Mchungaji Msigwa, Abwao waanza kwa kishindo kupigania katiba mpya

nickname

JF-Expert Member
Dec 20, 2009
544
147
WABUNGE wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) mkoani Iringa wameanza kazi kwa kishindo ikiwa ni pamoja na kupokea maombi ya wananchi wanaotaka Katiba mpya.

Wabunge hao: Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini) na Chiku Abwao (Viti Maalum), walipokea maombi hayo ya wananchi katika mkutano wa kuwashukuru wananchi wa jimbo la Iringa Mjini kwa kuchagua diwani wa CHADEMA Kata ya Mvinjeni pamoja na kumchagua Mchungaji Msigwa kuwa mbunge wa Iringa Mjini.

Katika mkutano huo uliotanguliwa na maandamano makubwa kutoka ofisi za CHADEMA wilaya ya Iringa Mjini, Mchungaji Msigwa aliwapongeza wananchi hao kuwa kuanza kuomba katiba mpya kwa sasa na kuwataka kuendelea kudumisha amani na utulivu wakati ombi lao likifikishwa mbele ya Bunge kwa ajili ya kujadiliwa zaidi.

“Ndugu zangu kwanza niwapongeze kwa kujitokeza kwa wingi katika mapokezi ya sisi wabunge wenu leo ila nawaomba maombi haya ambayo mmeyafikisha kwetu kama wabunge tutayafikisha bungeni,” alisema.

Hata hivyo mchungaji Msigwa alisema wapo baadhi ya madiwani wa CCM wamekuwa wakieneza uongo kwa wananchi kuwa hatua ya wao kuichagua CHADEMA ni mwanzo na mwisho wa kuendelea kupata maendeleo, jambo alilosema ni uongo wa wazi.

“Nawaombeni wananchi wa jimbo la Iringa mjini kaeni mkao wa kula hakuna mtu hata mmoja mwenye uwezo wa kukwamisha maendeleo na diwani atakayeshindwa kutimiza ahadi zake basi atakuwa hafai kuwa diwani na wananchi uchaguzi ujao mpigeni chini,” alisema.

Mchungaji Msigwa alisema kati ya mambo ambayo atayafanya katika jimbo hilo ni pamoja na kutekeleza ahadi zake na kufanya yale ambayo wananchi watamtuma kufanya na si vinginevyo.

Kwa upande wake, Abwao alisema ushindi wa CHADEMA katika jimbo hilo si ushindi wa bahati mbaya bali ni ushindi uliotokana na nguvu ya umma katika kukionyesha Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa fedha na mbinu chafu si matakwa ya wananchi katika karne hii.

Alisema CCM isitegemee kama itakuja kulichukua jimbo hilo tena na zaidi itaendelea kupokonywa majimbo mbalimbali ya mkoa wa Iringa hadi mkoa mzima wa Iringa utakapokuwa ngome ya CHADEMA.

Hata hivyo, alieleza kusikitishwa kwake na hatua ya Jeshi la Polisi kuendelea kutumiwa na CCM kuzuia mikutano ya CHADEMA na kuwa kufanya hivyo ni sawa na kuendelea kujenga chuki na wananchi pamoja na vyama vya upinzani.

“Nguvu ya umma ikiamua inaweza kufanya mkutano kwa nguvu japo hatupendi iwe hivyo ila tunaomba Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP) Saidi Mwema kuacha demokrasia ichukue mkondo wake badala ya kujaribu kutaka kuzuia mvua kwa mikono,” alisema Abwao.

Source: Tanzania Daima
 
Mtwivila,Gangilonga,Kihesa, Ngome.... nakumbuka baghi tu ya maeneo pale IR, hongereni
 
Back
Top Bottom