.

Katika kutekeleza majukumu yake, Baraza lilirejea Barua yake yenye Kumb. Na KC.175/305/01.D/20 ya tarehe 23/12/2020 kwa wakuu wa vyuo yenye kichwa cha somo kufuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya mitihani kwa wanachuo wenye mitihani ya marudio (supplementary) na wale wanaopaswa kurudia kusoma upya somo au masomo alilofeli (moduli walizofeli-repeat module).

Barua hiyo ilieleza kuwa, ofisi ya Baraza imekuwa ikipokea malalamiko ya wanachuo walio na mitihani ya marudio na wale wanaopaswa kurudia moduli walizofeli kwamba wanazuiliwa kuendelea na semista au ngazi ya tuzo inayofuata ilihali kuna baadhi ya Vyuo wanaruhusu wanachuo wao kuendelea na masomo ya semesta au ngazi nyingine ya tuzo huku wakisoma pia masomo wanayopaswa kurudia mitihani.

Kutokana na kilichoelezwa malalamiko ya wanachuo, Baraza lilitoa wito/ maelekezo kama ifuatavyo;

1. Kwamba ni kinyume cha sheria na miongozo ya mitihani ya mwaka 2004 kumruhusu mwanachuo mwenye aidha mitihani ya marudio (supplementary) au kusoma kusoma upya moduli alizofeli (repeat module) kuendelea na masomo ya semesta au ngazi ya tuzo inayofuata.

2. Mwanachuo mwenye hali tajwa hapo katika kipengele cha (1) hapo juu anatakiwa kufanya kufanya mitihani yake ya marudio /kurudia moduli alizofeli kwa semesta aliyopo na baada ya mitihani hiyo kusahihishwa na mamlaka husika (NACTE/Wizara ya Afya) na mwanachuo kufaulu ndipo ataruhusiwa kuendelea na semesta au ngazi ya tuzo inayofuata.

Nini kiini cha tatizo?

Maelekezo ya sheria, kanuni na miongozo ya mitihani haina shida yeyote, bali changamoto ni namna ambayo Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia idara ya Mafunzo na Baraza la taifa la Elimu ya ufundi linavyotekeleza mitaala husika.

Kwa mujibu wa Mitaala mitihani ya marudio (supplementary) itafanyika wiki sita baada ya kutangazwa kwa matokeo ya mwanafunzi (results declaration). Mathalani kwa wahitimu waliofanya mitihani yao ya muhula wa pili mnamo tarehe 12 August 2021 na kukamilika tarehe 10 Septemba 2021 matokeo yao ya awali (provisional results) yalitangazwa mnamo tarehe 15 Oktoba 2021, hivyo kwa maelekezo ya mitaala wanafunzi ambao wamefeli baadhi ya masomo (supplementary) watatakiwa kufanya mitihani yao ya marudio baada ya wiki sita, ambapo inatarajiwa kuwa kati ya mwezi Januari – Februari 2022.

Kwa mujibu wa kalenda ya masomo na maelekezo ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii , Jinsia , Wazee na Watoto kupitia idara ya Mafunzo na Baraza la taifa la Elimu ya ufundi(NACTE) zinaelekeza kuwa tarehe ya kuanza masomo ni 18/10/2021. Hivyo basi kama Vyuo vitafuata maelekezo ya Baraza, wanafunzi wote waliofeli masomo yao aidha somo moja, mawili au matatu hawataruhusiwa kuendelea na masomo kwa muhula unaofuata mpaka hapo watakapokamilisha mitihani yao ya marudio inayotarajiwa kufanyika mnamo Januari- Februari 2022. (yaani miezi mitatu baada ya kuanza kwa muhula wa masomo).

Je, nini athari yake kwa wanafunzi na wazazi?

Kwa mujibu wa matokeo ya awali yaliyotangazwa na mamlaka , zaidi ya asilimia hamsini ya wanafunzi wanatakiwa kufanya mitihani ya marudio , hivyo endapo wanafunzi hawa watafanikiwa kufanya mitihani yao mnamo Januari- Februari 2022, matokeo yao yanatarajiwa kutolewa baada ya miezi miwili ( yaani Machi- Aprili 2022), ambapo katika muda huu muhula wao wa masomo ulioanza 18/10/2021 utakuwa umekamilika. Hivyo kwa wale watakaobahatika kufaulu mitihani yao ya marudio, watatakiwa kusubiri kuanza upya katika muhula wa masomo wa mwezi Oktoba 2022, hii ina maana kwamba watalazimika kusubiri kwa takribani miezi kumi na mbili (12). Kitendo hiki kinaweza kuwa na athari kadhaa katika taaluma ya mwanafunzi, matarajio ya mzazi/mlezi na uendeshaji wa vyuo.

1. Idadi kubwa ya wanafunzi kujihusisha na mambo yasiyohusu taaluma na hivyo kupelekea kushindwa kuendelea masomo.

2. Watoto wa kike kuwa katika vishawishi vingi katika jamii kama vile mimba zisizo tarajiwa.

3. Baadhi ya wazazi/ walezi kukatiswa tamaa katika kugharamia elimu za wanafunzi hao kwa kuwa ongezeko hilo la muda ni nje ya matarajio na mipango yao.

4. Vyuo kushindwa kuendesha baadhi ya program ambazo idadi kubwa ya wanafunzi watakuwa wamefeli. Mathalani unaweza kukuta darasa la wanafunzi mia (100) ni wanafunzi watatu tu ambao wameweza kufaulu masomo yao yote.

5. Mwanafunzi kufeli somo (supplementary) haina tofauti na mwanafuzi ambaye atakakiwa kurudia muhula (repeat semester), hivyo kuwa na maana kwamba mwanafunzi yeyoye mwenye kufeli somo ni lazima atalazimika kukaa nje ya mfumo wa elimu kwa takribani mwaka mzima.

6. Kuchochea mazingira ya kuvuja kwa mitihani, ambapo kwa baadhi ya watumishi wa Idara ya Mafunzo wasio waaminifu wanaweza kujihusisha kuvuja kwa mitihani kwa lengo la kujipatia kipato. Tatizo ambalo pia limejitokeza kwa mitihani iliyofanyika August 2021 na kupekelea kuzuiwa kwa matokeo ya wanafunzi wa kozi ya utabibu mwaka wa pili (CMT 5 Sem II) ili kupisha uchunguzi.Ila lina athiri sana wanafunzi nchi nzima na hakuna mwenye jawabu juu ya hili na wanafunzi na wazazi wako wamechanganyikiwa hata kwa wasiohusika na hatima ya kuendelea na masomo au kutoendelea nayo hakuna aijuaye.

Nini mapendekezo yetu?

Sisi kama wazazi wa wanafunzi hawa ambapo pia baadhi yetu tumebahatika kuhudhuria masomo ya Vyuo Vikuu Nchini tunapendekeza Waziri wa Elimu kuwaelekeza Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (nacte) na Wizara ya Afya kutekeleza yafuatayo;

1. Suluhu ya dharura;

Kuwaruhusu wanafunzi hawa kuendelea na muhula wa masomo kama kawaida huku wakisubiri kufanya mitihani yao ya marudio hapo baadae. Hili limekuwa likifanyika katika Vyuo Vikuu (carry –over), ambapo mwanafunzi anapata fursa ya kuendelea na masomo huku akijiandaa na mitihani yake ya marudio.

2. Suluhu ya kudumu
  • Kubadili mtaala ili kuhakikisha wanafunzi wote wenye kufeli masomo (supplement) kufanya mitihani yao ya marudio kabla ya kuanza kwa muhula wa masomo. Na hili litawezekana tu endapo matokeo ya mitihani ya muhula wa pili yatatolewa mwezi Septemba, na mitihani ya marudio kufanyika wiki mbili – nne baada ya kutangazwa kwa matokeo. Utaratibu huu umekuwa ukitumika katika Vyuo Vikuu vyote Nchini.
  • Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia idara ya Mafunzo kukubali kukasimisha ( decentralize) zoezi ya uratibu wa mitihani ya mwisho wa muhula wa pili kwa kanda za Baraza la Elimu ya Ufundi , ambapo wanaweza kushirikiana kwa karibu na Vyuo katika kuendesha zoezi la mitihani.
  • Kutekeleza kanuni iliyounda Baraza. (NACTE ACT 1997 ya Part II article 6 sub-article 1,2,3&4 inayoruhusu vyuo vyenye ithibati kamili kuendesha mitihani yake na kutoa tuzo kwa jina la chuo husika wakati wao wakisimami ubora kwa kutuma wasimamizi wan je (external examiners) kama ilivyo sasa kwa mitihani ya mwisho wa muhula wa kwanza. Hili litasaidia Wizara na Baraza kubaki na majumuku yao ya usimamizi na uthibiti ubora.
Mhe. Waziri wa Elimu tunaomba hekima yako iliyotukuka na kama msimamizi mkuu wa mafunzo yote nchini, usaidie jambo hili kupata ufumbuzi wa muda mfupi na ufumbuzi wa kudumu.
 
Hongera sana kwa bandiko hili. Hakika inaonesha una uelewa mkubwa sana katika maswala haya ya elimu katika mfumo wa NACTE
Ni nini maoni yako kwa hawa wanafunzi waliodhuiliwa matokeo yao, je kuna uwezakano wa wao kurudia mtihani ama kuendelea?
 
Hoja yako ni nzuri sana. ahusika waliangalie. Pia tatizo la kuvuja kwa mitihani ni la siku nyingi sana,bado halijapatiwa ufumbuzi na linafanywa juu huko. Mitihani ya siku hizi haina Siri tena.
sijui haya mabadiliko lkn wakati sisi tunasoma ulikuwa hurusiwi kuendelea na masomo mpaka uwe umefaulu mitihani ya kurudia sasa napata uelewa ndo maana elimu yetu inazidi kudorora.hv unaendeleaje na masomo bila kupata uhakika kama utaclear masomo yako ya awali.je ukidisontinue itakuwaje?sielewi
 
sijui haya mabadiliko lkn wakati sisi tunasoma ulikuwa hurusiwi kuendelea na masomo mpaka uwe umefaulu mitihani ya kurudia sasa napata uelewa ndo maana elimu yetu inazidi kudorora.hv unaendeleaje na masomo bila kupata uhakika kama utaclear masomo yako ya awali.je ukidisontinue itakuwaje?sielewi
Lakini mitihani ya supplementary ilikuwa inafanyika kabla ya muhula wa masomo ili ukifaulu uweze kuendelea na wenzako. Kwa jinsi hapa ilivyo ni kwamba Chuo kinafunguliwa Octoba 2021. Mitihani ya supplementary inafanyika mwakani Januari au Februari 2022. Hivyo mwanafunzi huyu hata kama atafaulu atalazimika kusubiri muhula wa Septemba 2022 ili kuanza muhula. Hivyo atakuwa amepoteza zaidi ya mwaka. Na unakuta kuba wengi wao wana supp moja au mbili tu.
 
Kwakweli it's so painful kirudia mwaka mzima eti kwa ajili ya supplementary nanaamini utatuzi wa haraka utachukuliwa
 
Kwa kweli elimu ya Tanzania kwa kada za afya imewekewa mfumo mgumu sana . Vyuo vyengine itaratibu wa kufanya mitihani ya supp ni pale tu vyuo vinapofunguliwa
 
Back
Top Bottom