Misemo kumi bora ya Wahenga wetu

Tanzania Nchi Yetu Sote

JF-Expert Member
Mar 12, 2017
505
854
Hebu Pata Kumi Bora za Wahenga
________________________________________
Wahenga ni wazee wenye akili waliotutangulia maana siyo kila mzee ana akili kwa sababu hata wajinga wanazeeka. Mjinga anazeeka na ujinga wake. Vifo vya wajawazito vilipokithiri enzi hizo, wahenga walibaini chanzo ni ulaji wa mayai kipindi chote cha mimba na kusababisha mtoto kunenepa sana huko tumboni na kushindwa kupita kwenye njia ya uzazi. Basi kwa sababu hawakuwa na teknolojia ya visu wakaanzisha msemo kama, 'Mama mjamzito akila mayai, mtoto atazaliwa bila nywele' ili kuzuia excessive eating of eggs kwa wajawazito. Walitumia akili kuyatawala mazingira! Sisi tunatumia akili kujeruhiwa na mazingira. Ajabu! Hebu tupitie kumi bora za wahenga labda zitasaidia kuboost brains zetu tuweze kuyatawala mazingira maana mbu tu wanatuwahisha kaburini! Hii ni ishara akili zetu zimefungwa, hazifurukuti!

Moja, “Huwezi kusukuma gari bovu ukiwa umekaa ndani yake,” lazima uteremke chini, ukiendelea kulisukuma ukiwa humo utavunja viti na hapo ndipo utamtambua mwenye gari. Ni hekima za bure kwa ajili ya wajinga wanaodhani wanaweza kuubadilisha mfumo wakiwa ndani yake. Ukijaribu kufanya hivyo lazima uliwe kichwa! Kuchukia rushwa na wakati unaishi kwa rushwa ni sawa na kusukuma gari ukiwa ndani yake! Unasema unachukia uvunjaji wa demokrasia nchini na wakati chama chako kinavunja demokrasia ni sawa na kusukuma gari ukiwa ndani. Huo ni ujinga sugu! Kumbuka mabega hayazidi kichwa!

Mbili, “Samaki anayefumba mdomo wake, hashikwi na ndoano ya mvuvi” ni ushauri kwamba ufumbe mdomo wako kwani kuna watu wengi wana hamu ya kukutia ndoano kwa makosa yako. Kumbuka hakuna binadamu mkamilifu chini ya jua. Ulimi ni kama wembe mkali, ukiushika vibaya unakuchana. Sira anakwambia afadhali kuteleza sakafuni kuliko kuteleza kwa ulimi. Chunga ulimi kwani unang'ata zaidi ya meno!

Tatu “Maskini hana hoja, ana haja” ni busara kutoka kwenye kitabu cha Ukombozi wa Fikra ikiwa na lengo la kutukumbusha kwamba tufanye kila njia kuukimbia umaskini. Maskini haaminiki Duniani na hata Mbinguni. Mungu mwenyewe hafungi agano na maskini maana anajua atageuka tu. Kumbukumbu la Torati 8:18 inasema, “Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.Utajiri kwanza, halafu agano ndo linafuata. Njaa siyo nzuri! “Ibada ilipo karibia kuisha mhubiri akauliza, “Anayetaka kuokoka anyoshe mkono!" Watu wote kimya. Tajiri mmoja akapita mbele akasema; "Jamani mhubiri anauliza anaye taka kuokoka anyoshe mkono! "Mtoto mmoja akanyosha mkono. Tajiri akampa yule mtoto laki 3. Akawageukia waumini akauliza tena; anaye taka kuokoka anyoshe mkono, “Waumini wotee wakanyosha mikono, alipogeuka nyuma akakuta mhubiri naye kanyosha mkono.” Hayo ndiyo aisiyoenda Mungu ndo maana yuko makini na mtu mwenye njaa!

Nne, “No research no right to speak” ni busara ya wahenga wa kizungu inayotuasa kuacha kuishi kwa hisia. “Umeenda kutembea ukweni kwako baada ya chakula cha usiku unapewa chumba cha kulala, inapofika usiku unataka kutoka kwenda kujisaidia kwa sababu taa zimezimwa kwa bahati mbaya unapamia vyombo vya chakula sebleni. Kipindi unajaribu kupapasa uviweke sawa vile vyombo mara taa inawashwa na mama mkwe anaona umeshika vyombo anakwambia, “Baba kama hukushiba ungesema.” “Hapo ujue mama mkwe anaongozwa na hisia na hii ni hatari sana maana unaweza kuondoka na kamwe usirudi tena ukweni. Sasa wewe endelea kutumia hisia tu ndo utajua kumbe macho hayaonani lakini yanatazama pamoja.”

Tano, “Ondoa kibanzi jichoni kwako kwanza kabla ya kuondoa boriti kwa jicho la mwenzako” ni hekima inayotutaka tuwe makini sana kabla ya kuhukumu. “Baba mmoja alichoshwa na tabia ya uongo katika familia yake, akaamua kununua mtambo (robot) utakaomsaidia kutambua upi ni uongo na upi ni ukweli. Siku moja mtoto wake alirudi nyumbani toka shule likizo bila ripoti ya matokeo yake. Aliifcha kisa alikuwa amefeli sana, alipofika home baba akamuuliza ripoti ya matokeo iko wapi? Mtoto akasema ameisahau shulen ila amefaulu sana ana A zote ghafla lile robot likamzaba kibao yule mtoto ishara ya kuwa anasema uongo, baba akaghadhabika, akamwambia mtoto kwanini usiwe kama mimi baba yako? Kipindi nasoma nilikuwa napata A zoote hata ripoti sifichi kama wewe. Ghafla tena lile robot likamnasa mzee kibao ishara ya kuwa anaongopa, mtoto akatahamaki mara mama yake naye akaja akamuuliza mtoto ..." We mtoto mbona unamuongopea baba yako?" Ghafla tena lile roboti likamnasa mama kibao ishara kuwa anaongopa pia. Wahenga noma!

Sita, “Ukali wa wembe hauwezi kupasua kuni wala shoka kunyoa nywele” lengo la ujumbe huu ilikuwa ni kunusuru ndoa zetu! Maana ukiisha ingiza haki sawa kwenye ndoa kwisha habari yako! Kinachoongoza ndoa ni utii na akili basi. Yaani mwanamke aishi na mume wake kwa utii na mwanaume aishi na mke wake kwa akili. Yaani kwa tafasiri ya haraka ni kwamba kama hauna akili usioe na kama hauna utii usiolewe! Huo ndiyo ukweli na ukiamua kuupuza subiri kushughulikiwa maana ukweli siku zote huwashughulikia wanaoupuuza alisema Nyerere!

Saba, “Hujafa hujauumbika,” msemo huu ni fundisho kwa wale wenye tabia za kusema hawaongei na mbwa ila wanaongea na wenye mbwa. Hii dunia ni duara, siyo mraba! Kila mtu anathamani, ni suala la muda tu. Unajua maisha ni shughuli ya kusisimua na inasisimua sana pale unapoishi kwa ajili ya watu wengine alisema Hellen Keller. Ukiwapuza wengine na kuwajali wengine majawabu yake yatakushangaza. Kila wapiganaji waliposhinda vitani mfalme aliwapa zawadi. Kitendo hiki kilimuumiza sana mkata majani ya farasi. Mkata majani akavunjika moyo, hakuwalisha farasi vizuri. Jamaa walipokwenda vitani waliteketezwa wote kwa sababu farasi walikwenda vitani na njaa. Kumbe hakuna mbwa binadamu!

Nane, “haijalishi meno yanaun’gata ulimi mara ngapi lakini bado vinaishi mdomoni pamoja” maana ya busara hii ni umuhimu wa msamaha na kuchukuliana maana pamoja na mabaya anayokufanyia mtu, kumbuka kuna mazuri mengi. Ulimi usingefurahia utamu wa nyama bila meno! Kosa moja la mwenzio lisifute ule uzuri wote aliokufanyia. Hata mti unapopitia katika msukosuko unapunguza matawi na siyo mizizi.

Tisa,“Mwenye kuni hula vilivyoiva, lakini mwenye pesa hula vitamu” ni busara inayotukumbusha kutojisahau na mafanikio tuliyonayo kwani kuna neema katika kuongeza bidii. Siyo unajenga nyumba moja tu basi unaingia mkataba wa ponda mali kufa kwaja. Unamtangazia kila mtu kwamba umejenga, huna tofauti na kuku. Kuku kutaka yai moja anautangazia ulimwengu mzima na wakati ng'ombe anayetoa maziwa na kunywesha kijiji kizima hapigi kelele.

Kumi, “Tumia taulo lako vizuri maana kipande ulichofutia tako asubuhi waweza kufutia mdomoni jioni” ni busara inatufundisha kwamba ukipata chungu kipya usivunje kile cha zamani, umepandishwa cheo, unataka uwakojolee waliokufikisha huko. Yaani umesahau kwamba cheo ni dhamana. Tuonane siku nyingine kwa nikutwange 20 bora za wahenga!
 
"Pema ni pema usipopema,ukipema si pema tena."
Hivi siku hizi hakuna wenye akili kama wahenga,mbona hatupati methali na misemo mipya?
 
.....

Kumi, “Tumia taulo lako vizuri maana kipande ulichofutia tako asubuhi waweza kufutia mdomoni jioni” ni busara inatufundisha kwamba ukipata chungu kipya usivunje kile cha zamani, umepandishwa cheo, unataka uwakojolee waliokufikisha huko. Yaani umesahau kwamba cheo ni dhamana. Tuonane siku nyingine kwa nikutwange 20 bora za wahenga!

Hii siyo ya wahenga hii ni ya Mugabe.
 
"Pema ni pema usipopema,ukipema si pema tena."
Hivi siku hizi hakuna wenye akili kama wahenga,mbona hatupati methali na misemo mipya?
Hujamsikia Mugabe?
Je Kikwete? Ukitaka kula sharti uliwe kidogo
 
Back
Top Bottom