Mkapa, familia ya Nyerere, wafunguka;Mkapa kutaka akutanishwe na mbunge huyo.

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797


ALHAMISI, 15 MACHI 2012 06:42 NA BENJAMIN MASESE, DAR ES SALAAM


​

MVUTANO kati ya Mbunge wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere (CHADEMA) na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, umechukua sura mpya, baada ya Rais Mkapa kutaka akutanishwe na mbunge huyo.

Mkapa amefikia hatua hiyo baada ya mwanzoni mwa wiki kukaririwa akisema Vincent siyo familia ya Hayari Mwalimu Nyerere, kwa kuwa alipokuwa rais, hakuwahi kutambulishwa kuwa mbunge huyo ni sehemu ya familia ya Mwalimu.

Baada ya kutoa kauli hiyo akizindua kampeni za CCM jimboni Arumeru Mashariki wiki hii, Vincent, ambaye ni mtoto wa mdogo wake Mwalimu Nyerere kwa kuzaliwa, juzi alilazimika kujibu mapigo na kumtaka Mkapa aeleze chanzo cha kifo cha Mwalimu Nyerere.

Ili kumaliza tofauti zilizojitokeza, Mkapa amemwomba Mjane wa Mwalimu Nyerere, Mama Maria Nyerere, awakutanishe na Vincent ili kumaliza tofauti zilizojitokeza.

Ombi hilo lilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Msaidizi wa Mkapa, aliyejitambulisha kwa jina la Malago Malagashimba, alipokuwa akizungumza na MTANZANIA ofisini kwake.

Katika ufafanuzi wake kwa MTANZANIA, Malagashimba alikiri Rais Mstaafu Mkapa kusema Vincent siyo familia ya Mwalimu, lakini akasema inawezekana alitoa kauli hiyo kwa bahati mbaya.

"Hili suala tunalifahamu na tumelisoma kwenye vyombo vya habari, lakini ninachoweza kukwambia ni kwamba, anayeweza kulitatua kirahisi au kulitolea ufafanuzi sahihi ni Mama Maria Nyerere.

"Kwa kuwa Mama Nyerere bado yupo hai na ndio mtu mkubwa katika familia, ni vema akaulizwa na ndiye mwenye uwezo wa kuwakutanisha Mheshimiwa wetu Mkapa na Vincent Nyerere ili kulimaliza kifamilia kwa kuwakutanisha.

"Hili limesemwa kisiasa na hadi leo hii limeendelea kukua, tena limekuja kwa tuhuma, sasa tukianza kulizungumza kupitia vyombo vya habari linaweza kuchukua sura nyingine na kuibua mambo mengine.

"Kila mmoja akiamua kufanya alijualo au kwenda sehemu ya kutafuta ukweli utakapohitajika ushahidi, itakuwa kazi ngumu na yenye mlolongo, najua limekuja kisiasa.

"Kwa maana hiyo, nakuomba, nenda kwa Mama Maria Nyerere anaweza kutoa ufafanuzi na likaisha," alisema Malagashimba.

Hata hivyo, alimtetea Mkapa, kwamba inawezekana alipokuwa rais hakuwahi kutambulishwa, kwamba Vincent naye ni mmoja kati ya wanafamilia wa Mwalimu Nyerere.

VINCENT NYERERE

Wakati Malagashimba akisema hayo kwa niaba ya Mkapa, Vincent alizungumza na MTANZANIA kwa simu na kuonyesha kumshangaa Mkapa kwa kauli aliyoitoa.

"Namshangaa sana huyu mzee, nadhani ameanza kupoteza kumbukumbu, kwa sababu baba yangu, Mzee Kiboko Nyerere alipofariki, huyo huyo Mkapa ndiye aliyeleta fedha za rambirambi kwa niaba ya Serikali.

"Fedha hizo alinikabidhi mimi na nikazitumia kumalizia ujenzi wa kaburi la marehemu baba, sasa kama anasema mimi siyo familia ya Mwalimu nadhani ukoo wangu anaujua vizuri, sasa namuomba anitafutie huo ukoo.

"Kwa kuwa mnasema anataka tukutane, mimi sina tatizo namheshimu sana, namsamehe, sina tatizo naye na asikonde kabisa ila siku nyingine awe anafanya utafiti wa maneno anayosema," alisema Vincent.

PROFESA MWAKYUSA ANENA

Kutokana na uzito wa suala hili, MTANZANIA ililazimika kumtafuta Profesa Mwakyusa ili kutoa ufafanuzi juu ya suala hilo.

Akijibu madai ya kwamba mwalimu hakutaka kwenda kutibiwa nchini Uingereza, Profesa Mwakyusa alisema: "Kwanza napenda kukwambia uhusiano wa mgonjwa na daktari ni siri yao, nimesikia maneno hayo kupitia vyombo vya habari, hivi sasa nipo kijijini.

