Mbwa wa Manzese
Na Maggid Mjengwa,
NAKIKUMBUKA kisa alichopata kusimulia Mwalimu Nyerere kunako mwanzoni mwa miaka ya 80. Ilikuwa ni kwenye kilele cha sherehe za Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi pale uwanja wa Taifa, Dar Es Salaam.
Baadhi ya mabango ya wafanyakazi yaliyopita mbele ya Mwalimu siku ile yaliwakilisha ujumbe juu ya hali ngumu ya kimaisha iliyokuwa ikiwakabili wafanyakazi ikiwamo mishahara midogo na mengineyo.
Wakati huo Serikali chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere ilikataa masharti ya Shirika la Fedha Duniani na Benki ya Dunia pia. Hii ni kwa sababu, licha ya athari nyingine mbaya kwa masharti hayo kwa nchi yetu, uhuru wetu wa kujiamulia mambo yetu nao ulikuwa hatarini.
Ilipofika wakati wa kutoa hotuba Mwalimu Nyerere alisema;
Ndugu zangu watu wa Dari Salama ebu nisikilizeni; kulikuwa na mbwa wawili, mmoja wa Manzese na mwingine wa Oysterbay. Ikatokea siku moja mbwa wa Manzese akatembea hata akafika Oysterbay.
Kwenye moja ya nyumba za huko akamwona mbwa mwenzake aliye ndani ya geti. Mbwa yule wa Manzese akasogea getini huku akimshangaa mbwa wa Oysterbay aliyenenepeana na manyoya yanayoteremka machoni. Mbwa wa Oysterbay naye alimshangaa mwenzake wa Manzese aliyekondeana. Mbwa wa Oysterbay kwa mshangao akamwuliza mwenzake wa Manzese;
Hivi nawe ni mbwa kama mimi?!
- Naam, miye ni mbwa kama wewe.
- Sasa mbona umekondeana hivyo, njoo humu ndani kwa bwana wangu nawe uwe kama mimi.
Mbwa wa Manzese akajibu; Lakini wewe umefungiwa, mwenzio niko huru!
Kisa kile alichosimulia Mwalimu kilikuwa ni cha kifalsafa. Naamini katika alichokisema Mwalimu, nitaendelea kuamini hivyo hata katika muda wangu uliobaki humu duniani. Mwalimu alizungumzia dhana ya uhuru. Neno uhuru lina maana kubwa ingawa ni neno fupi sana. Asiye na uhuru ni mtumwa.
Leo hii naandika kwa furaha kuwajulisha kuwa nimengatuka kufanya shughuli za kiutendaji katika gazeti hili la KWANZA JAMII nililoshiriki kuliongoza tangu mwanzo wake hadi kufikia toleo la 16 juma la jana. Hakuna Jumanne ambalo halikufika mitaani tangu toleo la kwanza. Naam. Ni miezi minne ya kazi ngumu. Umefika wakati wa kuwaachia wengine ili nifanye mengine.
Nawashukuru kwa dhati kabisa wachangiaji wa makala na habari katika gazeti hili. Wengi wao wamejitolea na wanaendelea kujitolea. Wanaandika bila kulipwa chochote. Wanajitolea kwa jamii yao, kwa nchi yao.
Hawa ni wapiganaji, wanawake kwa wanaume, ambao bila kujitolea kwao, hakika gazeti hili ulisomalo lingekuwa marehemu mwezi mmoja tu baada ya kuanzishwa kwake.
Kwenu nyote mnaolitakia mema gazeti hili na nchi yetu kwa ujumla, tukae tukijua, kuwa mapambano ya kuipigania Tanzania na hata kulifanya gazeti hili liendelee kuwapo mitaani bado ni magumu sana. Hatuna sababu ya kukata tamaa.Tukishindwa kukimbia tutembee, tukishindwa kutembea tutambae.Na hata tukishindwa kutambaa, tupambane mpaka risasi ya mwisho, mpaka pumzi ya mwisho.
Ni nani basi anayechukua nafasi yangu?
Kijana Benedict Sichalwe amechukua rasmi jukumu langu kama mwenza. Sichalwe ana msimamo, hana makundi na anaheshimu maadili ya taaluma yake. Alianzia katika gazeti la Dimba mwaka 1993 na kwa sasa ametokea katika jarida la RAI baada ya kumaliza mkataba wake.
