WilsonKaisary
JF-Expert Member
- Apr 4, 2017
- 392
- 946
GRISELDA BLANCO - La Dama de la Mafia (Mwanamke wa Mafia)
.
Katikati ya PORI NENE la Biashara HARAMU iliyotawaliwa na WANAUME visiki. Muite "The Godmother of Drug-trafficking", Bilionea. Kwa miaka takribani 30 alisafirisha maelfu ya tani za UNGA kuingiza Marekani.
Alizaliwa mwaka 1943 Cartagena, Colombia. Akiwa na miaka 3 yeye na mama yake walihamia Medellin (mji wa Pablo Escobar), inasemekana hakupata bahati ya kwenda shule kabisa, na kutokana na hali ya maisha ya nyumbani kwao alianza uhuni akiwa na umri mdogo sana.
Akiwa na miaka 16 tu alitoroka nyumbani kwa mama yake kufuatia vitendo vya unyanyasaji wa kingono alivyokua akifanyiwa na mpenzi wa mama yake (#MeToo), maisha yake mtaani ilikua ni uporaji, kamari na uchangudoa. Ujanja na hulka yake ya unyama vilimpa blanco heshima mtaani.
Akiwa na miaka 20, Blanco alianza kujihusisha na biashara ya usafirishaji wa dawa ya kulevya akiwa chini ya genge la madawa la Medellin, enzi hizo genge la Medellin halikuwa maarufu sana. Blanco alikua akisafirisha cocaine kutoka Colombia na kuziingiza Marekani.
Genge la Medellin liliweza kuingiza kiwango kikubwa cha dawa za kulevya kwenye mipaka ya Marekani kwa kutumia chupi maalumu zilizokuwa zimebuniwa na kutengenezwa na Blanco mwenyewe. Wakati huo kitovu kikubwa cha biashara kilikuwa ni New york, Miami na South California.
Baada ya mafanikio makubwa miaka ya 1960's na 1970's mwanzoni. Katikati ya miaka ya 1970's, Blanco alifoji nyaraka za kusafiria na kuhamia Marekani ambapo aliweka kambi katika jiji la New York. Ndani ya Jiji la New York, Blanco alisimamisha biashara kubwa ya dawa za kulevya.
Kutokana na Ukubwa wa mtandao wa Blanco, Wakala wa kupambana na dawa za kulevya Marekani (DEA) wakaanza kumfuatilia. Mwaka 1975, baada ya "Operation Banshee" iliyoendeshwa na DEA walifanikiwa kudaka kilo 150 za cocaine na washirika 30 wa Blanco, wakati huo Blanco alikua.
kashausoma mchezo na ameshakimbia na kurudi Colombia. Baada ya sakata lake kupoa, Mwaka 1979 alirudi Marekani na wakati huu aliweka kambi katika jiji la Miami. Kurudi kwa Blanco nchini Marekani kulizaa mlolongo wa maasi na mauaji ya kinyama yaliyochagizwa na biashara ya dawa za kulevya. Blanco alihusika moja kwa moja na vurugu za wauza unga za miami maarufu kama "Cocaine Cowboys". Mamia ya watu waliuawa barabarani kila mwaka kutokana na biashara hii katika jiji la Miami na kupelekea kuanzishwa kwa kikosi maalumu "CENTAC 26". kilichokua na muunganiko wa polisi wa Miami na maafisa wa DEA. Mtandao wa Blanco wa kusambaza unga ulipanuka na inakadiriwa aliweza kuingiza takribani dola za kimarekani milioni 80 kwa mwezi. Kutokana na hulka yake ya ubabe na utumiaji wa mabavu dhidi ya washindani wake.
mwaka 1984 alikoswa koswa kwenye jaribio la kuuawa na akakimbilia California. Mwaka 1985, maafisa wa DEA walimvamia, kumkamata Blanco nyumbani kwake na kumshikilia bila dhamana. Baadae mwaka huo huo alipandishwa kizimbani na kushtakiwa akafungwa kifungo cha zaidi ya muongo.
Akiwa jela biashara yake ilikua ikiendelea kama kawaida, wakati huu ikiendeshwa na kijana wake Michael Blanco. Griselda Blanco alikaa jela kwa zaidi ya miaka 15 na mwaka 2002 alipata shambulio la moyo lililopelekea kuachiwa mwaka 2004 na kurudishwa kwao Medellin, Colombia.
Usiku wa Septemba 3, 2012 Blanco alifariki dunia baada ya kupigwa risasi mbili kichwani na begani na mtu aliyekua akiendesha pikipiki. Alipigwa risasi akiwa kwenye bucha la nyama karibu na kona ya mtaa namba 29 huko Medellin na muuaji alitokomea kusikojulikana.
GRISELDA BLANCO RESTREPO anabaki kwenye Historia kama mwanamama namba moja kwenye biasara ya dawa za kulevya kwa kipindi chote. Kwa ujumla anashikilia namba tatu nyuma ya wababe EL-CHAPO na ESCOBAR.
MWISHO