Benjamini Mkapa atinga mahakamani kutoa ushahidi kesi Ya Balozi Profesa Costa Mahalu

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,082
Amtetea Profesa Mahalu
headline_bullet.jpg
Ashangaa mashitaka yake
headline_bullet.jpg
Amtaja kuwa mwadilifu



Mkapa(15).jpg

Rais Mstaafu Benjamin Mkapa akisindikizwa kuelekea chumba cha mahakama kutoa ushahidi katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam jana.(PICHA:TRYPHONE MWEJI)



Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa (73), amekiri mahakamani kwamba alikuwa na taarifa za kuwepo kwa mikataba miwili ya ununuzi wa jengo la ubalozi wa Tanzania nchini Italia, na kwamba kama Rais (wakati huo) alibariki ununuzi huo kufanywa na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini humo, Profesa Costa Mahalu (63).


Kadhaka, Mkapa anakuwa Rais Mstaafu wa kwanza nchini kupanda kizimbani kutoa ushahidi wa kumtetea aliyekuwa mteule wake.

Profesa Mahalu na mwenzake wanakabiliwa tuhuma za kuisababishia serikali hasara ya Euro 2,065,827.60.

Mkapa alidai kuwa, yeye pamoja na serikali yake walifahamu utaratibu mzima uliotumika kuanzia mchakato hadi mikataba miwili ya ununuzi wa jengo hilo kukamilika.

Mkapa alitoa ushahidi wa utetezi wa Profesa Mahalu, jana mbele ya Hakimu Mkazi, Mfawidhi, Illivin Mgeta, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Jijini Dar es Salaam.

Akiongozwa na Wakili wa utetezi, Alex Mgongolwa, Mkapa alidai kuwa, kati ya mwaka 1995 na mwaka 2005 alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba Profesa Mahalu alikuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia.

Alidai kuwa, alifanya mazungumzo ya ana kwa ana na Profesa Mahalu kuhusu mchakato mzima na umuhimu wa kununua jengo la ubalozi nchini Italia ambalo lilinunuliwa kwa Euro 3,098,741.40 ili kuepukana na kero ya majengo ya kupanga.

Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Wakili Mgongolwa na Mkapa:

Wakili Mgongolwa: Shahidi katika mwaka 1995 na mwaka 2005 ulikuwa wapi na wadhifa gani?

Mkapa: Nilikuwa Dar es Salaam kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wakili Mgongolwa: Kabla ya kushika wadhifa huo ulipitia nyadhifa gani nyingine?

Mkapa: Kabla sijawa Rais niliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje, Balozi wa Tanzania nchini Nigeria, Canada na Marekani.

Wakili Mgongolwa: Ukiwa Rais wa nchi hii katika kipindi hicho, ulifahamu nini kuhusu ununuzi wa jengo la ubalozi nchini Italia?

Mkapa: Nilifahamu jengo la ubalozi wa Italia lilinunuliwa kwa Euro milioni 3.09 kwa maagizo ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wakili Mgongolwa: Unakumbuka Balozi wa nchi hiyo wakati huo alikuwa ni nani?

Mkapa: Nakumbuka, wakati huo Balozi alikuwa ni Profesa Mahalu.

Wakili Mgongolwa: Je, Mheshimiwa serikali mlifahamu utaratibu uliotumika katika ununuzi wa jengo hilo?
Mkapa: Ndiyo.

Wakili Mgongolwa: Nani alikufahamisha machakato mzima?
Rais Mkapa: Balozi wetu Profesa Mahalu.

Wakili Mgongolwa: Katika manunuzi ya jengo hilo ulipewa taarifa kuhusu masharti ya mmiliki?
Mkapa: Nilitaarifiwa kabla ya ununuzi kufanyika kwamba mmiliki anataka alipwe kwa awamu mbili tofauti.

Wakili Mgongolwa: Kupitia akaunti za nani?
Mkapa: Kupitia akaunti za muuzaji wa jengo.

Wakili Mgongolwa: Je, Mheshimiwa kama Rais wakati huo, ulitoa baraka kuhusu ombi hilo?
Mkapa: Serikali yangu ilitoa baraka na mimi nilitaarifiwa kuhusu hilo.

Wakili Mgongolwa: Walikubaliana mkataba kwa maandishi au kwa njia gani?
Mkapa: Ninachofahamu walitakiwa kulipwa kwa mikataba miwili, lakini kama kulikuwa na suala jingine sifahamu.

Wakili Mgongolwa: Aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi wakati wa uongozi wako, Martin Lumbanga, alikana kufahamu suala la mikataba miwili unasemaje kuhusu hilo?
Mkapa: Ninashangaa kwanini alisema hivyo, lakini serikali ilitoa idhini.

Wakili Mgongolwa: Kama wewe Rais ulijua inawezekana Lumbanga asijue suala hili?
Mkapa: Inawezekana asijue, lakini inakuwa vigumu sana.

Wakili Mgongolwa: Wewe ulijua na ukabariki?
Mkapa: Ndiyo mimi nilijua na nikabariki.

Wakili Mgongolwa: Kwa kumbukumbu zako, wizara ngapi zilihusika?
Mkapa: Wizara za Ujenzi, Ardhi na Fedha.

Aidha, Mkapa aliisomea mahakama taarifa iliyotolewa na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa (wakati huo Rais Jakaya Kikwete), aliyoitoa Bungeni kwamba kati ya mwaka 2001 na 2002 wizara ilinunua jengo la ubalozi nchini Italia kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi na ya Fedha.

Aliendelea kumnukuu Waziri wa Mambo ya Nje wakati huo Kikwete kwa kusema:

“Mheshimiwa Spika hati ya jengo hilo tayari iko wizarani,” alimalizia kusoma taarifa hiyo iliyotolewa bungeni kuhusu ununuzi wa jengo hilo.

Wakili Mgongolwa: Una taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu matumizi mabaya ya fedha juu ya ununuzi wa jengo hilo?
Mkapa: Hapana sikuwahi kupata malalamiko.

Wakili Mgongolwa: Nini ufahamu wako kama Mstaafu kwa aliyekuwa Balozi wako?
Mkapa: Profesa Mahalu ni msomi, mfanyakazi mzuri, mwadilifu na mwaminifu.

Wakili Mgongolwa: Mawasiliano ya Balozi na serikali yalikuwa namna gani?
Mkapa: Balozi anaweza kuandika barua kwa Wizara ya Mambo ya Nje, Katibu Mkuu Kiongozi au kwa Rais.

Wakili Mgongolwa: Ni lazima kuwasiliana kwa njia ya maandishi?
Mkapa: Hapana, mara nyingi kwa maandishi, lakini hata kwa njia ya mdomo.

Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Wakili Mwandamizi wa Serikali, Visent Haule na Mkapa:

Wakili Haule: Je, Mheshimiwa jumla ya fedha zilizotumika ni kiasi gani?
Mkapa: Euro milioni 3.098 ndiyo ninavyofahamu mimi.

Wakili Haule: Nani aliagiza upelelezi ufanyike kuhusu ununuzi wa jengo hilo?
Mkapa: Mimi sijui.

Wakili Haule: Uchunguzi wa kesi hii ulifanyika ukiwa madarakani?
Mkapa: Mimi sijui nilishtukia Balozi ameshtakiwa nikiwa nimetoka madarakani.

Wakili Haule: Lini ulipata taarifa?
Mkapa: Siku aliyoletwa mahakamani kwa mara ya kwanza nilisikia kutoka kwa watu niliowateuwa kushika nyadhifa mbalimbali wakati nikiwa madarakani na siku ya pili yake nilisoma kwenye magazeti ndipo nikahakikisha.

Wakili Haule: Nani alikupa taarifa kama mmiliki wa jengo anataka kulipwa kwa awamu mbili (akaunti mbili) tofauti?
Mkapa: Kwa njia ya mdomo.

Wakili Haule: Nani alikupa taarifa?
Mkapa: Profesa Mahalu ndiye alinipa taarifa za kupata jengo.

Wakili Haule: Alikupa kabla au baada ya ununuzi?
Mkapa: Alikuwa ananipa taarifa kabla kwa sababu wakati huo kuna nchi zilikuwa na shida kama hiyo.

Wakili Haule: Unasema ulitaarifiwa na hukuzuia kwani ulitakiwa kuzuia?
Mkapa: Ningeweza kuzuia kwa sababu nilikuwa Mkuu wa nchi, lakini niliona umuhimu wake kama Profesa alivyonieleza.

Wakili Haule: Ulimruhusu Profesa Mahalu kununua jengo kwa awamu mbili au?
Mkapa: Nilimruhusu Mahalu kununua jengo masuala mengine hayakuwa mikononi mwangu.

Wakili Haule: Wakati unatoa ruhusa hiyo kulikuwa na mtu mwingine?
Mkapa: Hapana.

Wakili Haule: Ulitoa kwa njia ya mdomo au simu?
Mkapa: Ilikuwa na mazungumzo ya ana kwa ana kabisa.

Wakili Haule: Baada ya maagizo hayo nani mwingine ulimuagiza kuhusu ununuzi wa jengo hilo?
Mkapa: Nilitoa maagizo utekelezaji ni suala la wizara.

Wakili Haule: Sawa. Je, nani alihusika?
Mkapa: Ilikuwa ni wajibu wake Profesa Mahalu kuieleza wizara yake kwamba hayo maamuzi yalikuwa sahihi.

Wakili Haule: Kwa hiyo, wizara hukuiambia chochote bali ni Mahalu tu ni kweli au siyo kweli?
Mkapa: Kama Rais ilikuwa wajibu wangu kutoa amri tu.

Wakili Haule: Mheshimiwa jibu kama kweli au siyo kweli?
Mkapa: Sikumbuki.

Wakili Haule: Je, unafahamu kuna viongozi wengine uliowahi kuwateua wakati wa uongozi wako na wameburuzwa mahakamani?

Mkapa: Ndiyo, nafahamu kuwa Basil Mramba, Daniel Yona na Gray Mgonja.

Naye Wakili wa Serikali Mwandamizi Ponsiano Lukosi, alimhoji shahidi kama ifuatavyo:

Wakili Lukosi: Mheshimiwa, Lumbanga alikuwa Katibu Mkuu Kiongozi wakati wa utawala wako?
Mkapa: Ni kweli.

Wakili Lukosi: Aliongoza miaka mingapi?
Mkapa: Miaka yote niliyokuwa madarakani.

Wakili Lukosi: Sifa za Lumbanga na Mahalu zinalingana?
Mkapa: Yah, ni sawa.

Wakili Lukosi: Lumbanga alikanusha kufahamu mikataba miwili ni sawa?
Mkapa: Nashangaa kama hili hakulijua.

Wakili Lukosi: Ulizindua lini jengo hilo la ubalozi?
Mkapa: Nilizindua Februari 23, mwaka 2003.

Wakili Lukosi: Ulikwenda Italia kuzindua jengo au?
Mkapa: Hapana, nilikwenda nchini Italia kikazi hivyo nikaalikwa kuzindua jengo hilo.

Naye Wakili wa Utetezi Mabere Marando alimhoji shahidi kama hivi:

Wakili Marando: Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) waliwahi kukuambia kama kuna uchafu umetokea kuhusu ununuzi wa jengo hilo?
Rais Mkapa: Hapana hawakuniambia.

Kesi hiyo inaendelea leo ambapo mshtakiwa wa pili, Grace Martin, atatoa ushahidi wake.

ILIVYOKUWA MAHAKAMANI

Mapema saa 3:45 asubuhi, Rais Mstaafu Mkapa, aliingia kwenye viunga vya mahakama hiyo akiwa kwenye gari yenye namba za usaji T 745 BQE aina ya Toyota Land Cruiser V8 ya rangi nyeusi pamoja na walinzi wake.

Rais huyo maarufu kwa jina la Mzee wa Uwazi na Ukweli, alikuwa amevaa kaunda suti ya rangi ya kijivu na viatu vya rangi nyeusi na aliongozwa moja kwa moja hadi ofisi ya Hakimu Mfawidhi kwa ajili ya kusubiri muda wa kuingia mahakamani kutoa ushahidi wake.

Saa 4:45 alianza kutoa ushahidi wa kumtetea Profesa Mahalu kwa kuongozwa na Wakili Mgongolwa hadi saa 7:17 mchana kisha kuondoka katika viwanja vya mahakama hiyo.

Mapema jana saa 1:45 asubuhi NIPASHE lilishuhudia walinzi wa Rais huyo wa zamani wakiwa katika viunga vya mahakama hiyo kwa ajili ya maandalizi ya bosi wao kufika mahakamani hapo.

Wakili Marando alisema kuwa Mkapa alipaswa kutoa ushahidi wake leo, lakini aliombwa kufika jana kwa kuwa leo atasafiri nje ya nchi.





CHANZO: NIPASHE

=====

KESI YA BALOZI MAHALU: Mkapa akunjua makucha

na Happiness Katabazi

HATIMAYE utetezi wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu, umetua rasmi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu jijini Dar es Salaam.

