Ochu
JF-Expert Member
- May 13, 2008
- 975
- 47
Na Burhani Yakub Lushoto
RAIS wa serikali ya awamu ya tatu, Benjamin Mkapa jana alikuwa kivutio wakati alipopangua maswali ya wanafunzi kuhusu wimbi la migomo kwenye vyuo vya elimu ya juu, akisema na yeye "sasa ni mwanafunzi mwenzao".
Mkapa alikuwa Chuo Kikuu cha Sekuco kilicho wilayani hapa akiwa amealikwa kutoa mada katika mdahalo wa wazi wa wanafunzi wa chuo hicho kikuu kishiriki cha Tumaini. Mkapa alishangiliwa sana na wanachuo kutokana na umahiri wake wakati wa kuwasilisha mada yake.
Lakini hali iligeuka wakati wa kipindi cha maswali baada ya naibu mkuu wa chuo hicho, Dk. Fanuel Shechambo kuwapa wanafunzi nafasi ya kuuliza maswali.
Mwanachuo aliyejitambulisha kwa jina la Ogaka Lameck wa mwaka wa kwanza ambaye anasomea Ualimu, alimtaka Mkapa kueleza kwa nini serikali inakwepa kutekeleza jukumu lake la kuwapa mikopo wanafunzi wa vyuo kikuu na hivyo kusababisha migomo ya mara kwa mara.
Mwanachuo huyo alifafanua kuwa migogoro ya wanafunzi ilikuwepo katika awamu zilizopita, ikiwemo ya Mkapa, lakini akasema kwa sasa migogoro hiyo inaonekana kuzidi na hivyo kuhoji kwa nini zisitafuwe njia za kuitatua kutokana na ukweli kuwa wasomi wa vyuo vikuuu ndiyo rasilimali ya maendeleo ya nchi.
Lakini Mkapa hakutaka kutoa maelezo marefu kujibu swali hilo akijitetea kuwa ameshamaliza kipindi chake cha uongozi na kwamba hivi sasa anasoma, ingawa hakutaka kuelezea anasomea nini.
"Mimi si rais kwa sasa," alisema rais huyo aliyeiongoza nchi kutoka mwaka 1995 hadi 2005. "Mimi ni mwanafunzi kama nyinyi... hamuoni kama mnatumia muda wenu kumuuliza maswali mwanafunzi mwenzenu,"aliongeza na kusababisha wanafunzi ukumbi wote kucheka.
Mkapa aliwahi kuongoza Wizara ya Sayansi na Elimu ya Juu mwanzoni mwa miaka ya tisini baada ya kumalizika kwa mgomo mkubwa wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam mwaka 1990 uliosababisha wanafunzi kurudishwa nyumbani kwa takriban miezi nane.
Katika kipindi chake cha urais hakukumbana na migomo mikubwa ya wanafunzi.
Katika siku za karibuni serikali imelazimika kufunga vyuo vikuu saba baada ya wanafunzi kugoma kuingia madarasani wakishinikiza kupewa mkopo kwa asilimia 100 badala ya utaratibu wa sasa wa kuchambua uwezo wa kiuchumi wa mwanafunzi na baadaye kuamua alipie kwa asilimia ngapi. Hata hivyo, serikali imekataa katukatu na kueleza kuwa sera hiyo ya uchangiaji elimu itadumu.
Akiwasilisha mada ya "Wajibu wa Elimu ya Juu Katika Maendeleo," rais huyo mstaafu alisema ili kujenga maendeleo ya kweli ni lazima kuwe na uwiamo katika utoaji wa elimu kwa kuzingatia jinsia na makundi ya walemavu.
Alisema kufanya hivyo kutasaidia kutawanya ujuzi na hivyo kuiwezesha jamii kuwa na uwezo wa kujitegemea.
Katika mada yake Mkapa alisema kwa Tanzania na nchi zinazoendelea ni lazima wasomi wa elimu ya juu waondokane na kasumba ya kutegemea kuajiriwa baada ya kuhitimu masomo na badala yake wajikite katika kubuni njia za uzalishaji na ufundi.
Akitoa shukrani kwa Mkapa, askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, DK. Steven Munga alimsifu kwa umahiri alioonyesha wakati akiwasilisha mada hiyo.
Dk. Munga, ambaye Dayosisi yake ndiyo inayoendesha chuo hicho alisema uongozi uliamua kumwalika Mkapa kutoa mada hiyo ikiwa ni mipango yake ya kuwaalika wasomi mashuhuri na kwamba mpango huo utakuwa ukifanyika kila mwaka.
"Tumemwalika Mkapa kwa kuwa ni kiongozi wa kwanza katika ukanda huu wa Afrika Mashariki kutunukiwa sahada ya falsafa ya udaktari na Chuo Kikuu cha Cape Coast cha Ghana," alisema Askofu Munga na kuviomba vyuo vingine vikuu nchini kumtumia kwa kuwa ameonyesha uwezo mkubwa.
Chuo hicho kilianzishwa rasmi mwaka jana kikiwa na jumla ya wanachuo 138 sasa wameongezeka hadi kufikia 450.