Mkasa Wa Kweli : Kuzimu Na Duniani

SEHEMU YA 15

Fuatilia sana tabia za kupoteza vitana nyumbani. Si vitana tu, vitu vyovyote vidogovidogo. Mara kalamu haipo, mara kuna CD ya muziki ilipotea, mara kuna glasi au kijiko hakionekani! Ujue unaishi nyumba moja na majini.
SASA ENDELEA MWENYEWE:


Kupotea kwa vitu hivyo mara nyingi kunasababishwa na wao kutovipenda vitu hivyo. Unaweza kununua kitana, wao, hasa yule unayeishi naye kwenye chumba kimoja hakipendi kitana hicho. Kwa hiyo anakichukua na kukitupilia mbali. Kwa upande wa wanawake, wengi hujikuta wakipotelewa na vibanio, vifuniko vya pafyumu, vioo, vitambaa vya mkononi na vitu vingine vinavyofanana na hivyo.


Wengi utawasikia wakiwalalamikia wasichana wao wa kazi kwamba wanapoteza vitu hivyo lakini kumbe siyo. Hii huweza kutokea hata kwa nguo za ndani.


Kifupi ili ujue unaishi nyumba moja na viumbe hao, mara nyingi utatokewa au kusikia vitu visivyo vya kawaida. Umelala, unasikia kwa mbali kama mlango wa uani unafunguliwa, ukienda hukuti mtu wala hakuna dalili kama kuliingia mtu.


Kwa wale wanaopanga nyumba, cha kujihadhari nacho ni hiki! Kama nyinyi ni wanandoa, mnaweza kujikuta mmehamia kwenye nyumba ambayo ugomvi haushi kila siku. Kitu kidogo tu, ugomvi.


Na ugomvi huo, mara nyingi utamsikia mke akipenda kusema anarudi kwao au mume akisema utaondoka humu ndani. Kama hakuna historia ya hivyo, hapo mjue kuna jini mnaishi nalo, sasa halitaki tabia zenu za kufanya tendo la ndoa wakati lenyewe lipo.
Basi, turudi kule kwenye ile sherehe. Baada ya kumalizika, majini waliondoka mmojammoja kwenda nje ambako walisimama sehemu moja.


Hapa niseme kidogo, naamini mmewahi kusimama eneo ambalo ghafla mkahisi joto. Basi ujue kuna majini zaidi ya kumi yamesimama hapo jirani yenu yakiendelea na shughuli zao.


Basi, pale nje, mmoja wao aliniambia natakiwa kutafuta baa tano nzuri ambazo zinajaza sana wateja na nikishazipata wao watakuja kuchukua jibu usiku wa kesho yake.
Nilikubaliana nao, wakanisimamisha wima, kisha wakaniambia ninyooshe mikono yote juu, nikafanya hivyo. Wakasema usiku mwema, tutaonana kesho.


Ilikuwa kufumba na kufumbua, nilikuwa nje nyumbani kwangu. Mlango ulikuwa umefungwa, lakini nilipoanza kutembea kuelekea mlangoni, ulifunguka wenyewe, nikaingia ndani.


Nilimkuta mke wangu ameshalala, lakini nilipoingia tu, alishtuka sana na kuanza kusali.
Alisema anamshukuru Mungu kwa kumshindisha salama na kumfikisha usiku ule salama kwa vile kuna wengi walitamani kuimaliza siku hiyo lakini wameshindwa, lakini yeye aliyepewa nafasi hiyo hajatumia ufundi wowote, hajatumia maarifa, hajatumia nguvu wala kipaji, bali ni neema ya Mungu tu.


Nilisimama kumsubiri amalize kusali. Alipomaliza tu, akaniangalia na kuanza kulia. Kabla sijamuuliza kisa cha kilio chake, nikasikia hodi wenyewe.
“Karibu mchungaji,” mke wangu alimkaribisha, akaenda kufungua mlango yeye huku akifuta machozi.


Nilisikia wakisalimiana sebuleni bwana asifiwe, bwana asifiwe. Nikaachana na wao, sikutaka kutoka bali nikapanda kitandani ili kulala.


