Mtoto wa mwenye nyumba-01 (simulizi fupi ya kusisimua)

Mpauko

R.I.P
Jan 19, 2019
2,323
3,353
MTOTO WA MWENYE NYUMBA-01
(simulizi fupi ya kusisimua)
ROBIN MIHO
0776741545

Ilikuwa ni saa kumi jioni James alipowasili nyumbani,Vikindu sokoni wilaya ya Mkuranga akitokea katika kibarua cha ujenzi wa uzio wa shule ya sekondari maarufu katika viunga vya Vikindu na maeneo jirani Bright Angels Sekondari.


Hapo ndipo alipojipatia tonge kwa siku ya leo akifunga hesabu kwa kuingiza takribani shilingi elfu kumi na nne za kitanzania,ni mara chache sana kuingiza kiasi kikubwa kama alichoingiza leo.



Akiwa mwenye furaha sana huku akibebelea mfuko uliojaa unga,mchele na maharage alisalimiana na mama yake bi Magdalena na mdogo wake Joana aliyekuwa kidato cha pili.


Baada ya salamu na habari mbili tatu bi.Magdalena akapokea mfuko ule na mara moja kuanza kuandaa chakula maana hawakuwa wamefanikiwa kula chochote tangu walipokula mlo wa usiku jana yake.



Saa kumi na mbili iliwakuta wakipata mlo nje ya nyumba yao ndogo ya udongo iliyoezekwa bati ikiwa na vyumba viwili na sebule moja.


Ni nyumba aliyoijenga James mara tu baada ya kufukuzwa katika nyumba za shirika la nyumba la taifa kufuatia kifo cha baba yao aliyetegemewa kwa kila kitu na familia hii ya watu wanne,baba yao mzee Nguvumali Mtakuja,bi Magdalena ,James na Joana akiwa ndiye kitindamimba.



Mzee Nguvumali alikuwa ni mwajiriwa wa shirika la reli Tanzania,hadi mauti yanamkuta kwa ajali ya pikpiki alikuwa amebakiza miaka mitatu tu kabla ya kustaafu.


Akiwa kama mtegemezi pekee wa familia ile baada ya kifo chake hakuwa ameacha mali yoyote ya thamani zaidi ya kiwanja huko Vikindu mkoa wa pwani ambako James akishirikiana na mama na mdogo wake walifanikiwa kujenga nyumba wanayoishi sasa,wakati huu James alikuwa amehitimu diploma ya usimamisi wa biashara.



"Jmes mwanangu" bi Magdalena aliita muda mfupi baada ya kumaliza kula.


"Naam mama"


"Mjomba wako Baraka alikuja mchana"



"Enhe anasemaje mama,au ndo nishakosa tena" James aliuliza kwa pupa,kwani ni mwezi mmoja tangu atume maombi ya kazi shirika la simu,TTCL ambalo ndioko alikofanya kazi mjomba wake,Baraka Mtakuja.



Bi.Magdalena akatabasam na kuinuka huku akimtaka James kusubiri,akaingia ndani, hakukawia akatoka akiwa na bahasha aliyomkabidhi James na kumtaka asome.


James akiwa na kihoro akafungua bahasha harakaharaka ingawaje bi.Magdalena alimtaka afungue taratibu asije akaichana,baada ya kufanikiwa kuifungua akaisoma kwa dakika kadhaa kisha akamgeukia mama yake huku machozi yakimlengalenga,ilikuwa ni barua ya kuitwa kazini,TTCL mkoa wa Mtwara kama afisa masoko mwandamizi.



Ilikuwa ni kama sherehe,kila mtu alifurahi sana na kwa vile zilisalia siku mbili tu kabla ya safari kuelekea Mtwara,maandalizi yalianza usiku huohuo mama hakuacha kumuusia kuishi vizuri na watu,kujilinda na kujiheshimu,James alimuahidi kuzingatia yote aliyoniusia,mama alifurahi na kumuombea baraka zote.


Hatimaye jumamosi iliwadia,ikiwa ndiyo siku ya safari ya James kwenda kuyaanza maisha mapya,alijihimu asubuhi mapema saa kumi na mbili ilimkuta akiwa Mbagala rangi tatu akisubiria basi la Buti la zungu.


Muda wote alijawa na tabasamu huku akiwa na begi dogo la mgongoni likihifadhi nguo chache za kuanzia maisha,hakuwa na kitu kingine chochote,kwani Mjomba alimtafutia hifadhi kwa rafiki yake kwa kipindi chote hadi atakapoamua mwenyewe kuhama.


Saa mbili na robo basi liliwasili na abiria wote wakaingia akiwemo James,safari ikaanza kwa kuliacha jiji pendwa la Dar Es Salaam,muda wote James hakuwa akiamini kinachotokea hadi walipoliacha kabisa jiji hili na kupotelea mikoa ya mwambao wa Pwani.


James aliamini kuwa milango ilikuwa imefunguka na zile ndoto za kuishi maisha ya raha mustarehe zilikuwa zinaelekea kutimia,laiti angelijua yatakayomkuta!..basi angelishuka na kurudi tu Vikindu.




Je! James atakutana na nini? Tukutane sehemu ya pili.
 
Karibu sana,mwandishi pia si muumini wa riwaya za mapenzi,ingawaje mapenzi ni kionjo kidogo sana katika riwaya hii.
 
Hakikisha hii stori yako inaisha, maana kuna stori huwa zinaishia juu juu tu...
 
Back
Top Bottom