Mkuu wa Mkoa aagiza shule zote za Sekondari za Dodoma kufunga CCTV Camera

JanguKamaJangu

JF-Expert Member
Feb 7, 2022
2,308
5,458
Makata.jpg

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka ametoa wito kwa Shule zote za Sekondari ndani ya Jiji la Dodoma kuhakikisha zinafunga CCTV Camera ili kusaidia kubaini watu wanaojihusisha na vitendo vya kiuhalifu katika maeneo ya Shule.

Ameyasema hayo wakati akizungumza na Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Miyuji iliyopo Kata ya Mnadani Jijini Dodoma, alipotembelea Shule hiyo kutoa pongezi kwa Bodi na Uongozi wa Shule hiyo kutokana na kuweka mfumo wa CCTV Camera kwa ajili ya suala la ulinzi na Usalama.

Amesema kumekuwa na matukio mengi ya kiuhalifu katika Jiji la Dodoma ikiwa ni pamoja na vitendo vya wizi na uharibifu wa miundombinu kutokana na kasi ya ukuaji wa Jiji, hivyo ni lazima Shule zote za Sekondari katika Jiji la Dodoma zikahakikisha kwamba zinakuwa na mfumo wa Camera ili kuwabaini wahalifu.

“Nitoe pongezi kwa Bodi ya shule pamoja na Uongozi wote kwa ujumla kwa kushirikiana mpaka kuweka mfumo wa CCTV Camera hili ni jambo kubwa sana Mmejiwekea ulinzi na wahalifu wataonekana.

“Kumekuwa na matukio mengi ya kiuhalifu tena ya kuaribu miundombinu yetu, milango ya shule inavunjwa, madawati yanaibiwa lakini kupitia CCTV Camera wahalifu watapatikana,na niagize shule zote kuanzia Msingi na sekondari zifungwe CCTV Camera,” amesema Mtaka.

Aidha, amezitaka kamati za Shule ndani ya Mkoa wa Dodoma kufanya uchambuzi wa Matokeo ya watoto waliopo Kidato cha Nne mwaka huu,ikiwa ni pamoja na matokeo yao ya kutoka Kidato cha Tatu kwenda kidato cha Nne na ufaulu wa Mitihani ya Majaribio kuanzia mwezi Januari hadi Juni na kupata alama za ufaulu daraja F kwenye masomo ya Sayansi,kuona namna ya kuwapunguzia mzigo wa maandalizi ya mtihani wao wa Taifa.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Miyuji Mwl.Greyson Maige akisoma risala mbele ya Mkuu wa Mkoa amesema Shule hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na upungufu wa walimu wa Sayansi,Shule kuwa karibu na maeneo ya makazi na biashara na hivyo kusababisha kelele.

“Changamoto kubwa kabisa ni kukosekana kwa Waalimu wa Sayansi yaani ni wachache sana na hii inapelekea Masomo ya Sayansi Wanafunzi wanakuwa wanafeli kila mara.

“Shule hii ipo katikati ya makazi ya Watu,pikipiki zinapita zinapiga kelele, saloon zinafungulia miziki ambapo inawatoa watoto katika akili ya kusoma na kuwaza ya nje na muda mwingine magari yanapita ns kufungulia mziki mkubwa hii inskuwa sio sawa kwa Wanafunzi wetu,” amesema Maige.

Aidha, amezitaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na ukosefu wa Viwanja vya michezo,uhaba wa Kompyuta, ukosefu wa vitabu vya masomo ya biashara,kukosekana kwa ukumbi wa Shule,kukithiri kwa utoro wa wanafunzi unaotokana na wengi wao kuishi katika mazingira magumu na ushirikiano mdogo wa wazazi na walezi hasa kuwaleta wanafunzi katika kambi ya kitaaluma.


Source: Swahili
 
Back
Top Bottom