Baada ya dakika kumi kupita, nikasikia wakisali huku wakikemea. Hiyo ilinipa shida sana mpaka nikawa silali. Nikawa nahamahama pale kitandani, mara nahisi moto.


asema moto na si joto. Mara nikawa nahisi kuchomwa na vitu vyenye ncha kali.
Nikajua yote yale ni kwa sababu ya yale maombi. Nilishindwa kulala, nikakaa.
Ilikuwa kufumba na kufumbua, nikaona watu watatu wamesimama mbele yangu. mmoja akasema:


“Tumeona mateso yako. Mke wako amekuwa kikwazo kikubwa sana kwetu. Mara nyingi ndiyo amekuwa akisimama kuzuia mipango yetu mikubwa kwako. Sasa tunasema tunapambana naye.”


Walipomaliza kusema hivyo, wakafutika machoni pangu, nikabaki mwenyewe. Mara nikasikia sebuleni sauti za maombi zimeongezeka mara tatu zaidi ya mwanzo. Nilijua hali imebadilika, jamaa zangu wamezuka sebuleni sasa mchungaji, mke wangu na wengine wanapambana. Mchungaji alikuja na watu lakini sikujua ni wangapi ila kwa zile sauti za kukemea walikuwa zaidi ya watatu.


Nilitoka kitandani, nikatembea hadi mlangoni, nikafungua na kutokea sebuleni ambapo nilikuta watu saba, akiwemo mke wangu, wakiendelea kukemea.


Mchungaji aliponiona, akawasimamisha wenzake. Kukawa kimya, lakini ghafla wakaanza tena. Safari hii mchungaji ikawa, mkono mmoja ameshika Biblia mwingine anautumia kunielekezea mimi huku akiendelea kukemea.


Ghafla, nilishikwa mkono kwa nyuma na kuvutwa. Aliyenivuta sikumwona, lakini nikajua ni wale jamaa zangu. Nia ya kunivuta ilikuwa kunirudisha chumbani. Lakini wakati naingia, mchungaji aliamuru wenzake na yeye wanifuate chumbani.


Sasa nyumba yote ikawa ni maombi tu. Kukemea kwa sana hali iliyonizidishia maumivu makali sana ya kuchomwa moto mwilini. Nilianza kujinyonganyonga kuashiria kwamba, maumivu ya moto niliyasikia kwa undani zaidi kuliko awali.


Nikawaona wale jamaa zangu nao wamejitokeza. Sasa ikawa wamejitokeza laivu!!
Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 16


Sasa nyumba yote ikawa ni maombi tu. Kukemea kwa sana hali iliyonizidishia maumivu makali sana ya kuchomwa moto mwilini. Nilianza kujinyonganyonga kuashiria kwamba, maumivu ya moto niliyasikia kwa undani zaidi kuliko awali.
Nikawaona wale jamaa zangu nao wamejitokeza. Sasa ikawa wamejitokeza laivu!!
SASA ENDELEA…


Lakini kwa maombi mazito ya mchungaji, wakapotea ghafla, kukawa kimya. Nilikaa kitandani nikiwa natweta kwa wasiwasi na hofu kuu!


Cha kushangaza, mchungaji palepale akawaambia wenzake waondoke kwenda kanisani. Alikuwa akitokwa na jasho jingi sana na mimi ninavyofahamu, mtu akiomba sana hasa pale anapopambana na pepo wachafu, jasho lazima.


Hapa niseme kidogo. wengi wanadhani kusali ni jambo la kawaida. Si kweli. Kusali ni mapambano tena mapambano makubwa sana. Mtu anaposali, pembeni yake au mbele yake kunakuwa na pepo wachafu ambao wanamrushia ‘mishale’ ili anayeomba achoke.
Mfano, umewahi kusali huku umefumbua macho. Kinachotokea ni kwamba, pepo


chafu anakufuata na kukuingia kimawazo. Si kimwili, kimawazo. Matokeo yake sasa, ukiona fagio chini huku unasali unawaza; ‘hili fagio karibu linaisha, itabidi ninunue jingine.’ Ukiona kapeti chini unawaza; ‘kapeti langu limechakaa sana, si sawasawa na lile la kwa mama Anna, lake jipya.’


Au utakuta mtu anaomba amesimama, akifumbua macho kuangalia ukuta, anajiwa na mawazo; ‘huu ukuta sasa ubadilishwe rangi, iwe ya bluu ya bahari. Rangi hii imepauka sana lakini nayo imekaa tangu mwaka juzi.’


Kwa mawazo haya, huwezi kusali sawasawa. Na mawazo hayo yote huwajia watu wanapokuwa kwenye maombi kwa lengo la kuvuruga mtiririko wa sala.
Basi, wote waliondoka, akabaki mke wangu tu. Tukawa tunatazamana bila kusema lolote. Mwili wangu ulikuwa umelegea kwa kuchoka huku nikiwa nawaza kupanda kitandani kulala.


“Hivi mume wangu kwani unanificha nini mimi?” mke wangu aliniuliza.
“Kwani nakuficha nini?”
“Wewe una mkataba na majini?”
“Sema sina mkataba wa majini,” mwanamke mmoja, mweupe alisimama ukutani ghafla na kuniambia maneno hayo.


“Sina mkataba na majini,” nilisema.
“Sasa ni kwa nini walikuja kukupigania kama huna mkataba nao?”
“Muulize walikuja kukupigania saa ngapi?” yule mwanamke alinielekeza.


“Walikuja kunipigania saa ngapi na wapi?” nilimjibu na kuongezea langu la na wapi.
Mke wangu hakunijibu, aliendelea kuniangalia kwa muda kisha akatingisha kichwa. Mimi nikamwangalia yule mwanamke, akaachia tabasamu na kusema:
“Mapambano ni makali sana, mkeo ameamua kutumaliza lakini sisi tumeweka kikao kwa ajili yake na kuamua kumuua mapema ili asije akaleta madhara.


“Tumekuwa tukimvumilia sana kwa ajili yako lakini sasa imefikia tamati. Lazima mkeo afe ili wewe ufanye kazi kwa usahihi mkubwa na kunufaika. Suala la namna gani utaishi tunajua sisi.


“Njia tutakayoitumia kumuua mke wako ni kwa kumkaba koo mara moja na kuvunja mishipa ya shingoni. Ili tumpe maumivu makali tunasubiri akiwa amekwenda kuchota maji. Atavunjwa shingo akiwa na ndoo kichwani.


“Kuhusu suala la msiba, mkeo akishafariki dunia hutatakiwa kulia ili kulinda uhai wako. Hutakiwi kuweka wazi huu mkakati. Hutakiwi kuweka matanga kwa siku kadhaa hapa nyumbani kwako. Ukishazika, weka wazi msimamo wako kwamba hakutakuwa na matanga na msiba utakuwa umekwisha.”


Alipomaliza maelezo au maagizo hayo, yule mwanamke alipotea ghafla mbele ya macho yangu! Nilifikicha macho ili kuangalia vizuri.
“Lakini kama hutaki kuniambia kilicho kwenye siri yako sawa,” alisema mke wangu. Akapanda kitandani kulala na mimi nikapanda kitandani kulala.


Nilikosa usingizi. Muda mwingi nilikuwa namfikiria mke wangu, eti kwamba majini watamuua. Tena watamuua kwa kumkaba koo na kisha kumvunja mishipa ya shingo. Na eti watamvizia akiwa ana ndoo ya maji kichwani ili kumuongezea maumivu! Iliniuma sana. Yale maneno ya yule jini mwanamke yalijirudia kichwani mwangu…


“Njia tutakayoitumia kumuua mke wako ni kwa kumkaba koo mara moja na kuvunja mishipa ya shingoni. Ili tumpe maumivu makali tunasubiri akiwa amekwenda kuchota maji. Atavunjwa shingo akiwa na ndoo kichwani.


“Kuhusu suala la msiba, mkeo akishafariki dunia hutatakiwa kulia ili kulinda uhai wako. Hutakiwi kuweka wazi huu mkakati…”
***
Kulikucha kwa tabutabu, mke wangu akatangulia kutoka kitandani huku akisema anakwenda kuchota maji. Niliogopa sana. Nilipotaka kumwambia asiende yule jini mwanamke akatokea ghafla.


“Hutakiwi kuweka wazi huu mkakati. Zingatia hilo kwa ajili ya usalama wa uhai wako. Hii ni amri, wala si maoni yetu,” alisema na kufutika.
Nilibaki namwangalia mke wangu, naye akasema:
“Kuanzia leo nimeamua kufunga na kuomba. Itakuwa kwa muda wa siku tatu.”
Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 17


“Hutakiwi kuweka wazi huu mkakati. Zingatia hilo kwa ajili ya usalama wa uhai wake. Na hii ni amri, wala si maoni yetu,” alisema akafutika.


Nilibaki namwangalia mke wangu, naye akasema:
“Kuanzia leo nimeamua kufunga na kuomba. Itakuwa kwa muda wa siku tatu.”
SASA ENDELEA…


Nilishangaa sana. Sikujua ni kitu gani kilimfanya mke wangu asubuhi hiyo aamke na kusema anaamua kufunga na kuomba tena akiwa anajiandaa kwenda kuchota maji bombani.
“We hufungi?” aliniuliza.


Nikamkatalia kwa kutingisha kichwa. Lakini kabla hajaondoka kwenda kuchota maji, alipiga magoti pembeni ya kitanda na kuanza kusali. Nilimsikia akimwomba Mungu ampe neema ya kuweza kufunga na kuomba kwani kwa nguvu zake kama binadamu hawezi.


Pia alisema ameamua kufunga na kuomba ili magumu yaondoke katika familia maana ahadi ya Mungu inasema mambo magumu hayawezi kutoka isipokuwa kwa kufunga na kuomba.
Baada ya hapo, alibeba ndoo yake na kuondoka huku akiimba nyimbo za Injili. Huku nyuma, wakatokea majini wanawake watatu mbele yangu, wakasimama kisha mmoja wao akasema:


“Ee! Tumesikia mkakati wa mke wako. Tunajua amepewa maono. Lakini hayatamsaidia kitu maana sisi tuna wewe. Tumekuja hapa ili kukupa maelekezo na lazima uyafuate.


“Hakikisha kabla mkeo hajarudi kutoka kwenye maji unafunga mlango ili akija asiingie moja kwa moja mpaka abishe hodi. Kitendo cha kubisha hodi kitamuondolea nguvu ya funga hivyo kwetu atakuwa mwepesi tu kumtendea tulichokwambia,” alisema mmoja wao.


Nilikubali kwa kutingisha kichwa, wakafutika palepale ghafla. Nilibaki natetemeka.
Nilisimama kwenda kufunga mlango kwa lengo la kumfanya mke wangu akija ashindwe kuingia mpaka agonge mlango au abishe hodi kama nilivyoagizwa na wale majini.


Baada ya kufunga mlango nikarudi chumbani, kitandani na kujilaza. Nilijua siku ya mke wangu kufariki dunia ilishafika. Ni dakika tu zilikuwa zikisubiriwa.
Mara, nilimsikia mke wangu akiimba nyimbo zake za Injili huku akiwa ameshaingia ndani. Nilitoka mbio ili kumuuliza amewezaje kuingia wakati nilifunga mlango.


“He! Ulipotoka tu nilifunga mlango, we umeingiaje?” nilimuuliza.
“Sijakuta mlango umefungwa, nimeukuta kama nilivyouacha,” alisema mke wangu huku akionekana kunishangaa sana.


Sikuwa na la kusema. Sasa ningesema nini wakati mtu ameshaingia. Nilijihakikishia mimi mwenyewe kwamba, mlango niliufunga bila wasiwasi wowote ule. Lakini aliingiaje?


Nikasikia sauti ndani ya moyo wangu ikisema: “Unacheza na nguvu za Mungu siyo? Unaulizaje mkeo aliingiaje ndani wakati ulifunga mlango huku ukijua amekutangazia ameanza kufunga?”
Niliogopa, nikazidi kuogopa. Nilichoamini ni kwamba, wale majini wangekuja wakati wowote ule na kunipa maelekezo mengine.


Mke wangu baada ya kutua ndoo ya maji tu, akaingia chumbani. Akaanza kuomba sana huku akipaza sauti. Palepale nilianza kusikia nachomwa moto mwili mzima, kuanzia kichwani hadi kwenye nyayo! Nikajua kumekucha.


Nilikimbilia sebuleni huku nikijishikashika sehemu mbalimbali za mwili kwa kuamini naweza kupunguza ile hali ya kuungua moto! Kweli, kiasi fulani nilijisikia nafuu kuliko nilivyokuwa chumbani.
Nilikaa sebuleni kwa matumaini kwamba, lazima wale majini wangetokea kunipa msaada au kutoa maelekezo mengine lakini wapi! Mke wangu alimaliza kusali, akatoka, akachukua ndoo na kwenda tena kwenye maji.


Sasa nilikuwa najiuliza wale majini watakujaje maana hakuna hata siku moja mimi nikawa na shida halafu nikawafuata huwa wanakuja wenyewe.


Nilisimama na kuingia chumbani, roho ikawa hainipi, nikarudi sebuleni, pia nikaona hakufai nikatoka nje kabisa. Nje nilisimama kama ninayeshangaa jambo lakini ghafla nikasikia sauti za wanawake ndani wakiniita, nikajua wamekuja sasa, nikaenda ndani haraka sana.


Niliwakuta sebuleni watatu, walisimama wakiwa wamechukia sana tena sana. Walinikazia macho pima. Nikajua mimi nimefanya kosa katika maelekezo yao ya awali kuhusu kufunga mlango. Mmoja wao akasema:


“Mke wako anajifanya ana uwezo mkubwa sana kuliko sisi! Ametendewa haki na kuukuta mlango uko wazi. Lakini sisi tunakuhakikishia mpaka inafika saa sita mchana wa leo, hatakuwa hai tena.”
“Sawa,” nilijibu kwa mkato. Mwingine akasema:


“Tunafuatilia hatua kwa hatua kuhusu mke wako. Usije ukaungana naye na wewe ukawa safari moja ya kuiaga dunia. Kuwa mvumilivu kwa litakalotokea. Hatukutaka kumfanyia hivyo mke wako lakini ameonekana kuwa kikwazo kwenye kazi zetu.”


Nilikubali kwa kutingisha kichwa kwamba nimewaelewa vizuri sana. Mara, mlangoni tukasikia sauti ya mke wangu akiendelea kuimba zile nyimbo za Injili, wale wanawake majini wakafutika haraka sana mbele ya macho yangu na kuniacha mimi natetemeka kwa wasiwasi na woga.


Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 18


Nilikubali kwa kutingisha kichwa kwamba nimewaelewa vizuri sana. Mara, mlangoni tukasikia sauti ya mke wangu akiendelea kuimba zile nyimbo za Injili, wale wanawake majini wakafutika haraka sana mbele ya macho yangu na kuniacha mimi natetemeka kwa wasiwasi na woga.


SASA ENDELEA MWENYEWE…


Mke Wangu aliingia ndani na ndoo yake ya maji huku akiwa hana wasiwasi wowote. Nilikaa kwa kuogopa. Mwili ulitetemeka wenyewe.


“Bado unachota maji?” aliniuliza mke wangu.


“Ndiyo, mpaka nifikishe ndoo kumi,” alinijibu kwa sauti iliyojaa ujasiri wa hali ya juu.


Nilijiuliza wale majini kabla ya kukimbia walitaka kuniambia nini zaidi maana walianza kwa kumlaumu mke wangu kwamba amepata bahati, amesaidiwa. Nikawa najiuliza sana.


Lakini pia nikajiuliza je, ni sahihi kwa mimi kuendelea kuwaamini majini huku viashiria vya wazi kwamba, hawana uwezo wa kumzidi Muumba vikiwa wazi?


“Mbona siku za mwanzo waliweza kujitokeza mbele ya mke wangu na kuongea na mimi? Kwa nini leo wasifanye vilevile ili nipate ujumbe kwa njia sahihi?” nilijiuliza mwenyewe.


Mke wangu alipotua ndoo ile, akachukua nyingine na kutoka. Kawaida yake akishajaza ndoo saba, baada ya hapo anajaza pipa kubwa. Nilimpa pole wakati akitoka.


Ile anatoka tu, wale majini wakarudi na kunifokea sana. Wakaniambia kwamba mawazo yangu kuwa wao hawana nguvu si sahihi.


“Sisi hatujashindwa kutokea huku mkeo akiwepo ila sema tu kwa sababu tunamuweka kwenye eneo ambalo asiwe na shaka tena kwamba kuna kitu tofauti.


“Tulipokuwa tunakutokea na yeye akiwepo aliweza kubaini mengi sana hasa kwa vile alikuwa akiona upepo unatikisa nyumba.


“Sasa kwa sababu umeamua kutokutuamini tunaondoka na wewe na utaishi tunapotaka sisi na utafanya kazi tunayotaka sisi,” alisema jini mmoja kwa sauti iliyojaa hasira.


Palepale mmoja wao akanifuata, akanishika kichwani, nikahisi kuchanganyikiwa na kupoteza uwezo wa kuona. Nilipokuja kufumbua macho, nilikuwa kwenye chumba chenye watu kibao, kama hamsini hivi na kila mmoja alikuwa bize na mambo yake.


“Kaa hapo,” sauti iliniamuru.


Nilikaa haraka sana. Nikasikia sauti nyingine ikisema:


“Utapewa kazi maalum muda si mrefu.”


“Sawa,” nilikubali huku nikitetemeka. Nilijua yote yale yalikuwa yakinipata kwa sababu ya kuwaza kwangu. “Kumbe majini wanaweza kujua tunawaza nini?” Nilijiuliza mwenyewe kisha nikayafuta haraka sana mawazo hayo ili nisije nikapewa adhabu nyingine.


“Simameni,” sauti moja yenye kishindo kikuu iliamuru.


Tulisimama wote ndipo nilipobaini kuwa, hatukuwa kiasi cha hamsini. Tulizidi hata watu mia mbili. Tulibanana sana japokuwa tulikuwa kwenye chumba kikubwa kupita kawaida.


“Mtatoka nje hapo, mtajua mnakwenda wapi na kufanya nini!” ilisema sauti.


Palepale tukaanza kutoka. Mzee mmoja akaniuliza:


“Hivi hapa ni wapi?”


“Mimi ni kama wewe. Nahitaji kujulishwa.”


“Hapa ni sehemu ambayo watu wa duniani waliochukuliwa na majini wanakutana na kufindishwa mbinu za kuumaliza ulimwengu kwa njia ya mauji, magonjwa mbalimbali au vifo vya kutatanisha,” alisema mtu mmoja, naamini ni jini kwani alitutokea mbele yetu ghafla huku akitembea kuelekea mlango mkuu wa kutokea.


Akaendeela kusema akinikazia macho mimi:


“Mfano wewe, kule Mlandege unakoishi ni salama lakini baadhi ya maeneo si salama. Iringa nayo imo kwenye orodha ya miji ambayo ina makao ya majini wakubwa. Ogopa sana pale njia panda ya kwenda Tosamaganga. Ogopa sana pale nje ya Uwanja wa Sabasaba. Ogopa sana pale Milima ya Gangilonga kwani ndipo penye lango kuu.


“Mji ambao kwa sasa tunapambana nao kwa sababu wakazi wake wanatusumbua ni Mkimbizi. Anga la mji ule ni zito kwetu na tunapambana kila siku.


“Ndiyo maana kuna makanisa yanaanzishwa halafu yanadumaa. Mkimbizi tunafanya kazi kubwa ya kuhamisha watu ikibidi hata nje ya mkoa ili wabaki wenye kuchangamana.”


Aliposema Gangilonga ndiko kwenye lango kuu, palepale nikakumbuka kwamba, nilipokwenda ujinini siku zile, niliporudi nilifika mjini nikitokea kwenye milima hiyo. Kumbe ni ya lango kuu la kuzimu!


Lakini ukiachana na hayo, lingine ni hayo maeneo ambayo yalitajwa kuwa ni hatari. Niliifikiria njia panda ya kwenda Tosamaganga, nikaufikiria mji wa Mkimbizi kwamba una wakazi wanaowasumbua majini. Lakini hapa sikuwa makini kujua hasa wanasumbua kivipi!


Ghafla mawazo yaliyonijia ni ya mke wangu. Kwamba, kule alipo, akirudi kutoka kwenye maji na kutonikuta, atajua nimekwenda wapi na kufanya nini.


“Kila mmoja atege sikio sasa ili tuelekezane,” ile sauti ilisema. Nikashangaa kwamba kumbe wote tulishatoka nje.


Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 19


Lakini ukiachana na hayo, lingine ni hayo maeneo ambayo yalitajwa kuwa ni hatari. Niliifikiria njia panda ya kwenda Tosamaganga, nikaufikiria mji wa Mkimbizi kwamba una wakazi wanaowasumbua majini. Lakini hapa sikuwa makini kujua hasa wanasumbua kivipi!


Ghafla mawazo yaliyonijia ni ya mke wangu. Kwamba, kule alipo, akirudi kutoka kwenye maji na kutonikuta, atajua nimekwenda wapi na kufanya nini.
“Kila mmoja atege sikio sasa ili tuelekezane,” ile sauti ilisema. Nikashangaa kwamba kumbe wote tulishatoka nje. SASA ENDELEA MWENYEWE…


Maelekezo yalitoka kwamba, kila mmoja alipo atajikuta yupo kwenye kundi linalomhusu na kwamba, huko atapatiwa maelekezo na msisitizo na baada ya hapo, kila mmoja ataoneshwa sehemu ya kuishi. Hiyo sauti ilisisitiza hivi:


“Napenda kuwaambia wazi kwamba tuna vita kubwa lakini ni lazima tushinde. Kuwaachia wanadamu wakamcha Mungu wao, kwetu sisi ni hatari sana. Dunia ipo katika nyakati ya haraka kuelekea kwenye hitimisho lake, lazima tupate wengi.”


Sauti hiyo ilipoacha kusema, mimi nikajikuta nimo ndani ya chumba kimoja chenye giza nene. Lakini kelele ziliashiria kwamba, mle ndani sikuwa peke yangu.


Lakini wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa ni je, ni akina nani ambao nilikuwanao ndani ya kile chumba? Maana hewa ilikuwa nzito sana ndiyo maana nasema kwamba, nilikuwa ndani ya chumba.
Mbaya zaidi, kelele zenyewe zilikuwa hazijulikani ni za nini? Yaani sauti zilizokuwa zinasikika, hazikuweza kunipa nafasi ya kujua kilichokuwa kikiongelewa!


Nilisikia kama watu wakisema: “Poleke…pikapika…kuwekokuweko…jumbi ilo…jumbi ilo…poleke pikapika…kuwepokuweko…jumbi ilo…jumbi ilo.”


Nilitega sikio kwa umakini sana, mara kukawa kimya! Hapo pia nilibaini kuwa, hata kama kweli nilikuwa ndani ya chumba lakini nilikuwa peke yangu. Zile kelele ni za mazingira ya mle ndani tu na hayakutokana na kiumbe chochote kuwemo.


Pia nilijua niko peke yangu baada ya kunyoosha mkono wangu wa kulia upande wa kulia, mbele na nyuma na wa kushoto vivyohivyo bila kushika kitu chochote kile.
“Upo peke yako lakini upo salama sana,” sauti nzito na nene ilisema huku ikiacha mtetemesho mkubwa.
“Sawa,” nilijibu.


“Wewe umechaguliwa kwenye kitengo cha kulisha majini kile chakula chao maalum,” ile sauti ilirudia kusema.
Nilishtuka kidogo kusikia hivyo kwani sikujua maana ya kitengo cha chakula cha majini tena kile maalum ndiyo chakula gani!


Utakuwa unahusika moja kwa moja na kuleta chakula hicho huku ukiwa kama wakala mkuu. Usichangamane na wengine. Wewe eneo lako litakuwa kwa wanawake wenye mimba tu,” ilisema hiyo sauti.


Baada ya kumaliza kusema maneno hayo, niliambiwa kitakachofuata sasa ni kuelekezwa kwa vitendo na si sauti tena kama awali.
Nilijikuta nipo kwenye chumba chenye wanawake wengi wenye mimba wakilia kwa machozi huku wakionekana kuombeleza na vilio vyao hivyo kwamba waonewe huruma.


Kiumbe mmoja kama binadamu kwa mbali, ila yeye mnene, hana shingo. Kwa maana kwamba, sehemu ya shingo ilijaa na kuwa sanjari na mabega, akiwa na macho ya pembe tatu huku meno yakitoka kwa nje kama ya mnyama ngiri, alikuwa akimfuata mwanamke mmojammoja na kumshika tumboni kisha mwanamke huyo hulia sana na kuanguka chini na kufuatia na damu nyingi kusamba sakafuni.
Alifanya hivyo kwa kila mwanamke mpaka wakaisha wote na walikuwa kama wanawake hamsini mle ndani. Alipomaliza aliingia kwenye chumba kimoja cha pembeni bila kuniangalia.


