Moyo Ulioonja Maumivu

Shunie

JF-Expert Member
Aug 14, 2016
152,966
453,702
Mtunzi Nyemo Chilongani sehemu ya 01


Gari aina ya Lamborghini Centenario LP 770 nyekundu yenye thamani ya zaidi ya dola laki tano ambazo zilikuwa ni zaidi ya bilioni moja lilisimama nje ya Ukumbi wa Mlimani City uliokuwa jijini Dar es Salaam.

Waandishi wa habari waliokuwa mahali hapo kwa ajili ya kuripoti Mashindano ya Miss Tanzania wakaanza kulisogelea gari hilo huku wakiwa na kamera zao mikononi mwao.

Walimfahamu mtu aliyekuwa ndani ya gari hilo, walihitaji kupata picha kadhaa kwa ajili ya magazeti yao, tovuti na hata mitandao ya kijamii.

Hata kabla ya mtu kuteremka, wakaanza kupiga picha mfululizo, hakukuwa na mwandishi aliyekuwa radhi kuondoka mahali hapo, kila mmoja alihitaji kupata japo picha moja tu ya sura yake.

Baada ya kukaa kwenye gari kwa sekunde zaidi ya hamsini, hatimaye mlango ukafunguliwa na msichana mrembo, mwenye sura nyembamba, mrefu na kidoti pembeni ya pua yake, akateremka na kutoa tabasamu pana.

Alivalia gauni refu jekundu la kumeremeta mpaka chini, viatu vilivyokuwa na visigino virefu, shingoni alikuwa na cheni ya kike iliyoonekana kuwa ya dhahabu kabisa huku kwenye mkono wake wa kushoto akiwa na saa ya thamani aina ya Rolex aliyoinunua nchini Ufaransa alipokuwa akiishi.

Msichana huyu aliitwa kwa jina la Violeth Joseph Zilikana. Alikuwa mmoja wa wanawake waliokuwa na uzuri wa ajabu nchini Tanzania.

Alikuwa maarufu na aliyekuwa na pesa nyingi, alikwenda sehemu yoyote aliyotaka duniani, alipewa mialiko mingi kutoka sehemu mbalimbali kutokana na kazi ya mitindo aliyokuwa akiifanya.

Umaarufu wake ulikuwa mkubwa mno, alijua kupendeza, watu wengi walimpenda na kutamani sana kuwa naye lakini kwa sababu mume wake alifariki dunia, hakuwa tayari kuingia kwenye uhusiano wa kimapenzi na mwanaume yeyote yule.


Screenshot_20181124-160825.jpeg
 
SEHEMU YA 02

Akaunti yake benki ilikuwa na kiasi cha shilingi bilioni 3.2, alijenga jumba kubwa lililokuwa Mbezi Beach huku akimiliki biashara nyingi nchini Afrika Mashariki.

Maisha yake hayakuwa Tanzania kwa sana, aliishi nchini Ufaransa huku akiendelea na kazi yake ya mitindo ambayo aliifanya kwa zaidi ya miaka mitatu.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa na maswali mengi kuhusu utajiri wa msichana huyu.

Ni miaka michache nyuma wakati akiwa na miaka kumi na tisa, tena huku akichipukia kwenye umaarufu nchini Tanzania aliolewa na mwanaume aliyeitwa Didier Polvat, raia wa Ufaransa aliyekuwa mbunifu wa mavazi duniani huku akimiliki kampuni yake ya Havana Fashion And Modelling ambayo ilifanya kazi dunia nzima kwa kuchukua wanamitindo mbalimbali.

Wawili hao walikutana wakati Didier alipokwenda nchini Tanzania kwa lengo la kutafuta warembo ambao wangeweza kufanya kazi katika kampuni yake. Mara baada ya macho yake kutua kwa Violeth alishtuka, hakuamini kama Tanzania ingekuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa.

Alimwangalia kwa matamanio, moyo wake ulimpenda kupita kawaida na hivyo kuomba ukaribu naye. Hilo halikuwa tatizo hasa kwa mtu kama Violeth ambaye alikuwana umaarufu mkubwa Tanzania lakini hakuwa na uwezo wa kujitangaza na kuwa zaidi ya hapo.

Wakaanza kuzungumza, wakaweka ukaribu, Didier hakutaka kukubali, alimuhitaji msichana huyo na hatimaye kumualika jijini Paris nchini Ufaransa kwenda kuhudhuria moja ya maonyesho yake ya mitindo nchini humo.

Violeth alikuwa gumzo kila kona, kila aliyemuona alishtuka, aliwafanya wanaume wote waweweseke kutokana na uzuri wake, alijua kutembea, alijua kuringa, alijua kutoa tabasamu na kubwa zaidi alijua kucheka na kuyafanya meno yake meupe yaonekane vilivyo.

Japokuwa Didier alitokea kumpenda sana Violeth lakini hakutaka kuwa na haraka kumtongoza na kumwambia ukweli wa kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.

Alimwangalia kwa macho yaliyobeba ujumbe mzito lakini hakutaka kumwambia kwa mdomo wake hivyo kuendelea kuyatumia macho yake katika kufikisha kile alichokuwanacho moyoni mwake.
 
SEHEMU YA 03

Alimchukulia chumba kwenye hoteli ya kifahari, alihitaji akae huko kwa kipindi chote ambacho angekuwa nchini Ufaransa, na kwa sababu Didier alikuwa mtu wa kwenda huku na kule, akamwambia Violeth kwamba lingekuwa jambo jema sana kama angeungana naye na kwenda huko.

“Wapi?” aliuliza msichana huyo.
“London nchini Uingereza, Sofia nchini Bulgaria, Roma nchini Italia na tutamalizia Brussels nchini Ubelgiji, naomba unipe ruhusa ya kwenda nawe mrembo,” alisema Didier huku akimwangalia Violeth machoni.

Msichana huyo hakuwa na jinsi, kwa sababu aliitwa, hivyo akakubali kuungana naye na kwenda huko.

Kwa kupitia nafasi hiyo, Violeth akaanza kujifunza mitindo, kutembea majukwaani na hatimaye kuwa mwanamitindo ambaye alikuwa chini ya kampuni aliyokuwa akiimiliki Didier.

Kila alipokuwa, Vaileth alikuwa gumzo, wanaume walimwangalia kwa macho ya matamanio kiasi kwamba mpaka Didier akaanza kuwa na hofu ya kuchukuliwa msichana huyo hivyo kupanga kumwambia ukweli kwa kuwa tu aliamini kuwa kama angechelewa kungekuwa na mwanaume mwingine ambaye angetumia nafasi yake kumchukua Violeth.

“Ninakupenda sana Violeth! Nilikupenda tangu siku ya kwanza nilipokutana nawe. Nahitaji kuwa nawe, naomba unipe nafasi,” alisema Didier kwa sauti ya chini iliyojaa ushawishi mzito wa kimapenzi.

Kwa Violeth ilikuwa vigumu kukubali, mara ya kwanza alikataa, hakuona kama alistahili kuolewa na Mzungu kama alivyokuwa Didier. Hakujiamini, aliogopa kumpa moyo wake mwanaume huyo na hiyo ndiyo ilikuwa sababu kubwa ya kumkataa.

“Sistahili,” alisema msichana huyo.
“Kwa nini?”
“Kuolewa? Hapana! Ninahitaji muda wa kuwa peke yangu kwanza,” alisema Vaileth.

Jibu hilo halikutosha kumfanya Didier arudi nyuma, bado alitakiwa kumwambia maneno mengi ya mahaba, kumpa ahadi ambazo aliamini siku zote za maisha yake angemfanyia na kumfanya kuwa mmoja wa wasichana waliokuwa na furaha katika maisha yao.

Hakuacha, japokuwa alikataa lakini aliendelea kumjali huku akimsisitizia kumuhitaji na kuwa naye katika maisha yake yote.
 
SEHEMU YA 04

Baada ya kufanya mitindo kwa miezi mitatu ndipo Violeth akaamua kumkubali Didier katika kipindi walichokuwa kwenye Ufukwe wa Ibiza nchini Hispania.
“Ninafurahi sana kusikia hivyo, kama nilivyokwambia, itakupenda katika maisha yangu yote,” alisema Didier huku akimwangalia Violeth.

Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa uhusiano wao, Violeth na Didier wakawa wapenzi. Uhusiano wao wa kimapenzi ukaanza kuripotiwa sehemu mbalimbali kwa sababu tu mwanaume huyo alikuwa na umaarufu mkubwa kwa kazi ya ubunifu aliyokuwa akiifanya.

Kupitia mpenzi wake, naye Violeth akaanza kupata umaarufu katika nchi za Ulaya na Marekani kitu kilichomfanya kuwa na furaha katika maisha yake yote.

Siku ziliendelea kwenda mbele na mwaka mmoja baadaye Didier akaamua kumuoa Violeth kwa ndoa iliyofungwa katika Kanisa la Lutherani lililokuwa katikati ya Jiji la Paris nchini Ufaransa.

Baada ya kuishi kwenye ndoa kwa mwaka mmoja tu, Didier akafariki dunia kwenye ajali ya ndege iliyotokea karibu na milima ya Himalaya alipokuwa akielekea nchini China kuonana na baadhi ya wanamitindo na kuwaingiza kwenye kampuni yake.

Violeth alipopewa taarifa ya kifo cha mume wake, alilia sana, hakuamini alichokisikia, wakati mwingine alihisi kama alikuwa akiota kwani hakuamini kama angeishi na mume wake kwenye ndoa kwa muda mfupi kiasi hicho.

Dunia nzima ilimuonea huruma, alikuwa msichana mzuri ambaye hakutakiwa kupitia yale aliyokuwa akipitia lakini hakukuwa na jinsi, alitakiwa kuamini kwamba kila kitu kilichotokea kilikuwa ni kweli, mume wake kipenzi alikufa kwenye ajali hiyo ya ndege.
*
*
*
Je, nini kitaendelea katika maisha ya msichana huyu?
 
SEHEMU YA 05

Utajiri wa Didier wote akakabidhiwa, kampuni zake na hivyo kuanza usimamizi akiwa peke yake. Kwake, pesa hazikuwa na faida yoyote ile, moyo wake ulimpenda sana Didier, alikuwa tayari kupoteza kitu chochote kile, hata pesa zote lakini si kumpoteza Didier.

Kazi alizokuwa akizifanya mume wake huyo, akaanza kuzifanya na kuzisimamia kwa nguvu zaidi. Akawa mtu wa kusafiri mara kwa mara kuonana na wanamitindo waliokuwa wakichipukia na kuwaingiza katika kampuni yake.

Mpaka anafikisha miaka ishirini na tatu, utajiri wake ukawa mkubwa lakini hakutaka kusubiri, bado aliendelea kuzunguka duniani kote, aliwatafuta wasichana na wavulana mbalimbali ambao aliwapa mikataba na kuanza kufanya kazi chini yake.

Baada ya kukaa sana nchini Ufaransa, akaamua kwenda Tanzania ambayo siku hiyo alikuwa ameteremka katika gari lake na kuelekea ndani ya Ukumbi wa mlimani City kwa lengo la kuangalia Kinyang’anyiro cha Miss Tanzania.

Waandishi wa habari waliendelea kupiga picha kila hatua aliyokuwa akipiga, ndani ya ukumbi huo mara baada ya kuingia tu minong’ono ya watu ikaanza kusikika, waliokuwa na simu zao, haraka sana wakazishika na kuanza kumpiga picha.

Kuwa na mtu kama Violeth ndani ya ukumbi huo kilikuwa kitu kikubwa mno. Msichana huyo alikuwa maarufu mkubwa, aliyekubalika kila kona, uwepo wake humo kilikuwa kitu kingine kabisa.

“Umependeza,” alisema msichana mmoja aliyekaa karibu na Violeth, alishindwa kuvumilia, akajikuta akimsifia.
“Ahsante sana!” alisema Violeth huku akitoa tabasamu pana.
 
SEHEMU YA 06

“Halo Cindy! Upo wapi?” ilisikika sauti ya mwanaume mmoja aliyekuwa amevalia shati jeupe na tai nyekundu, alikuwa ndani ya chumba kimoja cha hoteli akiongea na mtu aliyekuwa upande wa pili.

“Nipo nyumbani!”
“Hivi umesoma magazeti ya leo?” “Magazeti gani?”
“Ya udaku!”
“Hapana! Kwani kuna nini?” aliuliza msichana huyo.

“Unajufanya kichaa na hujui walichokiandika?” aliuliza mwanaume huyo kwa sauti kali kidogo.

Wakati mwanaume huyo akizungumza hayo, mkononi mwake alikuwa na Gazeti la Udakuzi lililokuwa likitoka mara mbili kwa wiki. Alikasirika, mbele ya ukurasa wa gazeti hilo kulikuwa na picha yake kubwa na ya msichana aliyekuwa akizungumza naye kwa simu.

Mbali na picha hiyo, pia kulikuwa na picha ndogo mbili ambazo ziliwaonyesha wakiwa hotelini, picha hizo alipigwa wakati akiwa amelala na msichana huyo ambaye ndiye aliyezipiga kwa staili ya selfie.

Alikasirika kupita kawaida, hakuamini msichana kama Cindy angeweza kufanya ujinga kama huo. Yaani alimsubiri akiwa amelala, akapiga picha na kisha kuwatumia waandishi wa habari.

Mwanaume huyo aliitwa kwa jina la Theo. Alikuwa mwanaumiziki aliyekuwa na jina kubwa Afrika Mashariki, alijulikana kila kona, aliheshimika kwa kuwa tu katika maisha yake alijua kuwaheshimu watu wa kila rika.

Hakuwa mtu wa skendo, aliishi maisha yake kwa siri kubwa, hakukuwa na mtu aliyemfahamu msichana wake, kila alipokuwa akiulizwa na waandishi wa habari jibu lake lilikuwa moja tu kwamba hakuwa na msichana yeyote yule.

Aliishi hivyo, pamoja na umaarufu wake wote zaidi ya wanamuziki wote Afrika Mashariki lakini alijiheshimu na kuishi maisha ya kisupastaa.

Alitembea na masupastaa wote wa kike lakini kwa siri sana, hakutaka kuyaweka maisha yake hadharani kwa kuwa aliamini kulikuwa na watu wengi hasa vijana ambao walitakiwa kuiga mfano wa maisha yale aliyokuwa akiishi.
 
SEHEMU YA 07

Kitendo cha Cindy, msichana aliyekuwa na umaarufu mkubwa kwenye mitandao ya kijamii kuzianika picha zake hizo kilimchanganya kupita kawaida.

Hakujiangalia yeye, aliangalia namna ambavyo watu wangepokea kile kilichokuwa kikionekana kwenye gazeti lile.

Aliingia mikataba na makampuni mengi, tena kwa kulipwa pesa nyingi, kitendo alichokifanya Cindy kilimaanisha kuhatarisha mikataba yake aliyokuwa ameingia na kampuni hizo. Alizungumza naye kwa hasira mno kwani hakutaka kabisa kulichafua jina lake.

Siku hiyo Afrika Mashariki nzima stori ilikuwa ni picha zake hizo tu, kila mmoja alishangaa, hakukuwa na mtu aliyeamini kwamba angefikia hatua ya kupiga picha za faragha akiwa na msichana.

Waandishi wa habari wakaanza kumtafuta, walimpigia simu, walihitaji kuzungumza naye kuhusu jambo hilo, halikuonekana kuwa la kawaida hata kidogo na ndiyo maana walihitaji kusikia kutoka kwake, alikuwa analizungumziaje jambo hilo.

Hakupokea simu hizo, alichanganyikiwa, hata kama angepokea, hakuwa na la kuwaambia kwa sababu tayari kila mmoja alijua dhahiri kwamba yeye ndiye aliyekuwa kwenye picha zile mbili.

“Cindy! Amenikera sana,” alisema Theo kwa hasira huku akiwa amekata simu.
Hakujua ni kwa namna gani angewaambia Watanzania na kuwaaminisha jambo la uongo kupitia picha zile, alikaa na kufikiria kwa dakika kadhaa ndipo akapata wazo.

Ilikuwa ni lazima awaaminishe Watanzania kwamba zile picha hazikuwa zake, yaani si picha halisi, zilitengenezwa kwa ajili ya kumchafua tu. Kabla ya kuwaaminisha watu hao jambo hilo, ilibidi akubaliane na Cindy kwanza, amwambie kuhusu mpango huo vinginevyo angemshtaki na kwenda kumfunga.

Haraka sana akampigia simu msichana huyo na kuanza kuongea naye, alimwambia ukweli kuhusu kile alichokuwa amekifikiria, Cindy alisikiliza kwa makini, moyoni mwake hakutaka kukubaliana naye kwa kuwa mpango wake mkubwa wa kuzisambaza zile picha ni kupata kiki tu, yaani aandikwe na umaarufu wake usipotee.
 
SEHEMU YA 08

“Yaani niseme picha zimeeditiwa?” aliuliza Cindy.
“Ndiyo!”
“Hapana! Siwezi! Ninaogopa,” alisema msichana huyo.

Maneno ya Cindy yalimtia hasira zaidi, yaani alimwambia hivyo kwa lengo la kusafisha mambo lakini matokeo yake alimwambia kwamba haiwezekani kufanya hivyo.

Alichokifanya Theo ni kumpa maneno ya vitisho kwamba angemshtaki kwa kuvujisha zile picha na kumfunga kwa sababu alikuwa na urafiki mkubwa na viongozi mbalimbali nchini Tanzania.

Hilo likamtia hofu Cindy, alijua kabisa ukaribu aliokuwanao Theo na viongozi mbalimbali wa nchi, alipomwambia kwamba angemfunga, alimaanisha na hivyo kuwapigia simu waandishi wa habari na kuwaambia kuhusu zile picha, ni kweli yule mwanamke alikuwa yeye ila yule mwanaume hakuwa Theo bali kulikuwa na mtu aliyeediti na kumuweka mwanamuziki huyo.

