Mikhail Gorbachev: Mtawala wa Mwisho wa Soviet aliyeipoteza nchi yake.

Kinyungu

JF-Expert Member
Apr 6, 2008
17,344
32,976
Akiwa na umri wa miaka 85, Mikhail Gorbachev anasumbuliwa na maradhi mbali mbali yatokanayo na umri wake. Hata hivyo bado ni mtu mcheshi, mwenye bashasha na kumbukumbu nzuri kuhusu yale yaliyotokea wakati akiwa kiongozi wa mwisho wa nchi ya Muungano wa Soviet. Ukifika nyumbani kwake katika jiji la Moscow, Gorbachev anaonekana mwenye furaha na mara moja atakuonesha mkongojo wake huku akisisitiza kuwa kwa sasa hawezi tena kutembea bila “mguu” huo wa tatu kama mwenyewe anavyouita.

Hivi karibuni mwandisi wa BBC, Steve Rosenberg akiwa Moscow alipata fursa ya kufanya mahojiano na Bw. Gorbachev ikiwa imepita miaka 25 tangu utawala wa Soviet ulipoanguka na kubadili kabisa siasa za dunia.

Akiwa ameketi kwenye kiti chake, Mikhail Gorbachev anaanza kwa kuyalaumu mataifa ya Magharibi kwa kuichokoza Russia.

“Kilichotokea kwa USSR ilikuwa ni pigo. Ilikuwa ni pigo kwangu na kwa wote waliokuwa wakiishi kwenye umoja wa Soviet”. anasema Bw Gorbachev. “Ilikuwa ni mapinduzi” anaendelea kusisitiza.

Tarehe 21/12/1991, Televisheni ya Russia ilitoa habari isiyo ya kawaida. Siku hiyo jioni mtangazaji alisema “Habari za jioni…..Hii ni habari……..Hakuna tena USSR…” alimaliza mtangazaji.

Siku chache kabla taarifa hiyo ya kuvunjika kwa USSR, viongozi wa Russia, Belorussia na Ukraine walikutana na kukubaliana kuivunjilia mbali USSR na kuunda umoja wao uliojulikana kama “Commonwealth of Independent States”. Wakati hayo yakiendelea, mataifa mengine nane yaliyokuwa yakiunda USSR mara moja nayo yaliamua kujiunga na jumuiya hiyo mpya. Hivyo kwa pamoja mataifa hayo yalimsaliti Bw. Gorbachev, kiongozi wa USSR ambaye alikuwa akipambana kuhakikisha kuwa USSR inabaki kuwa nchi moja.

“Nyuma yetu kulikuwa na wahaini…..ndiyo wahaini walikuwa nyuma yangu” anasisitiza Bw. Gorbachev huku akivuta pumzi kwa nguvu. “Waliamua kuchoma nyumba nzima ili wapate moto wa kuwasha sigara..,ilimradi wapate mamlaka. Wangaliweza kuyapata kupitia njia ya kidemokrasia, lakini hawakufanya hivyo…,wakachagua uhaini…Ilikuwa ni mapinduzi” anasisitiza Bw. Gorbachev.

Christmas ya tarehe 25/12/1991, Mikhail Gorbachev alitangaza kujiuzulu kama rais wa USSR. Siku hiyo huko Kremlin ambayo ni ikulu ya Soviet, bendera nyekundu ya USSR yenye nyota moja, mundu (sickle) na nyundo ilishushwa kwa mara ya mwisho.

“Tulikuwa tunaelekea kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe na nilitaka kuepuka hilo” anasema Bw.Gorbachev. “Mgawanyiko uliokuwepo katika jamaii yetu na changamoto zilizokuwapo katika nchi iliyokuwa imefurika silaha za kila namna zikiwemo za kinyuklia, zingaliweza kuacha maelfu ya watu wakiwa wamekufa. Sikutaka hilo litokee kwa mimi kuendelea kung’ang’ania madaraka. Kujiuzulu kwangu ilikuwa ni sawa na ushindi maana kwa kufanya hivyo niliokoa maisha ya mamilioni ya watu”.

Maoni yake kuhusu Raisi Putin

Kwenye hotuba yake ya kujiuzulu, Bw. Gorbachev alidai sera zake za Perestroika ziliwapa watu uhuru. Na kwa sasa ikiwa imepita miaka 25 tangu kuvunjika kwa USSR anadhani uhuru huo nchini Russia upo mashakani. ”Unajua mchakato wa mageuzi tuliouanza haujafikia mwisho. Ni lazima tuwe wakweli kuhusu hili….Kuna baadhi ya watu ambao wanaona uhuru kwa wananchi ni kero. Hawajisikii vizuri wananchi wakiwa huru” anasisitiza Bw. Gorbachev

Alipoulizwa kama anamaanisha Bw. Putin, mara moja alisema “Jaribu kuhisi ni nani ninaye maanisha…Hilo ni swali nakuachia ulijibu mwenyewe”

Kwenye mazungumzo Bw. Gorbachev anaepuka kumtupia lawama za moja kwa moja raisi Putin. Japo ameonesha wazi kuwa yeye na raisi Putin kuna mambo hawakubaliani. Alipoulizwa kama huwa raisi Putin anamwomba ushauri, Gorbachev anajibu “Tayari anajua kila kitu” Kila mtu anapenda kufanya mambo kwa jinsi anavyoona inamfaa yeye. Ni kama Wafaransa wanavyopenda kusema “C’est la vie”.


Raisi huyu wa mwisho wa USSR anaitupia lawama serikali ya Russia. Anasema serikali hii imejawa na urasimu na wezi wanaoiba utajiri wa nchi ili kuunda makampuni makubwa. Anamlaumu Bw. Igor Sechin ambaye ni boss wa kampuni kubwa ya umma ya mafuta Rosneft kwamba amekuwa kila mara akipenyeza maslahi yake kwenye masuala muhimu ya nchi.


Uchokozi wa nchi za Magharibi

Bw. Gorbachev anayalaumu mataifa ya Magharibi kwa kudai kuwa kila mara yamekuwa yakiichokoza Russia kupitia vyombo vya habari. “Vyombo vya habari vya Magharibi na nyie (BBC) mkiwemo mmekuwa mkipewa maelekezo maalum ili kumtuhumu raisi Putin. “Mnafanya hivyo mkidhani kuwa raisi Putin atajiuzulu au atajiweka kando na yanayoendelea Russia matokeo yake umaarufu na uungwaji mkono wa wananchi wa Russia kwa raisi Putin sasa umefikia 86% na labda karibuni utafikia 120%!”


Kuhusu raisi mteule wa Marekani Bw. Trump.

Ulikuwa ni urafiki binafsi wa Bw. Gorbachev wakati huo akiwa raisi wa USSR na raisi wa zamani wa Marekani Bw. Ronald Reagan uliosababisha kumalizika kwa vita baridi duniani. Ni nini maoni yake kuhusu mtu ambaye karibuni ataapishwa kuwa raisi wa Marekani?


“Sijawahi kukutana Bw. Trump. Nimewahi kuona tu majengo yake marefu lakini sijawahi kabisa kuonana naye hivyo sina mengi ya kusema juu yake”. “Ni hali ya kufurahisha sana..hapa Russia kila mtu alijua kwamba Democrats watashinda nikiwemo mimi, japokuwa sikuwahi kusema hadharani”.

Kwa wananchi wengi wa nchi za Magharibi Bw. Mikhail Gorbachev ni shujaa ambaye alisaidia kupatikana uhuru kwa wananchi wa Ulaya Mashariki na pia alisaidia nchi ya Ujerumani kuungana tena na kuwa nchi moja baada ya kuanguka kwa ukuta wa Berlin. Hata hivyo kwa nchi yake ya Russia, Mikhail Gorbachev ni kiongozi msaliti ambaye alipoteza nchi yao.


Alipoulizwa kama anakubaliana na madai kwamba anahusika na kuanguka kwa USSR, Bw. Gorbachev anajibu “Nasikitika kwamba wananchi wengi wa Russia hawaelewi ni nini hasa nilipanga kufanikisha na nini nilichofanikiwa”. “Kwa nchi yangu na dunia nzima Perestroika ilifungua uhuru wa ushirikiano na amani. Hata hivyo nasikitika sikuweza kusimamia hilo hadi likafikia mwisho”.

Kwenye uzee wake Bw Gorbachev amekuwa mtu wa kupenda kupiga kinanda kilichopo nyumbani kwake. Na nyimbo anazozipenda sana ni zile ya enzi za Soviet. Mojawapo ya nyimbo hizo ni ule uitwao “Kati ya zamani na kesho”. “Kati ya zamani na kesho ni kama kufumba na kufumbua macho” na “kitendo hicho ndicho tunachokiita maisha” anaimba Bw. Gorbachev huku akipiga kinanda.

Umoja wa Soviet ulivunjika kama kitendo cha kufumba na kufumbua macho. “Miaka 70 ni kitu gani kulinganisha na Dola ya Kirumi au Utawala wa Ottoman?” anauliza Bw. Gorbachev.


BBC, Steve Rosenberg anaona siyo sahihi kumlaumu Bw. Mikhail Gorbachev kwa kuvunjika kwa Muungano wa Kisoviet. Yeye anadhani tangu mwanzo wa kuundwa kwake Muungano wa Kisoviet ulianza na makosa hasa kwenye siasa, uchumi na itikadi yake. Hivyo ilikuwa ni taifa kubwa lililokwisha jitabiria kuishi kwa muda mfupi.


Dondoo muhimu kumhusu Mikhail Gorbachev.

1931: Alizaliwa maeneo ya vijijini huko Privolnoye karibu na mji wa Stavropol, Kusini mwa Russia ya Kisoviet

1955: Alipata digrii yake ya kwanza toka Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Umma cha Moscow na kuwa mwanachama wa Chama cha Ukoministi (CP)

1970: Alikuwa Katibu wa kwanza wa Chama Cha Ukomunisti huko Stavropol

1980: Alikuwa mjumbe kamili wa Kamati tendaji yenye nguvu ya Chama Cha Kikomunisti Cha Soviet yaani Politburo.

1985: Politburo ilimchagua kuwa Katibu Mkuu wa Cha Cha Kikomunisti

1987: Alianzisha mageuzi makubwa ya uwazi “glasnost” na marekebisho “perestroika”

1987: Aliingia makubaliano makubwa na Marekani ya kupunguza silaha za maangamizi za nyuklia.

1990: Alikubali nchi za Ujerumani Magharibi na Ujerumani Mashariki ziungane tena na kuwa nchi moja

1991: Alishikiliwa kwa muda kufuatia jaribio lililoshindwa la mapinduzi ambalo lilitekelezwa mwezi August na wakereketwa wa Kikomunisti; baadaye mwezi December aliamua kujiuzulu nafasi yake ya uraisi wa Muungano wa Soviet.

Makala hii imetafsiriwa na Kinyungu toka BBC

 
Huyu bwana Gorbachev ndiye Usocialist utamlaumu mpaka mwisho huyo alitumwa kukamilisha kazi kubwa ya muda mrefu sana ya kuuwa ukomunist ambayo aliifanya kwa mafanikio makubwa sana
 
Mzembe tu huyo.Ameacha historia mbaya duniani.Nikikumbuka legacy ya Stalin naishia kuamini kuwa Viongozi waliofuatia kuanzia Krushev waliamua wao kuwa wazembe wazembe na waoga.
 
Yaani Russia ni wazembe sana wanamuacha aendelee kula sembe mpaka leo hii msaliti mkubwa huyu wangempiga kiberiti hadharani akajutia usaliti wake
 
Yaani Russia ni wazembe sana wanamuacha aendelee kula sembe mpaka leo hii msaliti mkubwa huyu wangempiga kiberiti hadharani akajutia usaliti wake
 
Yaani Russia ni wazembe sana wanamuacha aendelee kula sembe mpaka leo hii msaliti mkubwa huyu wangempiga kiberiti hadharani akajutia usaliti wake

Kila Jambo Lina faida na hasara zake. Faida za kuanguka kwa Russia na uwepo wa Mikhail Kama Rais;

1) Kuanguka kwa USSR kulileta wimbi la Vyama vingi Africa na kushamiri Uhuru wa kujieleza

2) Mfumo wa Kizembe Duniani wa Ujamaa ulitoweka
3) Ujerumani iliungana tena

4) Vita Baridi Duniani iliisha

5) Vita visivyoisha vya kupiganishaAfrica vilianza kupungua
 
Mzembe tu huyo.Ameacha historia mbaya duniani.Nikikumbuka legacy ya Stalin naishia kuamini kuwa Viongozi waliofuatia kuanzia Krushev waliamua wao kuwa wazembe wazembe na waoga.
Nakumbuka maneno ya Lenin"communism is there to stay but capitalism & imperialism is moribund"
 
Mnaomlaumu Gorrbachev hamjui hasa nini kilipelekea USSR kuvunjika

mnamlaumu mtu asiehusika
 
Back
Top Bottom