Mohamed Said
JF-Expert Member
- Nov 2, 2008
- 20,910
- 30,253
Kitabu hiki kimeandikwa na kalamu ya Sheikh Mohamed Iddi na kimetiwa maneno ya utangulizi na Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Abubakar bin Zubeir bin Ally.
Hiki kitabu ukiachia sifa za mwandishi mwenyewe ukiingia kwa hawa waliotanguliza maneno yao kwa msomaji, Rais Ali Hassan Mwinyi na Mufti Abubakar Zubeir ni watu wenye sifa za pekee sana na msomaji hatoweza kukifaidi kitabu hiki na kukielewa ikiwa hatawajua hawa watu ni nani katika historia ya Tanzania baada ya uhuru wa Tanganyika mwaka wa 1961 na Mapinduzi ya Zanzibar mwaka wa 1964.
Tuanze na Sheikh Mohamed Iddi mwandishi wa kitabu.
Sheikh Mohamed Iddi ni mwanafunzi wa Sheikh Muhammad Ayoub na nikisema nieleze silsila ya Sheikh Muhammad Ayoub hatotoka hapa sasa hivi lakini itoshe tu kusema kuwa silsila ya mwalimu wake Abuu Iddi inaishia kwa Mtume SAW na yeye kapokea kutoka kwa Jibril na Jibril kutoka kwa Allah SW.
Hii ndiyo silsila ya mwandishi Sheikh Mohamed Iddi Mohamed, sheikh wa kwanza Tanzania Bara kuwa na kipindi cha televisheni kilichowapa watu wengi elimu bila hata ya wao kunyanyua mguu kwenda kwa mwalimu na wengi wamenufaika na wanaendelea kunufaika.
Sheikh Mohamed Iddi si mgeni katika uandishi na usomeshaje si wa dini peke yake bali hata mengine ya ulimwengu tunayoishi iwe ama siasa au mambo ya kijamii na katika juhudi zake hizi ametokea kuwa sheikh maarufu katika mitandao ya kijamii.
Mufti Sheikh Abubakar Zubeir ataingia katika historia ya Waislam wa Tanzania kama kiongozi wa pekee aliyekuja na mkakati wa pekee akiwa na nia ya pekee.
Inahitaji mtu kuijua historia ya nchi yetu ilivyoingiliana na historia ya Waislam katika mengi kuanzia wakati wa ukoloni wa Wajerumani, Waingereza hadi kufika nchi kukombolewa, ili kuelewa vipi Mufti Sheikh Abubakar Zubeir ni Mufti wa pekee.
Kwa ajili hii basi hii si ajabu kuwa fikra ya kitabu hiki cha kueleza misingi ya amani imetoka kwake akikusudia kuwatakia kheri nyingi Watanzania ambao dini kubwa mbili ni Uislam na Ukristo imani ambazo laiti ikiwa hazitaengwa kwa waumini wake kutendeana haki na uadilifu katika nafasi zao za maamuzi ndani ya vyombo vya umma na serikali amani ya nchi itakuwa hatarini.
Itakuwa hatusemi kweli kuwa yapo manung’uniko na yamekuwapo kwa takriban sasa zaidi ya miaka 50.
Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi yeye katawala jamii hii ya Watanzania akiwa Rais wa kwanza Muislam tena kutoka Zanzibar.
Katika utawala wake Rais Ali Hassan Mwinyi kashuhudia mengi na bila shaka kakutana na mengi ambayo kwa uzoefu wa Zanzibar alikotokea ambayo asilimia kubwa kabisa ni Waislam huku Bara kwake aliyoyaona na wakati mwingine kuyatolea maamuzi yalikuwa mageni na pengine wakati mwingine yalimtisha na labla akajiuliza hivi haya yanawezekanaje na yalifikiaje hata kuwa hivi?
Lakini ukoloni na serikali huru Tanganyika na baadae baada ya mapinduzi na muungano mabadiliko haya yalikuja na changamoto zake nyingi, changamoto ambazo taifa halijaweza kuzishinda hadi hivi leo juu ya nchi kuwa huru miongo mitano.
Laiti viongozi wetu wangelikuwa na utamaduni wa kuandika kumbukumbu zao bila shaka tungelisoma mengi sana aliyopitia Rais Ali Hassan Mwinyi katika utawala wake.
Tanzania bado ina changamoto ambazo katika nchi nyingi Afrika zimesababisha matatizo nmakubwa ya amani lakini Tanzania changamoto hizi wananchi wake wameweza kusistahamilia kiasi hii leo wanaandika kitabu kukumbushana kipi kifanyike ili hii amani tuliyonayo idumu na matatizo tuliyonayo tuyashinde kwa faida ya kizazi cha leo na hicho kijacho kesho.