“Kwa hiyo unataka kutuambia ni Adobe photoshop ndiyo imefanya kazi?” aliuliza mwandishi wa habari akiitaja programu iliyokuwa ikihusiana na kutengeneza picha kwenye kompyuta.

“Ndiyo! Jamani naomba mjue kwamba yule si Theo,” alisema msichana huyo.
Hakuishia hapo tu, akaingia kwenye mitandao yake ya kijamii na kutangaza kwamba zile hazikuwa picha halisi bali kulikuwa na mchezo uliokuwa umefanyika hivyo aliomba radhi.

Waandishi wa habari wakampigia simu na kumuuliza, hakubadili jibu lake, aliwaambia vilevile kwamba zile picha hazikuwa halisi, zilitengenezwa na kuwekwa picha ya mwanaume huyo.
“Ila uliniambia kwamba ni yeye!” alisikika mwandishi mmoja kwenye simu.

“Yaani wewe acha tu Imelda. Naomba unisaidie katika hili vinginevyo nitashtakiwa!” alisema Cindy.
“Kivipi?”
“Yaani wewe elewa hivyo tu,” alisema msichana huyo.

Hiyo ilikuwa mbinu ya Theo kujilinda kibiashara, hakutaka kuona Watanzania wakimuona mtu mbaya aliyewaharibu vijana wengine, alihitaji kuwa mfano mzuri kwa kila rika.

Mara baada ya msichana huyo kusema kwamba picha zile zilieditiwa, haraka sana Theo akaingia kwenye kazi ya kuwalipa baadhi ya watuna kuwataka kusambaza picha zile kwa kusema ni kweli zilieditiwa.
 
SEHEMU YA 09

Ilikuwa kazi kubwa na ambayo ilifanya kila kitu kuwa chepesi mno kwani watu hao walifanya kazi kwa nguvu kubwa na hatimaye kila mmoja kuamini kwamba zile picha zilieditiwa na hakukuwa na ukweli wowote ule.

Baada ya hapo, Theo aliendelea na maisha yake kama kawaida. Aliingiza kiasi kikubwa cha pesa, aliheshimiwa na kuonekana hakukuwa na msanii aliyekuwa na roho nzuri, mwenye nguvu ya kubadilisha hali yoyote ile isipokuwa yeye tu.

Pesa zilimnukia, alifanya kila kitu kwa umakini mkubwa, benki, mitandao ya simu, mashirika ya ndege na kampuni nyingine zilimfuata na kutaka kutangaza pamoja naye, kazi yake ikawa moja tu, kupiga pesa kila siku.

Alikuwa na mafanikio makubwa, akaunti yake ilikuwa na bilioni moja, alipambana kuhakikisha anakuwa na mafanikio zaidi ya hayo aliyokuwanayo kipindi hicho.

Baada ya kupita miaka miwili, huku akiwa na miaka ishirini na nne, Watanzania wakaanza kupiga kelele za kumtaka aoe na kujenga familia yake kwani miaka ilikuwa ikikatika na hakukuwa na yeyote ambaye alijua mwanaume huyo alikuwa akitoka na nani

Hicho ndicho kilikuwa kilio chake, ni kama kampeni kubwa ya kumtaka aoe ilianza kufanyika, kweye mitandao, watu waliweka mabango ya kumtaka mwanaume huyo amtafute mwanamke wa kumuoa ili maisha yake, utajiri wake uwe na mtu mwingine wa kumsimamia.

Mara ya kwanza alichukulia kama utani lakini baada ya siku kuendelea kwenda mbele huku Watanzania wakimsisitizia, aliamini kwamba kweli wakati huo waliamua, walihitaji kumjua mwanamke aliyekuwa na bahati ya kuolewa naye.
“Nioe?” alijiuliza.
*
*
*
Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 10

Hakuwa na majibu, akampigia simu rafiki yake wa kike aliyeitwa kwa jina la Christina kwa lengo la kuzungumza naye.

Huyo ndiye alikuwa mshauri wake, aliyejua mambo mengi kuhusu yeye, alikuwa mwanasheria wake, kila alichokuwa akikifanya, asilimia themanini alikuwa akimshirikisha.

Baada ya dakika kadhaa akaonana na Christina na kumshirikisha jambo hilo. Msichana huyo hakushangaa kwani aliyaona mabango kwenye mitandao ambayo yalimtaka mwanaume huyo kuingia kwenye uhusiano wa kimapenzi na kufunga ndoa.

“Unahisi huu ni wakati sahihi?” aliuliza Theo huku akimwangalia Christina na marafiki zake kadhaa waliokuwa sebuleni.
“Nadhani ni wakati sahihi.

Watanzania wanakupenda sana, kama wao wanataka uoe, oa tu,” alisema Christina huku akimwangalia Theo usoni.
“Mh! Ila naogopa!”
“Unaogopa nini?”
“Kuoa!”
“Kwani utakufa?”

“Hapana! Ila nahisi kama nitakufa kimuziki kama wengine!” alisema.
“Haiwezekani! Kila kitu ni kujipanga tu,” alisema christina.

Walizungumza mambo mengi, Theo hakuwa na cha kusema zaidi ya kuhitaji muda kwani jambo hilo halikuwa la kukurupuka hata kidogo.

Alikuwa kwenye wakati mgumu mno, moyo wake ulikuwa na uzito wa kumchagua msichana wa kumuoa.

Hakuamini katika mapenzi, alichokuwa akikijua ni kuwa msichana yeyote yule angekubaliana naye kwa sababu alikuwa maarufu, na kubwa zaidi alikuwa na pesa.
Alihitaji umakini sana katika kufanya uchaguzi, hakutarajia kukurupuka hivyo alianza kusubiri huku akitafuta.

Wanawake walimpenda, kila mmoja alihitaji kuwa naye ila hakutaka kabisa kumuonyeshea msichana yeyote yule dalili za kumtaka kimapenzi, alitulia kana kwamba hakuwa akiyaona yale mabango yaliyokuwa yakisambazwa katika mitandao ya kijamii.

Baada ya Watanzania wa kawaida kupiga kelele, hatimaye nao viongozi mbalimbali wakaanza kuandika kwenye akaunti zao kwamba huo ndiyo ulikuwa muda sahihi wa yeye kuoa.

Alishtuka, posti ya kwanza ambayo aliiona ilikuwa ni ya waziri mkuu, makamu wa rais, wabunge na viongozi wengine. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, hakuamini kama kila Mtanzania alitamani kumuoa akioa na kujenga familia yake.
 
SEHEMU YA 11

“Jamani! Ishu ya kuoa imekuwa dili sana?” aliuliza Theo.
“Hata mimi nashangaa, yaani kila mtu ni Theo tu, kwani watu wengine hawapo?” alisema rafiki yake aliyeitwa kwa jina la Ibrahim.

“Kwa hiyo nifanyeje?”
“Kama wanataka kuoa, oa tu!” alisema jamaa mwingine aliyeitwa King.

“Hapana! Si kirahisi hivyo! Kuoa kunatisha sana hasa unaposikia kuna jamaa anatembea na mkeo, sasa mimi si nitakuua,” alisema Theo.
“Kwa hiyo wewe unaogopa kusalitiwa?”
“Haswaaaa!”

Hicho ndicho kilichomtia hofu, hakutaka kuoa kwa sababu aliogopa kusalitiwa, watu waliongea sana lakini hakutaka kuwasikiliza, moyo wake ulimwambia kwamba endapo angeoa, kuna siku angemuua mke wake kwani asingeweza kuvumilia maumivu ya kusalitiwa.
Baada ya kupita miezi miwili ndipo kukawa na kinyang’anyiro cha Urembo wa Tanzania.

Alialikwa, alitumiwa kadi ya viti maalumu na hivyo kutakiwa kujiandaa.
Matangazo yalifanyika ya kutosha, kila kona alikuwa akisikika yeye tu, mashindano hayo ambayo yalianza kupunguza mvuto yakaanza kusikika kwa sababu tu Theo angekuwepo mahali hapo.

Alipendwa, alikuwa mfano wa kuigwa, kila mtu alitamani siku moja awe na jina kubwa kama mwanaume huyo hivyo alitakiwa kuonekana msafi kila kona na ndiyo maana alitumia nguvu nyingi kuhakikisha anajisafisha baada ya picha zake chafu na msichana Cindy kuvuja.

Kwa kuwa alialikwa katika kinyang’anyiro hicho, akaanza kuposti kwenye akaunti zake mitandaoni, watu wengi wakapata hamasa, haikuwa ya kwenda kuangalia bali kumuona Theo ambaye kila alipokuwa alikuwa gumzo na kubwa zaidi hakuwa mtu wa kuonekana mara kwa mara mpaka pale kutakapokuwa na jambo kubwa.

Muda ulipofika, akawachukua wapambe wake, wakaingia ndani ya gari na kuondoka kuelekea Mlimani City. Ndani ya gari hakutaka kuzungumza kitu chochote kile, alikuwa kimya, kichwa chake kilikuwa na mawazo mengi juu ya yale aliyokuwa ameambiwa.

Hakutaka kuoa kabisa lakini suala hilo lilivyokuwa linapelekwa na kuchochewa mpaka na viongozi wa nchi, akahisi kabisa angeshindwa kuvumilia, kama ni mzigo basi huo ulikuwa mkubwa na uliomzidi kabisa.
 
SEHEMU YA 12

Baada ya kufika hapo, wakaanza wapambe kuteremka. Waandishi wa habari ambao walikuwa nje walijua kabisa ni nani alikuwa akienda kuteremka, wakajiandaa kumpiga picha.
Theo alipoteremka, kila mmoja alihisi kuchanganyikiwa.

Mwanaume huyo alipendwa mno, picha zilipigwa nyingi, wengine wakajitahidi kumsogelea kwa lengo la kumuhoji lakini hakutaka kuzungumza kitu chochote kile zaidi ya kupiga hatua na kuelekea ndani.

“Hebu tuambie vizuri kuhusu zile picha,” alisema mwandishi mmoja huku akijitahidi kumsogelea Theo ila walinzi wake wakamzuia, hakuzungumza chochote kile zaidi ya kuachia tabasamu, tabasamu ambalo kwa waandishi tu lilionekana kuwa habari ya kuandikwa gazetini.

Akaingia ukumbini, watu walitulia lakini alipofika yeye tu, ukumbi mzima ukalipuka kwa shangwe kiasi kwamba wale ambao hawakumuona walitaka kujua ni mtu gani alikuwa ameingia, alikuwa rais ama la.

Theo alitembea kwa mwendo wa taratibu huku akisindikizwa na mtu mwingine humo mpaka kwenye viti vya VIP na kukaa karibu na Violeth.

Hakumfahamu, msichana huyo alijikausha, alimuona Theo akija pale alipokuwa na kukaa pembeni yake.

Alimjua mwanaume huyo, alikuwa supastaa, alijua ni kwa jinsi gani alishobokewa na wanawake wengi, hivyo yeye hakutaka kumshobokea mpaka pale atakapoanza mazungumzo yeye mwenyewe.

“Mambo mrembo,” alisema Theo huku akimsalimia Violeth, alipogeuka na kukutanisha macho, Theo ndipo akagundua alikuwa amekaa na msichana aliyekuwa akivuma kwa uzuri, kuolewa na mzungu na kufanya mitindo.

Badala ya Violeth kujisikia fahari, Theo ndiyo akaonekana kuchanganyikiwa. Mtu aliyekuwa pembeni yake, alikuwa na uzuri wa asili, alimpa mkono huku akimwangalia lakini macho yake hayakutoka usoni mwa msichana huyo.

Alibaki akimwangalia kama mtu aliyekuwa akimchunguza kitu kilichomfanya mpaka Violeth kushangaa na kuona aibu kwani kwa ule mtazamo ambao Theo aliutumia kumwangalia, alijua kabisa ulimaanisha nini.

“No! Don’t look at me like that!” (hapana! Usiniangalie hivyo) alisema msichana huyo kitu kilichomshtua Theo kutoka mbali kabisa.
“I can’t believe it,” (siamini) alisema huku akitabasamu.
“What?” (nini?)
 
SEHEMU YA 13

“Oh! I’ve nothing to say.” (Oh! Sina cha kuongea)
“No! Tell me, what is it?” (hapana! Niambie kitu gani)
“I’m the lucky guy in the world by now?” (mimi ni mtu mwenye bahati sana duniani kwa sasa) alisema Theo.
“Why?” (kwa nini?) aliuliza Violeth huku akitoa tabasamu pana.

“I have sat next to an extremely cute girl in the world,” (nimekaa pembeni ya msichana mrembo mno duniani) alijibu Theo na wote kuanza kucheka.

Theo hakutaka kufuatilia tena kinyang’anyiro kilichokuwa kikiendelea, alibaki akizungumza na Violeth tu. Muda wote alikuwa akimwangalia msichana huyo, uzuri wake ulimchanganya, hakujua ni kwa jinsi gani alibahatika kukaa pembeni yake.

Alijisikia amani, furaha kubwa huku moyo wake ukianza kuingiwa na mapenzi mazito ambayo hakuwahi kuwanayo kabla.

Kila alipomwangalia Violeth alisikia sauti moyoni mwake ikimwambia kwamba huyo ndiye mwanamke ambaye alitakiwa kuwa naye, kumuoa na kujenga familia pamoja.
“Violeth! Nilisikia kuhusu mume wako! Pole sana,” alisema Theo kwa sauti ya chini.

“Ahsante sana. Ila unaniangalia sana mpaka nasikia aibu,” alisema Violeth huku akiachia tabasamu.
“Najua! Nashindwa kuyatoa macho yangu kwako.”
“Kwa nini?”
 
SEHEMU YA 14

“Nashindwa tu. U msichana mrembo mno, ni kama sijawahi kuona mwanamke mzuri kama wewe. Violeth, naomba nikuombe kitu kimoja,” alisema Theo kwa sauti ndogo, ya taratibu, sauti ambayo ilimaanisha ni kwa jinsi gani alikuwa akiomba.

“May I take you out for dinner?” (naweza kukupeleka kwenda kula chakula cha usiku?) aliuliza Theo.
“Today?” (leo?)
“Hapana! Natamani iwe hata kesho,” alijibu.

“Is it a date?” (ni mtoko wa mapenzi mapya?)
“Hahaha! What do you think?” (Hahah! Unafikiria nini?)
“Sipo tayari!”

“Najua imekuwa ghafla sana, hata kama hautokuwa mtoko wa kimapenzi, naomba nitoke nawe tu, tukale chakula cha usiku na moyo wangu uridhike. Violeth, nakuomba sana,” alisema Theo huku kwa mkao ulivyobadilika ulionyesha alikuwa tayari kupiga magoti mbele ya msichana huyo.

“No!”
“Pleaseeee....” alisema Theo huku akitaka kupiga magoti.

“Hey! What are you doing? Are you insane! Don’t do that, pleaseeee,” (Hey! Unafanya nini? Una uwendawazimu? Tafadhali usifanye hivyo) alisema Violeth kwa sauti ya chini.
“Ni kwa sababu umekataa! Ninapiga magoti kama ishara ya kukuomba sana,” alisema Theo.

“Basi nimekubali! Naomba usipige magoti. Sawa?”
“Sawa.”
*
*
*
JE, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 15

Theo akatulia, moyo wake ulijisikia amani, aliangalia jukwaani kile kilichokuwa kikiendelea lakini wakati mwingine macho yake yalimwangalia Violeth.

Bado alichanganyikiwa kupita kawaida, alijua dhahiri kwamba huyo ndiye msichana aliyetakiwa kuwa wake maisha yake yote, kusingekuwa na mwingine ambaye alitakiwa kupata nafasi ya kuishi naye.

Watu waliokuwa nyuma ya mahali pale walipokuwa macho yao yalikuwa kwa watu hao wawili. Kila kitu walichokuwa wakiongea, walikisikia kwa mbali na hata tukio la Theo kutaka kupiga magoti waliliona.

Walishangaa, hawakuamini kile walichokiona, mwanaume kama Theo kutaka kumpigia magoti msichana, halikuwa jambo la kawaida hata kidogo, ila walipojiuliza kuhusu msichana mwenyewe, wao wenyewe wakahisi kwamba kweli alistahili kutaka kufanya hivyo.

Mashindano hayo yaliendelea mpaka yalipokwisha ambapo watu wakaondoka huku Theo na Violeth wakisimama na kuanza kueleka nje, tena huku wakiwa karibukaribu.

Walipofika nje, waandishi wa habari wakawasimamisha na kuanza kuwahoji, walikuwa na maswali mengi kuhusu shindano hilo, uwepo wao na hata mambo mengine. Waliyajibu maswali yao kwa ufasaha zaidi.

“Ila mmependeza mlivyokuwa wawiliwawili,” alisema mwandishi mmoja huku akiwaangalia, alikuwa akiwatania.
“Ahsante sana!” alisema Theo.
“Harusi lini?”
“Harusi gani?”
“Wewe na Violeth,” alijibu.

Alikuwa akitania lakini utani huo ulikuwa mtamu kwa Theo. Alimpenda msichana huyo hivyo hata alipoulizwa kuhusu suala la harusi, alibaki akitabasamu huku moyo wake ukitamani kumwambia mwandishi huyo aendelee kuchombeza kwa maswali yake matamu.

“Hakuna harusi hapa,” alijibu Violeth.
“Kwa hiyo ni marafiki tu? Ila si hata harusi huwa inaanzia kwenye urafiki,” alisema mwandishi huyo.

Lingekuwa linazungumziwa suala la kijinga mahali hapo, haraka sana Theo angemshika mkono Violeth na kuondoka naye ila kwa sababu kile kilichokuwa kikiulizwa kilikuwa kizuri kwa upande wake, akaona ni wakati wa kuendelea kusimama na kusikiliza.

Waandishi wengine waliokuwa pembeni nao wakasogea, kila mmoja alionekana kuvutiwa na jinsi watu hao walivyokuwa, walipendeza, maswali yakaanzia hapohapo kwamba inawezekana wawili hao walikuwa katika hatua za kuwa wapenzi.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom