Mjue Vyema Shamhuna Naibu Waziri Kiongozi Zenji

Mtu wa Pwani

JF-Expert Member
Dec 26, 2006
4,184
671
Shamhuna na kadhia ya uhuru wa habariNa Jabir Idrissa
ALI Juma Shamhuna ni Waziri wa Habari katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Ni mjuzi wa mambo na anajua huwa anajua hasa maana ya kile anachokisema.

Mwaka jana aliifuja taaluma ya uandishi wa habari kwa kusema si mhimili wa nne wa dola kama wanataaluma wake wanavyoamini.

“Nyinyi si mhimili wa nne bwana, mhimili gani usiotambuliwa na Katiba,” aliwaambia waandishi kadhaa wa habari waliokuwa nje ya ukumbi wa Baraza la Wawakilishi wakijitahidi kushawishi wajumbe wa baraza hilo kukataa muswada wa sheria uliokuwa unawasilishwa.

Muswada huo ulikuwa una vipengele kadhaa ambavyo kupitishwa kwake kulikuwa na maana ya kukwaza waandishi wa habari katika kukusanya na kutoa habari.

Ulielekezwa kwenye kuzuia kutolewa kwa taarifa nyeti zinazohusu wajumbe wa Baraza la Wawakilishi pamoja na taarifa za shughuli za baraza hilo.

Muswada ulipitishwa bila ya mabadiliko yoyote, huku tamko la waandishi wa habari wapatao 50 waliolipinga, likidharauliwa kama si lolote si chochote. Leo hii, sheria hiyo ipo na inafanya kazi na inaendeleza mfululizo wa sheria kadhaa zinazoshurutisha utoaji wa habari.

Lakini kwenye meza kuu ya kongamano la kutwa moja lililofanyika siku ya maadhimishio ya kimataifa ya uhuru wa vyombo vya habari lililoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) Ofisi ya Zanzibar, Shamhuna “alibadilika.”

“Natambua na serikali inatambua kuwa vyombo vya habari ni mhimili wa nne,” alisema katika hotuba ya ufunguzi wa kongamano hilo ambalo lilihudhuriwa na Rais wa MCT, Profesa Issa Shivji. Lilifanyikia Hoteli ya Bwawani, mjini Zanzibar.

Huyu ndiye Ali Juma Shumhuna. Ni mwanasiasa mwenye tambo nyingi na ambaye kubadilika, kwake si tatizo, bali ni jambo la kuzingatia tu wakati. Anapoona lazima kupinga kitu, anapinga kama ambavyo atafanya akiona kitu hichohicho “sasa ni wakati wa kukikubali.”

Aliwahi kupinga kuanzishwa kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Maji nchini (SUMATRA) pendekezo hilo lilipofikishwa mbele ya wawakilishi waliokutanishwa katika semina kwenye ukumbi wa Baraza wa mjini Wete, Kaskazini Pemba mwaka 2003.

Lakini miaka miwili baadaye, alikubali kuanzishwa mamlaka hiyo wakati muswada wake ulipowasilishwa barazani ili upitishwe na kuruhusu shughuli za SUMATRA ziruhusiwe hadi Zanzibar.

Wakati alipopinga, Shamhuna alikuwa mjumbe tu katika Baraza na akiongoza kikundi kilichojipa jina la Pentagon, alipolikubali, ni baada ya kuteuliwa Waziri wa Habari.

Kama kauli yake hiyo mpya kuhusu vyombo vya habari kuwa ni mhimili wa dola, imetoka ndani ya moyo wake, si tu kinywani mwake, yeye ndiye anayefahamu zaidi. Lakini inatosha kusema waziri anayesimamia masuala ya habari Zanzibar, ametambua umuhimu wa vyombo vya habari kuwa huru.

Kitu kimoja hajakisema: kwamba lile gazeti alilolitamkia kuwa “limezikwa kabisa” ndio haliwezi kupatiwa kibali tena cha kusajiliwa? Hiki bado ni kitendawili.

Mwaka 2006 alipokuwa akifanya majumuisho ya michango ya wajumbe wakati wa kujadiliwa kwa makadirio ya mapato ya bajeti ya wizara hiyo, alisema kuhusu gazeti la Dira, lililofungiwa mwaka mmoja tu baada ya kuruhusiwa kuchapishwa Zanzibar:

“Gazeti la Dira siyo tu kwamba limefungiwa. Kwa hakika hili limezikwa kabisa.”

Alitamka hayo wakati akijua fika kwamba kwenye meza ya Msajili wa magazeti, kulikuwa na jalada la kampuni ya ZIMCO, ya kutaka kupatiwa kibali cha kusajiliwa gazeti hilo.

Ni dhahiri alikuwa anamwamrisha msajili huyo au mtendaji mwingine yeyote katika wizara yake, asithubutu kulipatia kibali gazeti la Dira, ambalo baada ya kufungua kesi ya kupinga amri ya aliyemtangulia kuwa Waziri wa Habari, Salim Juma Othman, Jaji Bakari Ali Mshibe alisema kwa kuwa gazeti hilo halikuwa limesajiliwa kihalali, wenyewe wanaruhusiwa kuomba upya kibali na akasema serikali haitakuwa na pingamizi yoyote.

Sasa ni miaka miwili tangu maombi ya ZIMCO yafikishwe serikalini lakini hakuna majibu rasmi yaliyotolewa na Msajili. Wamiliki wa ZIMCO, akiwemo Salim Said Salim, aliyehudhuria kongamano la MCT, wanaamini kauli ya Waziri Shamhuna ndani ya Baraza la Wawakilishi yalikuwa majibu rasmi ya Serikali. Serikali ni zaidi ya Msajili, ofisa anayewajibika kwa Waziri Shamhuna.

Shamhuna ambaye pia ni Naibu Waziri Kiongozi, ni mmoja wa mawaziri wachache mno wa SMZ waliokuwa
wakiandika makala zilizochapishwa na Dira kwa majina bandia, zikitoa msimamo tofauti na wa serikali ya Rais Amani Karume.

Basi hii ndio hali ya mambo katika kada ya habari. Waziri Shamhuna pamoja na wakuu wa vyombo vya habari vinavyosimamiwa na serikali, wanaamini Zanzibar kuna uhuru wa kutosha wa habari.

Tena wanasisitiza kuwa serikali itaendelea kufanya kila iwezalo kuhakikisha vyombo hivi vinafanya kazi kwa uhuru zaidi. Ila wanasema pia lazima waandishi wa habari waheshimu maadili ya taaaluma pamoja na sheria za nchi.

Laiti kama kuheshimu maadili pamoja na sheria za nchi kunatosha kutambulisha mwandishi au chombo cha habari kuwa kinatumia vizuri uhuru wa habari, basi gazeti la Dira lisingefungiwa wala waandishi wanaoikosoa wasingedhalilishwa.

Lisingefungiwa kwa sababu kwa mwaka mzima liliokuwa linachapishwa, Serikali ilishindwa kutumia fursa adhimu ya kukanusha taarifa zilizokuwa zikitolewa dhidi yake, licha ya kupatiwa ukurasa mzima gazetini humo kila wiki kwa ajili ya kujieleza.

Wakati iliridhiwa na Kamati ya Maadili ya MCT, ilipofungua malalamiko dhidi ya DIRA mwaka 2003, serikali ilishindwa kesi ya madai iliyofunguliwa na ZIMCO kwenye Mahakama Kuu kupinga amri ya Waziri kulifungia gazeti hilo.

Uamuzi uliotolewa na Jaji Mshibe ulimaanisha kuwa Dira halikufanya kosa lolote katika umri wa uhai wake ndio maana hakuna palipoelezwa kwamba “lilitenda kosa.”

