Mshtakiwa Kesi ya Utoroshaji wanyama atoweka kama Sailesh Vithlani

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Mwandishi Wetu
7 Sep 2011
Toleo na 202

felisha.jpg

  • Aliomba akale Idd Dar, ‘akachupa'
  • Wakubwa wahofu kuzungumza

MTUHUMIWA wa kwanza katika kesi ya utoroshaji nje ya nchi wanyama pori hai 136 wa aina 14 tofauti, wakiwemo twiga wanne, Kamran Ahmed (29), aliyekuwa nje kwa dhamana, ametoweka nchini na inasadikiwa amekwenda kwao Pakistan, Raia Mwema limefahamishwa.

Habari zinasema kuna mazingira tata ya kutoweka kwa mtuhumiwa huyo ambaye alikuwa nje kwa dhamana yenye masharti ya kutosafiri nje ya mikoa ya Kilimanjaro ilikofunguliwa kesi dhidi yake na watuhumiwa wengine, na Mkoa wa Arusha alikokuwa akiishi.

Taarifa zinasema, Kamran anaweza kuwa aliondoka nchini Agosti 31 kwa ndege ya Shirika la Emirates; huku akiacha nyuma maswali mengi yasiyokuwa na majibu kuhusu hatma ya kesi iliyokuwa ikiwakabili yeye na washirika wake watano.

Mtuhumiwa huyo alifikishwa kwa mara ya kwanza katika Makahama ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Kobelo, Juni 11 mwaka huu, kwa tuhuma za kusafirisha na kutorosha nje ya nchi wanyamapori hai 136 wa aina 14 tofauti wenye thmani ya Shilingi 170,572,000.

Kamran na wenzake walifikishwa mahakamani baada ya kusuasua kwa upelelezi kuhusu kesi hiyo hadi taarifa za hujuma hiyo zilipofichuliwa kwa mara ya kwanza na Raia Mwema katika moja ya matoleo yake ya mwezi Mei kuhusu kutoroshwa nje ya nchi kwa wanyamapori hao.

Baada ya kufunguliwa kesi, Kamran alisomewa mashitaka sita tofauti yakiwamo ya uhujumu uchumi kwa kusafirisha na kuuza nje nchi wanyamapori hao ambao ni nyara za Serikali.

Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Jane Mbogo (33) ambaye ni raia wa Kenya, Hawa Hassan Mangunyuka (51), Mkurugenzi wa kampuni ya HAM Marketing ya Jijini Dar es Salaam, Afisa Mifugo katika uwanja wa ndege wa KIA, Martin Kimati (58), Veronica Benno (51) na Locken Kimaro (50) ambao wote ni maafisa usalama wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

Mtuhumiwa huyo, hata hivyo, aliachiwa kwa dhamana na Mahakama Kuu, Kanda Moshi, kwa masharti ya kusalimisha hati yake ya kusafiria na pia asitoke nje ya Mikoa ya Arusha na Kilimanjaro hiyo ikitokana na hatua ya Mahakama ya Hakimu Mfawidhi, Mkoa wa Kilimanjaro, kukataa kutoa dhamana kwa maelezo kuwa kesi za uhujumu uchumi hazina dhamana kisheria. Kamran alikuwa anatetewa na wakili wa kujitegemea wa mjini Arusha, Medium Mwale.

Mwale mwenyewe alifikishwa mahakamani mwanzoni mwa Agosti akituhumiwa kwa usafirishaji fedha haramu akiwa amekamatwa na kiasi cha shilingi bilioni 18 katika akaunti yake ambazo alishindwa kuzitolea maelezo. Mwale bado anashikiliwa katika Gereza la Kisongo, nje kidogo ya mji wa Arusha, akisubiri hatma ya kesi yake.

Taarifa zilizolifikia Raia Mwema, mwishoni mwa wiki, zilieleza kuwa Kamran aliondoka nchini Agosti 31 kwa ndege ya Shirika la Emirates na kurudi kwao Pakistan akipitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu J.K Nyerere, Dar es Salaam akiambatana na kaka yake na mshirika wake wa biashara, Norman Ahmed, ama maarufu kama Nommy.

Habari zaidi zinaeleza kuwa, wawili hao walitua Karachi, mji mkuu wa Pakistan, Septemba Mosi mchana, na taarifa kutoka kwa watu wao wa karibu zinadai kuwa hawatarajiwi kurejea nchini katika kipindi hiki ambacho kesi inayomkabili Kamran itatajwa tena Jumatatu (Septemba 12, 2011).

Taarifa za kuondoka nchini kwa mtuhumiwa huyo hadi sasa zinatatanisha kwani habari zisizothibitishwa zinaeleza ya kuwa aliondoka baada ya kupewa ruhusa na ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kilimanjaro ama ruhusa maalumu ya mahakama baada ya hati yake ya kusafiria kushilikiliwa na kwamba ruhusa hiyo ilikuwa ni kwenda Dar es Salaam kusherehekea Sikukuu ya Idd El Fitr.

Taarifa zinadai kuwa, mara ya mwisho mtuhumiwa Kamran na ndugu yake walionekana katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kilimanjaro (RCO) Obadia Jonas Nselu, kati ya Agosti 25 na 26, na inadaiwa kuwa baada ya majadiliano marefu waliweza kuwashawishi kurudishwa kwa hati ya kusafiria.

"Kuna uwezekano kuwa waliofanikisha mpango wa mtuhumiwa huyo kurudishiwa hati yake ya kusafiria walikuwa wamepewa malipo "rushwa" maana haiwezekani kama mtuhumiwa alikuwa anasafiri kwenda jijini Dar es Salaam kwa ajili ya sikukuu ya Idd basi apewe hati hiyo….hati za kusafiria ni kwa safari za nje ya nchi tu," alieleza mtoa taarifa wetu.

Habari zaidi kutoka kwa watu walio karibu na mtuhumiwa huyo zinadai kuwa Kamran alifikia uamuzi wa kuondoka nchini baada ya kuona kuwa mwelekeo wa kesi ni mbaya kwake; hasa baada ya taarifa kwamba Serikali ilikuwa imeunda timu mpya ya wapelelezi kukusanya ushahidi zaidi wa kesi hiyo.

Raia Mwema
imefahamishwaya kuwa timu hiyo ilifanya kazi kwa umakini na kufichua mtandao uliokuwa ukifanya biashara hiyo haramu kwa muda mrefu, ukiwahusisha baadhi ya maafisa wa juu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na ushahidi huo ulikuwa msingi mkuu wa kesi iliyokuwa inamkabili mtuhumiwa huyo.

Aidha taarifa zaidi zinaeleza kuwa mtuhumiwa huyo pia alikuwa ametishwa sana na ‘moto' uliowaka Bungeni wakati wa mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa wabunge wote waliotoa michango yao kumbana Waziri wa Wizara hiyo, Ezekiel Maige, kutoa majibu kuhusu wanyama hao waliotoroshwa nje ya nchi.

Wabunge pia walifikia uamuzi wa kutaka iundwe kamati maalumu ya kufuatilia wanyama hao ambao wanadaiwa kutoroshwa kwenda Doha nchini Qatar kwa kutumia ndege ya jeshi la anga la nchi hiyo.

Katika kujibu hoja za wabunge Waziri Maige aliwaeleza kuwa pamoja na kuwafungulia watuhumiwa wote kesi ya uhujumu uchumi Serikali pia ilimsimamisha kazi Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Obeid Mbangwa na watumishi wengine wawili, kupisha uchunguzi unaofanyika.

"Ni mlolongo wa matukio hayo makubwa yaliyotokea ndani ya mwezi Agosti ndiyo yanayotajwa kuwa yalimtisha sana Kamran kiasi akahisi ya kuwa kesi iliyokuwa inamkabili ni ngumu, hali iliyomfanya afikie uamuzi wa kuondoka nchini lakini kwa kutumia ushawishi wa kurudishiwa hati yake ya kusafiria,"anaeleza mtoa habari wetu.