"Mwalimu ni baba yangu, alikuwa mgonjwa wangu, nilikuwa naye karibu muda wote wa ugonjwa, kuhusu ugonjwa wake siwezi kuuzungumzia kwa sababu kiapo changu hakiniruhusu kabisa, naomba mniache tu ndugu yangu," alisema Profesa Mwakyusa.

Alipoulizwa kuhusu tuhuma kuwa aliahidiwa cheo na Rais Mkapa kwamba akishinda ubunge atapewa uwaziri, alisema yeye amekua mbunge wakati wa awamu ya pili ya Mkapa na kwamba hakuwahi kuwa waziri chini ya utawala huo. Alisema si kweli kuwa alipewa ahadi ya namna hiyo.

MADARAKA NYERERE

MTANZANIA ilimtafuta Mmoja wa watoto wa Mwalimu Nyerere, Madaraka Nyerere ili kupata ufafanuzi wa mvutano kati ya Mkapa na Vincent.

Madaraka alipoulizwa kwa kupitia mtandao wake, alisema. "Naomba kutoa maelezo yafuatayo kuhusu yanayozungumzwa kwenye kampeni za uchaguzi wa Arumeru

"Ili kuepuka kujiingiza kwenye masuala ya kampeni, nitajibu sehemu ndogo sana ya maswali yako. Nataka kuthibitisha tu kuwa Mhe. Vincent Nyerere ni ndugu yetu, ni mtoto wa marehemu baba yetu mdogo, Mzee Josephat Kiboko Nyerere," alisema Madaraka kwa kifupi.

Pamoja na majibu hayo, Madaraka alikuwa ameulizwa maswali kadhaa ambayo hakutaka kuyatolea ufafanuzi kutokana na sababu anazozijua yeye.

Maswali hayo yalianza hivi. "Baada ya maongezi yetu ya simu, ningependa kuuliza maswali yafuatayo.

"Katika mkutano wa kampeni wa Arumeru Mashariki, Mbunge wa Musoma Mjini ndugu Vicent Nyerere, alimtupia tuhuma Rais mstaafu ndugu Benjamin Mkapa juu ya kifo cha Baba wa Taifa na katika tuhuma zake Vincent alisema.

"Maamuzi ya kumpeleka Mwalimu Uingereza hayakuridhiwa na familia na Daktari wa familia na Profesa Mwakyusa hakushauri hivyo,je kama mwanafamilia unliongeleaje hili?.

"Vicent amedai pia Mkapa ndiye alimlazimisha Mwalimu akatibiwe Uingereza na Mwalimu hakutaka kutibiwa nje ya nchi, je lina ukweli ama unaliongeleaje hili jambo?.

"Kama familia, je mlijulishwa ugonjwa wa mzee hapa nchini ulikuwa hauwezi kutibika?na je, mlipata fursa ya kujua maendeleo ya ugonjwa wake na baada ya kifo mlipata fursa ya kujua kilichopelekea kifo chake?.

"Kauli ya Vicent inaonyesha kifo cha Mwalimu hakikua cha kawaida bali ni njama za Mzee Mkapa kutaka kumnyamazisha baada ya Mwalimu kupinga sera ya ubinafsishaji, kama familia unaliongeleaje hilo?.

"Taarifa tulizozipata mchana hapa Dar es Salaam, Mzee Mkapa amemuomba Mama Maria awakutanishe na Vicent Nyerere ili kumaliza tofauti zao, je una maoni gani?

"Nini maoni yako juu ya mahusiano ya Mwalim Nyerere na Mzee Mkapa wakati wote wa uhai wa Baba wa Taifa.

"Kama familia mnahisia yoyote mbaya juu ya Mzee Mkapa kutokana na kifo cha Baba wa Taifa?," yalisomeka maswali aliyoulizwa Madaraka.

Mwanzoni mwa wiki, Mkapa alipokuwa akizindua kampeni za CCM jimboni Arumeru Mashariki, alimshambulia Vincent pamoja na Chadema.

Katika hotuba yake hiyo, Mkapa alisema Vincent ambaye ni Naibu Meneja Kampeni wa CHADEMA, anafanya udanganyifu kisiasa wa kutumia jina la Baba wa Taifa wakati yeye siyo familia ya Mwalimu Nyerere.

Mkapa alisema "Mimi nimefanya kazi na Mwalimu Nyerere, hadi nimemzika, sijawahi kusikia jina kama hilo katika familia ya Mwalimu, huu ni udanganyifu wa hatari kwenye siasa, nawasihi wapinzani wetu waeleze sera zao nao wananchi watapima, waache uasi wao," alikaririwa Mkapa.

Kutokana na hali hiyo, Vincent hakutaka kukaa kimya, bali alilazimika kujibu mapigo ili kuweka mambo sawa.

Akiwa katika mikutano ya kampeni jimboni Arumeru Mashariki juzi, mbunge huyo alimshambulia Mkapa na kusema kwamba yeye ndiye aliyeasisi ufisadi na ubinafsishaji wa makampuni usiokuwa na tija nchini.

Pia alimtaka Mkapa aeleze juu ya kifo cha Mwalimu Nyerere na pia aeleze ni kwa nini alilazimisha kumpeleka Mwalimu nchini Uingereza akatibiwe wakati Daktari wake, Profesa David Mwakyusa, alikuwa na uwezo wa kumtibu.

Kwa mujibu wa Vincent, Mkapa anajua siri ya kifo cha Mwalimu Nyerere na kwamba alimlazimisha akatibiwe nchini Uingereza kwa vile alikuwa akimpinga juu ya sera yake ya ubinafsishaji wa mashirika ya umma.

Katika maelezo yake, Vincent alisema baada ya Mwalimu kufariki, Profesa Mwakyusa alishauriwa akagombee ubunge na kwamba atakaposhinda atateuliwa kuwa waziri, jambo ambalo alilifanya na aliposhinda ubunge akateuliwa kuwa Waziri wa Afya.

 
Mpaka mwisho wa kampeni tutasikia mengi sana!
ILa Ben kama ni kweli basi unatisha!
 
Ushauri wa bure Ben rudi arumeru kasawazishe mambo jukwaani na si hizo njia za panya.
 
kijana vicent inaonekana yuko makini sana na inaonekana anajua kila kitu alichokifanya mkapa kuhusu Mwalimu ndoo maana mkapa ameamua kuomba wasulihishwe kupitia mama maria, ila hapa cha msingi inabidi mkapa arudi arumeru akawaombe watanzania msamaha kwa uongo aliousema maana kule alikodanganyia ndoo akaombee msamaha ,,, inaonekana kumbe hizi sera za CCM ni za uongo ndoo maana wanaamua kujichanganya,,,
 
Unavyomwambia mtu kuwa yeye sio mtoto wa mzee fulani ni tusi kwa mama mzazi wa mtoto huyo.
Kumbe mwalimu umeuliwa na hawa mafisadi ili watunyanyase watanzania!!
Too sad
:A S 20: :A S-cry:
 
Yaonekana wazi kuwa uongozi katika nchi hii huendelea kuwa wa kupeana kwa wanandugu. Nasema hivi kwa kauli za Mzee Mkapa kwamba hakuwahi kusikia kabisa kwamba VICENT SI MTOTO WA MWALIMU NYERERE. Kuna haja au umuhimu gani wa kuujua ukoo mzima wa mwalimu Nyerere. Bado unabaki kuwa ule ukiritimba wa mawazo mgando wa kulipana fadhila Ukicheki mlolongo wa viongozi wazee wa nchi hii, utagundua kuwa watoto wao ndo wanatayarishwa kuchukua madaraka. Hata hivyo hili si jambo baya kama watoto hao wanakuwa na uwezo na kukubalika na wananchi. Cha ajabu ni kuwa kwa gharama yoyote ile watoto hawa huwa viongozi wetu. Cheki list. 1. Mzee Mwinyi, Mzee Makamba, Marehemu Mzee Karume .......... . Mungu na alaze maerehemu mwalimu mahali pema peponi Amina kwani ukoo wake bado umebaki karibu kuwa na misimamo ya mwalimu. Mimi binafsi na kwa upeo wangu mdogo wa masuala ya kisiasa katika nchi yetu natambua wazi kabisa kwamba ni nani anayetumia kauli za mwalimu kiuhalisia. Mwalimu Nyerere na uwekezaji/ubinafsishaji wapi na wapi yaani ilikuwa ni vitu viwili tofauti kabisa na wakati fulani aliwahi kuuliza ni kwa nini hata mashirika yalouwa yakifanya vyema katika uzalishaji yaliuzwa viongozi wakabaki wakiangaliana na mwalimu akawaambai 'mimi mtu mzima nikajua tushaliwa'

Eeeh Mungu tuepusha na hawa wafujaji wa maliasili za nchi yetu wakimtumia mwalimu kama ngao yao
 
Jamani naomba tukumbushane alichosema mkapa. Alisema vicent
  1. si mtoto wa mwalimu Nyerere
  2. si mtoto wa familia ya Mwalimu Nyerere
kama 1 ndio sahihi then he Mkapa was right!
 
Jamani naomba tukumbushane alichosema mkapa. Alisema vicent
  1. si mtoto wa mwalimu Nyerere
  2. si mtoto wa familia ya Mwalimu Nyerere
kama 1 ndio sahihi then he Mkapa was right!
Ndio maana anaomba kukutanishwa
 
Back
Top Bottom