Mwaka wa 2012 ni wa Kusimamia na Kupigania "Utu wa Mtanzania"

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
Katika salamu zangu za mwaka mpya mwaka jana nilidokeza kuwa mwaka 2011 ungekuwa ni mwaka ambapo ‘hekima’ ingewekwa majaribuni.
Nilielezea kuwa mwaka 2011 ungetuonesha sana ni jinsi gani viongozi wetu wanahitaji hekima na ni kwanini kukosekana kwa hekima kungetuletea matatizo zaidi na kuwagawa wananchi na viongozi wao zaidi na zaidi. Kuanzia matukio ya mauaji ya Arusha Januari 5, 2011 hadi matukio ya mwisho ya kufunga mwaka uliopita suala la hekima za viongozi lilikuwa ni kilele. Tumeshuhudia sote ni jinsi gani viongozi wetu wenye elimu na utajiri wa kila namna wakikosa hekima ya nini cha kusema au cha kufanya na hivyo kushindwa kuchukua hatua ambazo zingekuwa tofauti kama wangeongozwa na hekima.

Naomba kupendekeza kuwa mwaka huu mpya utaendelea kuwa na suala la hekima zaidi lakini kwa mara ya kwanza tutashuhudia Watanzania waking’ang’ania ‘utu wao’. Ninapozungumzia ‘utu’ wao ninazungumzia ile ‘hadhi ya kuwa mwanadamu mwenye kustahili tunu, haki, na heshima zimpasazo mwanadamu’. Kwamba mwaka huu utu wa Mtanzania hautapimwa tena kwa elimu, utajiri, nafasi au hadhi ya kijamii – bali utapimwa kwa kuangalia ubinadamu wake na mastahili yake kama mwanadamu.

Watanzania watakataa kudharauliwa

Kwa miaka nenda rudi wamekuwepo viongozi ambao ambao wanaamini kuwa Watanzania ni watu walio chini yao. Viongozi hawa huamini kuwa huweza kufanya lolote kwa sababu wanajua kuwa wao wako juu ya wananchi. Viongozi hawa hawana na wamepoteza kabisa unyenyekevu wa kuwa watumishi wa umma. Tumesikia mara nyingi kauli za dharau kutoka kwa viongozi wa aina hii na katika mwaka huu hakuna kauli ambayo imewakorofisha watu kama ya John Magufuli ambaye amewaambia wananchi wa Kigamboni kwa dharau kuwa kama hawataki kulipa ongezeko la nauli ya feri basi “wapige mbizi”! Angeweza kabisa kujenga hoja ya kuongeza nauli bila kuonesha kutokujali maisha ya wananchi na dharau (utter contempt of the people)

Ni kauli inayotukumbusha yale ya Basil Mramba aliyewaambia Watanzania kuwa hata ikibidi Watanzania wale “majani” ndege ya Rais itanunuliwa! Wengine imebidi tuanze kuhoji uwezo wa Magufuli kuongoza. Watu wengi tunajua kuwa hatujawahi kumsikia Magufuli akionesha uongozi bila kuwa na madaraka. Kwamba yEyote ambayo anasifiwa na wananchi ni kwa sababu ameshika madaraka. Sasa kiongozi anayetegemea madaraka ili kuonesha uongozi wake si kiongozi mzuri kwani atajificha katika mwamvuli wa madaraka kila anapofanya jambo. Kiongozi kama huyo akiwa nje ya madaraka hawezi kuongoza kwani hana cha kusimamia; hana ushawishi wa hoja wala maono ya kiuongozi! Yaani, Magufuli bila madaraka ni sifuli! Ndiyo maana anaweza kutumia hizi lugha za ubabe na dharau kwa Watanzania! Hawezi kujenga hoja za kushawishi bila kutumia ubabe unaotokana na cheo.

Sasa hii dharau imetoka wapi? Fikiria inakuwaje watu wanachukua majeneza yenye miili na kuyatupa barabarani bila kuwajibishwa? Fikiria inakuwaje watu wanafanya madudu ya kila namna ambayo ni dhulma ya utu wa Mtanzania lakini bado wanajiita ‘viongozi’! Ndio maana niliwatungia lile jina la “watawala wetu”! Leo hii wamekuwa kama wakoloni uchwara ambao wanaamini kuwa wao ndio zawadi ya Mungu kwa Watanzania na kuwa hakuna Mtanzania mwenye sababu wala uwezo wa kuwahoji, kuwapinga au kuwakatalia!

Bahati mbaya hii dharau yao mwaka huu itafikia kikomo kwani hata punda akizidishiwa mizigo hugoma! Ninatabiri kuwa mwaka huu Watanzania watakataa kudharauliwa, kupuuzwa na kunyanyaswa na viongozi wao. Huu ni mwaka wa kuwakatalia watawala! Mwaka huu hakuna Mtanzania akayekubali kupigwa kibao na kiongozi naye akainama kwa haya; watarudisha vibao kwa vibao! Mwaka huu hakuna Mtanzania ambaye atakubaliwa kubomolewa nyumba yake kwa sababu kiongozi fulani kasema wakati kesi zipo au mahakama hazijaamua! Tumeona dalili zake mwaka jana, na mwaka huu utakuwa ni ugomvi wa kudumu!

Tuliposema kuwa “tumedharauliwa vya kutosha, tumepuuzwa vya kutosha na tumenyanyaswa vya kutosha” hatukumaanisha na wakoloni tu! Leo hii Watanzania watakaa kudharauliwa, kunyanyaswa na kupuuzwa na viongozi wao! Watadai utu wao!

Watanzania watakataa kusukumwa

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema kitu kimoja wakati wa harakati za ukombozi wa Afrika kuwa binadamu hapendwi kusukumwa sukumwa! Alisema kuwa binadamu hapendwi kufanywa duni. Alisema pia kuwa binadamu siyo mbwa ambaye unaweza kumliwaza kwa kumtupia kipande cha nyama. Alikuwa anaelezea hilo baada ya Ujerumani Magharibi kuamua kuondoa misaada yake baada ya Nyerere kuruhusu Ujerumani Mashariki kufungua ubalozi wake nchini.

Wajerumaini walikasirishwa na uamuzi huo wa Nyerere na wakaamua kukatisha baadhi ya misaada yao na kuacha msaada wa karibu dola milioni tatu hivi. Nyerere aliwaambia na huo msaada wa dola milioni tatu chukueni! Aliwaambia sisi ni binadamu na hatuwezi kufanywa kama mbwa! Hatuwezi kunyanyaswa kwa misaada!

Sasa, kama nilivyosema kwenye dharau hapo juu suala la kusukumwa sukumwa ni matokeo haya ya dharau. Watawala na vyombo vyao huamini kuwa wanaweza kufanya lolote kwa yeyote bila kujali lolote (with absolute impunity). Ndiyo maana kule Tunisia askari wa jiji waliamua kumnyang’anya mmachinga mmoja vitu vyake kwa sababu ati hakuwa anafanya biashara kihalali! Matokeo yake yule mtu kwa vile alikuwa hana kingine cha kupoteza isipokuwa utu wake aliamua kujitia mafuta na kujichoma moto! Ndio ukawa mwango wa mwamko wa Waarabu ambao wamekuwa wakisukumwa na watawala wao kwa miaka karibu hamsini sasa! Matokeo yake ni Ghadaffi akatolewa nje, na Hosni Mubarak aanasimamishwa kizimbani!

Kuna imani potofu kuwa Watanzania wanapenda kusukumwa sukumwa na kupuuzwa. Leo utasikia polisi kafanya hiki mara utasikia waziri kafanye kile. Utasikia mara kiongozi fulani amefanya hivi mara utasikia mzee wa watu anafuatilia malipo yake hadi anaanguka mauti kwa sababu hakuna mtu wa kumsikiliza. Utasikia wafanyakazi wanalalamikia mishahara na posho zao hadi wanashirikia katika ufisadi hata wale ambao walikuwa hawataki vitendo hivyo! Wanapolalamika wanaambiwa wao “mbayuwayu!” Watanzania hawawezi kuendelea kusukumwa bila kukoma maana nao ni binadamu na wana utu wao! Ninaamini mwaka huu wapo Watanzania watakaokataa kusukumwa sukumwa na kudhauraliwa!

Watanzania watakataa kupuuzwa!
Katika demokrasia utawala hutoka kwa watu. Na katika demokrasia ya kweli utawala wa watu huonekana kwa jinsi ambavyo wananchi wanaweza kulazimisha na kusababisha serikali yao kubadili mwelekeo. Katika nchi za kidikteta (uwe wa mtu mmoja au chama kimoja au kikundi cha watu wachache) wananchi hawana nafasi; wao hulazimishwa kutekeleza yanayoamuliwa katika “vikao” na hakuna wa kuweza kubadilisha. Mtu yeyote anayejaribu kutaka asikilizwe huishia lupango au hata “kutoweka katika mazingira ya kutatanisha”.

Wananchi hupuuzwa! Yaani wanafanywa si kitu bali kama maroboti ambayo yanatakiwa kuitikia na kusema hewala kwa kila jambo linaloamriwa. Mawazo ya wananchi yanaulizwa juu juu tu bila kumaanisha. Mfano mzuri ni suala la Katiba Mpya kwa mfano. Japo wengi wanaamini kuwa Tume ya Maoni ikiundwa itakusanya maoni ya wananchi ukweli ni kuwa tume itakayoundwa haitakusanya maoni na kuyakubali maoni yenye nguvu!

Fikiria kwa mfano, wananchi wa Tanzania bara wakatoa maoni ya kutaka tuwe na serikali moja, hivi mnafikiria maoni hayo yatakubaliwa? Au itokee kuwa wananchi wa Zanzibar wakatoa maoni mengi zaidi ya kutaka kuvunja Muungano, hivi mnafikiria yatasikilizwa? Hivi leo hii katika kukusanya maoni, tuamue kumfanya Waziri Mkuu awe na nguvu zaidi kuliko Rais (yaani awe waziri mkuu mtendaji si kama sasa hivi alivyo wa picha) mnafikiri yatakuwa ni maoni yatakayosikilizwa?

Ukweli ni kuwa maoni yoyote yatakayotolewa ni lazima yaendane na kile ambacho watawala wanakitaka! Haijalishi maoni yatatolewa namna gani na ya namna gani lakini kwa kadiri ya kwamba yatapingana na wanachotaka wao yatapuuzwa! Ninachosema ni kuwa mwaka huu ni mwaka wa Watanzania. Kwa miaka hamsini Watanzania wamechukuliwa kama watoto ambao wanadekezwa na kupuuzwa.

Sasa wamekuwa watu wazima na wale waliozaliwa baada ya uhuru sasa wameanza kuwa na wajukuu na wengine wajukuu wao wameanza hata shule! Kwa ufupi ni kuwa Watanzania walioko sasa hivi wanajitambua zaidi na wanatambua zaidi utu wao. Sasa hivi kizazi cha mageuzi kimekomaa na kinaanza kutoka vyuo vikuu! Kwa ufupi, Tanzania iliyopo sasa imebadilika sana na inazidi kubadilika kila kukicha.

Ndugu zangu, ninapowatakia heri na fanaka za mwaka huu mpya nataka niseme tu kuwa Watanzania katika mwaka huu watakataa kudharauliwa, kusukumwa na kupuuzwa! Watakataa kufanywa si kitu katika nchi yao wao wenyewe! Mwaka huu hotuba tulizozizoea za “vikapanda vikashuka” za CCM na viongozi wake zitakatiliwa.

Watanzania watakataa kulishwa maneno kama halua na kunyeshwa ahadi kama uji wa ulezi! Hotuba zilizojaa namba nyingi zitakaliwa kama hazijajaa ukweli mwingi! Nilichokisema hapa hakiwahusu Watanzania wote; kinawahusu wale waliofunguka! Wale wenye kuabudu kwenye altare ya CCM na wenye kuitolea sanamu ya Nebukadneza (CCM) hatuwezi kuwasaidia kwani kufunguliwa kwao kutakuja kwa machozi! Watakapotambua kuwa sanamu yao wanayoiabudu “ina macho lakini haioni, ina masikio lakini haisikii, na ina miguu lakini haiendi, na wenye kuiabudu wanafanana nayo!”

Niandikie
 
Mkuu japo umenena,Lakini Huo uthubutu uko wapi? iLi hali Yule mchungaji Mtikila Katika kubwabwaja kwake alituita ........Kondoo? Ambao ni ukweli usiopingika????????
 
Mzee Mwanakijiji,

Mkuu wangu tuandike sana hapa JF lakini hakika hakuna wa kukuunga mkono..wameondoka wangapi toka Kolimba, nani alisimama na kudai haki, Kina Mwakeyembe wamebakia peke yao Hospital wakiuguza maradhi na nafsi zao peke yao hakuna hata mchango wa salaam..Tena siku hizi analaaniwa zaidi na EL kupambwa..

Sisi tunasema sana, tunajua sana kuuchonga lakini nadhani nidhamu ya woga ni mbaya kuliko hata Gaidi maana wenzetu wana malengo na wanajua wasichokitaka na kamwe huwezi kuwalazimisha..Bongo mkuu wangu utajikuta peke yako unless fedha unayo kupambana nao.. Kinyume cha hapo watakwambia mkono mtupu haulambwi. Tuliingia utumwa na ukoloni sii kwa kulazimishwa na tulipewa Uhuru wetu kwa hiari yao vile vile tofauti na Zanzibar.

I hope kuna fikra mpya za kufuta kwanza siasa za KINAFIKI... kama tukishindwa kufuta Unafiki basi ndio ngoma ile ile ya kushindwa kufuta Ufisadi ukitegemea nchi itaendelea tukizalisha zaidi..
 
call me the pessimist.....but siwaoni hao watanzania wa kukataa yote hayo........
naona malalamiko tu kuanzia wananchi mpaka viongozi.....kila mtu analalamika tu
no action.......

...BOSS na hili ndilo tatizo kubwa la nchi yetu. Sijui kama hili litatokea. Ile miaka ya 2007-2009 wakati wa ufisadi wa EPA, Kagoda, Meremeta, Richmond umepamba moto nikadhani Watanzania watakataa kuongozwa na mtu ambaye hana sifa ya kuwa hata mjumbe wa nyumba tano tano achilia mbali wa nyumba kumi kumi, lakini halikutokea lolote jamaa akaendelea na usainii wake tu huku malalamiko ya utendaji wake mbovu yakizidi kushamiri siku hadi siku. Tusubiri tuone, lakini BOSS mie nakuunga mkono.

 
Nini kinachopatikana 2012 ambacho kimekosekana 2011 and before kitakachowafanya watanzania "wajitambue"? Mimi sikioni...
 
Hayo ni mambo ambayo wengi tunatamani yatokee ila tusitegemee kwasababu bado waTanzania wengi hawajaamka. Kama ni dharau wameshazoea kiasi kwamba wanaona kawaida, kusukumwa ndio kabisa wanaona ndio namna pekee ya maisha, na kupuuzwa wala hakuwasumbui. Yani hawajui haki zao hivyo hata kuzitafuta hawawezi.
 
  • Thanks
Reactions: BAK
Back
Top Bottom