Mtoko wa Idd... Hapatoshi! (hadithi)

Mwendabure

JF-Expert Member
Mar 10, 2011
2,138
1,040
Wadau Idd Mubbarak!
Baada ya Bosi wangu yule Mchina kushindwa kutulipa kamshahara ketu ile jana kwa sababu alizodai ziko nje ya uwezo wake. Leo hii majira ya saa 4:30 hivi asubuhi. Nilikuwa njiani kurudi nyumbani kutoka kwa rafiki yangu niliyempigia simu jana na kumuomba anikopeshe pesa kidogo ili niweze kuiwezesha familia leo kujisosomoa japo kwa pilau la Nguru. Kwa bahati nilimkuta na akanipatia kiasi cha Sh. 1,5000 si haba kwa huku uswahilini inatosha na nauli ya kesho kwenda kwa yule mchina itatosha.
Ghafla simu yangu ikanizindua kutoka kwenye lindi la mawazo ya kumuombea mema rafiki yangu kwa moyo wa kujali alionao na kumlaani Mchina yule kwa "kunitoa mswaki" ile jana. Aliyenipigia simu alikuwa mai waifu wangu na ktk mazungumzo yetu ya simu alinitaka nirudi nyumbani hima ili nijionee kilichojiri hapo. Nilishitushwa na maelezo yake ila ikanibidi nikaze mwendo kupandisha kimlima mbele yangu na kupita vichochoro kadhaa hatimaye nilifika nyumbani. Nilipofika nikapita himahima bila kujali hata akina mama wapangaji wenzangu waliokuwa wamekaa hapo kwenye varanda wakichambua viungo aina kwa aina vyote vikiashiria kuwa baada ya saa kadhaa nyumba itajazwa vicheko vya kufurahia mlo wa sikukuu ya Idd ambayo kama ilivyo desturi ktk sikukuu zingine hapakosekani aina adimu na pekee za chakula kuwahi kupikwa au kuandaliwa ktk siku za kawaida.
Chumbani nilimkuta mai waifu wangu ameka ktk stuli amejiinamia na mbele yake juu ya kitanda kuna fungu la nguo ambazo kwa haraka niliweza kubaini kuwa ndizo nguo nilizozinunua mwezi uliopita kwaajili ya sikukuu hii ya Idd. Nilipigwa na butwaa na kujawa na shauku ya kutaka kujuwa kulikoni. Mawazoni nilidhani maiwaifu wangu ameingiwa na tamaa baada ya kuona nguo za mpangaji mwenzetu ambazo zimezidi uzuri kwa mtindo au thamani yake. Lakini kwa busara nilijiridhisha kuwa maiwaifu wangu hajawahi kuonyesha tabia au silka japo hulka ya tamaa iso tija. Katu! Kama ni kinyume cha hapo nilidhamiria kumuadhibu maiwaifu wangu kwa kiasi niwezavyo.
Nilimfuata mai waifu wangu pale alipokaa nami bila kukawia nilimtaka anijuze kilichomsibu, akanitaka niangalie zile nguo kwa kusichambua moja badala ya nyingine. Nami nilifanya kama alivyoazimia, nilichokiona kilitosha kumpokonya uhai yeyote mwenye
maradhi ya shinikizo la damu. Nilihisi moyo umekosea mpangilio ktk udundaji mapigo yake, kwa bahati hali hii ilichukua wasaa wa sekunde kadha hali ingekuwa si hali kama ingalichukua dakika japo moja kwa uchache.
Dera la maiwaifu wangu lilikuwa limeliwa na Panya pamoja na nguo za watoto wetu wawili zote zimetobolewa matobo yaliyofanya ziöekane kama vile ni nguo zilizochakaa na kwa hali hiyo zilikuwa hazifai tena kuvaliwa na mtu timamu wa akili labda awe hamnazo. Nilijongea kunako kabati letu pekee ambalo tulilichongesha kwa fundi miaka takriban sita tulipokuwa tumepanga kule Kinondoni Misufini kabla hatujahamia huku Mbagala Kibondemaji na linatufaa kwa kuhifadhia vyombo na baadhì ya nguo kwa pamoja kwani huku kwetu nguo nyingi huishia kwenye kamba au msumari ukutani na hazionji kabati mpaka kuishia kuchakaa kusikofaa. Japo ukiniuliza kipimo na aina ya mbao ilotumika kutengeneza kabati mimi sijui na vinginevyo nitakuhesabu una madharau dhidi yangu.
Panya kaleta maafa ndani ya nyumba tena katikati ya sikukuu. Dera jipya na la kisasa kwaajili ya maiwaifu wangu limekuwa tambara tena la deki! Gauni na taiti la bint yangu wa miaka mitano pamoja na Sarawili na Shati vya mwanangu wa kiume mwenye miaka tisa vimetobolewa sehemu tofauti kiasi hazivaliki na hazifai. Kilichobaki salama ni viatu tu katika mavazi ambayo nilihangaika kuhakikisha watoto na mai waifu wanafurahia siku hii kama wengine jamani! Mkosi gani huu!
Wazo likanijia nifanye ukaguzi wa dharura kujua kama panya amewezaje kuingia kabatini mle? Nilianza kwa kuondoa beseni na makorokoro mengine yalirundikana juu ya kabati, ghafla panya mkubwa alitoka ndani ya kabati na kupita kwa kasi ya mshale upande ule aliokuwa ameketi maiwaifu wangu kitendo kilimchofanya mke wangu ainuke na kurukia kitandani zilipo zile nguo muflisi huku akipiga ukelele ulioashiria woga wa kike, tulijikuta tukiangua kicheko bila kutaraji... Panya amefanikiwa kutuharibia na kisha kutufanya tucheke japo kwa muda mfupi huu kusahau maafa yalotufika.
Wakati huo tukiwa tunamalizia kicheko nilisikia sauti ambazo si za kawaida kutokea mle kabatini. Nilimuashiria maiwaifu wangu kwa kuweka kidole changu cha shahada kukatiza midomo yangu chinijuu naye alitulia ghafla kuashiria kuwa ameelewa ile ishara yangu. Nilizidi kutega sikio karibu kabisa na kabati ndipo nilipojikuta niking'aka "mna watoto wa panya humu, huyu panya kazalia humu" ina maana huyu mshenzi alikatakata nguo zetu ili kuwatengenezea wanawe godoro!? Alihoji maiwaifu wangu huku tayari ameshika mwamvuli mkuukuu uliokuwa umekunjwa na kuwekwa ktk kona moja ya chumba. Nilimsihi awe mpole na mwangalifu kuepuka uharibifu wa vifaa vingine ikiwemo na huo mwamvuli ambao ameushika akiashiria kuanza kumsaka Mama Panya na akimkuta amtandike nao!
"subiri tuviondoe hivi vitoto vyake kwanza mama yao atahama mwenyewe baada ya kuwakosa mafichoni" nilimuasa maiwaifu wangu na alinielewa kwa mara nyingine tena. Mara sauti ya kilio ya binti yetu inatuzindua kutoka ktk sakata hili na maiwaifu wangu anaelekea nje kujua kulikoni hicho kilio cha mtoto, ila mimi kama baba nilijuwa ni mbinu ya maiwaifu kumuwahi binti yetu asiingie ndani na kukuta yale maafa! Hapa ndipo ifa ya kuwa mzazi inapochukuwa nafasi yake kwa hakika na sifa hiyo anayo maiwaifu wangu.
"baba Naniliu kuna wageni huku nje" ni sauti ya maiwaifu akinijulisha ujio wa ugeni. Nilitupa jicho kwenye saa iliyotundikwa ukutani haikunichukua muda kubaini kuwa tayari ni saa 6:10 mchana na hali bado haijapata uelekeo wa mambo. Hakujapikwa hakujaliwa na muda unayoyoma kwenda machweo...!

ITAENDELEA KESHO.. sehemu ya pili na mwisho..
 
Labda mama panya katafuna makaratasi yalio andikiwa hii simulizi.
 
Jina lako jingine ni Chesi Mpilipili? Kwa wanaomjua mtu huyu alikuwa maarufu kwa hadithi za aina hii enzi zile za magazeti manne tu ya kiswahili Tanzania nzima-UHURU,MZALENDO,MFANYAKAZI NA KIONGOZI!
 
Back
Top Bottom