Mkapa ambaye ni shahidi wa pili wa kesi hiyo alitoa utetezi huo ambao unaweza kuandika historia mpya katika mwenendo wa kesi nchini, kupitia kiapo chake ambacho kimewasilishwa mahakamani na wakili wa mshtakiwa huyo, Mabere Marando.

Katika moja ya vipengele 13 vya kiapo hicho, pasipo kutaja jina, maelezo ya kiongozi huyo mstaafu yanamgusa Rais Jakaya Kikwete ambaye wakati Mkapa akiwa madarakani alikuwa ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Hiyo inakuwa ni mara ya kwanza kwa rais mstaafu, kutoa utetezi mahakamani kwa kesi inayomgusa mmoja wa waliokuwa wateule wake wakati akiwa madarakani.

Kesi hiyo Namba 1/2007 ambayo Mahalu anashtakiwa pamoja na Grace Martin inasikilizwa na Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Ilivin Mugeta.

Katika kesi hiyo, Mahalu na Martin wanatuhumiwa kwa wizi wa shilingi bilioni tatu katika ununuzi wa jengo la ubalozi mjini Rome.

Katika hati ya kiapo chake cha Machi 31 mwaka huu, ambayo imeandaliwa kwa mujibu wa Sheria ya Usajili wa Nyaraka (The Registration of Documents Act, Cap. 117 of 2002), Mkapa anaeleza kuwa kila kilichofanywa na Mahalu kilikuwa sahihi na kilikuwa na baraka ya serikali aliyokuwa akiingoza toka mwaka 1995-2005.

Ushahidi huo wa rais Mkapa ambao Tanzania Daima inayo nakala yake, umeorodhesha maelezo yake yaliyoainishwa katika vipengele 13.

Mkapa katika utetezi wake huo anadai kuwa mchakato mzima wa ununuzi wa jengo hilo la ubalozi lililoko katika mtaa wa Vialle Cortina d’Ampezzo 185 mjini Rome ulizingatia sera ya serikali ya upatikanaji au ujenzi wa majengo ya kudumu ya ofisi na makazi na kwamba ulizingatia maslahi ya taifa.

Hati hiyo ya kiapo ambayo tayari wakili Marando amesema ameishaiwasilisha pia Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) Eliezer Feleshi, inaanza kwa kusema, “Mimi Benjamin Mkapa, mtu mzima, Mkristo, mkazi wa Dar es Salaam, ninaapa kama ifuatavyo, ’nilikuwa Rais mtendaji wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa vipindi viliwili mwaka 1995-2005 na nina uhakika wa yote haya nitakayosema ndani ya kiapo hiki.’

Katika kiapo hicho Mkapa anadai pia kuwa alifahamishwa na watendaji wa serikali aliyokuwa akiingoza jinsi mchakato uliofanyika na ripoti za uthamini wa serikali zilizotumika katika kufikia hatua ya kununua jengo hilo la ubalozi.

Anadai kuwa tathmini ya jengo hilo ambalo Mahalu anadaiwa kufanya udanganyifu na wizi kwa kulipa fedha kinyume na ilivyotajwa katika mkataba ambayo ilifanywa na serikali ya awamu ya tatu kupitia wizara mbili tofauti, Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Ardhi na Maendeleo Mijini.

Anaendelea kudai kuwa, anatambua kuwa ripoti ya serikali ya uthamini wa jengo hilo iliandaliwa na Wizara ya Ujenzi kwa kiwango cha dola za Marekani milioni tatu na Wizara ya Ardhi kwa thamani ya euro milioni 5.5.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo kupitia mchakato wa ununuzi wa jengo hilo ulikuwa wa aina mbili, mmoja ni rasmi na mwingine wa kibiashara na kuongeza kuwa kwa mujibu wa taratibu ya serikali ya Italia na kuwa hilo lilifanyika kwa baraka za serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Utaratibu kama huo wa mikataba miwili ushawahi kufanywa na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pale ambapo ilionekana haja kwa kuzingatia maslahi ya taifa kwanza....na kuwa ni mimi ndiye niliyezindua jengo hilo la ubalozi Februari 23 mwaka 2003,” anadai Mkapa.

Shahidi huyo wa Mahalu anadai pia kuwa kwa mujibu wa kiapo chake anakumbuka vyema taarifa ya serikali iliyotolewa bungeni Agosti 3 mwaka 2004 iliyosema na kuthibitisha kuwa taratibu zote zinazohusiana na manunuzi ya jengo kwa mujibu wa maelekezo ya serikali, zilifuatwa na kwamba muuzaji wa jengo hiilo alilipwa fedha zote.

Kumbukumbu ambazo gazeti hili linazo zinaonyesha kwamba, Agosti 3, 2004, Kikwete alitoa maelezo bungeni kuhusu utata uliokuwapo awali kuhusu ununuzi wa jengo hilo la ubalozi.

Kikwete katika maelezo yake hayo ambayo yako pia katika kumbukumbu rasmi za Bunge (Hansard) anaeleza, “Mheshimiwa Naibu Spika mwaka 2001/02 wizara ilinunua jengo la ubalozi counsel katika ubalozi wa Rome katika jitihada za kuondokana na tatizo la kupanga majumba ya watu huko nje na pia kupunguza gharama za kuendelea kulipa pango la nyumba kila mwaka.

“Ununuzi wa jengo hili ulifuata taratibu zote za manunuzi ya majengo ya serikali kwa kuzishirikisha wizara za ujenzi, ardhi na maendeleo ya makazi pamoja na Wizara ya Fedha.

“...Jengo lilifanyiwa tathmini na wataalamu wetu na kukubaliana na ununuzi wa Euro 3,098,781.40 tarehe 6 Machi 2002 fedha za awamu ya kwanza katika ubalozi wa Rome zilipelekwa nazo zilikuwa shilingi 700,000,000 tarehe 28 Juni 2002 zilipelekwa shilingi 120, 000,000.

“Mwishoni mwa tarehe 26 Agosti mwaka 2002 zilipelekwa shilingi 1,000,000,000 jumla ya fedha zilizokuwa zimepelekwa zikafikia shilingi 2,900,000,000 na baada ya hapo ubalozi wetu ulitekeleza taratibu zote za ununuzi wa jengo na kumlipa mwenye nyuma kiasi hicho cha fedha,” alieleza Kikwete.

Akimwelezea Mahalu katika utetezi wake, Mkapa alidai katika kipindi chote alichokuwa rais wa nchi alifanya kazi na mshtakiwa huyo katika nyadhifa mbalimbali za utumishi wa umma na kwamba mshtakiwa huyo ni mtu wa tabia njema, mkweli, mwaminifu na mchapaji kazi.

Mkapa anahitimisha utetezi wake kwa kueleza kuwa, kutokana na mwenendo huo wa kutukuka, Rais wa Italia alimpatia moja ya tuzo za heshima yenye hadhi ya juu kabisa ya taifa hilo Profesa Mahalu, muda mrefu baada ya balozi huyo kuwa ameshaondoka nchini humo.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuwasilisha mahakamani ushahidi huo wa Mkapa jana, wakili Marando alisema mteja wake anakusudia kupeleka jumla ya mashahidi 10.

Mashahidi hao ni mteja wake (Mahalu), Mkapa, Rais Jakaya Kikwete, kwani wakati akinunua jengo hilo ndiye alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ambaye ndiye alimpa mteja wake nguvu ya kisheria ya kuendelea na ununuzi wa jengo hilo, aliyekuwa waziri wa Ujenzi wa John Magufuli na mashahidi wengine na aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba ambaye pia anakabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bil. 11.7.

Kuwasilishwa kwa hati ya kiapo cha Mkapa mahakamani hapo, kumekuja baada ya Hakimu Mkuu Mfawidhi Ilvin Mugeta kusema kuwa yeye ndiye amejipangia kusikiliza utetezi wa washtakiwa hao Aprili 28 mwaka huu.

Hatua ya Hakimu Mugeta kusikiliza utetezi huo inakuja baada ya Machi 28 mwaka huu, Jaji Sivangilwa Mwangesi ambaye ndiye aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo tangu awali kujitoa baada ya mawakili wa washtakiwa kuwasilisha sababu sita za kumwomba ajitoe kwa sababu kukosa imani naye Machi 25 mwaka huu.

Mapema mwaka 2007, Jamhuri kupitia mawakili wake toka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ben Lincoln na Ponsian Lukosi iliwafikisha mahakamani hapo kwa mara ya kwanza washtakiwa hao kwa makosa ya uhujumu uchumi, wizi wa zaidi ya euro milioni mbili wakati wakisimamia ununuzi wa jengo la ubalozi mjini Rome nchini Italia.
 
Back
Top Bottom