Mrema asema miaka 15 ya mfumo wa vyama vya vingi imekuza demokrasia

Mtu wa Pwani

JF-Expert Member
Dec 26, 2006
4,184
671
Mrema asema miaka 15 ya mfumo wa vyama vya vingi imekuza demokrasia
Ikunda Erick
HabariLeo; Tuesday,October 09, 2007 @00:06


Mrema akihutubia katika mkutano.
TANGU nchi ipate Uhuru wake mwaka 1961, mambo mengi yamebadilika na kuiwezesha kujitawala yenyewe kwa kufuata sheria na Katiba kutekeleza mipango yake ya maendeleo.



Wakati nchi inapata Uhuru, demokrasia kwa wananchi, ilikuwa bado changa. Kwa mfano, wakati huo wananchi hawakuwa na uhuru wa kutoa maoni na wala uhuru wa kuhoji mambo mbalimbali ya serikali ya kisiasa, kijamii na kiuchumi.



Hali hiyo iliwafanya watu wengi kuwa waoga. Walihofia kutoa kasoro au hoja tofauti na mawazo ya baadhi viongozi wa chama tawala, wakiamini kufanya hivyo ulikuwa ni usaliti.



Lakini, baada ya wananchi kupevuka akili na kuelewa mambo ya siasa, wachache walianza kuunda hoja, ambazo kwa njia moja au nyingine ziliwagusa viongozi au mfumo wa utawala.



Hali hiyo, ilifanya viongozi kuona kuwa ipo haja ya kuwa na vyama vingi vya siasa ili kuleta changamoto za kuwa na maendeleo zaidi.



Hali hiyo ndiyo iliyosababisha Serikali kupitisha Sheria ya Vyama Vingi mwaka 1992. Hivi leo vyama hivyo, vinatoa changamoto kubwa kwa wananchi na viongozi wa serikali, kwa kutoa mawazo yao na fikra zao kwa uhuru.



Augustine Mrema ni mmoja wa viongozi wakuu wa vyama vya upinzani. Kwa sasa yeye ni Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour Party (TLP). Kabla ya kujiunga na TLP, alikuwa Mwenyekiti wa chama kingine cha upinzani cha NCRR-Mageuzi.



Kabla ya kwenda NCCR alikuwa CCM, ambako aliwahi kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Ndani. Aliwahi pia kuwa Waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana. Pia, Mrema aliwahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini kwa tiketi ta CCM kwa miaka kumi. Aliwahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Temeke kwa tiketi ya NCCR.



Katika uchaguzi mkuu wa kwanza vyama vingi mwaka 1995, Mrema aligombea urais kwa tiketi ya NCCR. Mgombea urais wa CCM wa wakati huo, Rais mstaafu Benjamin Mkapa alishinda urais na Mrema alishinda nafasi ya pili. Mwaka huo chama chake cha NCCR kilipata wabunge zaidi ya 15.



Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000, Mrema aligombea Urais kwa tiketi ya TLP na kushika nafasi ya tatu na kupata wabunge watano. Aliyeshinda kiti cha urais mwaka huo alikuwa Rais mstaafu Mkapa. Profesa Ibrahim Lipumba alishika nafasi ya pili kwa kura.



Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, Mrema alishika nafasi ya nne na kupata Mbunge mmoja tu, Phares Kabuye wa Jimbo la Biharamulo Magharibi. Aliyeshinda kiti cha Urais mwaka 2005 ni mgombea wa CCM, Rais Jakaya Kikwete. Lipumba alishika nafasi ya pili na Freeman Mbowe wa Chadema alishika nafasi ya tatu.



Mrema alijiengua kutoka serikali ya CCM, baada ya kutofautiana na serikali ya wakati huo, kuhusiana masuala kadhaa. Nyota yake kisiasa ilikuwa inang’ara wakati huo na alikuwa anavuta watu wengi kwenye mikutano yake, tofauti na sasa ambapo chama chake cha TLP kimebaki na Mbunge huyo mmoja.



