Mheshimiwa Zitto na wana-CHADEMA.....

Engineer Mohamed

JF-Expert Member
Jul 27, 2007
451
9
Mheshimiwa Zitto Kabwe........

kwanaza nakupa kheri ya mwaka mpya 2008 wewe na wana-CHADEMA wote.
kwa vile hapa JF we Dare to Talk Openly...........
kwa heshima na taadhima tunakuomba utuwekee barua ulomuandikia Spika ili tuendelee kumkomalia NYANI na mapema 2008,tujue wapi PUMBA tutoe na tubakiwa na mchele safi.



Zitto: Sijatumia maneno ya kejeli



na Salehe Mohamed



MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), amesema maneno yaliyomo kwenye barua aliyomwandikia Spika Samuel Sitta, ni ya msingi na si kejeli wala dharau kama anavyoeleza spika huyo.
Alisema, mambo hayo ya msingi yanapaswa kufanyiwa kazi na Spika badala ya kukwepeshwa kama anavyofanya sasa kwa kudai barua hiyo imejaa maneno ya dharau na kejeli kwa Bunge.

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Zitto alisema hawezi kumwandikia Spika barua ya kejeli kwa kuwa anamheshimu kutokana na umri, cheo na ukomavu wake katika siasa.

Alisema Bunge ni mahali pa heshima, ndiyo maana alitumia busara kuandika barua hiyo akitaka haki itendeke.

"Siwezi kuandika maneno ya kejeli wakati nina hoja za msingi na ninahitaji zifanyiwe kazi ili niweze kupata haki yangu na kusafishwa jina langu," alisema Zitto.

Aidha, Zitto alifafanua kuwa hawezi kwenda mahakamani kama iliyoelezwa na Spika kwa vyombo vya habari hadi atakapopata majibu ya barua yake.

"Mimi nilimpelekea barua kutaka adhabu niliyopewa ya kusimamishwa bungeni Agosti mwaka jana ipitiwe upya hivyo naye anapaswa kunijibu kwa maandishi, baada ya hapo nitajua cha kufanya," alisisitiza Zitto.

Desemba 24 mwaka jana, Zitto aliwasilisha barua kwa Sitta, akitaka kupitiwa upya kwa adhabu aliyopewa ya kusema uongo bungeni.

Alisema kusimamishwa huko kulimfanya aonekane muongo ndani na nje ya Bunge, hivyo anamtaka Spika na baadhi ya mawaziri kuchukuliwa hatua kwa madai ya kuueleza umma kwamba yeye ni mwongo huku wakishindwa kuthibitisha madai yao.

Baada ya kupokea barua hiyo, Spika kupitia Katibu wake, Daniel Eliufoo, alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akieleza kuwa Zitto atapelekwa kwenye Kamati ya Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kuwa barua yake imejaa kejeli, ufedhuli na ubabe dhidi ya Bunge na Spika.


http://www.freemedia.co.tz/daima/2008/1/1/habari22.php




 
Nami naunga mkono. Mhe. Spika anasema barua ya Mhe. Zitto imejaa maneno ya kejeli. Hivyo, ni vyema Mhe. Zitto akaweka barua yake kwa Spika wazi ili nasi tuweze kuichambua na kujua ukweli uko wapi.
 
Mbona hiyo barua ya Zitto iliwekwa hapa tayati? Iliwekwa na Zitto mwenyewe. Search kwenye threads mbali mbali na mtaiona.
 
Barua hiyo hapo chini na imewekwa na Zitto mwenyewe, cha kushangaza amekanusha kwenye vyombo vya habari kuwa ka post barua hii kwenye net, hii ina maana Zitto wa JF sio Zitto Mbunge somebody ana play na jina lake tu.... hawa ndio viongozi wetu m-badala safari ipo ndefu mbele yetu...

Dar es Salaam.
24/12/2007



Spika wa Bunge,
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Dar es Salaam.



BUNGE KUPITIA UPYA ADHABU DHIDI YANGU

Tarehe 14/8/2007 Bunge lilipitisha azimio la kunisimamisha kazi za Bunge kwa jumla ya mikutano miwili.

Kwa mujibu ya kanuni za Bunge, wewe mheshimiwa Spika ndio unapaswa kuhakikisha kuwa utaratibu Bora unafuatwa Bungeni.

Kanuni ya 58(1) ya kanuni za Bunge, Toleo la mwaka 2004 (ambazo ndizo zinafanya kazi mpaka ninapoandika barua hii) inasema ifuatavyo:

Bila kuathiri masharti ya kanuni ya 4(2), Spika, atawajibika kuhakikisha kuwa utaratibu bora unafuatwa Bungeni, na uamuzi wake kuhusu jambo lolote la utaratibu utakuwa ni wa mwisho.

Msingi wa kanuni hii ni Kanuni ya 4(2) na 4(3) ambayo inasema

Kanuni ya 4

4(2) Spika ataongoza kila kikao cha Bunge na ndiye mwenye mamlaka ya kuamua mambo yanayoweza kuzungumzwa Bungeni.

4(3) Spika atawajibika kutilia nguvu Kanuni zote za Bunge, na endapo Mbunge yeyote hataridhika na uamuzi wa Spika anaweza kuwasilisha sababu za kutoridhika kwake kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni za Bunge ambayo itatakiwa ikutane mara moja kufikiria na kutoa uamuzi wake kwa Spika juu ya jambo hilo, na Spika atalijulisha Bunge uamuzi uliotolewa……….

Mheshimiwa Spika, kwa misingi ya kanuni zetu nilizozinukuu hapo juu ninaleta kwako maombi ili Kamati ya Kanuni za Bunge ipitie upya adhabu niliyopewa na Bunge ambayo mimi ninaamini haikuwa halali, haikufuata kanuni za Bunge, haikuzingatia tamaduni za Bunge (maamuzi ya Bunge yaliyopita) na kubwa zaidi haikunipa nafasi ya kujitetea.

Mheshimiwa Spika, mimi kama Mbunge katika Bunge lako ninaamini ya kwamba adhabu niliyopewa ilifikiwa kwa shinikizo la kiitikadi na hata kufikia kundi moja la wabunge kutumia vibaya wingi wao Bungeni (abuse of majority) na kuniadhibu bila kufuata kanuni za Bunge.

Nimeona, kwa kuwa demokrasia inakua nchini kwetu, ni vema niliombe Bunge kupitia upya adhabu ile na kama Bunge kupitia kamati ya Kanuni za Bunge likiona Kanuni za Bunge zilifuatwa nitaridhika na adhabu ile. Vile vile kama Bunge likiona kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa kanuni za Bunge, kwa bahati mbaya au kwa makusudi, basi niombwe radhi.

Mheshimiwa Spika, ombi langu hili mbele yako ni muhimu sana katika kulifanya Bunge lijiangalie na kurekebisha, kama inabidi, pale ambapo litakuwa limekosea. Hii itasaidia kuepuka makosa kama haya siku za usoni.

Mheshimiwa Spika, Kanuni za adhabu zimeanishwa katika Kanuni za Bunge Toleo la mwaka 2004. Kanuni husika ni kanuni namba 58, 59, 60, 61 na 62. Lakini pia kanuni hizi msingi wake, pamoja na masuala ya amani na utulivu Bungeni ni kanuni inayokataza kusema uongo Bungeni. Kanuni hii ni kanuni namba 50 ya kanuni za Bunge letu tukufu.

Mheshimiwa Spika, Bunge lina taratibu za kuleta hoja Bungeni. Taratibu hizi zimefafanuliwa kinagaubaga katika Kanuni za Bunge na zimeanisha wazi kabisa ya kwamba hoja haiwezi kutolewa juu ya hoja nyingine na kwamba muda wa kutoa taarifa za hoja umewekewa taratibu ndani ya kanuni za Bunge.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kanuni zetu zimesema wazi kabisa (59-3) kuwa iwapo Mbunge anashutumiwa kusema uongo Bungeni, au kutoa lugha ya kuudhi atapewa muda ili kuthibitisha hilo analoshutumiwa. Mimi mheshimiwa Spika, sio tu sikuwahi kushutumiwa kusema uongo bali pia wewe binafsi unajua sijawahi kupewa muda kuthibitisha chochote.

Muda wa kuwasilisha hoja yangu, ambao kwa masikitiko makubwa, viongozi wa Bunge mmeueleza kama ndio muda niliopewa kuthibitisha maneno yangu, ni muda wa kikanuni ambao niliomba mimi ili kuleta hoja binafsi na wala sio muda niliopewa kuthibitisha jambo lolote.

Mheshimiwa Spika maamuzi ya Bunge ya kunisimamisha kwa kusema uongo Bungeni (uongo ambao haujawi kusemwa ni upi) yalinidhalilisha mimi binafsi mbele ya jamii na kudunisha utu wangu. Adhabu niliyopewa iliniweka katika wakati mgumu sana na hata kunishushia heshima sio tu katika jamii ya Tanzania bali katika jamii ya kimataifa. Nimekuwa nikionekana ni Mbunge mwongo.

Mbaya zaidi baadhi ya Viongozi wa Bunge, ukiwemo wewe mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Katibu wa Mbunge mliendelea kuonyesha kuwa adhabu ile ni sahihi na kuwaaminisha wananchi kuwa mimi ni Mbunge Muongo.
Vile vile viongozi wa upande wa serikali akiwemo Waziri Mkuu, Mawaziri na Manaibu mawaziri wamenukuliwa na kurekodiwa na vyombo vya habari wakisema mimi ni Muongo kufuatia adhabu hiyo.

Adhabu niliyopewa na Bunge, ambayo naomba Kamati ya Kanuni za Bunge iipitie, imenidhalilisha sana kama mtu binafsi. Lakini pia adhabu hii ni ishara mbaya sana kwa demokrasia ndani ya Bunge let tukufu.

Mheshimiwa Spika, licha ya kwamba nina nafasi na Haki ya kuomba chombo kingine cha dola kama Mahakama kupitia adhabu hii, nimesita kufanya hivyo ili kulipa Bunge nafasi ya kujikosoa.

Ninaliheshimu sana Bunge na mimi kama Mbunge ningependa kuona Bunge likiheshimika mbele ya jamii, tena chini ya uongozi wako. Hii imethibitishwa kwa kuitumikia adhabu yote na kutotoa kauli yeyote iliyoingilia mamlaka ya Bunge kuhusiana na adhabu niliyopewa.

Ninawasilisha kwako, kwa unyenyekevu kabisa maombi yafuatayo

1. Bunge, kupitia Kamati ya Kanuni za Bunge, lipitie adhabu niliyopewa na Bunge tarehe 14/8/2007 na lijiridhishe kama Kanuni za Bunge zilifuatwa.

2. Bunge, baada ya kupitia vifungu vyote vya Kanuni za Bunge, ikiwemo kunisikiliza katika kikao cha Kamati, lipitie kauli zote za viongozi wa Bunge na wa Tawi la Utendaji (Serikali) kuhusu adhabu niliyopewa na kuona kama hawakuvunja kanuni za Bunge na sheria namba 3 ya mwaka 1988.

3. Kama Bunge likiridhika kuwa matamshi ya viongozi niliowataja katika namba 2 hapo juu, yanakiuka kanuni za Bunge kwa hali yeyote ile, basi wapelekwe katika kamati husika ya Bunge.

4. Bunge liniombe radhi kwa kunipa adhabu isivyo halali.

5. Bunge lijutie (repent) maamuzi iliyoyachukua na kuahidi mbele ya jamii ya Watanzania ambayo ndio inayotoa mamlaka ya utawala (Ibara ya 100 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano) kuwa halitarudia kuvunja kanuni za Bunge kwa makusudi na kumuadhibu mwakilishi wa wananchi mwingine yeyote bila makosa.

6. Bunge liahidi kuwa kamwe haitotokea Mbunge kuonewa kwa sababu za kiitikadi au kukomoa na kupiga marufuku vikao vya kamati za vyama vya siasa ndani ya Bunge kupanga njama za kuadhibu Wabunge bila makosa.

Mheshimiwa Spika, Ninaleta kwako maombi yangu haya nikiamini kabisa kuwa yatafanyiwa kazi kwa mujibu wa Kanuni za Bunge na hasa Kanuni namba 4(3) inayotoa mamlaka kwako kutilia nguvu matumizi ya Kanuni za Bunge na inayonipa nafasi mimi kama Mbunge kukata rufaa na kuonesha kutoridhishwa kwangu na maamuzi ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kanuni zetu maamuzi ya Bunge ni maamuzi ya Spika na vile vile maamuzi ya Spika (anapotekeleza mamlaka yake) ni maamuzi ya Bunge. Hivyo nimejiridhisha kabisa ya kwamba Kamati ya Kanuni za Bunge ina mamlaka ya kujadili suala hili.

Nakutakia kila kheri katika kuimarisha demokrasia ndani ya Bunge.

Wako mtiifu,




Kabwe Zuberi Zitto (Mb)
Mbunge wa Kigoma Kaskazini.


Nakala

1. Katibu wa Bunge
2. Kiongozi wa Upinzani Bungeni
 
Mbona ni barua ya kawaida sana. Sioni matusi au maneno ya kejeli. Nadhani Mhe. Spika ametumia ubabe katika kukataa kujibu barua hii.
 
Barua hiyo hapo chini na imewekwa na Zitto mwenyewe, cha kushangaza amekanusha kwenye vyombo vya habari kuwa ka post barua hii kwenye net, hii ina maana Zitto wa JF sio Zitto Mbunge somebody ana play na jina lake tu.... hawa ndio viongozi wetu m-badala safari ipo ndefu mbele yetu...

Tuwekee hiyo 'quote' aliyokanusha nasi tuione.
 
Mbona ni barua ya kawaida sana. Sioni matusi au maneno ya kejeli. Nadhani Mhe. Spika ametumia ubabe katika kukataa kujibu barua hii.

Nina wasi wasi Spika 6 asipo kuwa makini anaelekea kujifunga bao la pili la wazi wazi! kwani hili sakata laweza ibuka upyaaa!, and this time CHADEMA pleeeeeese msipoteze nafasi tena, CHOTA, narudia tena CHOTENI wanachama wa kutosha tayali kwa 2010.
 
Tuwekee hiyo 'quote' aliyokanusha nasi tuione.

Eeeh jamani. Mshaanza, hebu muacheni Zitto wetu. Ni kweli alisema. Na ni ukweli hakuitoa kwenye internet baada ya kumpelekea spika. Aliitoa baada ya barua yenyewe kuvuja katika vyombo vya habari, kutoka kati ya ofisi ya spika au ya kiongozi wa upinzani. Ndio yeye akamua kuitoa sasa ili wananchi barua yenyewe imesemaje haswa. Kwa hiyo isingevuja kwenye press na kuzua mjadala naye asingeitoa labda. We Masatu, usianzie zodo zodo hapa

Asha
 
Dua na Masatu.....

suali zuri sana hilo,tuwekeeni hizo source na cc tuone wenyewe.


Asha abdallah......

kiongozi wa UPINZANI BUNGENI nani?

Mheshimiwa Zitto......

tunafahamu kuwa sio sana kupitia JF,lakini tunaamini kuwa kuna watu wanakuletea news kama umetajwa ktk JF matokeo yake unakuja kujibu hoja zinazokuhusu,tunaomba na HILI UJE UTUJIBU TAFADHALI.
 
Eeeh jamani. Mshaanza, hebu muacheni Zitto wetu. Ni kweli alisema. Na ni ukweli hakuitoa kwenye internet baada ya kumpelekea spika. Aliitoa baada ya barua yenyewe kuvuja katika vyombo vya habari, kutoka kati ya ofisi ya spika au ya kiongozi wa upinzani. Ndio yeye akamua kuitoa sasa ili wananchi barua yenyewe imesemaje haswa. Kwa hiyo isingevuja kwenye press na kuzua mjadala naye asingeitoa labda. We Masatu, usianzie zodo zodo hapa

Asha

Masatu naye?! Nilitaka kumjibu hivihivi, naona umeniwahi. ahsante sana.
 
Is there anything to discuss here? Au ndiyo Spika 6 alikuwa anataka tuone lile alilosema "standards", sioni la maana la kujadili kama alitaka kutukuzwa kama Mungu basi kwakuwa Zitto hakumuita mtukufu ndio maana anaona hiyo barua ina kejeli! mimi siioni, labda sina busara!
 
Dua source ya habari ya Zitto kukanusha hii hapo chini kupitia gazeti "letu" la TanzaniaDaima unless kama huliamini....


Spika kitanzini

na Charles Mullinda
Tanzania Daima

NGUVU za Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sasa zinaelekea kuporomoka baada ya kambi yake kuu kuanza kumgeuka.
Sitta, ambaye mara kadhaa tangu aliposhika wadhifa wa Uspika amekuwa akijikuta katika migongano ya hapa na pale na wabunge na wananchi, amekuwa akiitegemea zaidi kambi ya wabunge vijana kumkingia kifua, wakiwemo wale wa kambi ya upinzani.

Kambi hiyo ya wabunge vijana, sasa imemgeuka Spika baada ya matukio ya hivi karibuni kuhusu uamuazi wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, ‘kukata rufaa’ akilitaka Bunge lipitie upya adhabu ya kusimamishwa aliyopewa mwezi Agosti.

Baada ya kupokea barua ya mbunge huyo kuhusu suala hilo, Spika alikaririwa akimbeza Zitto na kusema kuwa anamuonea huruma kutokana na kuonyesha kwake (Zitto) kutokomaa kisiasa.

Zitto ni mmoja wa wabunge mahiri katika kambi ya wabunge vijana, ambao mara kadhaa wamelitikisa Bunge kutokana na hoja zao na pia, ingawa ni mbunge wa upinzani, amekuwa moja ya nguzo muhimu za Spika hasa kwa mahasimu wake wa kisiasa wa ndani ya chama chake.

Habari zilizolifikia Tanzania Daima Jumapili, zilieleza kuwa Zitto, amemuweka Spika Sitta katika wakati mgumu baada ya kuendelea na msimamo wake wa kutaka adhabu yake ipitiwe, licha ya kauli ya Sitta.

Ingawa jana katika mahojiano yake na gazeti hili alisema hataki kulumbana na Spika Sitta katika suala hilo kwa sababu anamuheshimu sana, Zitto aliendelea kusisitiza kwamba anachotaka ni haki itendeke kwa sababu anaamini adhabu iliyotolewa na Bunge dhidi yake haikuwa sahihi.

“Ninamuheshimu sana Spika, sipendi kabisa kubishana naye, ninachokiomba ni haki itendeke kwa sababu ninaamini sikutendewa haki kwa kupewa adhabu ile, sijaridhika. Lakini kamati ikiketi na kupitia adhabu hiyo nitaridhika na maamuzi yake,” alisema Zitto.

Aidha, akizungumzia madai kwamba alisambaza barua yake hiyo kwa vyombo vya habari na katika mtandao wa ‘internet’, jambo ambalo Spika amekaririwa akieleza kuwa ni kinyume cha taratibu za Bunge, Zitto alisema hilo si kweli kwa sababu alitoa nakala kwa kiongozi wa upinzani bungeni na kwa katibu wa Bunge tu.

Huku akiongea kwa kuchagua maneno, Zitto alisema kamwe hana nia ya kutumia nafasi hiyo kutafuta umaarufu. “Sikutumia nafasi kujitafutia umaarufu kama inavyoelezwa, ningetaka hivyo ningezungumzia jukwaani, kwa sababu wakati naadhibiwa watu wengi walikuwa hawampendi Spika, hapo ndipo ningemchafua.

“Ninasema kweli, ningetaka umaarufu ningekwenda mahakamani, nina orodha ndefu ya wanasheria wazuri wanaotaka suala hili nilipeleke mahakamani na wao watalisimamia ili haki ipatikane, lakini mimi nasema hapana, na tangu nilipoadhibiwa nilikuwa kimya, nimetumikia kifungo kimya, hiyo yote ni kwa sababu ya kumuheshimu tu Spika, ni unyenyekevu wa hali juu,” alisema Zitto.

Inadaiwa kuwa msimamo huu wa Zitto na kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na Spika dhidi ya barua iliyoandikiwa na mbunge huyo, unaashiria kuwa Spika ana wasiwasi kuwa iwapo Kamati ya Kanuni za Bunge itaipitia upya adhabu hiyo, Bunge linaweza kujikuta matatani kwa kukiuka kanuni au desturi zake.

Wataalamu wa wafuatiliaji wa masuala ya Bunge waliozungumza na gazeti hili walieleza kuwa, Bunge linaendeshwa kwa kanuni na desturi ambazo huliongoza kufikia maamuzi yake, lakini katika kesi ya Zitto, vyote hivyo havikufuatwa.

Ukweli huu unathibitishwa na adhabu kadhaa zilizokwishatolewa na Bunge kwa wabunge ikiwemo aliyopewa aliyewahi kuwa Mbunge wa Temeke, Augustino Mrema baada ya kutamka bungeni kuwa serikali imepanga kumuua yeye (Mrema) na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Sharrif Hamad.

Mrema aliliambia Bunge kuwa habari hizo alipewa na aliyewahi kuwa Mkuu wa Usalama wa Taifa Imran Kombe. Bunge lilimpa Mrema siku tano za kuthibitisha maelezo yake, lakini alishindwa kufanya hivyo na kujikuta akiadhibiwa kusimama kufanya shughuli za Bunge kwa muda wa siku 40.

Baadhi ya wabunge walioadhibiwa kwa utaratibu wa kupewa siku za kuthibitisha kauli zao ni pamoja na Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa aliyetiwa hatiani kwa kuchezea taarifa za Bunge kuhusu sakata la fedha za matibabu zilizotumiwa na Hassy Kitine.

Mwingine ni Philemon Ndesamburo ambaye aliadhibiwa na Bunge baada ya kushindwa kuthibitisha kauli yake kuwa Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, aliwaambia wafanyabiashara wakitaka mambo yao yawanyookee, wajiunge na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kwa kuzingatia mlolongo huu wa matukio ya adhabu zilizokwishawahi kutolewa bungeni, kambi ya wabunge vijana imepanga kumshinikiza Spika kuiamuru Kamati ya Kanuni za Bunge kuipitia upya adhabu hiyo na kwamba matokeo yake yatachambuliwa ili kuona kama kamati hiyo inafanya kazi kwa kufuata haki.

Mmoja wa wabunge vijana kutoka Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Halima Mdee, alilieleza gazeti hili kuwa kambi ya wabunge vijana haikubaliani na msimamo wa Spika na inataka adhabu ya Zitto ipitiwe mpya kwa sababu hata Rais Jakaya Kikwete ameonyesha kwa vitendo kutokubaliana na adhabu hiyo.

“Adhabu aliyopewa Zitto ilitokana na hoja yake ya kutaka mkataba wa Buzwagi uchunguzwe, wabunge wa CCM waliungana kumpinga kwa sababu wanazozijua na ambazo sasa Watanzania wengi wanazijua, wakamsimamisha.

“Lakini ninaamini walimsimamisha kwa sababu za kiitikadi, ingawa mimi sikuwepo, hawa wamemsimamisha, rais kaunda kamati ya kupitia upya mikataba ya migodi ya madini ukiwemo huo wa Buzwagi, haijalishi hata kama kaunda kisiasa au kwa dhamira ya dhati, kinachoonekana hapo ni kwamba rais amekubaliana na hoja ya Zitto.

“Na kama rais amekubaliana na hoja ya Zitto, maana yake ni kwamba adhabu aliyopewa na Bunge haikuwa sahihi, sasa Bunge linapaswa lijitizame upya, vinginevyo kulishitaki ni sawa tu.

“Kwa Spika, kumuita mbunge mtoto ni jambo la ajabu sana kwa mtu tunayemuheshimu kama yeye, utoto wa mtu haupimwi kwa umri bali hoja zake, wanaomsikiliza Zitto akitoa hoja wanajua kama ni mtoto au la… katika hili atauona utoto wetu,” alisema Halima kwa kujiamini.

Pamoja na hayo yoye, kivuli cha Rais Kikwete nacho, ambacho kimekuwa kikiyaandama maamuzi ya Spika, kinaonyesha kumuweka katika hali ngumu zaidi kwa vile kimekuwa kikipingana naye kila mara.

Kwa uchache, Rais Kikwete alionekana kutofautiana na Spika pamoja na wabunge mapema mwaka jana, pale walipokosoa madai yao ya nyongeza ya mishahara na marupurupu wakati taifa likiwa katika hali ngumu ya chakula na ukosefu wa umeme.

Kikwete pia ameonekana kutofautiana na Spika na wabunge wa CCM baada ya kuunda kamati ya kupitia upya mikataba ya madini, jambo ambalo lilikuwa likidaiwa na Zitto kabla ya kusimamishwa na wabunge wa CCM.

Wafuatiliaji wa masuala ya Bunge wanaeleza kuwa iwapo Spika Sitta hatatumia busara zaidi katika kutatua mgogoro huu na kambi ya wabunge vijana, na hivyo kusababisha kufarakana nao, atakuwa amebakia peke yake jambo ambalo ni hatari zaidi kwa siasa za hapa nyumbani.

Wengi wamemtaka akumbuke kazi kubwa iliyofanywa na wabunge hao, wakati wa sakata lake na Mbunge Malima, ambapo baadhi ya vigogo ndani ya chama chake waliamua kumshughulikia huku wakiwa na dhamira ya dhati ya kumuengua katika Uspika.

Sitta aliokolewa na kambi ya wabunge vijana, baada ya Mdee kuwasilisha hoja bungeni, akilitaka Bunge kumuadhibu Malima kwa kumdhalilisha mbunge na kiti cha Uspika, hoja ambayo iliua nguvu za wapinzani wa Spika na kumpa mwanya wa kukwepa mashambulizi yaliyokuwa yakielekezwa kwake.
 
Kitila/Asha ulitaka Source...what next? baadhi yetu huwa tunafikiri negative tu...Hata kama mtu analiponda gazeti xyz, lkn si kwamba atakuwa hatetei..au ushamuweka masatu ktk kundi Fulani?
 
kama Zitto kambinga, thats means Zitto anaechangia JF sio ZITTO HALISI ni wa Kuchorwa...itabidi mwanakijiji atutungie msamiati kama alivyomtungia kikwete simba wa kuchora..
Kama hivyo Ndivyo ndio maana binafsi nilipinga wazo la mmoja wetu kuwa JF iendeshwe kama Taasisi then tuwachague watu wenye majina halisi humu JF kuongoza, kumbe wenye Majina Halisi nao wanapokumbwa na kashfa/au Issue HUCHOMOA KUHUSIKA KWAKO HUMU JF...
 
Ha! ndo maana sioni comment za zitto tena! pole sana. wanaposema mitandao ya internet wanamaana JF au? kudadadeki. JF jicho pana hata mzee wa jogoo lilimwona pale J'berg airport.
 
labda kejeli ni kwa "mtu mzima kuambiwa aombe msamaha na akiri kosa" si unajua tamaduni kwamba mtu mzima haambiwi kaj**ba?

aidha inategemea barua iliandikwa kwa nani. yaani spika au mh. sita. sasa kama iliandikwa kwa spika na ikawa imefikishwa ofisi ya spika na kupokelewa na haikuwa imeandikwa "siri/confidential" itabidi tujiulize ni nani aliyeivujisha kwenye vyombo vya habari?

nakumbuka zitto alipoiweka barua hapa jf alisema nia ni kuwapa wanachama kile chote alichoandika badala ya wanatu kutegemea nusu habari za magazeti
 
Masatu

Sasa shida iko wapi hapo. Zito alitoa barua hiyo hapa baada ya kuona kwamba aliyeandikiwa kesha ipata na kumpa muda wa kutafakari. Ulitaka Daily News waitoe ya uongo? CCM na Watanzania MAFISADI ndio wametufikisha hapa wanataka kila kitu kiwe siri. Hakuna ujinga ujinga huu wa siri kila kitu, kwani kuna ubaya gani hata kama hiyo barua ipo kwenye luninga. Technologia mjomba twende na wakati tupo karne ya 21 siyo ya 10.

Waambieni watoe report ya BOT au bado wanaipika. Jamani tuweke Utanzania mbele na tuache longolongo ambazo hazina faida na taifa.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom