Mdahalo wa wazi ulioandaliwa na UDASA kuadhimisha miaka 58 ya Uhuru tarehe 09.12. 2019

George Kahangwa

JF-Expert Member
Oct 18, 2007
547
147
CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM
Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam (UDASA)
S.L.P 35091 – DAR ES SALAAM - TANZANIA​


Chair: 0713 563 212
Secretary: 0784687530
Treasurer: 0756594250
Editor: 0756260602
E-mail: udasa@uccmail.co.tz





6 Desemba, 2019, Dar es Salaam.


TAARIFA YA UDASA KWA UMMA KUHUSIANA NA MDAHALO WA KUMBUKIZI YA SIKU YA UHURU TAREHE 09/12/2019

Ndugu wanahabari,

Awali ya yote tunakushukuruni kwa kuitikia wito wetu kama ilivyo kawaida yenu. Hii inaendelea inatudhihirishia weledi na nia ya dhati mliyonayo ya kushirikiana nasi Wanataaluma katika shughuli zetu za ujenzi wa taifa ambayo ni pamoja na kugawa maarifa na fikra chanya kwa umma wa watanzania, kufanya tafiti na kutoa ushauri wa kitaalamu.

Ikiwa ni siku tatu kabla ya tarehe 9/12/2019, siku ambayo taifa na watanzania tutasherehekea miaka 58 ya uhuru wa Tanzania Bara, tumewaiteni hapa kuwashirikisha habari ya tukio maalum ambalo Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDASA) imepanga kulifanya siku ya Kumbukizi hiyo ya Siku ya Uhuru.

Kwa ufupi, UDASA imeandaa mdahalo wa hadhara/ wa wazi ambao unalenga kuleta Wanataaluma na Wadau wengine wa Maendeleo katika umma wa Tanzania pamoja kujadili na kutafakari kwa pamoja kuhusu nafasi, wajibu, na mchango wa Wanataaluma katika maendeleo ya Taifa. Mdahalo huo utafanyika katika Ukumbi wa Nkrumah wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuanzia saa 8 (nane) mchana hadi saa 12 (kumi na mbili jioni). Mada kuu ya mdahalo huo ni “Miaka 58 ya Uhuru: Wajibu na Mchango wa Wanataaluma Katika Maendeleo ya Taifa”

Huu ni mdahalo wa aina yake na wa kipekee kwani tangia nchi ipate uhuru hatujawahi kupata nafasi ya kutosha, umma wa watanzania ukapata fursa huru na ya wazi ya kutathmini mchango na wajibu wa mwanataaluma na msomi wengine kwa ujumla katika maendeleo ya taifa kiutamaduni, kiuchumi na kisiasa. Tumefanya hivyo kwa sababu tunaamini kwamba safari iliyo mbele yetu kama taifa inahitaji mshikamano na ushirikiano wa karibu kati ya wasomi na makundi yote ya kijamii kutatua Changamoto za taifa letu na kuleta maendeleo ya watanzania wote katika Uhalisia wa maisha yao.

Ndugu wanahabari,

UDASA tumeandaa mdahalo huu kwa nia ya dhati tukiamini kuwa usomi wetu hauwezi kuwa na maana kwa watanzania kama hatuelewi watanzania wanategemea tuwe tukiwafaa kwa njia zipi. Huenda tunafahamu wajibu wetu kama Wanataaluma, lakini si vyema tukibakia kudhani kuwa ndio wajibu wetu na huku watanzania wanategemea vinginevyo kinyume na tunavyofanya.

Hivyo basi, mdahalo huu utatoa nafasi ya pekee na ya kihistoria ya kujadili na kupata mrejesho kutoka kwa watanzania kuhusu mwenendo wa wasomi nchini na matarajio ya watu kwa mtu aliyepata upendeleo wa kuelimika kwa kiwango cha juu. Tunategemea Mjadala utakaofanyika utakuwa chachu ya kuleta ushirikiano kati ya Wanataaluma na wadau wengine wa maendeleo wakiwemo ninyi wanahabari, viongozi wa ngazi mbalimbali, taasisi za kiserikali na za kiraia, watumishi wa umma katika kada mbalimbali, wanasanaa, na makundi yote kijamii.

Ndugu wanahabari,

Kutokana na umuhimu wa mdahalo huo, tunawaomba kwa niaba yetu muuhabarishe umma wa Tanzania, kwamba kila mwenye nafasi siku hiyo afike Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Ukumbi wa Nkrumah ili tujadili pamoja, tusahihishane, na tuwekane sawa ili kuifanya taaluma iwe na mchango wa moja kwa moja katika kuijenga Tanzania yenye maendeleo endelevu kwa kila mtanzania.

Tunategemea kuwa na muda wa kutosha kuruhusu kila aliye kuja na nia ya kuchangia hoja kufanya hivyo. Wapo waongeaji wakuu, lakini kazi yao kuu itakuwa ni kutupa mwanga tu kuhusu wajibu na mchango uliotolewa na wanataaluma katika kuijenga Tanzania katika zama tofauti. Hii itatusaidia kujiona wapi tunahitaji kujifunza ili kuifanya taaluma yetu iwafae watanzania.

Naomba kusisitiza kwamba, tunawakaribisha watu wote pasipo kujali tofauti za aina yoyote ile, na kuwasisitiza kuwahi mapema kwa kuwa huenda ukumbi usitoshe kutokana na watu wengi mahiri sana kuwa na shauku na kuthibitisha kuwepo kwenye tukio hilo.

Asanteni sana.

Dkt. George Leonard Kahangwa
Mwenyekiti wa UDASA
Desemba 6, 2019
 
Tumepeta changamoto kwenye suala hili. Tukithibitisha tutasema. Ila maandalizi ya live streaming yako vizuri.

Dkt, Nadhani jamii kubwa ya watanzania wataweza kushiriki vema kwa kutazama nakusikiliza kupitia kituo au vituo bora vya runinga hapa nchini hususan AZAM, ITV au STAR TV vyombo huru. Vingine vitatoa masharti kiasi kwamba itaathili uhuru wa wachangiaji.

Ni mtazamo wangu muwekeze nguvu na juhudi zote ili watanzania wa level zote washuhudie mojakwamoja mjadala huu.
 
Tungeomba katika mjadala wao wasiegemee Mrengo wowote wa kisiasa kujadili mstakabar wa nchi hii. Kama wasomi tutegemee kugusa Nyan ja zote katika maendeleo hususani kijamii,kisiasa na kiuchumi. Huu ni uwanja wenu kuondoa unafiki katika uhalisi. Kuonyesha usomi usio na uwoga..
Mungu Ibariki Nchi HII!!
 
Baadhi tuko nje ya miji sasa online mtandao siyo nzuri sana. Hivi vyombo vyote hivi bado inakua ngumu kupata nafasi au gharama ziko juu sana?
Dkt, Nadhani jamii kubwa ya watanzania wataweza kushiriki vema kwa kutazama nakusikiliza kupitia kituo au vituo bora vya runinga hapa nchini hususan AZAM, ITV au STAR TV vyombo huru. Vingine vitatoa masharti kiasi kwamba itaathili uhuru wa wachangiaji.

Ni mtazamo wangu muwekeze nguvu na juhudi zote ili watanzania wa level zote washuhudie mojakwamoja mjadala huu.
 
Baadhi tuko njee ya miji sasa online mtandao sio mzuri sana. Hivi vyombo vyote hivi bado inakua ngumu kupata nafasi au gharama ziko juu sana?

Kuna kapointi amekagusia Dkt hapo juu

Wamekumbana na Changamoto

Kuna mengi sana nyuma ya hii sentensi..... nitumie neno bovu kufupisha.... yaani vyombo vinaweza kuwa vimeufyata
 
Tunakushukuruni nyote mliofuatilia. Mdahalo ulirekodiwa hapa
Mwanzoni link ina shida kidogo,ila mbele imekaa vizuri, hususan sehemu ya mzee Butiku.
 
2 Reactions
Reply
Back
Top Bottom