Aliloliona ni kosa, kwamba Dira halikusajiliwa kihalali kwa mujibu wa sheria, halikuwa la wamiliki wake ambao waliomba kibali cha gazeti kulingana na sheria inavyotaka na walipewa majibu ya kuendesha gazeti hilo.

Nani waliokosea, si kazi ya ZIMCO kusem, na hilo halikupata kuulizwa hata mara moja. Hata wakati wa usikilizaji wa kesi hiyo, upande wa serikali haukuwahi hata mara moja kutoa hoja kuwa DIRA halikusajiliwa kisheria.

Ukweli huu pia ulithibitisha namna uamuzi wa mahakama ulivyokuwa wa kutatanisha. Kwamba jaji alitoa “shufaa” ambayo haikuwahi kuombwa na yeyote katika pande zilizokuwa mahakamani.

Inafurahisha kuona kongamano lilitoa sauti ya kutaka gazeti hilo liruhusiwe kuchapishwa kwa kuwa lilikuwa la manufaa makubwa kwa jamii.

Waandishi wa habari na wadau waliohudhuria kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari walikuwa na maoni yanayofanana kuwa hata kama uhuru wa habari upo, yapo mazonge mengi yanahitaji kurekebishwa ili kuuthibitisha.

Hata sheria zenyewe zinazohusu uanzishwaji wa vyombo vya habari zina matatizo mengi yakiwemo ya kuwapa viongozi wa serikali madaraka makubwa ya kufungia gazeti au kituo cha redio na televisheni “bila ya kulazimika kutoa sababu.”

Polisi, taasisi ya kidola yenye jukumu zito la ulinzi na usalama wa raia na mali zao, wamepewa mamlaka ya kuingia kwenye ofisi za taasisi ya habari na kuchakura watakacho na kuzuia watakacho.

Si hasha kwamba sheria hiyo mpaka leo imetambuliwa kama moja ya sheria mbaya (zinazokandamiza uhuru wa kiraia) zinazopaswa kufutwa kwa kupingana na Katiba ya nchi.

source mwanahalisi
 
Mwaka jana - “Nyinyi si mhimili wa nne bwana, mhimili gani usiotambuliwa na Katiba,” ...
Lakini kwenye meza kuu ya kongamano la kutwa moja lililofanyika siku ya maadhimishio ya kimataifa ya uhuru wa vyombo vya habari lililoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) Ofisi ya Zanzibar, Shamhuna “alibadilika.”

“Natambua na serikali inatambua kuwa vyombo vya habari ni mhimili wa nne,”...
Mkuu, hizi ndio siasa za Tanzania na hasa CCM inapoelekea kwenye uchaguzi. Kumbuka dharau za Mkapa dhidi ya waandishi wazawa na jinsi walivyomwajibisha Mapuri alivyochemsha karibu na uchaguzi ilhali alikuwa 'reflection' ya Mkapa!! Watasifia kwamba ni muhimili wa nne pale tunapoelekea uchaguzi!! Kidogo JK kajitahidi!

Hapa ni dhahili Mh. Shamhuna atagombea uRais wa Zanzibar 2010; anachojaribu kufanya ni kujivisha ngozi ya kondoo bila kujari kama anakula maneno yake au la!! Siasa za namna hii waandishi wa habari inabidi tuzishtukie, iwaje jana tulikuwa si muhimu kisha leo tunapoelekea uchaguzi tunapambwa na kupakwa mafuta?

Shamhuna ambaye pia ni Naibu Waziri Kiongozi, ni mmoja wa mawaziri wachache mno wa SMZ waliokuwa wakiandika makala zilizochapishwa na Dira kwa majina bandia, zikitoa msimamo tofauti na wa serikali ya Rais Amani Karume.
Huyu si kiongozi bali mrafi wa madaraka!! Ni kiongozi asiyefaa hata kidogo; kama kweli alikuwa akiandikia DIRA tena makala za kupinga misimamo ya utawala wa Karume, iweje sasa aligeuke baada ya kupata uongozi?!
 
