Waziri wa mambo ya nje wa China Bw. Wang Yi amekanusha tena “dai la mtego wa madeni” kuhusu ushirikiano kati ya China na Afrika alipokuwa ziarani nchini Kenya hivi majuzi. Alisisitiza kuwa China kamwe haijawahi kuzilazimishi nchi nyingine kufanya shughuli zisizotaka, na dai hilo ni kama “mtego wa maneno” uliotengenezwa na watu wasiotaka kuona Afrika inapata maendeleo.
Kwa muda mrefu, baadhi ya wanasiasa wa nchi za magharibi na taasisi za utafiti zenye upendeleo zinadai kuwa China inaziwekea nchi za Afrika “mtego” kwa kuzipatia mikopo, na wakati nchi hizo zitakaposhindwa kulipa madeni, China itanyang’anya mali za umma za nchi hizo kama vile uwanja wa ndege na bandari. Ni wazi kuwa dai hilo halina msingi. China haijawahi kumiliki mradi au mali yoyote ya nchi za Afrika ziliposhindwa kulipa madeni, lakini siku zote inaunga mkono na itaendelea kusaidia nchi za Afrika kuinua uwezo wao wa kujiendeleza.
Akitolea mfano wa Kenya, Bw. Wang Yi amesema miradi ya ushirikiano kati ya nchi mbili yote imepitia tafiti kabambe za kisayansi, na imenufaisha maisha ya watu wa Kenya na kuchangia nguvu ya maendeleo ya Kenya. Aidha, asilimia 80 ya madeni ya Kenya yalitolewa na mashirika ya kifedha ya pande nyingi, na sehemu kubwa ya madeni yaliyodaiwa na China ni mikopo nafuu.
Hali halisi ni kuwa uwekezaji wa China umekuwa chanzo muhimu cha fedha kwa nchi za Afrika, na kuzisaidia kutimiza malengo ya maendeleo ya kiuchumi. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, sekta ya miundombinu barani Afrika inahitaji dola za kimarekani bilioni 130-170 kila mwaka, na uwekezaji wa China umechangia sehemu yao. Hadi mwishoni mwa mwaka 2020, kulikuwa na kampuni zaidi ya 3500 za China barani Afrika, na uwekezaji wa moja kwa moja ulifikia dola za kimarekani bilioni 43 na kusaidia nchi za Afrika kujenga viwanda, kutengeneza ajira na kuboresha maisha ya watu.
Kutokana na janga la COVID-19, baadhi ya nchi zimekumbwa na taabu ya muda. China imejitahidi kutekeleza pendekezo la kundi la G20 la kuahirisha ulipaji wa madeni kwa nchi maskini zaidi duniani, na miongoni mwa nchi za kundi hilo, China imekubali kuahirishwa madeni kwa wingi zaidi, na kusaini makubaliano na nchi 19 za Afrika kuhusu kuahirishwa ulipaji madeni. Vilevile, China imesamehe mikopo isiyo na riba ya nchi 15 za Afrika iliyopangwa kulipwa hadi mwishoni mwa mwaka 2020. Kwenye mkutano wa 8 wa mawaziri wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika uliofanyika mwezi Novemba mwaka jana, rais Xi Jinping wa China alitangaza kuwa China pia itasamehe mikopo isiyo na riba iliyopangwa kulipwa hadi mwishoni mwa mwaka 2021 kwa nchi maskini zaidi za Afrika.
Ukweli una nguvu kuliko maneno. Marekani na nchi za magharibi zimepigia kelele "dai la mtego wa madeni" na kutengeneza simulizi ya "umiliki wa miundombinu", ikionyesha lengo lao la kuzilazimisha kuchagua upande kati ya China na Marekani bila kujali maendeleo ya nchi za Afrika. Akizungumzia hilo, Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria hivi karibuni alisema Nigeria inatafuta mkopo kulingana na mahitaji yake tu, na kama hakuna reli kati ya Lagos na Ibadan iliyojengwa na China, watu waishio miji hiyo miwili wangekuwa wanatembeleana kwa miguu tu . Kadhalika, wakati alipohojiwa na televisheni ya CNN akizungumzia mikopo ya China na "mzozo wa madeni" wa Kenya, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alisema nchi yake ina mpango mzuri wa madeni, na mbali na China, Kenya pia imepata mikopo kutoka Japan, Marekani na mataifa mengine mengi ili kuisaidia kufikia malengo yake ya maendeleo. Naye rais wa Rwanda Paul Kagame pia alisema Afrika inakabiliwa na pengo kubwa la fedha na inahitaji haraka fedha za kigeni, lakini kinachoshangaza ni kuwa, walioikosoa China zaidi ni wale "wanaosaidia kidogo sana"Afrika.
Kama alivyosema waziri Wang Yi, kwamba kama kweli kuna "mtego" wowote unaoikabili Afrika, basi ni "mtego wa umaskini" na "mtego wa kurudi nyuma". Ili kutatua matatizo yanayoikabili Afrika, maendeleo ni jambo la msingi. China ikiwa ni rafiki mwaminifu na mshirika wa dhati wa Afrika na watu wa Afrika, inafanya kila juhudi kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi barani Afrika kupitia mipango kama vile utaratibu wa "Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika" na "Ukanda Mmoja na Njia Moja", na kuzisaidia nchi za Afrika kutatua matatizo yao ya madeni.