beth
JF-Expert Member
- Aug 19, 2012
- 3,877
- 6,326
Serikali imesimika mitambo ya kufua hewa tiba (oksijeni) katika hospitali za rufaa za mikoa saba Tanzania.
Kusimikwa kwa mitambo hiyo kunajibu changamoto za wataalamu wa afya ili kuwahudumia kwa ufanisi wagonjwa wa dharura na kupunguza gharama za uendeshaji wa hospitali hizo na kuwezesha hospitali nyingine za halmashauri na vituo vya afya.
Hayo yamesemwa Ijumaa Aprili 30, 2021 na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima alipotembelea hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma kujionea jinsi walivyounganisha mitambo hiyo kwenye wodi ya wagonjwa mahututi na watoto.
Dk Gwajima amesema mitambo hiyo ambayo Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia (WB) hivi sasa imefungwa kwenye hospitali za rufaa za mikoa saba ya Dodoma, Mtwara ,Manyara, Mbeya, Amana Geita na Songea na hivyo wizara yake ipo njiani kukamilisha kufungia hospitali zote za rufaa za mikoa hapa nchini.
“Mitambo hii imefungwa kwa gharama isiyopungua Sh1.4 bilioni kila hospitali na inalenga kuzalisha mitungi 200 ya hewa hiyo kwa masaa 24 , na kila mtambo unayo sehemu ya mabomba yenye mita 400 yanayosafirisha hewa hii pia mitungi 73 imenunuliwa pamoja na mitambo hii kwa hivyo, haya ni mapinduzi makubwa,” amesisitiza.
Dk Gwajima alifurahishwa na uongozi wa hospitali hiyo kwa kukamilisha kufunga mitambo hiyo na kuanza kutoa huduma kwenye wodi ya wagonjwa mahututi(ICU) pamoja na wodi ya watoto na hivyo wameweza kuunganisha vitanda 78 kutoka vitanda 10 vya awali na kufanya jumla ya vitanda 88 kupatiwa huduma hiyo hospitalini hapo.
“Hatua hii itapunguza kwa kiwango kikubwa gharama za kuhudumia mgonjwa mwenye mahitaji ya hewa hii. Wito wangu tuitumie vizuri na kuzingatia na kuhakikisha matengenezo kinga yanafanyika kwa ufanisi,” amesema.
Dk Gwajima amesema uwekezaji huo umeweza kujibu changamoto ya kipindi cha mlipuko wa Covid-19 ulioripotiwa nchini Machi 2020 na hivyo kusababisha kuongezeka kwa mahitaji ya hewa ya oksijeni na kuwa gharama zake zilipanda.
“Niwapongeze sana waganga wafawidhi wa hospitali za rufaa za mikoa kwa kuja na wazo hili la kufunga mitambo hiyo kwenye hospitali zetu na hivyo tutaweza kusaidia hospitali za wilaya na vituo vya afya na hivyo kuwapunguzia matumizi ya fedha ya kununua oksijeni, haya ni mapinduzi makubwa kwa Serikali yetu,” amesisitiza Dk Gwajima
Kwa upande kwa kuepuka magonjwa ya kuambukiza ambayo yameanza kuyakumba mataifa mengine, waziri huyo amewataka waganga wakuu wa mikoa na wafawidhi kwenye hospitali za rufaa za mikoa kuendelea kutoa elimu kwa umma kwa kutumia redio zilizopo kwenye maeneo yao ili kuwaondolea wananchi hofu na kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza ikiwemo Corona.
Naye mganga Mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma Dk Ernest Ibenzi alisema wanatarajia kufunga mitambo ya kujazia hewa tiba hiyo ili kuweza kusaidia vituo vya afya vilivyo jirani na kusambaza huduma hiyo kwenye hospitali nzima.
Chanzo: Mwananchi
Kusimikwa kwa mitambo hiyo kunajibu changamoto za wataalamu wa afya ili kuwahudumia kwa ufanisi wagonjwa wa dharura na kupunguza gharama za uendeshaji wa hospitali hizo na kuwezesha hospitali nyingine za halmashauri na vituo vya afya.
Hayo yamesemwa Ijumaa Aprili 30, 2021 na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima alipotembelea hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma kujionea jinsi walivyounganisha mitambo hiyo kwenye wodi ya wagonjwa mahututi na watoto.
Dk Gwajima amesema mitambo hiyo ambayo Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia (WB) hivi sasa imefungwa kwenye hospitali za rufaa za mikoa saba ya Dodoma, Mtwara ,Manyara, Mbeya, Amana Geita na Songea na hivyo wizara yake ipo njiani kukamilisha kufungia hospitali zote za rufaa za mikoa hapa nchini.
“Mitambo hii imefungwa kwa gharama isiyopungua Sh1.4 bilioni kila hospitali na inalenga kuzalisha mitungi 200 ya hewa hiyo kwa masaa 24 , na kila mtambo unayo sehemu ya mabomba yenye mita 400 yanayosafirisha hewa hii pia mitungi 73 imenunuliwa pamoja na mitambo hii kwa hivyo, haya ni mapinduzi makubwa,” amesisitiza.
Dk Gwajima alifurahishwa na uongozi wa hospitali hiyo kwa kukamilisha kufunga mitambo hiyo na kuanza kutoa huduma kwenye wodi ya wagonjwa mahututi(ICU) pamoja na wodi ya watoto na hivyo wameweza kuunganisha vitanda 78 kutoka vitanda 10 vya awali na kufanya jumla ya vitanda 88 kupatiwa huduma hiyo hospitalini hapo.
“Hatua hii itapunguza kwa kiwango kikubwa gharama za kuhudumia mgonjwa mwenye mahitaji ya hewa hii. Wito wangu tuitumie vizuri na kuzingatia na kuhakikisha matengenezo kinga yanafanyika kwa ufanisi,” amesema.
Dk Gwajima amesema uwekezaji huo umeweza kujibu changamoto ya kipindi cha mlipuko wa Covid-19 ulioripotiwa nchini Machi 2020 na hivyo kusababisha kuongezeka kwa mahitaji ya hewa ya oksijeni na kuwa gharama zake zilipanda.
“Niwapongeze sana waganga wafawidhi wa hospitali za rufaa za mikoa kwa kuja na wazo hili la kufunga mitambo hiyo kwenye hospitali zetu na hivyo tutaweza kusaidia hospitali za wilaya na vituo vya afya na hivyo kuwapunguzia matumizi ya fedha ya kununua oksijeni, haya ni mapinduzi makubwa kwa Serikali yetu,” amesisitiza Dk Gwajima
Kwa upande kwa kuepuka magonjwa ya kuambukiza ambayo yameanza kuyakumba mataifa mengine, waziri huyo amewataka waganga wakuu wa mikoa na wafawidhi kwenye hospitali za rufaa za mikoa kuendelea kutoa elimu kwa umma kwa kutumia redio zilizopo kwenye maeneo yao ili kuwaondolea wananchi hofu na kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza ikiwemo Corona.
Naye mganga Mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma Dk Ernest Ibenzi alisema wanatarajia kufunga mitambo ya kujazia hewa tiba hiyo ili kuweza kusaidia vituo vya afya vilivyo jirani na kusambaza huduma hiyo kwenye hospitali nzima.
Chanzo: Mwananchi