Duh!

asante mtu wa pwani..huyu jamaa bado yuko madarakani tuu?


yes ni naibu waziri kiongozi na pia waziri wa habari utangazaji na michezo,ofisi yake ipo pale migombani zanzibar.
wizara yake kuna vichwa vitupu,naibu waziri wake ni mheshimiwa mahmoud thabit kombo,katibu mkuu ni dr dadi shajjack(jamaa kutoka pemba).
 
Wenzangu, salaam?

Nadhani sasa ni wakati muafaka wa kuweka wazi yale madili aliyofanya huyu bwana kwa jina la Ammy Mpungwe...wakati akina yona na mkapa wakiandaliwa kesi kwenda kwa vyombo vya sheria haitokuwa sawa huyu bwana akiachwa...si vizuri kumsahau...nadhani huyu ni fisadi mwalimu...huenda wengi wao wamejifunzia kwao...nadhani huyu ndo mwalimu wao hawa woote mnaowaona sasa...alicheza michezo michafu kuanzia pale NBC, TBL, TANESCO (yeye ndo alialeta wale wazungu), Madini kule mererani...and was/ is among the top men in their boards...si mnakumbuka alikuwa balozi kule south africa? nadhani kuna mtu alimtuma akafanye madili yale na alipomaliza akaacha ubalozi na kurudi bongo kusimamia uendeshaji wake...
 
mbali ya yote mheshimiwa alipoenda jimboni kwake donge alizungumza vyengine na alipoona mambo hayako shwari akazungumza vyengine na BBC huyu ndie Mkuu Shamhuna.

ZFA na wao wanamjua vyema Alhajj Shamhuna na nimesikia wameowa nyumba moja na aliekuwa Mhariri wa gazeti la dira Marehemu Ali Nabwa
 
yes ni naibu waziri kiongozi na pia waziri wa habari utangazaji na michezo,ofisi yake ipo pale migombani zanzibar.
wizara yake kuna vichwa vitupu,naibu waziri wake ni mheshimiwa mahmoud thabit kombo,katibu mkuu ni dr dadi shajjack(jamaa kutoka pemba).

Kwa kuongeza tu ni Katibu Mkuu pekee katika serikali ya SMZ kutoka Pemba. Na kuhusu kuandiak katika gazeti la Dira Shamhuna aliwahi kuandika makala nyingi kueleza mtazamo wake kinyume na Serikali ya Karume. Jabir asingaliandika hii habari bila ushahidi kwani anajijua kuwa ni mmoja wa waandishi wanaonuka kwa SMZ.
 
Kwa kuongeza tu ni Katibu Mkuu pekee katika serikali ya SMZ kutoka Pemba. Na kuhusu kuandiak katika gazeti la Dira Shamhuna aliwahi kuandika makala nyingi kueleza mtazamo wake kinyume na Serikali ya Karume. Jabir asingaliandika hii habari bila ushahidi kwani anajijua kuwa ni mmoja wa waandishi wanaonuka kwa SMZ.

kumbe unamjua mjambiani huyu fupi?
 
Kwa kuongeza tu ni Katibu Mkuu pekee katika serikali ya SMZ kutoka Pemba. Na kuhusu kuandiak katika gazeti la Dira Shamhuna aliwahi kuandika makala nyingi kueleza mtazamo wake kinyume na Serikali ya Karume. Jabir asingaliandika hii habari bila ushahidi kwani anajijua kuwa ni mmoja wa waandishi wanaonuka kwa SMZ.

bwana shamhuna ana vituko yule,kabla hajapewa fupa na karume alikuwa mdau mkubwa wa gazeti la dira na alikuwa anaikandia kwa sana serikali ya karume ktk articls zake za dira,na hata kule baraza la wawakilishi alikuwa anaichachafya sana SMZ.
 
ikiwa kutokuwa na msimamo ndo rule namba one, matokeo yake keshayaona maana hata kwenye nec hayumo kwenye halmashauri kuu hayumo


huyu alikuwa ktk kundi la Dr salmini na akina DR Bilal na alikuwa akisapport chini chini Jahazi Asilia kwa ufupi kaskazini walikuwa wanamsikiliza na kuamini ni mtu wao.


serikali ya karume ilipoingia iliziondoa picha za Dr salmini kwa haraka sana maofisini jambo ambalo lilizidi kuwakera kambi yake.

cha kushangaza mkuu baada ya kupewa fupa, amewageuka wenziwe na hao wapiga kura wake.

na baada ya kupewa unaibu waziri kiongozi ndio amepanga ratiba ya kwenda kuswali ijumaa donge ili apite jimboni kwake kwa vin'gora hadi watani wake wamembandika jina kuwa rais wa donge
 
mtu aliewahi kuwa karibu na mheshimiwa shamhuna hawezi kutofautisha uwezo wake na wa mheshimiwa mwakiyembe ila sina uhakika kuhusu hii sifa ya kubadilika kutokana na wakati mwakyembe anayo?

nnaamini kama serikali ya mseto ikiundwa sishangai nikamkuta shamhuna akiwa kiongozi wa juu anaeipigia debe kuwa ni suluhisho pekee
 
kumbe unamjua mjambiani huyu fupi?

Na kwa ufupi kamzidi Shamhuna lakini bado kijana ni machachari katika kutetea maslahi ya Taifa.

bwana shamhuna ana vituko yule,kabla hajapewa fupa na karume alikuwa mdau mkubwa wa gazeti la dira na alikuwa anaikandia kwa sana serikali ya karume ktk articls zake za dira,na hata kule baraza la wawakilishi alikuwa anaichachafya sana SMZ.

Shamhuna ni kigeugeu kuliko kinyonga yeye huangalia maslahi yake tu na hajali nini watu watasema - wakati wa upanuzi wa shule ya Donge alikuwa hatoi ushirikiano unaostahili kama Mwakilishi lakini wanadonge wenyewe walipochukua juhudi za kukamilisha ujenzi alijiweka kimbele mbele na kumkaribisha Karume kwenda kufungua - nasikia wenyewe wanasema iko siku wataliondoa jiwe la ufunguzi, sijui watampa mtaalamu wa mikasi kufanya hiyo kazi.
 
Na kwa ufupi kamzidi Shamhuna lakini bado kijana ni machachari katika kutetea maslahi ya Taifa.



Shamhuna ni kigeugeu kuliko kinyonga yeye huangalia maslahi yake tu na hajali nini watu watasema - wakati wa upanuzi wa shule ya Donge alikuwa hatoi ushirikiano unaostahili kama Mwakilishi lakini wanadonge wenyewe walipochukua juhudi za kukamilisha ujenzi alijiweka kimbele mbele na kumkaribisha Karume kwenda kufungua - nasikia wenyewe wanasema iko siku wataliondoa jiwe la ufunguzi, sijui watampa mtaalamu wa mikasi kufanya hiyo kazi.

kumbe wewe unamjua maana pia alipoiingia aliwagawanya waanzilishi wa ujenzi na kuwafanya makundi makundi yule bwana kwa maslahi yake hachezi
 
Hivi kuna haja ya kuwa na "naibu Waziri Kiongozi" kweli?. Au ndiyo urasimu tu na mambo ya kuhakikisha "tunagawana matunda ya mapinduzi"?
 
Hivi kuna haja ya kuwa na "naibu Waziri Kiongozi" kweli?. Au ndiyo urasimu tu na mambo ya kuhakikisha "tunagawana matunda ya mapinduzi"?
Cheo hicho kagawiwa ili kumpunguza makali ya kupinga kila hoja ya SMZ...
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom