BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,825
- 287,849
Mambo yakizidi bubu huzungumza!
Juvenalis Ngowi
Tanzania Daima
NATIMIZA sehemu ya wajibu wangu kwa kuanza kumwomba Mola wangu aniongoze na kuniangaza kwa namna ya pekee ninapowakilisha wazo langu jepesi kwa wasomaji wa safu hii.
Yeye ndiye mweza wa yote na haishangazi tunamuita Mwenyezi, Muweza. Huyu ndiye aonaye hadi kwenye uvungu wa mtima wa mtu na hata vilivyofichwa na kufunikwa chini ya busati, yeye anaviona.
Juma hili nimeshangazwa na habari kuhusu rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa. Wengine humuita Mzee wa Utandawazi. Huyu si tu alikuwa mwanafunzi wa darasani wa Mwalimu Nyerere, lakini alikuwa chaguo na kipenzi chake wakati akigombea urais kwa mara ya kwanza mwaka 1995.
Mkapa ninayemfahamu ni bingwa wa takwimu, ni mtaalamu wa kufikisha ujumbe aliokusudia. Anafahamu kuchagua maneno atakayotumia na sikushangaa nilipoambiwa kitaaluma rais huyu mstaafu ni mwanahabari.
Sifa zake hazifanani hata chembe na habari ninayoizungumzia. Kwamba alikataa kujitetea au walau kutoa maoni yake kuhusu shutuma na tuhuma zilizoelekezwa kwake.
Kukataa peke yake kusingenishangaza. Ila inapodaiwa eti alikataa kwa kuwa amestaafu siasa, nashindwa kuelewa. Ubongo unakataa kuikubali sababu hiyo.
Angekataa kwa sababu ana hiari ya kujitetea au kukaa kimya hilo ni jambo jingine.
Kwamba ameona tuhuma hizo hazina uzito wa kujibiwa, ingeweza ikawa sababu. Lakini hii ya kusema amestaafu siasa si sababu ya kufanya wapembuzi yakinifu wafunge mdomo.
Mosi, tuhuma zilizotolewa sio za kisiasa. Kwa rais mstaafu huyu ziliwahi kuelekezwa tuhuma nyingi. Walianza waliomtuhumu kufanya biashara akiwa katika ofisi kuu nchini. Wakahoji hakukuwepo mgongano wa masiahi? Wengine wakaanza kuyakumbuka maneno ya Mwalimu kwamba Ikulu ni mahali patakatifu. Rais mstaafu akakaa kimya kabisa. Rais aliye madarakani naye akawaasa wanaochokonoa mambo hayo wamwache mzee wetu apumzike. Asiulizwe swali. Na imeshasemwa wazi kwamba hatachunguzwa.
Baada ya hapo zikashuka shutuma nyingine zinazoenezwa na kambi ya upinzani kuhusu rais huyu mstaafu na wenzake kadhaa. Hapa wengine walijitokeza kujibu tuhuma.
Wengine wakajiapiza kwenda kujisafisha mahakamani. Wengine wamebaki kimya.
Nisingetegemea kwamba rais mstaafu naye angejitokeza aseme anakwenda kujisafisha mahakamani. Lakini pia sikutegemea aseme anabaki kimya kwa kuwa amestaafu siasa.
Tuhuma zilizotolewa si siasa. Ni tuhuma zinazogusa uchumi wa nchi. Nituhumu zinazogusa watu walio katika nafasi ya utendaji.
Hata kama zinatolewa katika majukwaa ya kisiasa na wanasiasa bado zinabaki ni tuhuma zinazohoji uadilifu wa mtu au watu.
Hiyo si siasa hata kidogo. Tuhuma za kufanya biashara akiwa katika ofisi takatifu si siasa.
Ni hoja ya kuangalia kama kuna msuguano wa masilahi ya nchi kwa upande mmoja na ya mtu au watu binafsi kwa upande mwingine. Ni hoja ya kuangalia kama sheria, taratibu, desturi, mazoea na kanuni za maadili zimekiukwa au vinginevyo. Hiyo si siasa.
Lakini hata ingekuwa siasa, haina maana kwamba baada ya kustaafu hapaswi kuwajibika kwa matendo yake. Inawezekana vitabu vya sheria vimemzungushia wigo wa kutowajibika kwa aliyoyafanya akiwa mamlakani, bado kuna uhalali wa kimaadili utaendelea kudai majibu sahihi kwa kila kilichofanyika. Kustaafu hakufuti rekodi iliyoandikwa nyuma. Kustaafu hakufanyi kiu ya maswali iliyoibuka izimwe.
Kustaafu hakufuti makosa wala hakubadilishi haki ya kujua kama yote yako vema.
Lakini kiu ya mwanadamu ya kujua ni kubwa na kwa kawaida uvumilivu una kikomo ndio maana waswahili wakawa na msemo wao kwamba bubu akizidiwa husema.
Watanzania waliofahamika kuwa watulivu na tusiopenda kuchokonoa mambo hasa ya wakubwa, wamebadilika. Hii ni dalili kwamba bubu anakaribia kusema. Idadi ya mambo yanayohojiwa inaongezeka. Idadi ya tuhuma bado ni ndefu kwa watu mbalimbali.
Watu wameanza kutumia njia za mitandao kusambaza habari mbalimbali. Tumesikia wananchi wakiwazomea viongozi wa juu wa serikali katika matukio kadhaa. Huku ndiko kusema kwa bubu.
Tumeona maandamano japo madogo ya wafanyakzi wakidai nyongeza ya mishahara.
Tumeshuhudia watu wengi wakipinga uamuzi wa Bunge kumsimamisha Zitto Kabwe. Bubu wamefikia mahali sasa wanaanza kusema. Nani alijua jambo kama la Zitto lingeweza kubadili hali ya siasa za nchi hii?
Ikiwa mambo kama haya yanatokea halafu wananchi wanajibiwa kwamba nimestaafu, tujue bado tunapalilia tatizo.
Tumesoma kwenye vyombo vya habari kuhusu madai ya Butiku.
Ingawa madai hayo ni ya kisiasa, ni muhimu yapatiwe pia majibu kama kuna nia ya kweli ya kukinusuru Chama Cha Mapinduzi, lakini na taifa pia kwa ujumla. Ni vyema mtu ajue kama kinachosemwa ni kweli au uongo. Kama ni kweli tujue kama ni sahihi au la. Kukaa kimya ni kuacha ombwe ambalo hakuna hakika litajazwa na nini.
Hapo ndipo tatizo lililopo, maana chochote kinaweza kutokea kulijaza.
Lakini hoja nyingine pia ni ikiwa wananchi hawana haki ya kujua mambo yanayowahusu kwa sababu mhusika amestaafu siasa.
Kimsingi wananchi ndio waajiri wa rais. Kutoka kwake madarakani hakupaswi kuzuia waajiri wake wasihoji namna alivyofanya kazi waliyompa. Kama alifanya vyema sawa.
Ikiwa alifanya vibaya anapaswa kuwajibika hata kama si kisheria basi walau kimaadili. Shutuma zinaporoshwa kutoka upande mmoja, wadau wote wana haki ya kufahamu ukweli au uongo wa shutuma hizo.
Anayeshutumiwa ana nafasi nzuri zaidi ya kutoa maelezo ya upande wake kabla hatujajumlisha moja na moja kupata mbili.
Kustaafu siasa bado hakuondoi haja hii ya msingi ya kutaka kujua kama rais mstaafu aliyatumia vyema madaraka yake au la.
Lakini kwa anayepima joto la uelewa wa wananchi kwa sasa atajua kwamba kinachoendelea sasa si siasa.
Wananchi wameambiwa kuhusu maisha bora. Wamepigiwa magitaa kwamba Tanzania yenye neema iko njiani. Lakini wakati huohuo zinasambaa habari kwamba tunapoteza fedha nyingi au rasilimali nyingi kwa njia isiyo halali.
Wananchi wanaanza kuelemewa na maneno yenye matumaini ambayo hata hivyo sasa yanaanza kubadilika. Bubu anaanza kuzidiwa na taratibu anaanza kusema!
Mtu mweledi hupambanua mambo. Tanzania ina watu wengi wa jinsi hii. Wana macho wanaona. Wana akili wanatafakari. Wanaweza kutambua alama za nyakati. Hivyo wanapouliza hawafanyi dhihaka. Rasilimali za taifa si suala la siasa. Ole wetu kama uchumi tumeufanya kuwa hoja ya kisiasa. Kama ni hivyo, Tanzania yenye neema na maisha bora kwa wote. Wakati bubu wanataka kusema, wakubwa wanasema wao wamestaafu!
Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu 0784 265 072 au barua pepe: kevinmakyao@hotmail.com
Juvenalis Ngowi
Tanzania Daima
NATIMIZA sehemu ya wajibu wangu kwa kuanza kumwomba Mola wangu aniongoze na kuniangaza kwa namna ya pekee ninapowakilisha wazo langu jepesi kwa wasomaji wa safu hii.
Yeye ndiye mweza wa yote na haishangazi tunamuita Mwenyezi, Muweza. Huyu ndiye aonaye hadi kwenye uvungu wa mtima wa mtu na hata vilivyofichwa na kufunikwa chini ya busati, yeye anaviona.
Juma hili nimeshangazwa na habari kuhusu rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa. Wengine humuita Mzee wa Utandawazi. Huyu si tu alikuwa mwanafunzi wa darasani wa Mwalimu Nyerere, lakini alikuwa chaguo na kipenzi chake wakati akigombea urais kwa mara ya kwanza mwaka 1995.
Mkapa ninayemfahamu ni bingwa wa takwimu, ni mtaalamu wa kufikisha ujumbe aliokusudia. Anafahamu kuchagua maneno atakayotumia na sikushangaa nilipoambiwa kitaaluma rais huyu mstaafu ni mwanahabari.
Sifa zake hazifanani hata chembe na habari ninayoizungumzia. Kwamba alikataa kujitetea au walau kutoa maoni yake kuhusu shutuma na tuhuma zilizoelekezwa kwake.
Kukataa peke yake kusingenishangaza. Ila inapodaiwa eti alikataa kwa kuwa amestaafu siasa, nashindwa kuelewa. Ubongo unakataa kuikubali sababu hiyo.
Angekataa kwa sababu ana hiari ya kujitetea au kukaa kimya hilo ni jambo jingine.
Kwamba ameona tuhuma hizo hazina uzito wa kujibiwa, ingeweza ikawa sababu. Lakini hii ya kusema amestaafu siasa si sababu ya kufanya wapembuzi yakinifu wafunge mdomo.
Mosi, tuhuma zilizotolewa sio za kisiasa. Kwa rais mstaafu huyu ziliwahi kuelekezwa tuhuma nyingi. Walianza waliomtuhumu kufanya biashara akiwa katika ofisi kuu nchini. Wakahoji hakukuwepo mgongano wa masiahi? Wengine wakaanza kuyakumbuka maneno ya Mwalimu kwamba Ikulu ni mahali patakatifu. Rais mstaafu akakaa kimya kabisa. Rais aliye madarakani naye akawaasa wanaochokonoa mambo hayo wamwache mzee wetu apumzike. Asiulizwe swali. Na imeshasemwa wazi kwamba hatachunguzwa.
Baada ya hapo zikashuka shutuma nyingine zinazoenezwa na kambi ya upinzani kuhusu rais huyu mstaafu na wenzake kadhaa. Hapa wengine walijitokeza kujibu tuhuma.
Wengine wakajiapiza kwenda kujisafisha mahakamani. Wengine wamebaki kimya.
Nisingetegemea kwamba rais mstaafu naye angejitokeza aseme anakwenda kujisafisha mahakamani. Lakini pia sikutegemea aseme anabaki kimya kwa kuwa amestaafu siasa.
Tuhuma zilizotolewa si siasa. Ni tuhuma zinazogusa uchumi wa nchi. Nituhumu zinazogusa watu walio katika nafasi ya utendaji.
Hata kama zinatolewa katika majukwaa ya kisiasa na wanasiasa bado zinabaki ni tuhuma zinazohoji uadilifu wa mtu au watu.
Hiyo si siasa hata kidogo. Tuhuma za kufanya biashara akiwa katika ofisi takatifu si siasa.
Ni hoja ya kuangalia kama kuna msuguano wa masilahi ya nchi kwa upande mmoja na ya mtu au watu binafsi kwa upande mwingine. Ni hoja ya kuangalia kama sheria, taratibu, desturi, mazoea na kanuni za maadili zimekiukwa au vinginevyo. Hiyo si siasa.
Lakini hata ingekuwa siasa, haina maana kwamba baada ya kustaafu hapaswi kuwajibika kwa matendo yake. Inawezekana vitabu vya sheria vimemzungushia wigo wa kutowajibika kwa aliyoyafanya akiwa mamlakani, bado kuna uhalali wa kimaadili utaendelea kudai majibu sahihi kwa kila kilichofanyika. Kustaafu hakufuti rekodi iliyoandikwa nyuma. Kustaafu hakufanyi kiu ya maswali iliyoibuka izimwe.
Kustaafu hakufuti makosa wala hakubadilishi haki ya kujua kama yote yako vema.
Lakini kiu ya mwanadamu ya kujua ni kubwa na kwa kawaida uvumilivu una kikomo ndio maana waswahili wakawa na msemo wao kwamba bubu akizidiwa husema.
Watanzania waliofahamika kuwa watulivu na tusiopenda kuchokonoa mambo hasa ya wakubwa, wamebadilika. Hii ni dalili kwamba bubu anakaribia kusema. Idadi ya mambo yanayohojiwa inaongezeka. Idadi ya tuhuma bado ni ndefu kwa watu mbalimbali.
Watu wameanza kutumia njia za mitandao kusambaza habari mbalimbali. Tumesikia wananchi wakiwazomea viongozi wa juu wa serikali katika matukio kadhaa. Huku ndiko kusema kwa bubu.
Tumeona maandamano japo madogo ya wafanyakzi wakidai nyongeza ya mishahara.
Tumeshuhudia watu wengi wakipinga uamuzi wa Bunge kumsimamisha Zitto Kabwe. Bubu wamefikia mahali sasa wanaanza kusema. Nani alijua jambo kama la Zitto lingeweza kubadili hali ya siasa za nchi hii?
Ikiwa mambo kama haya yanatokea halafu wananchi wanajibiwa kwamba nimestaafu, tujue bado tunapalilia tatizo.
Tumesoma kwenye vyombo vya habari kuhusu madai ya Butiku.
Ingawa madai hayo ni ya kisiasa, ni muhimu yapatiwe pia majibu kama kuna nia ya kweli ya kukinusuru Chama Cha Mapinduzi, lakini na taifa pia kwa ujumla. Ni vyema mtu ajue kama kinachosemwa ni kweli au uongo. Kama ni kweli tujue kama ni sahihi au la. Kukaa kimya ni kuacha ombwe ambalo hakuna hakika litajazwa na nini.
Hapo ndipo tatizo lililopo, maana chochote kinaweza kutokea kulijaza.
Lakini hoja nyingine pia ni ikiwa wananchi hawana haki ya kujua mambo yanayowahusu kwa sababu mhusika amestaafu siasa.
Kimsingi wananchi ndio waajiri wa rais. Kutoka kwake madarakani hakupaswi kuzuia waajiri wake wasihoji namna alivyofanya kazi waliyompa. Kama alifanya vyema sawa.
Ikiwa alifanya vibaya anapaswa kuwajibika hata kama si kisheria basi walau kimaadili. Shutuma zinaporoshwa kutoka upande mmoja, wadau wote wana haki ya kufahamu ukweli au uongo wa shutuma hizo.
Anayeshutumiwa ana nafasi nzuri zaidi ya kutoa maelezo ya upande wake kabla hatujajumlisha moja na moja kupata mbili.
Kustaafu siasa bado hakuondoi haja hii ya msingi ya kutaka kujua kama rais mstaafu aliyatumia vyema madaraka yake au la.
Lakini kwa anayepima joto la uelewa wa wananchi kwa sasa atajua kwamba kinachoendelea sasa si siasa.
Wananchi wameambiwa kuhusu maisha bora. Wamepigiwa magitaa kwamba Tanzania yenye neema iko njiani. Lakini wakati huohuo zinasambaa habari kwamba tunapoteza fedha nyingi au rasilimali nyingi kwa njia isiyo halali.
Wananchi wanaanza kuelemewa na maneno yenye matumaini ambayo hata hivyo sasa yanaanza kubadilika. Bubu anaanza kuzidiwa na taratibu anaanza kusema!
Mtu mweledi hupambanua mambo. Tanzania ina watu wengi wa jinsi hii. Wana macho wanaona. Wana akili wanatafakari. Wanaweza kutambua alama za nyakati. Hivyo wanapouliza hawafanyi dhihaka. Rasilimali za taifa si suala la siasa. Ole wetu kama uchumi tumeufanya kuwa hoja ya kisiasa. Kama ni hivyo, Tanzania yenye neema na maisha bora kwa wote. Wakati bubu wanataka kusema, wakubwa wanasema wao wamestaafu!
Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu 0784 265 072 au barua pepe: kevinmakyao@hotmail.com