'Mtoto aliyenusurika mauaji Musoma asimulia alivyookoka

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
MTOTO wa miaka minne aliyenusurika katika mauaji ya watu 17 wa familia tatu za ukoo mmoja katika eneo la Buhare, nje ya Manispaa ya Musoma, mkoani Mare, ameeleza namna alivyojiokoa dhidi ya wauaji kwa kuingia uvunguni.

Kituo cha Redio Clouds jana kilirusha sauti ya mtoto huyo (jina lake limehifadhiwa) akijieleza kwamba alifanikiwa kuingia uvunguni mwa kitanda mara baada ya wahalifu hao kuanza kuwakata kwa mapanga ndugu zake.

Mtoto huyo ambaye kwa mujibu wa mwandishi wa kituo hicho alionekana kisaikolojia kuathirika kutokana na tukio hilo, alisikika akisema hakuweza kuwatambua wavamizi kutokana na jinsi walivyojifunika makoti meusi.

Akielezea walivyoonekana, mtoto huyo ambaye kwa mujibu wa mahojiano redioni alikuwa amefuatana na watu wazima, akiwamo kiongozi wa ukoo, alidai kuwa aliwaona watu wanne waliokuwa na makoti meusi na viatu alivyovitaja kwamba vinafanana na vya kuchezea mpira.

Alisema aliwasikia wakiwataka wanafamilia hao kutoa fedha na kuwaambia wasipotoa, watawaua.

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Enos Mfuru, wakati wa maziko ya miili ya watu waliouawa kwenye tukio hilo ambalo kati ya marehemu 17, kati yao, 11 ni watoto wenye umri wa kati ya miezi 11 na miaka 13 wakiwamo wazazi wake, aliahidi kwamba Serikali itamhudumia mtoto huyo.

Mfuru alisema mtoto huyo atasomeshwa na Serikali. Naye Mbunge wa Musoma Vijijini, Vedastus Mathayo (CCM), aliahidi kumsaidia.

Mfuru alisema Serikali itahakikisha inagharimia matibabu kwa majeruhi wa tukio hilo waliolazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Mara mjini Musoma. Maiti hao 17 walizikwa juzi katika tukio lililohudhuriwa na mamia ya watu.

Taarifa zinasema mauaji hayo yalifanyika kutokana na kinachosadikiwa kuwa ni kulipiza kisasi. Polisi katika taarifa yake ya juzi, ilisema watu watano walikuwa wamekamatwa wakihojiwa juu ya tukio hilo.

Miili 16 ilizikwa katika kijiji cha Mgaranjabo nje kidogo ya Musoma na aliyekuwa mwanafunzi wa sekondari ya Mkirira, Joseph Sofareti, alisafirishwa kwenda kijijini kwao Kome, Musoma Vijijini baada ya heshima za mwisho kutolewa.
 
Back
Top Bottom