Anaongeza mtoa habari wetu: " Kuna uwezekano pia mpango wa kuondoka kwa Kamran uliratibiwa na baadhi ya maafisa wa juu wa Wizara ya Maliasili na Utalii ambao tuhuma za usafirishaji wanyama zimewagusa, lengo likiwa ni kuvuruga kesi iliyoko mahakamani kwa kuwa upande wa mashitaka utakuwa umeyumbishwa na kuondoka kwa mtuhumiwa namba moja."

Akizungumzia yaliyojitokeza katika sakata hilo, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Yusuf Ilembo alieleza kuwa hana taarifa za kuondoka nchini kwa mtuhumiwa huyo wala hawajawahi kutoa ruhusa kwake ya kuondoka kwenda popote.

"Unajua suala hilo lilikuwa chini ya Kamanda wa Polisi (Absolom Mwakyoma), lakini sina taarifa zozote za suala hilo. Ndiyo kwanza nasikia kutoka kwako,"alisema Kaimu Kamanda huyo.

Mara ya mwisho, Raia Mwema ilipowasiliana na Kamanda wa Upelelezi, Obadia Jonas Nselu, mwanzoni mwa wiki hii, hakuwa tayari kulizungumza akisema, hata hivyo, ya kuwa alikuwa kwenye kikao.

Hali ilikuwa ni hiyohiyo kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Eliezer Feleshi ambaye alieleza ya kuwa hafahamu habari za kuondoka kwa mtuhumiwa huyo na kumwomba mwandishi ampigie baadaye.

Hatua ya kuondoka kwa mtuhumiwa huyo kwa vyovyote vile itawasha upya moto mkali kuhusu sakata la kutoroshwa kwa wanyama hao hai nje ya nchi, na itakuwa pigo kubwa kwa upande wa Serikali na waendesha mashitaka wake.

 
As Usual... Our Dear Country kwanini then tusitumie InterPol?

Well, One day we will get our country back... & U know Death Penalty is part of the Punishment.
 
nazidi kuichukia serikali ya goigoi jk. Hii ni dharau sasa, kwanini wasimwamuru akamatwe hata huko kwao, kama hawawezi tufunge ubalozi wao nchini.
 
Haya yote yanafanywa na sisi Watanzania! au viongozi tulikodi Rwanda na Burundi! kama tulikodi kwanini tusiwaaambie waturudishie nchni yetu mikononi mwetu wao waondoke warudi kwao.
 
nazidi kuichukia serikali ya goigoi jk. Hii ni dharau sasa, kwanini wasimwamuru akamatwe hata huko kwao, kama hawawezi tufunge ubalozi wao nchini.

Waziri wa Mambo ya nje alipaswa kujibu maswali mengi sana toka zamani ila kaa kimia anaangaika na bendera ta NTC! Wanyama wa Tanzania hana muda nao wala haimuhusu.
 
Hivi ile rada tuliyoinunua kwa bei ya vijisenti inafanya kazi gani mpaka ndege ya kijeshi kutoka Qatar inatua nchini tena sio porini bali ni uwanja wa kimataifa na kupakia wanyama. Hii chain ya kupewa kibali cha kutua chini aviation wanatakiwa kujibu hapa mana ndege hairuki wala kutua bila kupata landing permit au flyover permit kutoka aviation sasa kama ni kubreak the ice uchunguzi uanzie aviation, then immigration then ndo mahakama na kuendelea.
 
Tunatarajia habari hii ni sahihi kama ilivyoletwa na si hisia na tutakwenda nayo hadi itakakpokanushwa na wahusika.

Nina shangazwa na mambo kadhaa yanayonifanya nijiulize hivi kwanini tunaendelea kuandaa sherehe za uhuru? Uhuru upi kama ni nchi ya watu tunaoishi kama wanyama wa serengeti. Wanyama wa serengeti kwa sababu wao kila mmoja ana lake na linapotokea la kutokea ni majaaliwa hakuna kuwajibika ua kuwajibishana.

Habari kama hizi zinakuwa ni siri kubwa na serikali inayojali watu wake isingengoja hadi wakati huu bila taifa kujua.
Najaribu kufikiri harakati zilizokuwepo wakati Mh Mbowe anakamatwa na kupelekwa Arusha. Ulinzi uliokuwepo na heke heka za serikali ungedhani ni mhalifu wa kimataifa. Wahalifu wa kimataifa hawatendewi kama Mbowe tunangoja tu kusikia katika magazeti na majiradi kama si blogs.
Hiyo ndiyo miaka 50 ya uhuru.

Kwa upande mwingine sishangai kwasababu si Shailesh Vithlani bado anatafutwa na serikali na haijui alipo hata kama anapishana na misafara ya viongozi huko majuu wakati wakienda shopping au matibabu ya mafua.
Sasa lipi geni kwa huyu mpakistani aliyekuja na dege la kijeshi kutoroka?

Kisichoelezwa na serikali ni swali lile rahisi, je ndege ya kijeshi iliingia vipi nchini bila kufuata itifaki? Na hapa tena najiuliza kipi cha kushangaza, mtuhumiwa aliyekuja na dege na kutoroka, au ndege ya kijeshi kuingia anga zetu bila taarifa!!

Hati ya kusafiria iliyokuwa mikononi mwa vyombo vya sheria imetowekaje na katika mazingira gani.
Mtuhumiwa si alikuwa na wadhamini, je wadhamini wake wanasemaje na wamechukuliwa hatua gani.
Hivi sikukuu ya Idd kwa mtuhumiwa muhimu kama huyu ni bora kuliko uwepo wake anapohitajika kwepo!!

Kwangu mimi huyu mtuhumiwa ni muhimu katika kuvuruga ushahidi.

Yaweza kuwa ushahidi unawagusa hawa:
1.Katibu mkuu wa wizara husika kama mtendaji wa kila siku na mfanyakazi wa umma
2.JWT ambalo linaweza kutueleza ndege ya kijeshi ilitua nchini mwetu kwa kufuata taratibu gani na idhini ya nani kuchukua wanyama.
3.Mkuu wa idara ya wanyamapori ya mkoa. Atueleze alikuwa na taarifa zipi na alifanya nini au hakujua nini
4.Mkuu wa usalama wa mkoa wa Arusha kwa ujumla wa usalama wa sehemu yake katika mambo ya ulinzi hasa ujio wa dege na utoroshaji wa wanayama na mengineyo
5.Mkuu wa usalama wa kiwanja cha KIA
6.Mkuu wa polisi wa KIA
7.Afisa mifugo wa mkoa wa Arusha
8. Mkuu wa hifadhi walipochukuliwa wanyama hao
9. Afisa mifugo KIA
10. Wengineo waliokuwa zamu siku hiyo KIA katika maeneo wanyama hao walikopitia

Baada ya hapo tutamuuliza waziri wa maliasili ameshughulikiaje suala la ndege ya kijeshi kutua nchini bila taarifa akishirikiana na mwenzake upande wa jeshi la ulinzi (JWTZ)

Kama hao hapo juu hawatabanwa na sheria, basi kama habari inavyosema ushahidi utakuwa umevurugwa kulinda mambo makubwa zaidi tusiyotakiwa kuyajua.
 
Nguruvi3,
Nakubaliana na wewe. Huyu jamaa ameachwa atoroke kwa sababu kesi yake ingegusa wengi. Hapa Marekani alipokuwa na kesi yule mkuu wa IMF pasipoti yake ilichukuliwa na hakurudishiwa mpaka kesi iliposimamishwa. Wakuu wa mashtaka walijua kuwa huyu ni raia wa Pakistan. Kwanza asingestahili kupewa dhamana na pili angewekwa mahali ambapo angekuwa chini ya ulinzi 24/7
 
Hii ndiyo TZ yazaidi uijuavyo jameni,Inakera sana,Kwanza huyo Mpakistani ana Kibali fake chakuishi Nchini yeye na wafanyakazi wake wote wa Kipakistani hapa Arusha vimeotu,Uhamiaji nao wanahusika hapa
 
Kichefuchefu. Kama ni kweli watu wanaohusika si watuachie ofisi zetu kwa nia njema tu?
 
HII ndo tz,HIyo kesi imekwisha,waliobakia wataambiwa na mahakama
hakuna kesi ya kujibu sababu mshtakiwa mkuu hayupo.
Na mafisadi majina yao hatuta yapata maana wamemtorosha mshtakiwa
kwa makusudi.
 
Nasubiri kuuangalia umakini wa IGP Said Ally Mwema, no doubt rco kapiga hela na kurudisha hati hizo za kusafiri kwa mtu anayeenda "Dar es Salaam". ina maana hata huyu rco hayuko concerned kwa ufisadi dhidi ya nchi yetu ulioratibiwa na huyu mtuhumiwa?
 
Naomba nitukane kidogo jamani, machozi yananitoka, kweli kuna serikali au ni uhuni, ujinga, ushenzi na ulimbukeni? kwanini nisitoe machozi kwa ajili ya nchi yangu na ikibidi na damu initoke pia? kosa ni kuzaliwa Tanzania? liko wapi jeshi? iko wapi intelijensia ya Taifa? au walijua wakakaa kimya kwa maslahi ya watu fulani? Ni magari gani yaliwaleta wanyama hawa hadi airport? Nani kaiweka nchi yetu rehani? Kuna sababu gani ya kuendelea kuishi katika ushenzi kama huu? Mungu Ibariki Tanzania tuuone ukweli zaid
 
Sheria inasemaje kupewa Mgeni dhamana? watanzania wapo jela wanasota hata dhamana hawapewi lakini mgeni inakuwa haraka sana kupewa Dhamana kuliko mzawa. Nchi hii kuna Viongozi wasiofuata maadili. Inaumaa
 
Hii ni Dharau kubwa sana kwa JK na kundi lake,kuna usalama wa Taifa cjui nao wanafanya nini. Mi ctaki tena makazi ya hapa Tz na mwenye uwelewa ya uhamiaji anijuze kwn nataka nihamie SOUTH SUDAN,nimechafukwa na roho kwa hali iliyopo ndani ya Taifa langu la Tanzania. Mwenye mwongozo anikute PM.
 
Waandishi wa habari sasa ndio wanausalama wetu ndio wapelelezi wetu ndio walinzi na tegemeo letu la mwisho.
Tumekata tamaa na vyombo vyetu vyote vya ulinzi na usalama wetu.Hatuko salama tena.
Sitashangaa kusikia watanzania wanaolalamikia huu upuuzi wakikamatwa,kutishwa,kuteswa,kufungwa au hata kuuwawa.
 
Naomba nitukane kidogo jamani, machozi yananitoka, kweli kuna serikali au ni uhuni, ujinga, ushenzi na ulimbukeni? kwanini nisitoe machozi kwa ajili ya nchi yangu na ikibidi na damu initoke pia? kosa ni kuzaliwa Tanzania? liko wapi jeshi? iko wapi intelijensia ya Taifa? au walijua wakakaa kimya kwa maslahi ya watu fulani? Ni magari gani yaliwaleta wanyama hawa hadi airport? Nani kaiweka nchi yetu rehani? Kuna sababu gani ya kuendelea kuishi katika ushenzi kama huu? Mungu Ibariki Tanzania tuuone ukweli zaid

intelijinsia? kwani kazi yake ni kushughulikia mambo kama haya?, intelijensia si inahusika na kuangalia kama maandamano ya CDM kutatokea vurugu? AU?
 
sasa kama wanyama wanatoroshwa itakuwa mtu?..kwani mtu mmoja au wanyama 20 ni kipi rahisi kutoroshwa? siku moja niliwahi kusikia mtu anasema hakuna serekali hapa bali kuna genge la wahuni ndio linaongoza hii nchi
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom