Mkasa Wa Kweli : Kuzimu Na Duniani

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,425
SEHEMU YA KWANZA


“KAMA kweli kuna malipo ya ubaya na uovu basi mimi nililipwa kwa yale ya uovu. Lakini namshukuru sana Mungu kwani alijua dhamira yangu ikafika mahali akakataa hivyo akaamua kuniokoa mwenyewe kutoka kwenye mateso ambayo mimi nilijua ni ufahari,” anasimulia Mussa Kibwana kuhusu mkasa wake wa kutisha wa namna alivyokuwa akitumika kuchukua roho za watu na kuzipeleka kwenye mateso.


Ilikuwa Jumapili moja, miaka ya 90, saa kumi jioni nikiwa natoka kazini, Ruaha, Iringa narudi nyumbani eneo moja linaitwa Mlandege.


Kwa miaka ile usafiri mkubwa wa mji wa Iringa ulikuwa ni mabasi ya kutoka Iringa mjini kwenda eneo linaitwa Tanangozi, hivyo kwa wafanyakazi wanaofanya kazi Ruaha ili warudi mjini ilikuwa lazima wasubiri usafiri huo kwa muda.


Tofauti na sasa ambapo kuna vibasi vinatoka mjini na kumalizikia Ipogoro au mpaka Kibwabwa.


Basi, mimi siku hiyo niliamua kurudi mjini kwa kupitia njia ya mkato. Njia hii inakatisha kwenye mawe makubwa kutoka Ipogoro hadi eneo linaitwa Kitanzini kisha naingia eneo linaitwa Mshindo na kupanda basi hadi Mlandege.


Nikiwa nimemaliza nusu ya safari, nilikutana na mwanamke mmoja amesimama. Nilijua amechoka kwani kwenda mjini kutoka Ipogoro unapanda mlima. Ni kawaida ya wapandaji wengi kupumzika au kutembea polepole mpaka wanaumaliza mlima huo.


Nilimsalimia mwanamke huyo na kumpa pole kwa safari, akasema hataki pole yangu kwa sababu alikuwa ananisubiri mimi.


Nilishangaa sana kwa vile sikumfahamu au niseme sikuwa namkumbuka mwanamke huyo. Ilibidi nisimame na kumkazia macho kwa maana ya kuitafuta sura yake kama ningeweza kumkumbuka, lakini wapi!


Alivaa gauni la kuishia miguuni lenye mchanganyiko wa rangi mbalimbali za maua. Nikamuuliza:


“Kwani mwenzangu unaitwa nani na unanisubiri kivipi?”


“Mimi naitwa Maua. Nakusubiri maana nimekuona unavyopanda, mimi naogopa kupanda peke yangu,” alisema mwanamke huyo.


Maneno yake niliyaona kama ni ya ulaghai tu, niliamini kuna ambacho kiko nyuma ya hapo. Mlima ule watu ni wengi, japo si sana. lakini kwa muda ule wa saa kumi haikuwa rahisi kutokuwepo kwa watu, kwani mara nyingine hata saa mbili usiku watu wanapanda na kushuka.


Basi, nilimwambia siamini maneno yake kwa vile hakuna kitu ambacho kingemfanya aogope. Tena wakati namkuta, kuna watu wawili walikuwa nyuma yangu na mbele yake niliwaona wanawake watatu wakipanda huku wakizungumza kwa sauti.


Lakini swali jingine ni kwamba, aliposema alikuwa akinisubiri mimi alijuaje kama nipo nyuma yake kwani mlima wenyewe una konakona. Alikosa jibu la moja kwa moja akabaki akisema alikuwa anajua lazima kuna mtu anakuja.


Tulitembea wote, yeye akiwa kushoto kwangu mpaka tukawa tunakaribia kufika. Akaniambia yeye amefika tayari. Nilishangaa kwani tulikuwa hatujatokea kwenye nyumba za wakazi.


Nilimuuliza anakoishi akanionesha kwa mkono upande wa kulia wakati wa kupanda ambako kuna mawe na mitimiti. Kifupi ni kichakani kwa wakati huo.


“Sasa pale unaishi wapi?” nilimuuliza.


“Unataka kuona?”


“Ndiyo.”


Hapo tulikuwa tumesimama, akasema nimwangalie anapokwenda kuingia. Kweli, alitembea kwenye kichaka huku nikiwa namshangaa. Mimi moyoni mwangu niliamini yule mtu alikuwa na mambo mawili, mchawi au hana akili nzuri. Lakini mwonekano wake haukuashiria kwamba hana akili nzuri.


Ghafla nikamwona anaingia kwenye jumba moja kubwa sana. limepakwa rangi nyeupe lote huku sehemu ya madirisha ikizungushwa na rangi nyekundu. Nilifikicha macho ili nione vizuri lakini nikaendelea kuona kichaka kisha kicheko kutoka upande ule.


Si mimi tu, hata ungekuwa wewe ungetoka mbio. Basi mimi nilitoka mbio, tena mbio kama nafukuz wa na simba wakati kumbe niliyoyaona yalifutika machoni pangu. Nikatokezea kwenye sehemu watu wanauza vyakula mbalimbali na ndiyo eneo linaloanza kuitwa Kitanzini.


Baadhi ya watu ambao wao ndiyo walikuwa wakianza kushuka, wakaniuliza kinachonikimbiza, lakini sikuwajibu.


Niliingia mitaani mpaka nikafika Mshindo na kupanda gari hadi Mlandege.


Nilifikia kujitupa kitandani. Mke wangu, akanifuata kutaka kujua kama naumwa kwani siyo kawaida yangu.


“Nilichokiona mke wangu si cha kawaida. Leo ndiyo nimeamini kwamba kuna watu si wazuri.”


“Kwani umeona nini wewe, niambie vizuri.”


Je, unajua nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 03


Nilifika kazini kwa muda uleule wa kawaida. Nilipenda sana kuwashirikisha wafanyakazi wenzangu juu ya tukio lote la jana kwenye ndoto lakini kila nilipofikia hatua ya kutaka kusema, nilikuwa nasita au kujisikia hali ya kupuuzia.


ENDELEA SASA…


Muda wa kazi ulipokwisha, nilijiondoa kazini. Mbele barabarani likatokea gari la Sido, dereva akasimamisha maana tunafahamiana, nikapanda kwa ajili ya kuelekea mjini.


Tulipofika kwenye kona ya barabara ya kwenda mjini Iringa na ile inayonyoosha kwenda Morogoro Dar au niseme ile inayokwenda kitongoji cha Ndiuka, sasa dereva anakata kushoto. Gari lilitoa mlio mmoja wa puu! Dereva akasimama pembeni.


Tulishtuka wote, tukashuka kwenye gari na kwenda mbele kuangalia kuna nini. Dereva alifungua boneti na kuangalia lakini hakubaini kitu. Mpaka hapo, gari halikuwa limezima wala kuonesha dalili kwamba haliwezi kuendelea na safari.


“Jamani, haya ni magari tu. Ni chuma, kwa hiyo na vyuma pia huwa vinachoka,” alisema dereva wakati akiingia kwenye gari. Na sisi wengine pia tukaingia kwa mwongozo wake huo.


Safari ilianza, gari likatembea hadi kufika kwenye kuanza kupanda kilima cha kwenda mjini. Cha ajabu sasa, gari lilipofika usawa wa ile njia ya kufika mjini kwa miguu, likalia tena puu! Safari hii likasimama kabisa kwamba haliwezi kuendelea tena na safari.


Tulishtuka tena wote, dereva akaangalia mbele akasema haoni tatizo. Akarudi ndani na kupiga stati, halikuweka.


Tulianza kuuliza cha kufanya. Dereva akasema sisi kama tunaweza tukatize njia ya kwenye kilima kwenda mjini yeye anasubiri magari mengine ya Sido kwa imani kwamba, atapata msaada wowote ule.


Abiria wengine walikataa kwenda mjini kwa kupanda kilima hicho kasoro mimi tu ambapo niliwadanganya kwamba kwa vile nina safari ya kwenda kitongoji kinaitwa Frelimo halafu pia kitongoji kingine kinaitwa Mkimbizi hivyo lazima niwahi. Wakakubali.


Nilipanda kilima. Lakini nilipofika umbali wa kama mita hamsini tu, gari likawaka. Nilishtuka, kidogo nirudi lakini moyoni nikasema acha waende, pangine mimi ndiyo nina mkosi. Naweza kusema narudi kupanda, mbele kidogo likaharibika tena.


Basi, nilizidi kupanda kilima. Lakini niseme wazi kwamba gari lilipowaka, niliwasikia wakicheka halafu mmoja wa abiria akasema waziwazi; ‘unajua abiria wengine wana mikosi bwana’. Niliumia sana, sikujali.


Mbele yangu alikuwa anashuka mwanaume. Lakini pia nyuma yake kulikuwa kuna mwanamke anamfuata. Walionesha hawakuwa safari moja.


Nilianza kupishana na mwanaum e, akanipa pole ya kazi kwa kabila la Kihehe.


“Makasi.”


“Hale,” nilimjibu tukiwa tumeshapeana migongo. Sasa mbele yangu nilikuwa nakabiliana na yule mwanamke. Yeye alionekana kama anapunguza mwendo kwa mambo mawili. Kwanza, anataka nipite mimi kwanza, kwa sababu sehemu hiyo ilikuwa finyu. Pili, alikuwa akinifahamu, sasa alitaka tusimame wote ili tusalimiane.


Kwa hiyo hali hiyo ilinifanya na mimi nipunguze mwendo mpaka nikasimama kabisa. Tulikutana macho, akatabasamu na kusema:


“Unanikumbuka?”


Nilikunja sura kumfikiria nilimwona wapi na kitu gani kilichotufanya tukutane lakini sikupata jibu.


“Hapana,” nilimkatalia.


“Asubuhi?” aliuliza hivyo tu basi.


“Asubuhi imefanyaje?” nilimuuliza.


“Ulikuwa unatoka pale sijui kwako,” alisema.


Niliinua kichwa chini na juu kama ishara ya kukumbuka alichosema.


“Oohooo! Umeshindaje?”


“Nimeshinda salama. Nakuona unatoka kazini!” alisema.


“Eee. Kumbe unaishi huku Ipogoro?” nilimuuliza nikimkazia macho. Nikabaini kwamba, alikuwa na macho meupe sana kama karatasi na kile kiduara cheusi kilikuwa cheusi sana kama mkaa.


Lakini pia nilibaini kwamba, nyusi zake zilikuwa nyingi kiasi cha urefu wa kama nywele za kichwani zilizopunguzwa.


Nahisi alilijua hilo, kwamba nimebaini kitu usoni mwake maana alikimbiza macho pembeni, akasema:


“Mimi naishi Tagamenda.”


Tagamenda ni eneo lenye kituo cha umeme wa Tanesco. Lakini ni mbali kidogo. Ina maana yeye anashuka mpaka Ipogoro kisha anapanda gari pale.


“Sawa. Mimi pale uliponiona asubuhi ndiyo maeneo ya nyumbani kwangu,” nilimwambia, akasema anajua kama mimi naishi pale.


“He! Kumbe wewe si mgeni wa eneo lile?” nilimuuliza.


“Hapana. Si mwenyeji sana bali kuna mwanaume anaishi pale na tuna kazi naye maalum.”


“Mnaishi naye wapi?” nilimuuliza.


“Pale ulipotoka wewe,” alisema.


Muda wote huo hakukuwa na mtu aliyekuwa akishuka wala kupanda. Na si kawaida.


“Mimi pale ni kwangu, naishi na mke wangu na mabinti zangu watatu, sina mpangaji wala ndugu mwingine wa kiume. Sasa huyo unayemsema wewe ni yupi?” nilimuuliza kwa sauti yenye maswali kibao.


Je, unajua nini kilitokea?
 
SEHEMU YA 06


“Swali zuri sana umeuliza. Tunataka kumaliza utaratibu wa Kimungu huko duniani. Hatuko tayari dunia iwe sehemu salama ya kuishi, ikiwa hivyo watu watamsifu Mungu badala ya kutusifu sisi. Hilo hatuko tayari nalo.”
TAMBAA NAYO MWENYEWE SASA…


“Kwa hiyo?” niliwauliza.


“Unaijua vizuri Iringa?”
“Naijua.”
“Tunataka kukupa kata yako. Utakuwa unashughulikia maeneo ya kuanzia Sabasaba, Kihesa, Mtwivila mpaka Mkimbizi pamoja na maeneo yake ya ndani. Maeneo ambayo sijakutajia yana watu wake.


“Kazi yako kubwa itakuwa kuhakikisha unavuruga mfumo wa dawa za binadamu. Lengo letu kubwa zisifanye kazi kwenye mwili kama ilivyokusudiwa. Lakini pia utatakiwa kuhakikisha unatibua mfumo wa amani uliopo.
“Wewe ndiye utakayesimamia ulaji hovyo wa chakula kwa lengo la kuiharibu miili. Yaani binadamu wa maeneo hayo wawe na mfumo mbovu wa ulaji.”


Nahisi walishaniteka kiakili kwani hapo sasa na mimi nilikuwa nakwenda tu bila kukataa wala kuuliza itakuaje mpaka alipomaliza kusema ndiyo akaniuliza kama nina maswali.
“Sina. Labda tu nataka kujua namna nitakavyofanya hiyo kazi nitakuwa naishi wapi?”
“Nyumbani kwako palepale Mlandege.”


“Kwa nini msinipange Kata ya Mlandege?”
“Ina mtu kama nilivyokwambia.”
Nilifurahi sana kusikia nitakuwa nakaa nyumbani kwangu. Kama wangeniambia nitakuwa nakaa kwao katika makazi yale ambayo niliamini ni ujinini.


Jambo moja ambalo kama naliamini ni kwamba, mpaka nafikia hatua ya kuwa mtulivu na kuwasikiliza hata mimi sikuwa mimi. Tayari nilikuwa na tabia kama zao.
“Haya sasa simama ili uingie ndani kwenye chumba maalum kwa ajili ya kusimikwa ili kufanya kazi na sisi,” alisema yuleyule mmoja kati ya wale watatu.


“Nina swali lingine,” nilisema nikiwa sijasimama. Wao walishasimama, hivyo wakakaa kama wanyenyekevu.
“Mimi nitafaidika na nini?”
“Unataka ufaidike na nini?”
“Mimi nataka kujengewa nyumba kubwa nzuri ya kuishi na familia yangu. pia nataka kuwa mfugaji mkubwa lakini sina mtaji.”


“Kama shilingi ngapi?” aliniuliza mmoja wao ambaye si yule wa kwanza aliyekuwa akizungumza na mimi.
Niliwaza haraharaka kisha nikaropoka.
“Shilingi milioni kumi na tano.”


Palepale, yule aliyeniuliza aliinua mkono wake wa kushoto juu. Ukaganda kwa dakika kama moja. Kufumba na kufumbua, mkononi mwake kukawa na mfuko mkubwa kama wa rambo lakini wenyewe mgumu sana. mweupe!
Akanitupia mapajani mwangu. Nilipoangalia ndani nikakutana na noti mpya tupu! Tena zilitoa hadi harufu ya pesa.
“Mnazipata wapi hizi pesa wakati nyie huku hamna viwanda?” niliwauliza.


Waliangaliana kisha mmoja wao akaja na kunishika mkono akanisimamisha. Alianza kutembea na mimi na kuniambia sasa napelekwa kwenye chumba maalum cha kuapishwa na swali langu la wanapata wapi pesa walilipuuza.
Alifungua mlango mmoja, akaingia ndani na mimi nikaingia. Mle ndani mlikuwa na mwanamke au naweza kusema mrembo. Ni mrembo kwa namna alivyokuwa amevaa, sura na rangi yake ya ngozi. Tulikutanisha sura, akaachia tabasamu na kunikaribisha.


“Huyu ana safari ya kwenda kusimikwa. Lakini kabla ya kwenda kule namba 666, hebu msimulie kuhusu maisha yetu na yao duniani maana ameuliza tunapata wapi pesa?” alisema yule mwanamke huku akitoka.
Ni wanawake tupu lakini cha ajabu mambo yao yote yalionesha wanajiamini kupita maelezo. Yaani sijamwona hata mmoja mwenye uso wa wasiwasi wala wa kukata tamaa.


“Karibu ukae,” yule dada alinikaribisha. Akaniuliza:
“Wewe ni mwanamke au mwanaume?”
Nilimshangaa sana.
“Ina maana hata ndevu zangu huzioni?” nilimjibu kwa swali.


“Mimi sijawahi kuona mwanamke wala mwanaume. Ila wote najua wapo. Kuna wengine nimewasaidia bila kujua ni wanawake au wanaume mpaka waliponiambia wenyewe.”
“Haya! Mimi ni mwanaume,” nilisema.
Palepale alisimama na kuzunguka kiti, akaja kunikumbatia na kunibusu huku akilazimisha ulimi wake kuingia kwenye kinywa changu.


“Kuna nini kwani?” nilimuuliza kwa sauti ya wasiwasi.
“Jamni wakija wanaume huku kidogo na mimi naridhika. Wenzangu huwa wanafaidi kidogo maana mara nyingi huwa wanakuja kule duniani,” alisema yule jini mrembo.


“Kwa hiyo unataka nini?” nilimuuliza huku nikiwa nampangua kutoka mwilini mwangu.
“Penzi jamani!” alisema huku akinivutia kwenye kiti chake.
“Kubali kulala na mimi nitakupa siri kubwa ya huku na hutadhurika. Lakini ukikataa lazima madhara yatakupata,” alisema huku akiwa amenikumbatia upya.


Je, unajua nini kilitokea?
 
SEHEMU YA 07


“Kubali kulala na mimi nitakupa siri kubwa ya huku na hutadhurika. Lakini ukikataa lazima madhara yatakupata,” alisema huku akiwa amenikumbatia upya.


SASA ENDELEA…


Nilimuuliza nifanye nini na yeye wakati anajua kwamba kuna mtu ameniingiza kwake. Je, akiniona itakuaje?


“Hilo niachie mimi. Kuna chumba changu hakuna anayeingia zaidi ya mimi mwenyewe,” alisema yule msichana akionekana kuwa mrembo zaidi ya wale wengine. Hata kwa umri, yeye alionekana ni mdogo kwao. Kwa hiyo, angewezaje kunitunzia uhai wangu!


“Nadhani una wasiwasi na mimi, siyo?” aliniuliza.


“Sana.”


“Kuhusu nini hasa? Labda naweza kukusaidia.”


“Umesema kwamba kama nahitaji usalama wangu nilale na wewe ili wasinidhuru. Ina maana kuna mpango wa kunidhuru?”


“Siwezi kusema kama mpango huo upo au la! Ila nimekwambia lala na mimi ili nikueleze mengi zaidi. Kama hutaki basi tuendelee, nikuelekeze mambo fulani kuhusu duniani.”


Sasa hapo nikahisi kwamba kama kweli kuna mpango wa kunidhuru utaendelea. Kwa hiyo ikabidi nikubaliane naye ingawa pia niliwaza kuwa, huenda ilikuwa ni mtego wake wa kutaka kufanya mapenzi na mimi lakini asinisaidie lolote.


“Hebu tujadili kwanza la mwanzo,” nilisema.


“Lipi?”


“Kulala na wewe ili nisidhurike.”


“Lile lilishapita, basi tena. Kama mpango wa kukudhuru upo upo tu. Huna jinsi. Ilitakiwa palepale useme moja. Ndivyo tulivyoumbwa sisi. Tabia zetu si kama zenu kule duniani.”


Nilishindwa cha kufanya, ikabidi nitulie tu ili nione kinachoedelea. Akaendelea:


Haya sasa, mimi niko na wewe hapa. Tunachotaka sisi huku ni kuifanya dunia kuwa sehemu ya sisi. Wanadamu waishi kama wanadamu lakini maisha yenu yawe chini ya sisi.


Ukweli ni kwamba, dunia ina viumbe wanaonekana lakini pia wapo hao viumbe wakiwa hawaonekani. Wasioonekana ni wengi zaidi kuliko wanaoonekana.


Nilishtuka sana kusikia hivyo, kwamba kuna viumbe wanaoonekana na wasioonekana. Na kwamba wasioonekana ni wengi kuliko wanaoonekana. Mimi hilo nililikataa moyoni kwamba hakuna kitu kama hicho.


Hata kama hukubaliani na mimi lakini huo ndiyo ukweli. Sasa nakusimulia maisha yetu kule duniani. Kwa sasa tupo duniani kwa wingi wetu tukitenda kazi. Wenzetu wanaoishi kule hawana mchezo. Kwa bahati njema sana tumekuwa tukipata urahisi wa kuishi kule.


Imefika hatua tumejenga familia na zinaendelea kuishi. Nataka kukupa mfano mmoja. Kama maeneo unayoishi wewe kuna familia ambayo haina ushirikiano wowote na majirani, wao ni wao. Tambua hao ni sehemu ya sisi bila kujali ni weusi au weupe.


Aliposema hivyo nikakumbuka kwamba, maeneo ninayoishi kuna bwana mmoja anatambulika kwa jina la Myuropu! Huyu bwana Myuropu tulimpa jina kutokana na maisha yake yalivyo.


Ni yeye na familia yake tu, hakuna mtu mwingine. Ana mke na watoto wawili, basi. Hana cha hausigeli wala ndugu. Haendi kwenye misiba ya majirani zake wala hashiriki chochote na majirani hao.


Tumekuwa tukimsema kwamba, siku akifiwa na sisi hatutatokea kwenye msiba wake, akiumwa hatutakwenda kumjulia hali. Lakini hatujawahi kusikia kafiwa wala anaumwa, si yeye, si familia yake.


Asubuhi, mchana, jioni familia ipo ndani. Mara mojamoja sana kuiona inatoka kutembea kwa miguu. Hajulikani anafanya kazi gani wala anapataje pesa za kuendeshea maisha yake. Kwa staili hiyo ya maisha ndiyo maana akapewa jina la Myuropu.


Myuropu maana yake m-Ulaya. Yaani Mzungu. Tumezoea Wazungu ndiyo wana maisha ya wa nyumba ya pili asimjue wa nyumba ya tatu.


Basi, nikaanza kuhisi kwamba huenda Myuropu naye ni miongoni mwa viumbe vilivyoamua kuja kuishi duniani. Ila sasa yule mrembo akanikatisha na kuniambia kitu kingine ambacho kilinitoa kwenye fikra zangu za awali.


Alisema: Wale wanaoishi duniani wako kama nyie. Wanaugua kama nyie na wanakwenda hospitali zenu. Mnapanga nao foleni kama kawaida ili kumwona daktari.


Nilimkatisha kwa swali: Kwa hiyo hapo ina maana kwamba unazungumzia majini sasa?


Akanijibu: Ndiyo haswaa! Nazungumzia sisi mnaotuita majini.


Akaendelea: Si hivyo tu. Kwa sasa wameenea mpaka imefika mahali wanafanya kazi za kijamii hivyo wanapanda mabasi ya usafiri wa abiria kama binadamu wengine. Hata wewe hapo kule Mlandege unakoishi, umeshawahi kupanda basi ukaa siti moja na jini.


Nilishtuka sana kusikia kauli hiyo. Sikuamini. Ikabidi nivute kumbukumbu nyuma kama nimewahi kupanda basi halafu nikakaa na mtu ambaye nilimtilia shaka, nikajiridhisha kwamba hakuna!


Akaendelea: Sina maana kwamba lazima umkumbuke mtu uliyewahi kukaa naye siti moja. Inawezekana hayupo unayemkumbuka lakini nakuhakikishia yupo uliyewahi kukaa naye. Je, hujawahi kupenda basi halafu ukakaa na mwanamke mmoja akawa anapiga chafya sana mpaka ukawa unakereka?


Aliposema hivyo tu nikalikumbuka hilo tukio. Niliwahi kupanda basi Kihesa kwenda Miyomboni. Ni kweli, kuna mama mmoja nilikaa naye akapiga chafya mara nyingi sana mpaka nikasikia kero, kidogo nimwambie.


Nikamjibu: Ni kweli, naikumbuka siku hiyo. Wewe umejuaje lakini?”


“Kwani unataka nikwambie mambo zaidi ya hapa?” aliniuliza huku akiwa amenitumbulia macho mpaka nikaanza kuogopa.


Je, unajua nini kilitokea?
 
SEHEMU YA 08


Nilibaini pia kwamba, nilikuwa nimetokea kwenye nyumba za eneo hilo ambazo zipo jirani na milima. Hivyo nilitembea kwa mwendo wa kuchoka mpaka nikafika eneo la Shule ya Msingi Gangilonga.


SASA ENDELEA MWENYEWE…


Nikatoka hapo tena nikatembea hadi kwenda kutokea kituo cha daladala cha kwenda mjini lakini mimi nilipitiliza hadi Mlandege.


Nilifika nyumbani, nikakaribishwa na mke wangu huku akinipa pole na kazi za siku hiyo. Nilishangaa sana kugundua kuwa, hakuwa akijua lolote kuhusu mimi. Hakujua yaliyonipata.


“Mke wangu unaniona nipo kawaida?” nilimuuliza, akacheka na kujibu:


“Kwani umebadilika nini mume wangu?”


“Je, nikisema natoka mbali sana?”


“Mbali ahera au?”


“Mbali ni ahera tu?” nilimuuliza.


“Na kuzimu labda.”


Nilishtuka kumsikia akijibu hivyo, nikanyamaza na kuanza mazungumzo mengine mbali na hayo. Lakini ghafla upepo mkali sana ukavuma mle ndani kwangu, nikawa na wasiwasi mkubwa kwani iliashiria kwamba, upepo ule ungeweza kuanua hata paa la nyumba kwa jinsi ulivyokuwa mkali.


“Ni nini hii hali?” aliniuliza mke wangu, sikumjibu kitu. Sikumjibu kwa sababu mimi mwenyewe nilihisi ni upepo uliotokana na jamaa zangu wale, yaani majini.


Kufumba na kufumbua, sura ya jitu la kutisha ilionekana juu ya dali ikiniangalia kwa hasira na kusema:


“Si ruhusa hata kumwanishia mke wako mazungumzo ambayo yatampa wasiwasi. Wakati unatoka, mimi nilikwambia ya kule yawe ya kule. Usalama wa maisha yako upo kwa kutunza kila tulichosema. Sawa?”


“Sawa,” nilijibu kwa kutetemeka, palepale upepo ukatulia na ile sura mbaya ikapotea.


Ilikuwa sura yenye umbile la binadamu mwenye masikio marefu kupita ya sungura. Macho yake yalikuwa ya duara tena mekundu sana. Alipokuwa akizungumza na mimi, midomo yake ilikuwa ikitoa miale ya moto. Lakini alinukia manukato mazuri.


“Mume wangu yaani mimi nakulalamikia kuhusu upepo wewe unaimba nyimbo za dansi. Ina maana ndiyo ulikuwa unaufukuza upepo au?”


“Nilikuwa naimba wimbo gani wa dansi?” nilimuuliza mke wangu.


“Si ulikuwa ukiimba wimbo sijui wa bendi gani ya zamanai sana.”


Palepale nilinyamaza kimya. Nilibaini kwamba, kumbe kule kusema kwangu na ile sura, mke wangu alisikia kama naimba. Moyoni nilisema safi sana, kumbe sijabainika na ndiyo uhai wangu unavyotakiwa kulindwa kwa mujibu wa ile sauti.


Usiku uliingia sana, nikaenda kuoga, nikarudi kula, ukafika muda wa kwenda kulala. Mke wangu akasema anatangulia, ana usingizi. Mimi niliendelea kubaki sebuleni kwa muda nikiwa naanza kuhisi kama kusinzia vile.


Ghafla nikawa kwenye barabara kuu ya kutoka Iringa mjini kwenda eneo la Kihesa. Nilisimama katikati ya barabara eneo la Miyomboni ambapo gari moja lilikuwa linakuja kwa mwendo wa kasi kutoka eneo ambalo zamani kulikuwa na Jengo la Sinema la Highland, nikalinyooshea mkono, likanikwepa mimi na kwenda kutumbukia kwenye mtaro pembeni.


Kishindo cha hilo gari wakati wa kufika kwenye mtaro kilifuatia na ukimya wa hali ya juu. Nikajua waliokuwemo ndani ya gari hilo, mawili. Wamefariki dunia au wamejeruhiwa vibaya sana, kiasi kwamba hawawezi hata kuzungumza.


Nilitembea kwa mwendo wa kawaida mpaka pale. Bado vumbi jingi liliifunika gari kiasi kwamba ilikuwa si rahisi kujua kuna nani na nani ndani yake.


Ghafla nilizungukwa na watu watatu, wa aina ya kule ujinini. Ni wanawake wote. Kila mmoja, mkononi alishika bakuli la bati.


Walinifuata, mmoja akanishika mkono wangu wa kushoto na kuutingisha kwamba ananipongeza kwa kazi nzuri.


Kisha wao wakatembea hatua kwa hatua mpaka kwenye gari kabisa, wakafungua mlango mmoja ambapo mlango wa pili, gari liliulalia wakati wa kupinduka. Mimi niliendelea kusimama kuwaangalia.


Baada ya dakika kama moja tu, wakatoka wakiwa na mabakuli yao. Nilibaini ndani ya mabakuli hayo mlikuwa na damu kwa sababu ya wekundu!


Wakaja mpaka niliposimama mimi, wakasimama sanjari. Kufumba na kufumbua wakapotea usoni mwangu. Kufumba na kufumbua, mimi nikaamka kitandani, nyumbani huku nikikohoa kwa nguvu.


Nilishangaa kumwona mke wangu akiwa macho, hana hata lepe la usingizi.


“Mbona hulali? Huna usingizi?” nilimuuliza mke wangu.


“Nashangaa, sina usingizi wala sitaki kulala. Sijui kuna nini? Chumba nakiona kizito sana lakini jioni nilikwenda kanisani, mchungaji akaniambia nina majaribu mazito sana mbele yangu, nijitahidi kumwomba Mungu.”


Nilishtuka kwa maneno hayo ya mke wangu. Kwangu yaliashiria kwamba, kiroho mchungaji wake alijua kuna jambo ndani ya familia yangu.


“Ungelala ili ijulikane moja, kesho tutaendelea na mambo mengine,” nilimwambia.


Lakini kabla ya kulala, akaniangalia na kusema: “Lakini na wewe mbona kama ulikuwa unaweweseka ukiwa usingizini halafu unaota ndoto za ajabuajabu?”


“Ni hali tu. Kwani wewe hujawahi kuweweseka?” nilimjibu.


“Nimewahi lakini wewe zaidi. Halafu nikawa nasikia kama sauti za wanawake zikikupongeza. Ilikuwa nini?”


Nilishtuka sana kusikia hivyo kwani kama unakumbuka ndugu mwandishi ni kweli wale wanawake walinipongeza kwa kazi nzuri ya kupindua gari. Lakini nilijiuliza, inawezekana kweli kwamba, mtu akusikie upo kwenye ndoto unazungumza halafu akawasikia na unaoongea nao?!


Nilikataa moyoni lakini nikasema kama ni kweli, basi mke wangu atakuwa anapewa ujumbe kupitia nguvu kubwa ya Mungu.
 
SEHEMU YA 09


“Nashangaa, sina usingizi wala sitaki kulala. Sijui kuna nini? Chumba nakiona kizito sana. Lakini jioni nilikwenda kanisani, mchungaji akaniambia nina majaribu mazito sana mbele yangu, nijitahidi kumwomba Mungu.”


Nilishtuka mwenyewe kwa maneno hayo ya mke wangu. Kwangu yaliashiria kwamba, kiroho mchungaji wake alijua kuna jambo ndani ya familia yangu.
SASA ENDELEA MWENYEWE…


“Ungelala ili ijulikane moja, kesho tutaendelea na mambo mengine,” nilimwambia.
Lakini kabla ya kulala, akaniangalia na kusema: “Lakini na wewe mbona kama ulikuwa unaweweseka ukiwa usingizini halafu unaota ndoto za ajabuajabu?”


“Ni hali tu! Kwani wewe hujawahi kuweweseka?” nilimjibu na kumuuliza.
“Nimewahi lakini wewe zaidi. Halafu nikawa nasikia kama sauti za wanawake zikikupongeza. Ilikuwa nini?”


Nilishtuka sana kusikia hivyo kwani kama unakumbuka ndugu mwandishi ni kweli wale wanawake walinipongeza kwa kazi nzuri ya kupindua gari. Lakini nilijiuliza, inawezekana kweli kwamba, mtu akusikie upo kwenye ndoto unazungumza halafu akawasikia na unaoongea nao?!


Nilikataa moyoni lakini nikasema kama ni kweli, basi mke wangu atakuwa anapewa ujumbe kupitia nguvu kubwa ya Mungu.


“Hapana, labda wewe ulisikia watu wakizungumza kwenye redio ya jirani. Yaani mimi niote ndoto halafu wewe uwasikie ninaoongea nao? Inawezekana kweli?” nilimuuliza.
“Ndiyo na mimi nashangaa, nimesikia kabisa wanawake wakisema kukupongeza nikajiuliza sana. Mtu anaweza kuwasikia watu wanaoongea na mtu anayeota ndoto?!”
“Ndiyo maana nimekwambia mke wangu wewe ulisikia watu wa kwenye redio ya nyumba ya jirani. Unajua ukweli wote kwamba huwezi kuwasikia watu wanaoongea na mtu anayeota ndoto, sasa wewe hushangai?”


“Nashangaa. Lakini je, na wewe kwenye ndoto hakuna wanawake waliokuwa wanakupongeza kwa jambo lolote?”
“Sijawaona.”


Basi, tulilala mpaka kunakucha. Siku hiyo mimi nilichelewa kuamka tofauti na kawaida yangu saa kumi na moja na nusu mpaka kumi na mbili kamili. Mke wangu alipoamka alianza kusali. Hali ile ilinipa shida sana. Niliota ndoto eti napita mtaani halafu kuna watu wakaanza kunikimbiza.


Nilikimbia mpaka nikafika wakati miguu ikaishiwa nguvu, nikaanza kutembea kwa kasi huku wale watu wanaonikimbiza wakiwa wameshika mapanga na mikuki wakinikaribia.


Ili kukwepa kuuawa, niliamua kusimama na kuwageukia, nikanyoosha mikono ya kusalimu amri, kwamba niko chini yao. Walinikamata, wakanichukua mpaka kwenye tanuri la moto kwa ajili ya kunitupia humo. Sasa wakati wanataka kunirusha, nilipiga kelele nikiomba msamaha lakini nikiwa silijui kosa langu kwao.


Walinikatalia, wakaanza kuhesabu moja, mbili, ile wanataka kusema tatu ili wanirushe sasa, nilishtuka kutoka usingizini mpaka nikakaa kitandani. Nikawa nahema, macho nimeyatoa pima. Mke wangu akanishika mkono na kuniuliza kuna nini! Nilimwambia ndoto.


“Ndoto imefanyaje mume wangu?”
“Nimeota ndoto mbaya sana.”


“Umeotaje kwani?” aliniuliza mke wangu huku bado akiwa amenishika mkono mmoja. Nilikuwa bado nahema sana mpaka nikashindwa kuzungumza. Mkono mmoja nilijishika kifuani nikihema kwa kasi.


“Umeotaje kwani mume wangu?” aliniuliza tena mke wangu. Alionekana kuwa na shauku kuu ya kutaka kujua.


“Nimeota nakimbizwa na watu wenye mapanga na mikuki.”
“He! Huyo ni shetani na ameshindwa katika Jina la Yesu,” alisema mke wangu kwa sauti ya kukemea, nikasikia kama nachomwa moto mwili mzima.
“Ikawaje sasa?” aliniuliza tena mke wangu.


“Sikukubali, nikaanza kukimbia, wakawa wananikimbiza. Nilifika mahali nikawa nimechoka sana sasa, nikaamua kutembea lakini wao waliendelea kunikimbiza, ikabidi nisamame na kuwageukia, nikawaomba samahani. Wakakataa, wakanishika na kutaka kunirusha kwenye tanuri la moto. Sasa wakati wamenibeba juujuu wakihesabu moja mbili mpaka tatu ili wanirushe, ilipofika mbili ndiyo nimejikuta nimeshtuka.


“Pole sana, nadhani kuna wabaya. Na mimi nimeamka nikaanza kusali na kukemea kwa ajili ya familia yangu. Ni shetani tu mume wangu, lakini ameshindwa katika…kabla hajamaliza Jina la Yesu, niliziba masikio kwa vidole ili nisisikie kwani niliamini yale maumivu ya moto muda ule yalitokana na yeye kusema hilo jina la Yesu.


Lakini licha ya kuziba masikio, bado nilisikia maumivu makali sana. kumbe kinachochoma si kusikia jina bali hata likitajwa jirani na wewe pia tosha. Nikasema kwa sauti mamaaa! Mke wangu akasimama, akanishika mabegani.
Itaendelea wiki ijayo.


“Nini tena jamani?”
Kilichoendelea hapo sikumbuki, nika kama nilipoteza fahamu lakini nilipokuja kuzinduka, nilimwona mke wangu akilia kwa uchungu huku akiwa amepiga magoti na kulalia kitandani kwa upande wa kifuani huku akisali.


Alipobaini nimezinduka, alikaa na yeye kitadani, akaniangalia kwa macho yenye huruma na wasiwasi kisha akasema:
“Unajua saa hizi ni saa ngapi?”


Niliangalia saa nikabaini ni saa sita na dakika kumi na mbili mchana. Nilishtuka sana, nikaangalia nje kwa kutoamini, nikamtajia muda kama alivyoniuliza. Akaniuliza tena.
“Unajua kilichotokea kwako?”


Je, nan wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 10


Lakini licha ya kuziba masikio, bado nilisikia maumivu makali sana. Kumbe kinachochoma si kusikia jina bali hata likitajwa jirani na wewe pia tosha. Nikasema kwa sauti mamaaa! Mke wangu akasimama, akanishika mabegani.
SASA ENDELEA MWENYEWE…


“Nini tena jamani?”
Kilichoendelea hapo sikumbuki, ni kama nilipoteza fahamu lakini nilipokuja kuzinduka, nilimwona mke wangu akilia kwa uchungu huku akiwa amepiga magoti na kulalia kitandani kwa upande wa kifuani huku akisali.


Alipobaini nimezinduka, alikaa na yeye kitadani, akaniangalia kwa macho yenye huruma na wasiwasi kisha akasema:
“Unajua saa hizi ni saa ngapi?”


Niliangalia saa nikabaini ni saa sita na dakika kumi na mbili mchana. Nilishtuka sana, nikaangalia nje kwa kutoamini, nikamtajia muda kama alivyoniuliza. Akaniuliza tena.
“Unajua kilichotokea kwako?”
“Sijui mke wangu, waweza kunisimulia ukitaka lakini kama hauko tayari hata mimi sitakulazimisha,” nilimwambia hivyo.


Lakini wakati nasema hivyo, nilikumbuka kwamba, nilishaonywa na wale viumbe kuhusu kuzungumzia mambo ya kule nilikokuwa lakini pia nikajisemea moyoni kwamba, haitawezekana niwe na hatia wakati anayesimulia hali ilivyokuwa ni mke wangu na si mimi na wala yeye hajui hali ilikuaje kule.


“Mume wangu kwanza pole sana. lakini pili, najua yote yaliyokupata si wewe bali ni nguvu iliyokuzidi. Mchungaji alikuja hapa, mimi nilimfuata baada ya kuona hali yako inazidi kuwa mbaya.


“Alipofika akakufanyia maombi, ukaanza kusema mambo makubwa sana na ya kushangaza. Kwa kweli, mimi mwenyewe nilikuwa nakuogopa sema mchungaji alinipa ujasiri hasa baada ya kuomba sana.


“Sikumbuki ni lini ulikuwa haupo hapa nyumbani kwa siku kadhaa, lakini ulisema ulisafiri kwa siku kadhaa kwenda kwenye makazi ya majini lakini kwa mchungaji ndivyo ulivyosema na mchungaji alisema ile haikuwa kauli ya akili zako ila maombi yake.
“Mume wangu ukiwa kwenye makazi ya majini, ulifundishwa mambo mengi lakini kubwa walikutana wewe uwe wakala wao wa hapa duniani.”


Wakati mke wangu ananisimulia hayo, mwili ulikuwa unasisimka kwa sababu nilijua siku zangu za kuishi hapa duniani ziliisha. Maana ilionesha katika kuombewa kwangu na mchungaji, nilisema siri zote za kule ujinini. Nilitamani nimwambie mke wangu asitishe maelezo yake ili niwe na amani.


“Ulisema kule ujinini ulipelekwa na wanawake watatu waliokubeba pale Huindini. Mchungaji alishangaa sana, yaani mume wangu ulinena mambo mazito sana.”
“Mke wangu, achana na hayo mazungumzo, we huamini kwamba nilisema kwa sababu nilikuwa sijitambui. We mwenyewe si umesema hujawahi kuniona sipo hapa nyumbani?”


“Ndiyo na mimi nikashangaa hapo.”
“Basi ujue kwamba, nilisema kwa maneno ya kuweweseka kama vile nilikuwa naota njozi.”
“Itakuwa kweli mume wangu. Lakini mimi bado nina maswali mengi kuhusu wewe, hasa siku mbili hizi.”


Wakati tunaendelea kuzungumza na mke wangu akinisimulia nilivyokuwa naanika mambo ya kule ujinini, ghafla wanawake wawili walitua mle ndani, wakasimama kwenye kona ya mlango. Nilitaka kushtuka, wakanionesha ishara niwe mtulivu.
Niliwakumbuka ni wawili kati ya wale watatu walionipeleka ujinini. Nikatulia kimya mke wangu akauliza:


“Mbona kama nasikia harufu ya manukato?”
“Hata mimi,” nilimjibu.


“Labda kuna watu wanapita nje,” alisema yeye. Mimi nikakaa kimya.
Nilijua kuwa, manukato yale yalitoka kwa wale wanawake walioingia.
“Lakini mume wangu nilikwambia kwamba ulikuwa unaota, kuna wanawake wakasikika wakikupongeza kwa kazi nzuri, hivi we hujiulizi ni vipi? Kwa nini mimi niwasikie watu unaoongea nao kwenye simu?”


Kabla sijamjibu, mwanamke mmoja kati ya wale alisema kwa sauti:
“Kwa swali hilo kaa kimya tafadhali!”
Nilishtuka nikiamini kwamba, sauti ya yule mwanamke ilisikika vyema na mke wangu kwani alizungumza Kiswahili sawasawa na kwa sauti ya juu.


Lakini cha ajabu, nikamwona mke wangu akiangalia juu ya paa la nyumba na kusema kuwa kuna upepo mkali umepita. Mimi nilikaa kimya!
“Kwa hiyo wewe mume wangu kwa mtazamo wako huna baya la mambo ya majini?”
Yule mwanamke akasema tena kwa sauti ya juu:


“Mjibu hakuna baya na asiendelee kuuliza.”
Kabla sijamjibu mke wangu, nikamwona anainua tena kichwa kuangalia juu. Akasema:
“Mbona kuna upepo unatikisa bati na kupita, unatokea wapi?”
“Mimi sijui. Lakini kuhusu swali lako kwamba hakuna baya la majini, mimi naona hakuna baya mke wangu.”


“Unataka kusema mchungaji wangu anayetumia damu ya Bwana Yesu kuomba, maono yake si ya kweli?”
Niliwaona wale wanawake wakipepesuka, mikono wakaikinga kama wanaokwepa joto la moto uliokokwa
 
SEHEMU YA 11


“Unataka kusema mchungaji wangu anayetumia damu ya Bwana Yesu kuokoa, maono yake si ya kweli?”


Niliwaona wale wanawake wakipepesuka, mikono wakaikinga kama wanaokwepa joto la moto uliokokwa.ENDELEA MWENYEWE SASA…


“Si ya kweli mke wangu. Nadhani tuachie hapo,” nilimwambia kwa sauti iliyojaa amri na ukali kidogo.
Mke wangu alitulia, wale wanawake walipotea ghafla kisha wakarudi tena.
“Mkeo anataka kutufanya nini sisi? Hajui kwamba tunaweza kumtoa roho kabisa?” walisema kwa pamoja.


Mke wangu akaangalia juu tena na kusema:
“Jamani huu upepo huu sasa. Si unaweza kuezua paa la nyumba!”
Mimi ndiyo nilikuwa najua kwamba, sauti za wale wanawake ndizo zilisababisha kutikisika kwa paa la nyumba.


“Jamani msameheni ni mke wangu,” nilisema.
“He! Mume wangu yaani paa linayumba kwa upepo mkali hivi halafu wewe unaimba,” aliniambia mke wangu.


Ina maana kwamba, wakati mimi nawaambia wale wanawake hivyo, mke wangu aliona mimi naimba.
Basi, wale wanawake waliniaga wakapotea machoni pangu huku wakiahidi kurudi usiku kwa ajili ya kazi maalum.
***
Ilikuwa usiku wa saa sita, nilichelewa kulala siku hiyo lakini nilikuwa nimejilaza tu kitandani nikiangalia paa, nikahisi joto kali sana na ukichukulia Mkoa wa Iringa ni wenye baridi kali, kumbe ni wale wanawake wanakuja, wakaonekana ghafla chumbani kwangu.


Walisimama ukutani wakinitazama kwa macho makavu. Mmoja wao akaniita kwa ishara ya mkono. Niliinuka kitandani, nikashusha miguu na kutembea hadi walipo.


Mmoja wao akaniwekea mkono kichwani, akaugandisha kwa muda wa kama dakika tano nzima bila kusema lolote. Niliusikia mwili ukiwa wa baridi sana, kuanzia utosini hadi miguuni.


“Utatoka hapa sasa hivi, utatembea hadi nje, ukifika huko utapewa maelekezo mengine, sawa?”
“Sawa,” nilijibu bila kuuliza, wakapotea.
Nilirudi kitandani nikakaa. Nikaanza kujiuliza kama lile tukio nilikuwa naota au ni kweli.


“Unapoteza muda kufikiri, toka ukafanye kazi,” sauti ilisikika ndani ya chumba bila kumwona msemaji.


Nilisimama kama niliyepigwa shoti ya umeme, nikiwa kwenye mavazi ya kulalia tu, nikatoka hadi nje. Wakati nafungua milango, yaani wa chumbani kwenda sebuleni na wa sebuleni kutoka nje, nilikuwa natumia nguvu kubwa sana na kuibamiza.
Nje, nilikuta kundi la watu wamesimama kwa mbele kama waliokuwa wakinisubiri mimi.


Walinifuata, wakanishika mkono na kugeuka, tukatembea kuelekea barabara kuu. Kule, tukakutana na wengine kama wao.


Nao wakanishika mkono. Cha ajabu ni kwamba, wakati wananishika, mwili wangu ulikuwa ukiingia baridi sana. halafu sijui walitumia maarifa gani kunishika kwani waliweza kunishika wote japokuwa walikuwa wengi.


Tulikwenda mpaka kwenye ofisi za posta ambazo zipo eneo la bustani ya halmashauri ya mji. Tukasimama hapo. Mmoja wao akaniambia natakiwa kwenda hospitali ya mkoa ambako si mbali na ofisi hizo za posta.


Kule nilitakiwa kwenda kuchukua vivuli vya wagonjwa ambao bado wana nguvunguvu, yaani afya zao hazijatetereka sana.
“Una swali?” yule mmoja wao aliniuliza.
“Vivuli navichukuaje?” nilimuuliza.


“Kila mgonjwa unamshika kwa mkono wa kushoto. Kwa kufanya hivyo ndiyo maana ya kuchukua vivuli vyao. Wakati unaingia hakikisha unapofika tu mlangoni geuka na kuingia kinyumenyume huku unatembea kwa hatua ndefu. Una swali jingine?”
“Vina kazi gani hivyo vivuli?”


“Sisi huwa tunatengenezea dawa ya kujichubulia. Wanawake wengine wanapenda kujichubua, lakini asili ya zile dawa ni sisi na ndiyo tuliyoleta ufundi huu kwenu duniani.”
“Sawa.”


Niligeuka, nikatembea nikiwaacha wamesimama pale. Lakini wakati nakwenda moyoni nikawa najiuliza ni kwa nini nikachukue vivuli vya wagonjwa? Je, wagonjwa hao baada ya kuwachukua vivuli watakuwa katika hali gani wenyewe?


Nikakumbuka kwamba, swali hilo sikuwauliza, nikageuka ili kurudi kwanza pale ili nikawaulize, lakini ile nageuka tu, nikawaona wamesimama mbele yangu. Ina maana walitembea nyuma yangu.


“Kuna tatizo gani tena?” waliniuliza.
“Je, nikiishachukua hivyo vivuli, hao wenye vivuli au niseme wagonjwa, watakuwa katika hali gani kiafya?”


Walicheka sana, wakacheka wee na waliponyamaza walinyamaza wote. Wakaniangalia japokuwa ilikuwa usiku lakini niliwaona walivyonikazia macho.
“Hiyo sasa si kazi yako kujua. Baada ya kuchukua vivuli kazi yako itakuwa imeisha mara moja. Wewe nenda.”


Niligeuka na kutembea kwa masikitiko sana. nilijua nikishachukua vivuli, wahusika watakata roho palepale na ndiyo maana pia hawakutaka kuniambia.
Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 12


“Hiyo sasa si kazi yako kujua. Baada ya kuchukua vivuli kazi yako itakuwa imeisha mara moja. Wewe nenda.”
Niligeuka na kutembea kwa masikitiko sana. Nilijua nikishachukua vivuli, wahusika watakata roho palepale na ndiyo maana pia hawakutaka kuniambia.
SASA ENDELEA:


Niliingia hospitali huku nikikumbuka masharti yote, hivyo wakati naingia, nikageuka na kutembea kinyumenyume. Nilipishana na nesi mmoja akiwa amebeba mfuko wa rambo.
Nikapita hadi kwenye wodi moja ya wagonjwa wanawake wenye watoto. Pia nikaingia kinyumenyume. Nikasimama katikati ya wodi. Wagonjwa wote walikuwa vitandani, wengine macho, wengine usingizini. Waliokuwa macho, kuna waliokuwa wakiugulia kwa maumivu, wengine walikuwa macho tu.


Hakuna aliyeonesha dalili kwamba, ananiona mimi pale niliposimama. Nikatembea kumfuata mwanamke mmoja, yeye alikuwa macho lakini mtoto wake alikuwa amelala. Nilipofika karibu yake, nikamnyooshea mkono, nikauchezesha kisha nikaurudisha kwangu.


Nikaenda kwenye kitanda kingine ambacho mama alilala, lakini mtoto wake alikuwa macho na anachekacheka. Niliposogea karibu tu, yule mtoto akaniangalia na kuanza kulia sana. Alilia kwa ukali mpaka nikaogopa.


Kifupi yule mtoto aliniona lakini hakuwa na uwezo wa kusema kwamba anaona nini. Hapa labda niseme tu kwamba, watoto ambao hawajafikia uwezo wa kusema wana uwezo wa kuona viumbe au vitu visivyoonekana. Lakini wakishapewa uwezo wa kusema mama, pale, ile, nataka, ona, huyo anaondolewa uwezo wa kuona visivyoonekana.


Na ili kuwaelimisha kuhusu hili, napenda kuwakumbusha kwamba, mara nyingi mitaani tunakoishi, kuna tabia kwamba, mtoto akipenda kulia sana usiku, baadhi ya imani za watu zinasema hajapenda jina alilopewa.


Wengine wanafikia hatua ya kumbadilishia jina mtoto, watampa la babu yake au bibi kama ni mwanamke au lolote lenye asili ya kabila lake. Wapo wanaosema mtoto analia kwa sababu mizimu imechukia. Hakuna cha mizimu.


Mara nyingi mtoto kulia usiku, sababu kuu ni kuwaona wachawi au majini ndani ya chumba. Mwangalie mtoto anapolia anaangalia wapi. Akikimbiza kichwa ujue anashuhudia maajabu.


Na pia, ili uamini kuwa mtoto analia usiku kwa sababu ya kuona visivyoonekana, ukimbeba na uso wake kuuelekeza ukutani hunyamaza. Kama ataendelea kulia ujue kama ni mchawi amekwenda mpaka ukutani na kumwangalia huku akimtisha.


Jiulize ni kwa nini watoto wadogo kulia ni nyakati za usiku tu? Na ndiyo muda ambao wanga au majini yanazunguka sana.Ila sema majini ni mara chache sana kumliza mtoto kwani wao wana tabia ya kujigeuza na kuwa na sura ya upole na tabasamu laini.


Basi, nilichofanya, nilisimama, nikajishika kichwani, palepale nikawa kama mwanamke mzuri. Nilijiangalia sana. Ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kujibadili kuwa mwanamke mrembo.


Yule mtoto akaacha kulia, akaanza kuniangalia na kutabasamu. Mama yake alishaamka wakati huo na alikuwa akimshangaa mwanaye kwa kulipuka na kilio.
Nilimsogezea mkono, nikavuta kivuli, nikageuka, nikaenda kwenye kitanda kingine. Ile nafika tu, mama wa mtoto akakurupuka na kuanza kufoka:


“Umefuata nini wewe? Umetumwa ee? Nesi, huyu mwanaume kaingia ndani ya wodi.”
Nilishtuka sana, nikawa natoka mbio huku nesi akija kwenye kile kitanda na kuuliza yuko wapi?


“Huyo unapishana naye hapo. Huyo anakupita.”
Nesi alisimama na kuangalia huku na kule. Lakini nilimpita kama basi liendalo kasi bila kuniona. Nilipofika nje, nilishtuka sana kuona nimebainika kwenye ile wodi. Tena wakati natoka na yule mwanamke anasema natoka nje, wenzake walikuwa wakinitafuta bila mafanikio.


Niliwakuta wale wamesimama palepale nilipowaacha. Nikiwa nahema kwa nguvu niliwaambia kidogo nikamatwe. Mmoja akasema:


“Tulikuona, tukakuacha. Nani alikwambia ujibadilishe kuwa mwanamke? Wewe huwezi kujibadili mpaka ruhusa yetu. Una bahati sana kwani ilikuwa uuawe palepale lakini tukakuacha. Ila tulikuondolea uwezo kwa sehemu, ndiyo maana aliyeweza kukuona ni yule mwanamke mmoja tu, wengine hawakukuona.”


Niliogopa, nikatetemeka sana. Yule aliyekuwa akiongea, akaniangalia sana kisha akaendelea kuniambia:
“Binadamu mwenye uwezo wa kujibadili ni mchawi tu. lakini kwa yule anayefanya kazi na sisi hana uwezo huo. Uwezo huo tunao sisi, tunaweza kuwa wanawake, wanaume, wazee, vijana, watoto, hata vyovyote vile.”


Niliomba msamaha sana, wakasema wamenisamehe kwa sababu sijaonesha jeuri, lakini walichoamua tangu mwanzo baada ya mimi kujigeuza ni kunisubiri nirudi kisha wanitoe roho nife moja kwa moja.


Lakini akilini nilijiuliza tabu yote ile, kutaka kote kuniua, kwani mimi nitafaidika na nini? Nilibaki kimya kwa muda, nikasema:


“Jamani nina swali muhimu sana kwenu ambalo limenijia baada ya kunisamehe.”
Yule msemaji wao wa tangu awali akaniambia kwa sauti yenye amri.
“Si unataka kuuliza kuhusu utakachopata kwa mambo yota haya?”


Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 
SEHEMU YA 13


“Jamani nina swali muhimu sana kwenu ambalo limenijia baada ya kunisamehe.”
Yule msemaji wao wa tangu awali akaniambia kwa sauti yenye amri.
“Si unataka kuuliza kuhusu utakachopata kwa mambo yote haya?”
ENDELEA MWENYEWE…


“Ni kweli,” nilikiri huku nikianza kuogopa kwa maana kwamba kama wamejua bila kusema nini kitaendelea?
“Unachotakiwa kufanya ni kuhakikisha unatenda sawasawa na matakwa yetu, hilo tu, basi.”


Nilikubali kwa kutumia ishara ya kichwa na shingo. Wakasema nikalale ila kwa usiku wa kesho yake nitatakiwa kufanya kazi moja ngumu sana lakini sitakuwa peke yangu, nitashirikiana na majini.


Niliwauliza ni kazi gani hiyo, wakasema kuna sherehe ya kuzaliwa kwa mtoto wa mmoja wao. Huyo mtoto ni wa mwanamke jini aliyezaa na mwanaume mtu. Lakini mtoto anaishi ujinini.


Hapa naomba niseme kidogo mwamba, wapo wanaume wengi tu wa duniani wamezaa na wanawake wa ujinini. Lakini pia kuna wanawake wa duniani wamezaa na wanaume wa ujinini.


Kinachotokea ni kwamba, unakuta mwanaume anatokea kumpenda msichana jini bila mwenyewe kujua kuwa yule ni jini. Anatembea naye kwa tendo la ndoa kisha hawaendelei na uhusiano.


Yule msichana kumbe ni jini na alijitokeza duniani kwa kutaka kuzaa na binadamu tu. Baada ya hapo anarudi ujinini kulea mimba yake mpaka anajifungua.
Na kwa msichana wa duniani vivyohivyo, anatongozwa na mwanaume, kumbe jini, wanakwenda hotelini na kukutana kwa tendo la ndoa. Baada ya hapo, mwanaume anarudi ujinini na msichana huku duniani anapata mimba, baba hajui aliko.


Basi, tuliachana hapo, nikarudi nyumbani kulala. Kesho yake niliamka nikiwa nina nguvu za ajabu. Mwili ulikuwa kama umepumzika kwa siku saba, kumbe wapi! Mwenyewe nilishangaa sana.


Siku ya pili, nilipotoka kazini jioni ya saa kumi na mbili, nilisikia sauti ikiniambia nisitoke kwenda popote baada ya kufika nyumbani kwangu na nilitakiwa kuoga na kujipaka mafuta ya mgando, maelekezo mengine ningepewa.


Nilifanya hivyo, baada ya kuoga nilijipaka mafuta ya mgando na kukaa sebuleni. Baada ya saa kadhaa, kwenye saa mbili usiku, upepo mkali sana ukavuma, nikajua wenyewe wanakuja.


“Hivi saa ni saa mbili na nusu, simama uondoke. Unasubiriwa nje kwa ajili ya kwenda kwenye sherehe,” sauti iliniambia, nikafikicha macho, hakukuwa na mtu.


Nilikuwa nimevaa, nikatoka nje na kuwakuta wanawake wawili ambao walinishika mikono, kila mmoja wa kwake. Kufumba na kufumbua tulikuwa tumekaa kwenye ukumbi mmoja maarufu sana hapa Iringa.


Wateja walikuwepo wakiendelea na mambo yao lakini baadhi ya meza hazikuwa na wateja. Pembeni kulikuwa na meza, walikaa watu kama kumi na kuendelea. Wale wanawake wakanipeleka kule na mimi nikajua ndiko kwenye sherehe.
Kweli, palikuwa na wanawake mchanganyiko na wanaume. Mwanamke mmoja alikuwa na mtoto kama wa miaka miwili hivi.


Meza ilipambwa na keki, mishumaa, vitambaa vyekundu, mabakuli, vikombe vya kuwaka kama almasi, mahotpoti na kadhalika. Lakini kwa pembeni yake chini palikuwa na seti ya muziki na DJ alisimama hapo.


Kwa haraka nilichobaini ni kwamba, wateja wengine ndani ya ukumbi ule walikuwa hawawaoni wale watu. Pia, kuna mtu katika wale watu alikuwa akitoka mara kwa mara na kwenda kusimama mbele ya meza na kunyoosha kidole mlango mkuu.


Awali sikujua ni kwa nini, baadaye nilibaini kwamba, mtu yule alikuwa maalum kwa kuwazuia wateja waliokuwa wakiingia na kuonesha dalili ya kuja kukaa tulipokuwepo sisi.


Nililigundua hilo baada ya wakati fulani kuwaona watu wawili, nadhani ni mke na mume wakiingia mlango mkubwa na kuja uelekeo wetu ambapo yule mtu alitoka kwenye meza na kwenda kusimama mbele halafu aliwanyooshea kidole kisha akawa anakipeleka kidole hicho usawa wa meza nyingine kabisa na wale watu nao walielekea huko mpaka kwenye meza nyingine, wakakaa. Yaani ilikuwa kama anawaelekeza.


Hapa kabla sijaendelea, nataka kuwapa wasomaji somo moja. Ni kwamba, kwenye mabaa na maeneo mengine wanayokutanika watu kuna mambo mengi ya ajabu ambayo hayaonekani.


Maandiko yanasema Mungu aliumba viumbe vinavyoonekana na visivyoonekana. Sasa ni mara nyingi tu, visivyoonekana vinapenda kukaa sehemu ambayo vinavyoonekana vipo.


Mfano kwenye baa, dalili kubwa kwamba viumbe vinavyoonekana navyo vipo vimekaa kwenye viti ni wateja kukauka au kuingia na kupenda kukaa upande mmoja tu wa viti vya baa hiyo.


Utakuta baa nzuri sana, lakini viti vitupu muda mwingi. Lakini ukweli ni kwamba, hapo si kwamba wateja hawataki kuingia bali kuna majini nayo yanapenda kukaa kwenye baa hiyo wakifanya mambo yao.


Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 14


Utakuta baa nzuri sana, lakini viti vitupu muda mwingi. Ukweli wa hapo ni kwamba, eneo hilo si kwamba wateja hawataki kuingia bali kuna majini nayo yanapenda kukaa kwenye baa hiyo wakifanya mambo yao ya kila siku.
SASA ENDELEA…


Sasa hapo, wewe binadamu wa kawaida, utasema viti vitupu kwenye baa lakini kumbe vina watu wamekaa na wanaendelea na mambo yao huku wakikuangalia. Ukisema uende roho inasita au unajikuta miguu inakata kona na kwenda kukaa sehemu nyingine kabisa. Hapo ujue miongoni mwa hao majini kuna mmoja ambaye amekuelekeza kukaa huko.


Na dalili kubwa kwamba baa unayoingia siku hiyo wamekaa majini, hasa kama baa hiyo itakuwa ni ile uliyoizoea siku zote ni kwamba, utajikuta umekaa sehemu ambayo hujaizoea. Na hili utagutuka baadaye sana ukiwa umeshakaa na kuendelea na vinywaji.
Kitakachokutokea, utajiuliza ghafla kwa nini mimi leo nimekaa eneo hili ambalo huwa silipendi kabisa.


Kuna mambo mengi sana katika yasiyoonekana. Wengi wamekuwa wakilalamika biashara fulani haiendi vizuri bila kujua kwamba, majini yameingilia kati.


Mfano, mtu anafungua gesti nzuri sana, ipo mahali pazuri sana, tena si ajabu ni jirani kabisa na kituo kikuu cha mabasi yanayokwenda mkoa, lakini gesti hiyo haiwagi na wateja hata siku moja. Kama kuna vyumba ishirini, vinne vitapata watu, vinavyobaki vinalala vyenyewe.


Ujue hapo kuna majini ambao wameamua kupiga kambi kwenye gesti hiyo. Kinachotokea ni kwamba, majini yamekuja duniani na yanataka kufanya kazi fulani, sasa wakakae wapi, wanapata mwafaka wa kukaa kwenye gesti hiyo. Wanagawana vyumba mpaka vinabaki hivyo vinne tu.


Sasa kazi yao kubwa hao majini ni kuhakikisha mmoja wao, anasimama nje kuhakikisha wateja hawaji baada ya nyumba vinne kujaa.


Wengi utawasikia wakisema labda gesti hiyo, huenda nyumba iliyotumika iliwekewa madudu. Kwa hiyo tajiri wa gesti anatafuta mganga wa kienyeji eti kwenda kuagua wakati uganga wenyewe unaongozwa na majini.
Katika hali kama hii, mwaguzi mkubwa si mganga wa kienyeji bali viongozi wa dini mbalimbali.


Basi, bethidei ilifanyika, lakini kwa utaalam wa kimajini muziki wa baa ukawa unaleta matatizo ya kukatikakatika mara kwa mara hivyo sisi muziki wetu ukawa unasikika sawasawa lakini bila wateja kujua hilo kwani na wao walionekana kuendelea na shughuli zao.


Halafu hapa pia nataka kusema kwamba, huwa inatokea, unakuta baa imepoa sana! yaani unakwenda baa, hakuna muziki wa redio wala wa tivii lakini vitu vyote vipo, yaani redio ipo na tivii ipo.


Mara nyingi katika mazingira kama haya ujue kuwa, kuna majina wapo hapo wanaendelea na shughuli zao. Pengine wamefika kula na wanaongea mambo yao au wameamua tu kutumia baa hiyo kuongea mambo yao hata kama hawali chochote.


Zipo kumbi za harusi nazo zinadoda. Ukumbi upo pazuri, maegesho ya magari yapo, tena upo karibu na barabara lakini haupati wateja. Ukiona hivyo ujue kuna majini nao hufanya sherehe zao siku za mwishoni mwa juma au wikiendi.
Kawaida ya majini ni hiyo, wakiweka kambi mahali kwa hapa duniani huwa hawana tabia ya kuhamahama, mara huku, mara kule.


Tabia hii imekuwa ikiwaumiza binadamu wengi kwa maana ya kuingiliwa katika maeneo yao ya biashara. Wako watu wanapanga baa ili kufanya biashara, baada ya mwaka mmoja wanahama, anakuja mwingine, baada ya mwaka mmoja anahama. Basi inakuwa hivyohivyo.


Hali hii pia hutokea kwenye nyumba za kupanga. Kuna nyumba wapangaji wanahama kila mwaka. Ukiwauliza wanaohama wanaweza kukupa sababu nyingine kabisa. Lakini ukweli ni huohuo.


Ila sasa, kwenye nyumba mara nyingi majini hutumia vyumba vilevile ambavyo binadamu wengine wa kawaida hutumia. Ndiyo maana kuna watu hulalamika kwamba, wanaamka wakiwa wamechoka sana. Mwili mzito sana, usingizi haujaishi sawasawa au mpaka wengine wanasema hawapati usingizi wa kutosha.


Mara nyingi, ukiwa unaishi na majini kwenye nyumba moja wao wana tabia ya kumkandamiza binadamu. Mfano, ukilala kitandani kama na yeye jini chumba chake ni hichohicho, basi ukishalala anakubeba na kukulaza sakafuni.


Kama wakirudi na kukukuta sebuleni, pia wana tabia ya kulalia au kumkalia mtu kwenye mapaja. Sasa kama unaangalia tivii ukitaka kujua umekaliwa na majini, utajikuta unapenda kuzima tivii ili ukae kimya au mara nyingine utapenda kubadilibadili vituo vya tivii bila kujua ni kituo gani hasa unataka kuangalia.


Unapokwenda kuoga, unaweza kukuta maji ndoo nzima lakini umemaliza yote na bado sehemu fulani za mwili zina povu la sabuni. Hapo ujue umeoga na mmoja wa majini.
Kwa majini haya yanayopenda kukaa na binadamu kwenye makazi mamoja ni mara chache sana kukufanyia vituko au visa ambavyo mtu utajua. Ila ni kwa kutumia vigezo hivyo vidogovidogo.


Fuatilia sana tabia za kupoteza vitana nyumbani. Si vitana tu, vitu vyovyote vidogovidogo.
Usikose kusoma mwendelezo wiki ijayo katika gazeti hilihili.


Mara kalamu haipo, mara kuna CD ya muziki ilipotea, mara kuna glasi au kijiko hakionekani! Ujue unaishi nyumba moja na majini.


Kupotea kwa vitu hivyo marra nyingi kuna sababishwa na wao kutovipenda vitu hivyo. Unaweza kununua kitana, wao, hasa yule unayeishi naye kwenye chumba kimoja hakipendi kitana hicho. Kwa hiyo anakichukua na kukitupilia mbali. Kwa upande wa wanawake, wengi hujikuta wakipotelewa na…


Je, wewe msomaji unajua kilichotokea?
 

Similar Discussions

4 Reactions
Reply
Back
Top Bottom