Baada ya muda, wakatoka viumbe kama yeye, wawili wakiwa wamebeba beseni kubwa lililojaa damu mpaka kumwagika. Wakaliweka chini kisha wakarudi kwenye kile chumba.


Mara, wakatoka viumbe wengine watatu. Wao walikuwa wakubwa zaidi kimaumbile na walivaa tofauti na wale waliotangulia. Walionekana kama ndiyo mabosi wao. Wakaja kusimama pembeni ya lile beseni, wakaangalia kisha wakaondoka na kuingia kwenye chumba kingine upande wa kushoto.
Walipozama tu, wakaja wale watu wawili, wakalichukua lile beseni. Wakaingia nalo kwenye kile chumba walichoingia wale niliosema ni kama viongozi wao kwa jinsi walivyovaa.


Kufumba na kufumbua na mimi nilikuwa kwenye kile chumba walichoingia wale viongozi na wale wenye beseni lenye damu. Lakini wale waliopeleka damu hawakuwepo.


Nilifikia kwa kusimama wima. Nikawaona wale watu wakubwa wakianza kunywa ile damu kwa kutumia vikombe vyekundu ambapo walikuwa wakichota na kupeleka kinywani huku wakicheka sana kuashira kwamba, walichokuwa wakikipeleka kinywani kilikuwa kikiwafurahisha sana.


Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 20


Kusema kweli mimi nilishtuka sana, nikataka kupiga kelele za kuomba msaada lakini nilipokumbuka kwamba pale ni ujinini nikaacha kwani niliamini nisingeweza kupata msaada wowote na zaidi sana huenda ingechangia kifo changu.


“Mwingine.”


Ile sauti iliamuru tena, akaingia mwanamke mmoja ambaye alikuwa akitetemeka. Mlango ulipofungwa tu, tukasikia milio ya risasi. Mingi sana. Kama kuna watu walikuwa na bunduki, basi walizidi hata kumi kutokana na ile milio.


Ilipokoma kusikika, ikaja ile sauti ya kuamuru mtu mwingine aingie, mwanaume aliyekuwa mbele ambaye ilibidi aingie akarudi nyuma ya mtu aliyekuwa nyuma yake.


Sijui mimi niliupata wapi ujasiri nikajikuta nikisema mimi nakwenda. Lengo langu lilikuwa kujua kuna nini kule na je, tunayoyasikia ndiyo yanayofanyika kule ndani?


Niliwapangua watu kwenda mbele ili nikaingie mimi. Lakini kabla sijafika, nilisikia ile sauti ikisema ‘narudia tena, mwingine’.


Nilisukuma mlango, nikazama ndani lakini nilifikia kuanguka chini na kupoteza fahamu.

Niliposhtuka, nilikuwa katikati ya watu chini. Watu wenyewe ni waumini wa kanisani kwa mke wangu. Mke wangu pia alikuwepo na mchungaji wake, wote waliniangalia.


Ilionekana walikuwa wakisali, kujitokeza kwangu ndiko kuliwafanya wanyamaze. Nilipoangalia vizuri nikagundua nipo sebuleni kwangu.


“Pole sana bwana, habari za kuzimu?” aliniambia mchungaji huku akiwa ameshika Biblia.
Sikumjibu, nikainuka na kukaa kwenye kochi. Mchungaji akanisimulia kuwa, baada ya kutoweka nyumbani, mke wangu alimpa taarifa, ikabidi wafunge na kuomba kwa siku tatu na siku hiyo ndiyo ilikuwa ya tatu, wakaamua kuja kumalizia nyumbani kwa maombi mazito.


Mchungaji alisema aliona katika maono nikiwa nasulubiwa katika mikutano ya kuzimu, hivyo alizidisha maombi ili kunifungua katika kifungo hicho.


Niliwashukuru sana wote, hasa mke wangu. Mchungaji akaniambia nipige magoti ili aniongoze sala ya toba. Mpaka leo hii mimi ni muumini mzuri wa kiimani katika kanisa la kiroho analosali mke wangu, lipo mjini Iringa.


MWISHO.
 

Similar Discussions

4 Reactions
Reply
Back
Top Bottom