Binafsi nimejifunza mengi katika kuliongoza gazeti la kada hii ya KWANZA JAMII. Kuna walionisaidia bila kunipa masharti yeyote, nawashukuru sana. Nawashukuru pia hata wale walioonyesha utayari wa kunisaidia ingawa kwa masharti. Niliyakataa masharti yao kwa kutamka huku nikiwatazama usoni, bila kuwaonea haya.
Anayenifahamu anajua kuwa naweza kukubaliana na kufanya kazi na yeyote yule katika kilicho na maslahi kwa nchi yetu bila kujali itikadi, dini , rangi au kabila la muhusika. Nitafanya hivyo hata kama kwa kujitolea tu.
Ukweli sina chama, na sijawahi kuwa mwanachama wa chama cha siasa. Sina makundi. Nina marafiki karibu katika vyama vyote vikubwa vya kisiasa hapa nchini. Wakati wa mchakato wa uchaguzi wa 2005, kwa kuandika makala mbili za kumwelezea Dr. Salim Ahmed Salim na nyingine kupinga ubaguzi wa kisiasa uliofanyika dhidi yake, basi, kuna walioamini kuwa nilikuwa mmoja katika kambi ya Dr. Salim.
Ukweli sikumfahamu Dr. Salim kwa kukutana naye hadi Februari 5 mwaka huu nilipomtembelea na kukutana naye kwa mara ya kwanza ofisini kwake. Azma yangu kuu ilikuwa ni kusalimiana na kufahamiana naye, basi.
Siku zote naamini, kuwa kama thamani ya mwandishi haijulikani, basi, mwandishi huyo ana thamani kubwa, na kinyume chake. Hakuna anayejua thamani yangu kwa maana ya bei ya kuninunua.
Nilipoanzisha jarida la michezo la GOZI SPOTI sikuzungumzwa sana. Gozi Spoti lilidumu kwa mwaka mmoja. Ajabu nilipoanzisha gazeti hili la KWANZA JAMII , haraka nikasoma mitandaoni watu wakinijadili. Ikasemwa kuwa KWANZA JAMII linamilikiwa na mafisadi, hivyo basi hata mimi nimenunuliwa na hata kuitwa fisadi.
Kila mtu ana uhuru wa kikatiba wa kutoa maoni yake. Naheshimu uhuru huo na nitaendelea kuupigania. Hata hivyo, waliozungumza hayo juu yangu ni watu wasionifahamu. Nami sikupoteza hata dakika moja kulumbana na watu wasionifahamu na wala wasiojitambulisha kwa majina yao halisi.
Baadhi ya wanaonifahamu wanajua nilianzisha na kuendesha gazeti nikiwa kidato cha pili shuleni pale Sekondari ya Tambaza. Niliandika kwa kalamu ya wino na kwa mkono katika karatasi za A-4. Niliweza kubandika kwenye ubao wa matangazo kile nilichoandika, kikasomwa na wanafunzi wenzangu hata walimu . Hiyo ni historia yangu pia.
Nitafanya nini sasa?
Nitabaki kuwa mwandishi wa makala kupitia safu hii. Kuna mengi ya kuandika, na nina azma ya kuandika kitabu. Maana, katika miaka yangu ya uandishi, nimekutana na watu wa kada mbali mbali. Mathalan, kuna bwana mmoja mwenye dhamana ya uongozi alipata kuniuliza; hivi wewe unaandika ili kumfurahisha nani?
Mwezi Novemba, 1996 nilikuwa kijijini Ilula, Rais Mkapa akiwa na mwaka mmoja madarakani alikwenda huko kufungua mradi wa umeme uliokamilika. Kwenye hotuba yake, Mkuu wa Mkoa wa wakati huo, Bw. Nicodemus Banduka alimwambia Mheshimiwa Mkapa kuwa mkoa umemwandalia ngombe wawili wa maziwa. Watasafirishwa kwa njia ya gari kwenda Ikulu. Ilikuwa ni zawadi ya ngombe si kumfurahisha Mkapa, bali kujipendekeza kwa Mkapa. Nani alimwambia Mkuu wa Mkoa kuwa Rais ana shida ya maziwa?!
Hivyo basi, swali nililoulizwa na Bwana yule lilikuwa; hivi wewe unaandika ili kujipendekeza kwa nani? Kitabu nitachoandika kitaitwa Ngombe wa Ikulu. Ni mkusanyiko na mwendelezo wa fikra zangu. Natumaini nitaishi kukiandika na kukichapa. Ahsanteni.
0788 111 765
CHANZO: http://www.kwanzajamii.com
Na Maggid Mjengwa,
NAKIKUMBUKA kisa alichopata kusimulia Mwalimu Nyerere kunako mwanzoni mwa miaka ya 80. Ilikuwa ni kwenye kilele cha sherehe za Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi pale uwanja wa Taifa, Dar Es Salaam.
Baadhi ya mabango ya wafanyakazi yaliyopita mbele ya Mwalimu siku ile yaliwakilisha ujumbe juu ya hali ngumu ya kimaisha iliyokuwa ikiwakabili wafanyakazi ikiwamo mishahara midogo na mengineyo.
Wakati huo Serikali chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere ilikataa masharti ya Shirika la Fedha Duniani na Benki ya Dunia pia. Hii ni kwa sababu, licha ya athari nyingine mbaya kwa masharti hayo kwa nchi yetu, uhuru wetu wa kujiamulia mambo yetu nao ulikuwa hatarini.
Ilipofika wakati wa kutoa hotuba Mwalimu Nyerere alisema;
Ndugu zangu watu wa Dari Salama ebu nisikilizeni; kulikuwa na mbwa wawili, mmoja wa Manzese na mwingine wa Oysterbay. Ikatokea siku moja mbwa wa Manzese akatembea hata akafika Oysterbay.
Kwenye moja ya nyumba za huko akamwona mbwa mwenzake aliye ndani ya geti. Mbwa yule wa Manzese akasogea getini huku akimshangaa mbwa wa Oysterbay aliyenenepeana na manyoya yanayoteremka machoni. Mbwa wa Oysterbay naye alimshangaa mwenzake wa Manzese aliyekondeana. Mbwa wa Oysterbay kwa mshangao akamwuliza mwenzake wa Manzese;
Hivi nawe ni mbwa kama mimi?!
- Naam, miye ni mbwa kama wewe.
- Sasa mbona umekondeana hivyo, njoo humu ndani kwa bwana wangu nawe uwe kama mimi.
Mbwa wa Manzese akajibu; Lakini wewe umefungiwa, mwenzio niko huru!
Kisa kile alichosimulia Mwalimu kilikuwa ni cha kifalsafa. Naamini katika alichokisema Mwalimu, nitaendelea kuamini hivyo hata katika muda wangu uliobaki humu duniani. Mwalimu alizungumzia dhana ya uhuru. Neno uhuru lina maana kubwa ingawa ni neno fupi sana. Asiye na uhuru ni mtumwa.
Leo hii naandika kwa furaha kuwajulisha kuwa nimengatuka kufanya shughuli za kiutendaji katika gazeti hili la KWANZA JAMII nililoshiriki kuliongoza tangu mwanzo wake hadi kufikia toleo la 16 juma la jana. Hakuna Jumanne ambalo halikufika mitaani tangu toleo la kwanza. Naam. Ni miezi minne ya kazi ngumu. Umefika wakati wa kuwaachia wengine ili nifanye mengine.
Nawashukuru kwa dhati kabisa wachangiaji wa makala na habari katika gazeti hili. Wengi wao wamejitolea na wanaendelea kujitolea. Wanaandika bila kulipwa chochote. Wanajitolea kwa jamii yao, kwa nchi yao.
Hawa ni wapiganaji, wanawake kwa wanaume, ambao bila kujitolea kwao, hakika gazeti hili ulisomalo lingekuwa marehemu mwezi mmoja tu baada ya kuanzishwa kwake.
Kwenu nyote mnaolitakia mema gazeti hili na nchi yetu kwa ujumla, tukae tukijua, kuwa mapambano ya kuipigania Tanzania na hata kulifanya gazeti hili liendelee kuwapo mitaani bado ni magumu sana. Hatuna sababu ya kukata tamaa.Tukishindwa kukimbia tutembee, tukishindwa kutembea tutambae.Na hata tukishindwa kutambaa, tupambane mpaka risasi ya mwisho, mpaka pumzi ya mwisho.
Ni nani basi anayechukua nafasi yangu?
Kijana Benedict Sichalwe amechukua rasmi jukumu langu kama mwenza. Sichalwe ana msimamo, hana makundi na anaheshimu maadili ya taaluma yake. Alianzia katika gazeti la Dimba mwaka 1993 na kwa sasa ametokea katika jarida la RAI baada ya kumaliza mkataba wake.
Binafsi nimejifunza mengi katika kuliongoza gazeti la kada hii ya KWANZA JAMII. Kuna walionisaidia bila kunipa masharti yeyote, nawashukuru sana. Nawashukuru pia hata wale walioonyesha utayari wa kunisaidia ingawa kwa masharti. Niliyakataa masharti yao kwa kutamka huku nikiwatazama usoni, bila kuwaonea haya.
Anayenifahamu anajua kuwa naweza kukubaliana na kufanya kazi na yeyote yule katika kilicho na maslahi kwa nchi yetu bila kujali itikadi, dini , rangi au kabila la muhusika. Nitafanya hivyo hata kama kwa kujitolea tu.
Ukweli sina chama, na sijawahi kuwa mwanachama wa chama cha siasa. Sina makundi. Nina marafiki karibu katika vyama vyote vikubwa vya kisiasa hapa nchini. Wakati wa mchakato wa uchaguzi wa 2005, kwa kuandika makala mbili za kumwelezea Dr. Salim Ahmed Salim na nyingine kupinga ubaguzi wa kisiasa uliofanyika dhidi yake, basi, kuna walioamini kuwa nilikuwa mmoja katika kambi ya Dr. Salim.
Ukweli sikumfahamu Dr. Salim kwa kukutana naye hadi Februari 5 mwaka huu nilipomtembelea na kukutana naye kwa mara ya kwanza ofisini kwake. Azma yangu kuu ilikuwa ni kusalimiana na kufahamiana naye, basi.
Siku zote naamini, kuwa kama thamani ya mwandishi haijulikani, basi, mwandishi huyo ana thamani kubwa, na kinyume chake. Hakuna anayejua thamani yangu kwa maana ya bei ya kuninunua.
Nilipoanzisha jarida la michezo la GOZI SPOTI sikuzungumzwa sana. Gozi Spoti lilidumu kwa mwaka mmoja. Ajabu nilipoanzisha gazeti hili la KWANZA JAMII , haraka nikasoma mitandaoni watu wakinijadili. Ikasemwa kuwa KWANZA JAMII linamilikiwa na mafisadi, hivyo basi hata mimi nimenunuliwa na hata kuitwa fisadi.
Kila mtu ana uhuru wa kikatiba wa kutoa maoni yake. Naheshimu uhuru huo na nitaendelea kuupigania. Hata hivyo, waliozungumza hayo juu yangu ni watu wasionifahamu. Nami sikupoteza hata dakika moja kulumbana na watu wasionifahamu na wala wasiojitambulisha kwa majina yao halisi.
Baadhi ya wanaonifahamu wanajua nilianzisha na kuendesha gazeti nikiwa kidato cha pili shuleni pale Sekondari ya Tambaza. Niliandika kwa kalamu ya wino na kwa mkono katika karatasi za A-4. Niliweza kubandika kwenye ubao wa matangazo kile nilichoandika, kikasomwa na wanafunzi wenzangu hata walimu . Hiyo ni historia yangu pia.
Nitafanya nini sasa?
Nitabaki kuwa mwandishi wa makala kupitia safu hii. Kuna mengi ya kuandika, na nina azma ya kuandika kitabu. Maana, katika miaka yangu ya uandishi, nimekutana na watu wa kada mbali mbali. Mathalan, kuna bwana mmoja mwenye dhamana ya uongozi alipata kuniuliza; hivi wewe unaandika ili kumfurahisha nani?
Mwezi Novemba, 1996 nilikuwa kijijini Ilula, Rais Mkapa akiwa na mwaka mmoja madarakani alikwenda huko kufungua mradi wa umeme uliokamilika. Kwenye hotuba yake, Mkuu wa Mkoa wa wakati huo, Bw. Nicodemus Banduka alimwambia Mheshimiwa Mkapa kuwa mkoa umemwandalia ngombe wawili wa maziwa. Watasafirishwa kwa njia ya gari kwenda Ikulu. Ilikuwa ni zawadi ya ngombe si kumfurahisha Mkapa, bali kujipendekeza kwa Mkapa. Nani alimwambia Mkuu wa Mkoa kuwa Rais ana shida ya maziwa?!
Hivyo basi, swali nililoulizwa na Bwana yule lilikuwa; hivi wewe unaandika ili kujipendekeza kwa nani? Kitabu nitachoandika kitaitwa Ngombe wa Ikulu. Ni mkusanyiko na mwendelezo wa fikra zangu. Natumaini nitaishi kukiandika na kukichapa. Ahsanteni.
0788 111 765
CHANZO: http://www.kwanzajamii.com