Migomo katika Vyuo Vikuu na serikali ya awamu ya Nne

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,460
39,928
i116_1212.jpg


Wanachuo UCLAS wagoma

2007-02-23 09:29:20
Na Sabato Kasika

Wanafunzi zaidi ya 1000 wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ardhi na Usanifu Majengo (UCLAS), jijini Dar es Salaam, wamegoma kuingia darasani wakilalamikia kukatwa fedha zao za mafunzo kwa vitendo yanayotarajiwa kuanza wiki ijayo.

Mgomo huo ulianza jana asubuhi ambapo wanafunzi wa mwaka wa kwanza hadi wa tano wanaochukua masomo mbalimbali yakiwemo ya mipango miji, upimaji ardhi, uhandisi mazingira na usanifu majengo, walikuwa wakiushinikiza uongozi wa chuo kuwalipa fedha zao.

Akizungumza na Nipashe, Rais wa chuo hicho, Bw. Ndatwa Ng?evilabuze, alisema awali wanafunzi wa awamu ya mwisho walikuwa wakipewa Sh. 3500 kwa ajili ya malazi na chakula na Sh. 6000 kila siku kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

Alisema kwa sasa wamepata taarifa kuwa pesa hizo za mafunzo zimekatwa kwa kila mwanafunzi Sh. 50,000 ambapo wao wanahoji kuwa ukataji huo umeangalia vigezo gani.

(Wanafunzi wa Mlimani walipogoma mapema mwaka huu)

04.10.2007 0847 EAT
Muhimbili wagoma


*Ni kutokana na baadhi yao kukosa makazi
*Mkuu wa Chuo asema hosteli hazijakamilika
*Awaambia hamkufuata mabweni bali masomo

Na Said Mwishehe

WANAFUNZI zaidi ya 1,400 wa Chuo Kikuu cha Sayansi za Afya (MUCHS) Dar es Salaam, wamegoma kuingia darasani kutokana na wenzao mwa mwaka wa kwanza kukosa sehemu za kuishi.

Mgomo huo ulianza jana saa sita mchana, baada ya Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo hicho (MUHASSO), Bw. Edwin Chitage, kutangaza rasmi mgomo huo kupitia Baraza la Chuo, ambao kumalizika kwake kutatokana na kutotimizwa kwa madai waliyoyatoa kwa uongozi wa chuo.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Wanafunzi chuoni hapo, Bw. Chigate alisema wamefikia uamuzi wa kugoma ikiwa ni hatua ya kuushinikiza uongozi wa chuo kuwatafutia makazi mapya baada ya kuona wanafunzi wa mwaka wa kwanza 124 hawana makazi ya kuishi na wengine zaidi ya 1,000 wakitangatanga kwa wenzao kutokana na kupanga mbali na chuo.

©2007Business Times Limited .

Wanafunzi IFM wagoma

2007-06-05 10:45:49
Na Godfrey Monyo


Wanafunzi wote wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) cha jijini Dar es Salaam, wamegoma kuingia madarasani kwa lengo la kuushinikiza uongozi wa chuo hicho kuwarudisha wenzao waliofukuzwa.

Nipashe ilifika chuoni hapo jana saa 3:40 asubuhi na kuwakuta wanafunzi hao wakiwa wamekusanyika katika makundi makundi wakijadili hatma ya wanafunzi wenzao waliotimuliwa.

Mbali ya wanafunzi kukusanyika nje ya chuo hicho, pia walikuwa wakipiga kelele na kuimba nyimbo mbalimbali zilizolenga kuushinikiza uongozi wa chuo hicho kusikia kilio chao na kuwarejesha masomoni wenzao watatu waliofukuzwa tangu Mei 29, mwaka huu akiwemo Rais wa Serikali ya Wanafunzi, Bw. Baltazar Boniface.

Wanafunzi Chuo Kikuu Mzumbe wagoma
John Nditi, Morogoro
HabariLeo; Friday,October 26, 2007 @00:01

WANAFUNZI wa mwaka wa kwanza na wa pili wapatao 1,800 wa Chuo Kikuu Mzumbe mkoani hapa, wametangaza kuanza mgomo wa kutokuingia darasani kuanzia jana.

Mgomo wao ni kupinga uamuzi uliochukuliwa na chuo hicho wa kutowafanyia udahili wanafunzi watakaoshindwa kulipa ada ya muhula wa kwanza. Wanafunzi hao wamesema watagoma kwa muda usiojulikana.


Wanafunzi hao wameamua kugoma baada uongozi wa chuo hicho kuchapisha waraka Oktoba 19, mwaka huu unaotoa maelekezo mapya ya udahili kwa mwaka 2007/08 kwa wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza na wa pili wanaofadhiliwa na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

Kwa mujibu wa waraka huo uliosainiwa na Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Joseph Kuzilwa, idadi kubwa ya wanafunzi wanaofadhiliwa na Bodi hiyo wamekwisha kulipa ada ya tuisheni kwa mwaka wa masomo 2007/2008.

Hata hivyo, baadhi ya wanafunzi hao ambao wamegoma kulipa kima cha chini cha asilimia 50 ya ada hiyo ambayo ni Sh 400,000 kwa muhula wa kwanza.

Kwa mujibu wa waraka huo, mwanafunzi atakayekubaliwa kupatiwa chumba cha kuishi katika mabweni ya chuo hicho ni yule atakayekuwa ametimiza masharti yaliyotolewa na uongozi wa chuo hicho.


Wanafunzi DUCE wagoma

2007-11-29 10:30:19
Na Eshy Mushi na Anneth Kagenda


Wanafunzi 56 wa mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu cha Ualimu Dar es Salaam (DUCE), wamegoma kuingia madarasani kama njia ya kushinikiza kupewa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

Wamedai kuwa, hatua ya uongozi wa DUCE, kukataa kusaini fomu za mikopo walizoziwasilisha, imewafanya washindwe kuhudumiwa na HESLB.

Hayo yalisemwa jana na baadhi ya wanafunzi hao walipokuwa wakizungumza na Nipashe chuoni hapo.

SWALI:

Hivi mwaka ujao 2008 tunaweza kwenda bila kuwa na mgomo kwenye chuo chochote kikuu? Ninyi wenzetu mlioko ughaibuni mara ya mwisho kuwa na mgomo wa wanafanzi kwenye nchi zenu/vyuo vyenu ilikuwa lini?
 
Wanafunzi wengi wa chuo cha maji jijini Dar nao wamegoma leo baada ya kucheleweshewa fedha zao za chakula.. !
 
1. Du nawaonea sana huruma hawa wanafunzi wanpoteseka kwa kucheleweshewa mikopo- kuishi kwa taabu!

2. Taabu migomo siku zote ni kutetea tu maslahi yao kama wanafunzi- wakigoma kutetetea maslahi ya taifa kama kupinga rushwa, uharibifu wa mazingira na kuporomoka kwa ubora wa elimu- ingeleta impact kubwa zaidi, kwa jamii. Mnakumbuka migomo ya Wanafunzi Indonesia na maandamano hadi Bungeni yalimwondoa Suharto? Wanafunzi wa Tz bado ni kudai tu posho zimechelewa!
In early 90s waligoma AHM akafunga UD kwa mwaka mzima- madai yao yalikuwa ni zaidi ya posho zao kuchelewa! Siku hizi hakuna wenye ujarisi wa wakati ule!
 
Kaka

It is time for the real final push! Ushindi ni Lazima. This guy has to go or this system has to change...I am thinking loud

Nikikumbuka "Msolla 'hola!', Lowassa 'anakula', Wanafunzi Ukraine ‘wanalilia' chakula;
Wewe je?

http://www.chadema.net/makala/mnyika/mnyika_22.html

Nasisimkwa!

U wapi uhalisi wa msemo watu wachache wanaweza kulaghaiwa kwa muda mchache lakini si watu wote wakati wote?

