Mwanahabari Huru
JF-Expert Member
- Mar 9, 2015
- 14,243
- 34,899
Tumepata taarifa muda mfupi uliopita kuwa, ndugu yetu, kamanda mwenzetu na mpiganaji mwenzetu, *Mdude Nyangali Chadema* ambaye amekuwa akishikiliwa na Jeshi la Polisi, Vwawa, Mbozi, mkoani Songwe tangu Jumatano ya wiki hii, amesafirishwa kupelekwa Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo.
Hadi jana jioni polisi mkoani Songwe, kupitia kwa RCO walikuwa wamekataa kumpatia dhamana na kwa kauli aliyonukuliwa, RCO alisema kuwa hawatamwachia wala kumpeleka mahali popote, ikiwemo mahakamani, hadi atakapokubali kuandikisha maelezo polisi.
Tangu siku aliyokamatwa Jumatano majira ya saa nne asubuhi, kwa kufuatwa na askari polisi akiwa ofisini kwake hapo Vwawa, hakukuwa na maelezo yaliyonyooka kutoka kwa polisi kuhusu tuhuma zinazomkabili kiasi cha polisi kumkata, kumhoji na kumshikilia siku zote hizi.
Wakati akikamatwa kulikuwa na maelezo pengine yasiyokuwa rasmi kutoka kwa mmoja wa polisi wake kuwa amekamatwa na atasafirishwa kwenda mahali pengine (mkoa mwingine) ambako inadaiwa kuwa amefanya hilo kosa analotuhumiwa nalo.
Alipofikishwa Kituo cha Polisi Vwawa, akaambiwa kuwa amekamatwa na atahojiwa kwa ajili ya kuunganishwa kwenye kesi inayohusu vurugu zilizotokea wakati wa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mji Mdogo wa Mlowo, kesi hiyo tayari iko mahakamani ambayo pia Mbunge wa Jimbo la Mbozi, Pascal Haonga (CHADEMA) anashtakiwa.
Siku hiyo ya Jumatano Mdude alitumia haki yake ya kisheria ya kutaja anuani yake tu hapo polisi na kuwaambia polisi maelezo mengine yuko tayari kuyatoa mahakamani si hapo kituoni.
Polisi walikataa kumwachia kwa dhamana wakisema kuwa atafikishwa mahakamani siku inayofuata ambayo ilikuwa Alhamis. Hawakufanya hivyo bila sababu yoyote ile ya msingi. Jana Ijumaa ndiyo wakatoa hiyo sababu kwamba lazima akubali kuandikisha maelezo vinginevyo hawatamwachia.
Asubuhi ya leo wakati makamanda wetu wamefika kituoni kwa ajili ya kumpelekea chakula, wamekuta taarifa hizo kuwa hayupo kasafirishwa kupelekwa Dar es Salaam.
Hadi sasa haijaeleweka kwanini polisi wanamshikilia Mdude siku zote hizo bila kumwachia kwa dhamana au kumfikisha mahakamani. Na bado hawajasema kosa alilofanya kiasi cha kusafirishwa kupelekwa Dar es Salaam.
Chama kinafuatilia suala hili. Tayari mawakili wanalifanyia kazi, ikiwa ni mwendelezo wa hatua za kisheria zilizoanza kuchukuliwa tangu juzi hasa kwa ajili ya kuwataka polisi wamfikishe mahakamani Mdude Nyangali Chadema ama wamwachie.
Itakumbukwa kuwa hii sasa ni mara ya pili mpiganaji mwenzetu Mdude Nyangali Chadema anakamatwa na kushikiliwa na jeshi hilo na kusafirishwa kupelekwa Dar es Salaam. Mara ya kwanza alikamatwa na kushikiliwa kwa muda mrefu bila kufikishwa mahakamani pamoja na makamanda wengine hadi Mwanasheria Mkuu wa Chama, Tundu Lissu aliposimamia suala lao ndipo wakajulikana wako kituo gani na baadae wakarudishwa kwenda kushtakiwa katika maeneo yao, ambapo Mdudr alishinda kesi hiyo ya makosa ya mtandaoni aliyofunguliwa dhidi yake.
Kwa taarifa hii pia tutoe wito kwa makamanda wa Dar es Salaam ambako Mdude analetwa, tuoneshe ushirikiano na undugu wetu kwa mwenzetu kama tulivyofanya last time kwake na wale wenzake lakini kama ambavyo tunalazimika kufanya kwa makamanda wenzetu wengine ambao wanajikuta katika hali kama aliyonayo Mdude.
Wakati Chama kupitia kwa wanasheria kinalifuatilia na kulifanyia kazi suala hili kwa uzito mkubwa kwa hatua za kisheria, sisi wengine pia tumsaidie kwa namna iliyoko ndani ya uwezo wetu.
Mdude amekuwa mmoja wa wapiganaji mahiri wanaotumia haki yao ya uhuru wa maoni kuikosoa na kuishauri Serikali ya Rais John Magufuli kupitia maandishi. Hivyo basi, tumuunge mkono, kwanza kwa kupiga kelele dhidi ya manyanyaso anayopewa ya kukamatwa na kushikiliwa kinyume cha sheria hadi dunia nzima ijue kuwa Mdude ni ishara ya kwamba Serikali hii imeamua kukandamiza uhuru wa maoni.
Tupige kelele dhidi ya udhalimu wa namna hii anaofanyiwa Mdude na watu wengine. Lakini pia tusichoke kutimiza wajibu wetu wa kikatiba na kisheria, kuwakosoa na kuwashauri watawala wa serikali hii hadi waelewe kuwa nchi hii ni ya Watanzania wote na wao wana dhamana tu ya kuongoza. Wananchi ndiyo wanayo mamlaka ya mwisho. Hivyo kama hawaridhiki na mwenendo wa Serikali au Rais au viongozi fulani fulani, na hivyo kuathiri hali yetu kama nchi kisiasa na kiuchumi, wananchi wanayo haki ya kusema na LAZIMA wasikilizwe.
Tutaendelea kuwapatia taarifa juu ya suala hili. Asanteni.
Tumaini Makene