Alipoondoka CCM na kujiunga na NCCR, baadhi ya viongozi wa CCM walisema “Ni afadhali hakuanzisha chama chake kipya. Ni afadhali amejiunga na NCCR…tunawajua wale NCCR…kuna siku watakorofishana naye na kumtimua.” NCCR ya wakati huo ilikuwa ikiongozwa na akina Mabere Marando na Ndimara Tegambwage.



Akizungumzia mfumo wa vyama vingi katika kipindi cha miaka 15, Mrema anasema kwamba yapo mafanikio na matatizo kadhaa, yaliyojitokeza katika kipindi hicho.



Kuhusu mafanikio, Mrema anasema tangu kuundwa kwa vyama vingi mwaka 1992, uwezo wa vyama vya siasa kukosoa utawala uliopo madarakani kwa uwazi unakua.

Hali hiyo ni tofauti kabisa na enzi za chama kimoja cha siasa.Wakati huo ilikuwa vigumu kukosoa utawala na haikuwa rahisi kutoa maoni kwa uwazi.



“Demokrasia jamani inaendelea kukua, watu wameelimika na wanaendelea kuelimika kila kukicha, hata hoja wanajua kuunda. Pia kwa upande wa kuikosoa serikali iliyo madarakani, jambo hilo hivi leo linafanyika na haya ni mafanikio ya kuwa na vyama vingi vya siasa nchini . Hata hali ya uchumi na jamii navyo kwa pamoja vinakua katika kipindi hiki,” anasema Mrema.



Mafanikio mengine ni uhuru wa kuendesha mikutano. Mrema anasema vyama vikubwa vya upinzani, kama vile Chama cha Wananchi-CUF, Chadema, NCCR na TLP, vimeweza kufanya mikutano mbalimbali nchi nzima, yenye kuwaeleza wananchi mapungufu. Wananchi wengi wamekuwa wakihudhuria mikutano hiyo na kupata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali, yanayowakosoa hata viongozi wa upinzani na serikali.



Mrema anasema siku za nyuma hali hiyo ilikuwa haiwezekani, kwani wananchi wengi walikuwa waoga kujitokeza kwenye mikutano ya siasa.



“Wazo la kuwa na vyama vingi kwa kweli lilikuwa zuri na bora, sasa wananchi wengi wana uwezo wa kujiamini wenyewe na kusimama hadharani iwe kwenye mkutano au mijadala na kuhoji jambo, kitu ambacho ni cha msingi sana kwani uwezo wa kuhoji ni ishara ya kupanuka kifikra na hivyo kukua kimaendeleo, kwa sababu kama unaweza kuhoji jambo
leo, kesho utakataa kunyonywa na hivyo utakuwa mjanja hata sokoni ukipeleka mazao yako utasema bei ni hii na utauza, hivyo mfumo wa vyama vingi umeleta mafanikio makubwa ya kimaendeleo miongoni mwa wananchi na Taifa pia,” anasisitiza Mrema.



Pia, anasema katika kipindi cha miaka 15, vyama vya upinzani sasa vimeweza kuwadhibiti baadhi ya viongozi wa serikali ambao mienendo yao ilikuwa tofauti.



Anasema hivi sasa vyama vya upinzani vimekuwa vikiwasema hadharani baadhi ya viongozi wenye mienendo tofauti bila serikali kuingilia kati na kunyamazisha na kwamba kitendo hicho ni cha kijasiri. Anasema wakati wa mfumo wa chama kimoja, hali hiyo isingeweza kuvumilika, kwani waliothubutu kufanywa hivyo waliwajibishwa.



“Ni jambo zuri kuona viongozi wa serikali wa ngazi za juu, wanawawajibisha wale wachache wanaokiuka taratibu na mpangilio wa majukumu ya kazi kwa kujinufaisha wao, wapo viongozi waliopewa adhabu kwa mujibu wa sheria, kwa kuichafua nchi na bado wataendelea kuwajibishwa, hii yote ni pamoja na jitihada za vyama vya siasa kuwazungumzia na serikali kufuatilia. Kwa kweli demokrasia inakua,” anasema Mrema.



Mafanikio mengine ni kufanya maandamano. Mrema anasema hivi sasa hakuna tena vikwazo zisivyo na msingi kwa wananchi au vyama vya siasa kufanya maandamano ya amani ya kupinga au kudai haki zao za msingi, kama Katiba inavyosema



Anasema huko nyuma maandamano yalizuiwa bila kutolewa hoja au kama hoja zilitolewa, hakuna aliyehoji wala kupinga, hivyo demokrasia ilikuwa changa sana. Wananchi walikuwa waoga na ndio maana maendeleo yalikuwa duni. Wakati huo hakuna mwananchi aliyekuwa jasiri kutafuta ubia na wafanyabiashara wa nje, kwa kuhofia kufilisiwa.



Pamoja na mafaniko hayo, Mrema anasema bado yapo matatizo kadhaa yanayokwamisha kuwepo kwa demokrasia zaidi
miongoni mwa wanasiasa na jamii kwa ujumla.



Anataja moja ya matatizo hayo kuwa ni kuwepo kwa sheria ya uchaguzi iliyopitwa na wakati, ambayo haileti uwanja ulio sawa wa mashindano ya siasa kati ya wapinzani na chama tawala cha CCM.



Anatoa mfano mapungufu ya sheria hiyo, ndiyo yaliyofanya viongozi wa vyama vya upinzani kuitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iondoe kwanza mapungufu hayo, kabla ya
kufanyika kwa uchaguzi wa madiwani katika Kata 16 nchini hivi karibuni.



Anasema vyama vya upinzani vinataka marekebisho mbalimbali ya sheria hiyo, ikiwemo kufanya marekebisho ya Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, lililoandikwa mwaka 2004. Anasema Tume ilipinga hoja yao hiyo. Msimamo huo wa Tume ndio uliowafanya waende mahakamani kuiomba pingamizi kwa Tume kuendesha uchaguzi huo hadi kasoro zirekebishwe.



“Huu ni moja tu ya mfano, iko mingi kama hii, sisi tulisema daftari la wapiga kura lifanyiwe marekebisho kabla ya uchaguzi, kwa sababu wapo wananchi waliofikia umri wa kupiga kura yaani miaka 18, wapo pia wananchi waliojiandikisha kipindi hicho lakini wamefariki, pia wapo waliopoteza shahada zao za kupiga kura. Sasa tukienda hivyo hivyo huoni tunakiuka haki za msingi za wananchi wenye kustahili kupata haki yao ya kupiga kura,?” alihoji Mrema. Anasema kwa mazingira kama hayo, siyo rahisi kukawa na uwazi na usawa wa demokrasia.



Mrema anasema tatizo lingine ni Katiba ya nchi. Anasema Katiba hiyo ina kasoro kadhaa, hivyo inatakiwa kurekebishwa ili kuifanya iwe Katiba ya vyama vingi na siyo ile ya kuegemea chama kimoja cha siasa.



Alitoa mfano wa suala la kuwa na Mgombea Binafsi. Alisema suala hilo limekuwa likipingwa na chama tawala licha ya kukubalika kisheria. Anasema kambi ya upinzani iliwahi kupeleka mahakamani suala hilo la Mgombea binafsi na kushinda kesi, lakini chama tawala kililipinga.



Anataja tatizo lingine kuwa ni kukithiri kwa masuala ya rushwa na migogoro ya siasa, ambayo yameongeza mifarakano baina ya watu na vyama, badala ya kutangaza demorasia na uwazi.



“Bado demokrasia haijatawala kama inavyotakiwa, kwa kuwa hata katika chaguzi mbalimbali zilizofanyika na zinazoendelea kufanyika nchini, uwazi haupo,” anasema



Hata hivyo Mrema anahitimisha kwa kusema kuwa “Jambo la busara na la kuzingatia kwa serikali iliyo madarakani ni kuhakikisha inafanyia kazi matatizo hayo na mengine yanayojitokeza katika mfumo huo, ili kuhakikisha kuwa unakuwepo usawa wa vyama vya siasa katika kukuza demokrasia kwa faida ya taifa na wananchi wake.”

source habari leo
 
Atulie.....apambane na afya yake ajiuguze amepata shavu kutibiwa bure nje ya nchi kwa cheo cha Parole kisheria inatakiwa Mwenyekiti Parole aw Jaji Mstaafu.....sheria imekiukwa apewe ulaji hasa matibabu.....ale taratibu!!
 
Back
Top Bottom