Ngongo
JF-Expert Member
- Sep 20, 2008
- 18,895
- 31,106
Mbunge wa Bukoba Vijijini anayemaliza muda wake, Nazir Karamagi
Kashfa za Richmond na Buzwagi zimeendelea kumtoa jasho Mbunge wa Bukoba Vijijini anayemaliza muda wake, Nazir Karamagi, wakati wanachama wa Chama Cha mapinduzi wanapomuuliza maswali katika mikutano ya hadhara ya kampeni za kura za maoni.
Tangu kuanza kwa mikutano hiyo katika matawi na kata 11 katika tarafa za Bugabo, Kyamtwara na Katerero baadhi ya wanachama wanaopewa fursa kuuliza maswali baada ya wagombea kujieleza, Karamagi amekuwa akiulizwa kuhusu kashfa za kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Richmond na sakata mkataba wa mgodi wa dhahabu wa Buzwagi.
Maswali mengine ambayo Karamagi anakumbana nayo ni kuhusu ahadi yake ya kupeleka umeme katika eneo la Ikimba.
Hali hiyo imewafanya baadhi ya wanachama kuhamaki na kutishia kumdhuru mwanasiasa huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko kabla ya kuhamishwiwa Wizara ya Nishati na Madini katika serikali ya awamu ya nne.
Katika kata ya Katerero, mkutano uliofanyika katika kijiji cha Rwagati jana asubuhi, wanachama walichachamaa na kumfanyia fujo Karamagi kwa madai ya kukerwa na mbunge huyo, huku wengi wakimshinikiza ajitoa na kuwaachia nafasi hiyo vijana wengine.
Katika mkutano huo uliokuwa umehudhuriwa na wanachama wengi wa kata hiyo, iliwalazimisha polisi kufanya kazi ya ziada ya kuwatuliza baadhi ya vijana na wanachama waliokuwa wakimzonga Karamagi.
Mbali na wanachama hao pia walikuwepo wananchi kutoka eneo la Kemondo ambao nao walijumuika kumzonga mbunge huyo.
Josephat Rwamugira, alimuuliza Karamagi kwa nini asing'atuke kutokana na kashfa nzito za kitaifa zilizomchafua na kwamba zinakichafua chama.
Akijibu swali hilo, Karamagi alikana kuhusika na Richmond kwa maelezo kuwa yeye aliingia katika wizara ya Nishati na Madini akitokea Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko wakati mkataba wa Richmond ulikwisha kusainiwa.
Karamagi alijitetea kuwa alilazimika kujiuzulu kwa dhana ya uwajibikaji kama kiongozi mkuu ndani ya wizara hiyo.
Majibu hayo ndiyo yaliyosababisha taharuki na kutoka kwa wanachama na wananchi wengine waliofika katika mkutano huo, ambao walianza kumzomea mbunge huyo.
Yusuf Razaki, alimuuliza Karamagi kuwa tangu awe mbunge mwaka 2005 ametembelea jimbo hilo mara ngapi.
Karamagi alijibu swali hilo kwa kunukuu tarehe ndani ya kijitabu alichokiandaa.
Gosbert Sostenes, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Kaja, alimuuliza Karamagi kwamba atawezaje kutimiza ahadi yake ya kupeleka umeme katika Wilaya ya Bukoba Vijijini wakati alishindwa kufanya hivyo akiwa Waziri wa Nishati na Madini.
Katika maelezo yake, mwanafunzi huyo alisema kuwa shule nyingi za jimbo la Bukoba Vijijini hazina umeme na ni tatizo kwa wanafunzi wa mchepuo wa Sayansi kutokana na kutokuwa na maabara ambazo vifaa vyaka vinatumia umeme.
Aidha, alimweleza Karamagi kuwa kama asingelisomea katika shule zenye umeme asingelipata shahada alizonazo.
Akijibu swali hilo, Karamagi alisema kuwa kabla ya kujiuzulu Februari mwaka 2008, alishaandaa na kukamilisha mipango ya kupeleka umeme katika Wilaya ya Bukoba.
Wakati Karamagi akipata msukosuko huo, wagombea wengine wanaoomba uteuzi wa CCM walikuwa wakishangiliwa.
Wengine wanaoomba uteuzi wa CCM ni Kamaludin Mustafa, Muzamilu Kachwamba, Novatus Nkwama na Jasson Rweikiza.
Source: Nipashe.
My Take.
Kweli Dr Mwakyembe aliwahi kusema waTanzania siku hizi si mabwege.Natamani Lowassa,Rostam,Msabaha wakumbane na maswali kama haya.