Mjumbe wa CPC ajitolea kuwasaidia watoto wa kike kupata elimu

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
fsafdgfds.png


vcbcvbfhjghfj.jpg

Mwaka 1995 ulikuwa ni mbaya sana katika maisha ya Zhang Guimei, kwani ni mwaka ambao alimpoteza mume wake mpenzi aliyefariki kutokana na kuugua saratani, baada ya kutumia akiba yao yote kumpatia matibabu.

Zhang Guimei ambaye amechaguliwa kuwa mjumbe wa Mkutano Mkuu wa 20 wa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC), alizaliwa mwaka 1957 mkoani Heilongjiang, na alikwenda mjini Dali, mkoa wa Yunnan mwaka 1974, ambako alikuwa mwalimu pamoja na mume wake.

Baada ya mumewe kufariki, aliamua kuhama kutoka mji wa Dali na kwenda kufundisha katika kaunti ya Huaping iliyoko sehemu za milimani katika mji wa Lijiang, mkoani Yunnan. Uamuzi huo haukubadilisha maisha yake tu, bali pia maisha ya watoto wanaoishi katika maeneo ya ndani zaidi milimani. Ingawa alihamia huko katika kipindi kigumu zaidi katika maisha yake, lakini aliweza kupeleka nuru iliyoangaza maisha ya wengine.

Bibi Zhang, aliona kuwa watoto wengi wa kike wanaacha shule, na alipotembelea familia zao, aligundua kuwa umasikini na wazazi kutounga mkono kumsomesha mtoto wa kike na kuwalazimisha kuolewa mapema, ndio sababu kuu za watoto wa kile kuacha shule.

Jambo hili lilimfanya kuchukua hatua ya kuanzisha shule za sekondari zinazotoa kipaumbele kwa watoto wa kike katika eneo hilo. Alijaribu kuchangisha fedha ili kutimiza mahitaji ya watoto hao, lakini watu wengi hawakuwa na imani naye, wakiamini kuwa alikuwa ana njama za kuwaibia.

Mwaka 2007, alipata fursa ya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Mkutano Mkuu wa 17 wa CPC, na baada ya kufanya mahojiano na kueleza nia yake ya kuwaendeleza kielimu watoto wa kike, serikali ya Lijiang ilimsaidia kutimiza ndoto hiyo, na mwaka 2008 Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Lijiang Huangping ilianzishwa, na Zhang kuwa mkuu wa shule hiyo.

Tangu kuanzishwa kwa shule hiyo, wanafunzi zaidi ya 2,000 wa kile wamepata fursa ya kupata elimu na kuwa na maisha mazuri, na shule hiyo kuwa moja kati ya shule bora katika mji wa Lijiang.

Suala la elimu kwa mtoto wa kike limekuwa likitiliwa sana mkazo katika zama hizi, kwani mtoto wa kike ana haki sawa ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume.

Katika baadhi ya nchi za Afrika, elimu kwa mtoto wa kike ilikuwa ikipuuzwa, kwani wazazi waliamini kuwa mtoto wa kike hana haja ya kupata elimu kwani ataolewa na kuanzisha familia, na hivyo kuwa na tatizo kubwa la ndoa za utotoni. Lakini hivi sasa hali imebadilika, na tunashuhudia watoto wa kike wakifanya vizuri katika sekta ya elimu sawasawa, na hata kuwazidi watoto wa kiume.

Mwalimu Zakia Kassim wa Shule ya Msingi Sunrise mjini Dar es Salaam, Tanzania, anasema elimu kwa mtoto wa kike ni muhimu sana kwani humsaidia kujitambua, ikiwa na maana kuwa atakuwa na uwezo wa kujikinga na mimba pamoja na ndoa za utotoni, na atafahamu nafasi yake katika jamii, na kwamba yeye ana haki ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume, na pia anaweza kujishughulisha na biashara ama kufanya kazi ili kujiingizia kipato na kuacha kuwa tegemezi.

Katika kuhakikisha kuwa mtoto wa kike anapata nafasi ya kusoma na kujiendeleza zaidi kielimu, Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake nchini Tanzania (TAMWA) kimeendesha kampeni kadhaa za kuongeza uelewa kwa wazazi na walezi kuwasomesha watoto wa kike.

Mkurugenzi wa TAMWA Dr. Rose Reuben anasema, kupitia kampeni hizo kwa kushirikiana na asasi nyigine za kijamii, hivi sasa wanafunzi wa kike waliopata ujauzito wanaruhusiwa kurudi shule baada ya kujifungua, jambo ambalo linaonyesha kuwa nchi hiyo inajali sana maendeleo ya mtoto wa kike.

Hatua hiyo pia inamwezesha mtoto wa kike kuweza kupambana na kukabiliana na changamoto mbalimbali za maisha katika siku za baadaye, na kikubwa zaidi, ni kuchangia katika maendeleo yao wenyewe binafsi, familia, na taifa kwa ujumla.

Kwa ufupi, elimu kwa mtoto wa kike ina umuhimu mkubwa katika kumjengea msingi bora wa maisha yake ya baadaye, kwani kumsomesha mtoto wa kike, ni sawa na kusomesha jamii nzima!
 
Back
Top Bottom