BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
KONA YA MLALAHOI: Mshahara kima cha chini wizi mtupu
Na Adam Mwakibinga
Mwananchi
Mwananchi
CHANGALAMACHO ni mlalahoi anayefanya kazi moja muhimu sana na yenye kuhitaji uvumilivu wa hali ya juu, kwa kifupi ili uweze kufanya kazi anayofanya Changalamacho unatakiwa uwe na moyo kwelikweli kutokana na mazingira ya kazi yenyewe (UALIMU).
Wako wanaoiita kazi hiyo ni kazi ya wito nami nakubaliana nao kwa asilimia zote kwamba ni sahihi kuiita kazi ya wito kwani bila kuwa na wito hutofanya kazi hiyo.
Mshahara anaopata Changalamacho anasema ni ule wa kima cha chini yeye mwenyewe amediriki kuutaja waziwazi bila kificho ili walalahoi wenzake tumuhurumie na hana kitega uchumi chochote anachokitegemea kumuongezea kipato zaidi ya huo mshahara anaopata.
Anasema mshahara anaopata ni shilingi laki moja na elfu thelathini na tano (135,000), lakini mpaka kuupata lazima mbinde ipite, amekuwa akijaribu kujibana lakini wapi bado ngoma nzito kwake.
Anajuta kuifahamu kazi ya ualimu, pamoja na kwamba ndio mtambo wa kutengeneza kila mtaalamu duniani kote, hilo halina ubishi.
Changalamacho ana watoto watatu wanaomtegemea mbali na watoto hao pia ana mke ambaye hana uwezo wa kufanya kazi kwa hiyo naye ni tegemezi wake, vilevile anakaa na mama yake mzazi ambaye umri wake afaa kuitwa ajuza.
Ni mkazi wa mjini tena jijini na si kijijini hivyo amepanga vyumba viwili kimoja analala yeye na mkewe na kingine wanalala watoto wake watatu wote wa kike pamoja na bibi yao.
Mlalahoi Changalamacho anasema kila akijitahidi kupanga bajeti ya nyumbani kwake hupata ugonjwa wa moyo kwani haipangiki na inamuumiza kichwa kutokana na ukweli kwamba mshahara anaoupata haukidhi haja ya familia yake.
Upangaji bajeti yake kwa mwezi ni kama ifuatavyo: kodi ya vyumba viwili alivyopanga ni shilingi 30,000 kila chumba ni shilingi 15,000 kwa mwezi nyumba aliyopanga iko nje kidogo ya jiji, mchele kilo 10 ni shilingi 12,000 kilo moja ni shilingi 1,200, sembe kilo 10 ni shilingi 7,000 kilo moja ni shilingi 700, mkaa gunia moja shilingi 18,000, sukari kilo tano shilingi 6,000 kilo moja ni shilingi 1,200.
Maharage kilo tano shilingi 6,000 kila kilo moja ni shilingi 1,200, mafuta ya kula galoni moja shilingi 3,000, chumvi paketi 2 shilingi 400, viberiti vya shilingi 480, sabuni ya kufulia(unga) nusu kilo shilingi 1,200, mche mmoja wa sabuni ya kusugua(hutumia kwa kuogea na kuoshea vyombo) shilingi 1,200, mafuta ya kupaka kopo moja shilingi 1,000. Kuchangia ankara ya nishati ya umeme wa Luku ni shilingi 10,000 kwa mwezi.
Dawa ya meno gramu 80 shilingi 650, nauli kwa ajili ya usafiri wa daladala shilingi 14,000 kwa siku ni shilingi 700, shilingi 350 kwenda kazini na shilingi 350 kurudi nyumbani hii ni kwa Changalamacho peke yake na ile ya watoto wake watatu ni shilingi 12,000 kwa mwezi yaani kila siku mtoto mmoja huondoka na shilingi 200 shilingi mia moja kwenda na mia moja nyingine kurudi, kwa maana hiyo watoto hawa huwa hawali mchana mpaka watakaporudi nyumbani halikadhalika Changalamacho mwenyewe.
Mpaka hapo mlalahoi Changalamacho amebakiwa na shilingi 6,270 kwa ajili ya kununulia dagaa, nyanya, vitunguu na mchicha japo kwa wiki mara moja, bado hajaweka karo za watoto, mavazi na akiba ya pesa kwa ajili ya matibabu na dharura nyingine, hata hivyo anasema kiasi cha vyakula pia amevibana hulazimika wakati mwingine kukopa madukani vinapokwisha kabla ya mwezi kumalizika.
Changalamacho anamuomba mbunge wake ambaye yeye hupata kiasi kama hicho cha mshahara wa kima cha chini (135,000) kwa ajili ya posho ya siku moja tu akiwa bungeni amsaidie kupanga bajeti angalau isaidie kumaliza mwezi.Afanaleki eti binadamu wote ni sawa! Amani juu yenu. Kwa maoni mawasiliano ni 0756 202532.