JJ
 
Yaani sijawahi kuwaona wana mazingaombwe kama wa kina Kikwete. Baada ya kuwarudisha wale watoto toka Ukraine ambako walikuwa wanaendelea na masomo vizuri; unajua nusu yao wamerudishwa Urusi kusoma tena? don't ask me why
 
Yaani sijawahi kuwaona wana mazingaombwe kama wa kina Kikwete. Baada ya kuwarudisha wale watoto toka Ukraine ambako walikuwa wanaendelea na masomo vizuri; unajua nusu yao wamerudishwa Urusi kusoma tena? don't ask me why

Nitauliza, mahali mwafaka, wakati mwafaka!

Nakutakia mapambano mema. Natoweka tena

JJ
 
Yaani sijawahi kuwaona wana mazingaombwe kama wa kina Kikwete. Baada ya kuwarudisha wale watoto toka Ukraine ambako walikuwa wanaendelea na masomo vizuri; unajua nusu yao wamerudishwa Urusi kusoma tena? don't ask me why

Ni kuhalalisha tu kwamba mwanzoni hawakufuata utaratibu na kujaribu kuponya majeraha ya kisiasa. Ni njia ya tu wagawe uendelee kuwatawala. Lakini furaha yangu ni kwamba walau wengine wameweza kupata nafasi ya kuendelea na masomo. Historia inatabia ya kuendelea kutoa hukumu, na itatoa!

JJ
 
Wanafunzi IMTU waandamana kudai mikopo

na Agnes Mlundachuma


WAKATI serikali ikilalamikia upungufu wa madaktari nchini, baadhi ya wasomi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Tiba na Teknolojia (IMTU), wamesimamishwa masomo baada ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kushindwa kuwakopesha fedha za kulipia ada.

Kusimamishwa masomo kwa wanafunzi hao kuliwalazimu kuandamana hadi Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknoknlojia ili kujua hatma ya fedha za mikopo walizoahidiwa na serikali.

Jumla ya wanafumzi 137 walifika katika ofisi za wizara hiyo ili kutoa malalamiko yao.

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Biseko Mlebo alisema wameshangazwa na hatua ya Bodi ya Mikopo kuwataarifu kwa barua kwamba watapewa mikopo kwa kiasi kisichozidi sh milioni 2.6 huku kiasi kinachobaki kufika sh milioni sita wakitakiwa kujilipia.

Alisema, suala hilo limewashitua kwa vile walisaini katika bodi hiyo kwa madhumuni ya kupewa mkopo wa sh milioni sita ikiwa ni ada ya masomo kwa mwaka katika chuo hicho.

Mlebo, alisema barua hiyo imezima ndoto za watoto wa maskini wanaohitaji kusoma ili kupunguza matatizo ya afya vijijini.

Alisema, tatizo la upungufu wa madaktari limelalamikiwa na madaktari wenyewe wakati wa mkutano wao wa 41 uliomalizika hivi karibuni uliobainisha kuwa Tanzania ni nchi ya mwisho duniani kwa uhaba wa madaktari.

Pamoja na idadi hiyo ndogo, madaktari wanakimbilia nje ya nchi kutokana na maslahi kidogo ikilinganishwa na nchi nyingine.
 
Yaani huwa najiuliza hivi kweli hadi kitokee nini ndio Rais Kikwete atajua Msolla amefeli na kupata zero!? au Prof. hawezi kufeli?
 
Mwanakijiji,
Kama ulikuwepo mawazoni mwangu..lini Pofesa akaondoka na zero?... Je sio sisi tunaotaka kuona CV ya kila kiongozi aliyeteuliwa kwa kigezo kuwa elimu yake ni ishara bora ya uongozi. Kina Mkandara hapa tulishindwa shule mapema wakati nafasi 10 za chuo kikuu zikigombea wa watu 10000, yaani kwa lugha yetu kukosekana kwa nafasi chuoni basi wewe ume fail ndio tumejazana mtaani tukipiga domo tindi vijiweni.
Well, ndio hivyo huyu ni Profesa na mtawala wa kudumu akiondoka Elimu kesho utamkuta uchumi ama Ikulu, uongozi nchi zetu hutokana na nasaba kwa lugha ya karibu nitasema majina yao yametajwa ktk biblia tukufu ya mtakatifu CCM..
Utanisamehe mkuu pamoja na kwamba kuendesha gari sio sawa na kuongoza wizara lakini kuna wakati hujiuliza hivi hata kuendesha gari la abiria kunahitaji kuwa profesa?
Je, kuna uhakika gani wa usafari salama kama dereva atakuwa mwenye shahada ya engineer wa magari tofuti na yule mwenye liseni ya udereva..Ndio haya ya kina Msolla wenyewe shahada kubwa lakini kupanga gear mlima kitonga hawajui wanzie wapi!
 
wamelala, hawataki kufikria. wanadhani wakiamka wakati wowote basi watakaloamua ndilo sahii hata kama ni bovu ilimradi aliyeamua ni prof.

ninadhani hata washauri wake wanamuogopa kumuuliza, kisa eti yeye ni professor. yawezekana hata muungwana anaogopa hizi falsafa za kigiriki.

ila watu hawataangalia cha falsafa, lungenge, wala nguo na magari waliyoyavaa. watu wa kawaida watawaburuza kwenye mahakama zao huku wakiwahoji walikuwa wapi wakati wananchi walipokuwa wakiteseka; pale ambapo hali zao za maisha ziligeuka ndoto; pale ambapo matumaini yashule yalididimia huku wakiwaza namna watakavyo kula nusu dola kwa siku ili walipie matibabu na hela ya tahadhari.


TANZANIA NI SHAMBA KUBWA ILA WATENDAKAZI NI WACHACHE TUMUOMBE MUNGU AONGEZE WATENDAKAZI KATIKA SHAMBA LAKE
 
oohh poor Tanzania...wakati haya yakitokea sekta ya utalii pale ikulu yazidi kukuna kichwa on how kukip busy idara hiyo kuhusiana na bosi wao ndugu Jk kuzidi kula dunia tuu as keshaichoka nchi!dats why hawezi jua wala sikia habari za maana kama hizo!
 
halafuu jamani naomba kuuliza what things or makosa will make a leader wa serikali ya kishkaji ya Jk..step down on his own if not ku stepishwa down na mkuu wake??
 
Miaka mitano itamhukumu zaidi ya mahakama zote!
Kifupi sasa hivi kesi bado inazidi kujijenga na itakapo fika wakati yooote yaliyokwisha pita yatavutwa mafaili yake... ole wake wale wote mnaochuma leo ktk uongozi huu maanake kutakuwa hakuna cha msalie!.
Yamefanyika Malawi, Zambia, Kenya na baadhi ya nchi za kiafrika kwa hiyo tuwe na subra.. mwendo mdundo, Africa tumesha choka mapinduzi ama umwagaji damu, siku hizi husubiri upepo (kura) utakapo badili mwelekeo ndio mashuzi yote hunuka!
 
1,000 watimuliwa Chuo Kikuu Ardhi

2008-10-05 14:37:50
Na Restuta James

Baraza la Chuo Kikuu Ardhi (ARU), limewasimamisha masomo wanafunzi zaidi ya 1,000 wa shahada ya kwanza walio mwaka wa pili hadi wa tano kwa muda usiojulikana.

Uamuzi wa baraza hilo ulitangazwa jijini Dar es Salaam jana na Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Idrissa Mshoro alipozungumza na waandishi wa habari.

Alisema chuo kimefikia uamuzi huo kutokana na kuona hali ya hatari ambayo ingesababisha uvunjifu wa amani chuoni hapo.

``Hii imeonekana ni njia sahihi ya kurejesha amani hapa chuoni,`` alisema.

Profesa Mshoro, alifafanua kwamba ``baraza litachambua wanafunzi ili kubaini waanzilishi na vinara wa mgomo na tutawachukulia hatua kadri sheria na kanuni za chuo zinavyoainisha.``

Alisema chuo kitahakikisha kinawarudisha chuoni wanafunzi wote wanaokidhi masharti ya usajili mapema iwezekanavyo.

Serikali ya wanafunzi hao imelaani kitendo hicho na kueleza kwamba kinaongeza ufa wa elimu kwa matajiri na masikini.

Rais wa Serikali ya Wanafunzi (ARUSO), Massawe Antony, alisema ``tunalaani uamuzi huo wa baraza na tunautaka uongozi uwarudishe wanafunzi wote chuoni haraka kwa kuwa kuwafukuza wanafunzi kunawaathiri kisaikolojia... kimsingi uongozi ulipaswa kutumia busara kutatua matatizo ya wanafunzi, kuwasimamisha ni kuahirisha tatizo kwa sababu wanafunzi hawa watarudi na umaskini wao.``

``Tunalaani pia kitendo cha kamanda wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam kwa kukataa kutoa kibali cha maandamano ya wanafunzi,`` alisema.

Wanafunzi hao pia wameitaka serikali kupitia upya sera ya elimu ya juu inayotaka uchangiaji wa elimu kwa kuwa inaweka tabaka kwa walionacho na wasionacho.

Wanafunzi walitangaza mgomo usio na kikomo ambapo waligoma kuingia darasani tangu Septemba 30 hadi Oktoba 3, chuo kilipofungwa.

Wanafunzi walikuwa wanapinga kuzuiliwa kwa matokeo ya wenzao 227 na kutaka yatolewe bila pingamizi, wanafunzi wa mwaka wa kwanza kutakiwa kulipa Sh. 400,000 kama sehemu ya ada pindi wanaporipoti na utaratibu wa chuo wa kutowasajili wanafunzi bila kulipa ada.

Hata hivyo, uongozi wa chuo umesema kwamba upo tayari kusikiliza mwanafunzi mmoja mmoja ili kufanya makubaliano ya kulipa kwa utaratibu maalum.

SOURCE: Nipashe
 
Mgomo kesho unafanyika chuoni hapo kutokana na ukandamizaji unaofanywa na menejimenti ya chuo kwa wanafunzi chuoni hapa. Prof mmoja anaitwa Mlacha ndo chanzo cha matatizo yote, hana utu, yeye kwake pesa ndo utu. Wanafunzi wamechoshwa na ukandamizaji wake. Hashauliki huyu bwana. Sasa kazi inaanza kesho na ole wake watoto wa maskini wana hasira sana nae.
 
Mgomo kesho unafanyika chuoni hapo kutokana na ukandamizaji unaofanywa na menejimenti ya chuo kwa wanafunzi chuoni hapa. Prof mmoja anaitwa Mlacha ndo chanzo cha matatizo yote, hana utu, yeye kwake pesa ndo utu. Wanafunzi wamechoshwa na ukandamizaji wake. Hashauliki huyu bwana. Sasa kazi inaanza kesho na ole wake watoto wa maskini wana hasira sana nae.

Kazi ipo mwaka huu......unaweza kuweka details zaidi kafanya nini huyu prof au yeye ni ndo accountant? au anahold kitengo gani?
 
Mgomo kesho unafanyika chuoni hapo kutokana na ukandamizaji unaofanywa na menejimenti ya chuo kwa wanafunzi chuoni hapa. Prof mmoja anaitwa Mlacha ndo chanzo cha matatizo yote, hana utu, yeye kwake pesa ndo utu. Wanafunzi wamechoshwa na ukandamizaji wake. Hashauliki huyu bwana. Sasa kazi inaanza kesho na ole wake watoto wa maskini wana hasira sana nae.

Mh mbona mapema sana kulikoni Dodoma? hebu mwenye maelezo ya kutosha kuhusu ukandamizaji wa Prof. Mlacha na management nzima auweke hapa ili tuweze kumjadili. Nimeshtushwa kidogo na habari hizi sio dalili nzuri kwa chuo hiki kipya kinachojitahidi kuchanua kwa kila hali.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom