MWAKA 2016 kwa kheri nenda kama alivyoenda MAMA

Mbao za Mawe

JF-Expert Member
May 11, 2015
23,373
54,744
Sina budi kuandika machache ambayo yametokea katika huu mwaka kwani ni mwaka ambao unaondoka ukiwa na historia ndefu sana katika maisha yangu.

Binadamu ni rahisi sana kuandika kumbukumbu zote zinazomtokea hapa duniani na kumbukumbu hizi hubaki kama sehemu mojawapo ya maisha yake.

Kipindi mwaka unaanza niliamini kuna hatua zangu katika maendeleo zingesogea mbele ila japo sio sana ila naona kiasi fulani nimepiga hatua japo sikupata kile nilicholenga ila kuna kitu nimejifunza hata kama sikupata chochote.

Tarehe moja mwezi January mwaka 2016 ni tarehe iliyoanza kwa masikitiko makubwa sana na unyonge wa aina yakr katika maisha yangu kwani nilikuwa nipo katika sintofahamu juu ya uhai wa mwanamke aliyenileta duniani ,ilikuwa ni mwanzo mgumu sana maana sikuwahi kuuguliwa na mtu wangu wa karibu katika maisha yangu na nilijawa na mawazo na hasa ikijalisha kuwa umekaa na mgonjwa unasubiri Mungu achukue roho yake kwani kitaalamu hali ilikwisha shindikana na binadamu asingeweza kurudisha afya ya mgonjwa ambaye alikuwa mikononi mwetu.

Mwaka 2016 ni mwaka wa ajabu sana kwangu na ulinipa nafasi ya kujua wema na wabaya ambao wako katila msafara wangu ,na hii ilinisaidia sana kuwachambua wale wote waliokatika msafara wangu.

MWAKA WA MAJONZI:
Kumbukumbu zangu zinaanza hapa baada ya kupata uhakika kuwa mama mzazi hawezi kupona na tulikuwa tunasubiri akate roho ,kiukweli ulikuwa wakati mgumu sana kwangu hata wakati nikiwa kazini nakumbuka nilikuwa ni mtu wa kulia mara kwa mara na wakati mwingine kazi yangu ilikuwa inashindwa kufanyika katika usahihi wake kwani nilikuwa natumia muda mwingi kukaa pekee yangu na kulia kila nikiwaza ni namna gani tutabaki katika familia baada ya mmoja kati ya watu muhimu atakaondoka hapa duniani.

SAFARI YA KUELEKEA NYUMBANI:
Hii haikuwa safari ya kawaida kwenda nyumbani ,maana wakati anaugua mama mimi nilikuwa mbali kidogo na Nyumbani nakumbuka siku hiyo nikiwa nawasiliana na dada (mama alisikia sauti yangu na kuomba simu aongee na mimi) sauti ya kukata tamaa na yenye Upendo ilisikika katika sikio langu na alitaka niende nyumbani kesho yake nimwone (alikuwa kakata tamaa ya kuishi), nilitii wito wake na kuomba ruhusa kazini na kuelekea nyumbani (sikusubiri kuondoka kesho yake niliondoka mchana).

KUWASILI NYUMBANI:
Baaa ya safari ya masaa kama manne niliwasili nyumbani nikiwa na huzuni moyoni na nikiwa sina raha kwani nilikuwa nina uhakika muda si mrefu nisingekuwa na mama yangu.

Wakati nipo njiani kuelekea nyumbani nikiwa kama mita 300 kufika nyumbani nilisikia kilio (hali hii ilinifanya kukosa nguvu na kila nilipozidi kukaribia niliona idadi ya watu pale nyumbani na moyo wangu ukawa umeamini kuwa roho ya mama tayari imeuacha mwili ,nilizidi kwenda kwa majonzi huku nguvu zikiwa si zote ndani ya mwili wangu , Mbele alikuwa ni mdogo wangu aliyekuja mbio kunipokea swali la kwanza kuuliza (Mama anaendeleaje na nani analia huku nikijizui kutokwa na machozi) ,alinijibu mama bado anaumwa na yeye ndiye analia ,kiukweli usiombe uuguliwe na ujue kuwa mgonjwa wako hana tiba zaidi ya kufa.

Nilipofika nyumbani huku nikizidi kujikaza na kutaka kuonesha uso wa furaha kwa wote waliokuwa pale nyumbani ,kwa wadogo zangu na ndugu na jamaa ,nilimkuta mama akiwa sebuleni na akiendelea kulia huku akiwa anatoa wosia kwa waliomzunguka na kuwasihi wawe na mapenzi na wasiwe na chuki hapa duniani (sikumsemesha kwa hali aliyokuwa nayo na jinsi nilivyokuwa ) sauti ya mdogo wangu nayo ilisikika ikilia chini kwa chini kwani tayari kila mtu alijua kinachoendelea . Baada ya kilio cha mama kutulia nilisikia sauti yake "Mwanangu umekuja kuniona, mama yako ninaumwa sana" nilimpa pole na kumsisitiza asikate tamaa kwani atapona na kurudi katika hali yake japo kupona kwake ingekuwa ni miujiza (alikuwa kaharibika ini,bandama na figo).

KESHO YAKE;
Ilipofika asubuhi akiwa kitandani na wauguzi wake nilienda kumsalimia na nilipofika alionesha kuchangamka na kunisalimia japo kwa shida na kuomb aongee nami , tuliongea kama dakika kumi na katika yale maongezi ndipo nilijua kuwa sina mama kwani maongezi yake hayakuwa na matumaini kabisa , alienda mbali zaidi na kunipa baadhi ya mali zake na kutumia lugha rahisi kuwa hanipi urithi bali nakupa zawadi mwanangu hata kama nitapona vitabaki kuwa zawadi zako na sio kuwa ni urithi ( ukweli ni kwamba nilijakaza sana na kumwonesha ushindi upo japo ni kwa kiwango cha ajabu sana).

Baada ya maongezi yake aliniruhusu niendelee na kazi nyingine pale nyumbani na kiukweli mambo yalizidi kupasua kichwa changu.

SAFARI YA KURUDI KAZINI;

Baada ya siku kama tatu nilirudi kazini na akinisisitiza nisije kupuuzia baadhi ya vitu tulivyoongea siku ile asubuhi, nilirudi kazini na kufanya kazi kwa majuma kadhaa huku akiendelea kuugua mama yangu na kuzidi kukosa imani ya kuishi.

SAFARI YA MWISHO KUELEKEA NYUMBANI MAMA AKIWA HAI:

Nakumbuka ilikuwa ni siku ya ijumaa niliondoka na kwenda nyumbani huku nikiwa na huzuni njiani maana asubuhi ya siku ile nikiwa safari nilimbiwa hali yake ilikuwa mbaya na kufikia hatua watu wakaanza kulia wakidhani amefariki.

Nilifika nyumbani na mara hii alikuwa hawezi kuongea hata sentensi moja kutoka kinywani mwake ,nilimshika mkono huku na yeye akinishika na kunitazama usoni (alionesha kuna kitu angependa kuongea na mimi ila kinywa chake kilikuwa kimeziba na kufunguka tena ilikuwa ni mtihani.

Sikulala jioni niliondoka na kurudi kazini kuendelea na kazi, Feb 15 kama ilivyo kawaida dunia husheherekea siku ya wapendanao na mimi niliitumia siku hiyo kuongea na wasikilizaji wa kipindi changu na huku nikuwaomba waombee afya ya mzazi wangu.

Nikiwa na mawazo hata ufanisi katika kufanya kipindi ulitoweka (ilikuwa usiku) na baada ya kuendesha kipindi kwa takrbani saa moja niliweka wimbo maalum kwa ajili ya mama yangu na kuomba wasikilizaji waungane nami kumwombea ili arejee hali yake ya kawaida.

Baada ya kubao kile kuisha mwili wangu hasa kifua kilikuwa kimelowa machozi na kichwa kilianza kuuma na hali ile ilinifanya nipange nyimbo katika vitual dj na kuwaaga wasikilizaji kabla ya kipindi kuisha (huku nikitoa sababu ambazo si za kweli zimepelekea kipindi kutokuendelea) baadae nikalala.

Asubuhi nilirudi katika makazi yangu na kuendelea na mambo mengine.

Nakumbuka baada ya siku hiyo siku iliyofata (siku mbili baadae) nilikuwa sipo katika hali nzuri nililala mchana na kuijiwa na ndoto zisizoeleweka na mwili wangu ulijisikia mchovu kweli ,nilitafuta chakula nikala na kuendelea na siku hiyo , nakumbuka vizuri ilikuwa ni saa tano na simu yangu ilipata sms usiku yenye neno pole (zilikuwa ni namba mpya katika siku yangu) na baada ya muda kidogo ile namba ilipiga na nilipopokea nilimgundua aliyepiga na akaniambia umepata taarifa? Kutokana na sms yake ya Mara ya kwanza nilijua tayari mama kafariki na nilimjibu ndio taarifa ninayo akasema pole nikamjibu asante ,akauliza unakuja lini nikamwambia asubuhi.

Sikukaa muda ikaingia sms WhatsApp ya rafiki yangu akinipa habari za msiba ,nilijipa moyo wa kushinda hatua hiyo na nililala huku macho yakiwa na machozi usiku kucha na hatimaye kukakucha huku akili ikidhani ni ndoto kumbe lah ! Asubuhi niliamka na kujiandaa na kuelekea nyumbani kwa ajili ya mazishi.

Kiukweli mwaka huu ilikuwa ni mwaka wa kilio na majonzi kwangu siwezi kuusahau adha ambayo niliipata na ninayoipata baada ya kukosa uwepo wa mama kwa takrbani miezi 10 sasa.

Kwaheri mwaka 2016 nenda salama kama alivyoenda mama.

Mwisho kabisa nishukuru uwepo wa JF maana imekuwa inanipa faraja na furaha pale niwapo na mawazo hasa pale kumbukumbu zangu zinaporudi nyuma na kukumbuka Mwaka huu .

(Asante sana wote na hii itakuwa ni thread yangu ya mwisho katika huu mwaka ila tutazidi kuwa wote hadi pale JF itakapokuwa forum ya kipekee hapa nchini na nje ya nchi)

MUNGU awe nasi na atup wepesi katika maisha yetu hapa ulimwenguni na wale waliokatika vifungo mbalimbali vya magonjwa kazi na mengineyo awaoneshe njia mwaka 2017 ,wale watafutao kazi pia awakumbuke..
 
Pole kwa msiba wa mama
Ni njia yetu sote muhimu kwako ni kumuombea huko aliko apumzike kwa amani
Ni vyema kumkumbuka na kuendelea kuyaenzi yale aliyokuusia
Pole sana na Mwenyezi Mungu aipumzishe roho yake mahali pema apumzike kwa amani.
 
Pole sana ndugu yangu.
Licha ya kuwa habari yako ni ndefu yenye ujumbe uliojitosheleza nimefanikiwa kuisoma yote.

Nimejifinza mengi katika habari hii rafiki yangu ila kubwa nililolizingatia ni pale ulipo fanya maamuzi ya kwenda nyumban Mchana ule ule pasina kusubiri kesho yake.

Pole sana rafiki najua aina ya ukiwa ulionao.
Mungu wetu ni mwema wakati wote.
 
Pole sana mkuu. Mwenyezi mungu akupe amani na mwaka ujao wenye furaha. This made my cry, I can not imagine my life without my mama. I'm really, really sorry to hear this story.
 
Pole sana kwan kuondoka kwa mama dunia hii n kama umebak mwenyewe .... hayupo ambaye atakuwa na moyo kama wa mama ,, tuwapende mama zetu ingali wakiwa hai na tuwaheshimu siku zote .... Mm kwang mung hata akininyima utajiri ni sawa imradi tu amenipa zawadi iliyo bora na wala haiishiwi thaman sku zote za maisha yang .... NAKUPENDA SANA MAMA DALO
 
POLE SANA NAMWOMBA MUNGU AKUTIE NGUVU BWANA ALITOA BWANA ALITWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE...MUOMBEE MAMA APUMZIKE KWA AMANI YAENZI MEMA YOTE ONGEZA UPENDO NA MSHIKAMANO KATIKA FAMILIA...NA TAMBUA KWAMBA HIYO NI SAFARI YETU WANADAMU WOTE NAMWOMBA MUNGU AKUTUNZE
 
Pole sana Mkuu. Pole mno. Najua huwezi kuusahau lakini piga moyo konde na maisha yaendelee.
Yametokea na ni ngumu yeye kurudi haina budi nikubali kile kilichopo mbele yangu kuwa si kwa mapenzi yangu bali muumba
 
Pole sana kwan kuondoka kwa mama dunia hii n kama umebak mwenyewe .... hayupo ambaye atakuwa na moyo kama wa mama ,, tuwapende mama zetu ingali wakiwa hai na tuwaheshimu siku zote .... Mm kwang mung hata akininyima utajiri ni sawa imradi tu amenipa zawadi iliyo bora na wala haiishiwi thaman sku zote za maisha yang .... NAKUPENDA SANA MAMA DALO
Asante kwa kumthamini mama nimeona umuhimu wake baada ya kuondoka hapa duniani
 
Pole kwa msiba wa mama
Ni njia yetu sote muhimu kwako ni kumuombea huko aliko apumzike kwa amani
Ni vyema kumkumbuka na kuendelea kuyaenzi yale aliyokuusia
Pole sana na Mwenyezi Mungu aipumzishe roho yake mahali pema apumzike kwa amani.
Amen ndugu yangu,unaweza kusahau yote ila si mama hata kama ni kichaa akiondoka utaona umuhimu wake
 
Dah hizi thread zinaumiza sana sana. Usikie kama simulizi tu
 
Inasikitisha sana ...Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema mama yetu mpenzi,at least mkuu ulipata muda wakujiandaa psychological,I mean mlikuwa mnajua kwamba bimkubwa safari yake imeshakaribia tofauti na yule wa ghafla mnasikia hayupo,ila kifo kisikie kwa jirani...kuna wakati nafikia kukufuru Mungu kwa kujisemea kwamba bora nianze mimi kwanza ila sio mtu ninaempenda kama mama yangu,ila mwisho wa siku anaepanga ni Mungu sio sisi!pole sana kiongozi.
 
7 Reactions
Reply
Back
Top Bottom