Mchakato Haramu, Rasimu Haramu Hata Wakifanya Karamu...

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,461
39,928
katiba+2.jpg

Na. M. M. Mwanakijiji


Kuna kila dalili kuwa rasimu ya Katiba Mpya iliyozinduliwa kwa shangwe na vigelege siku chache zilizopita inaonekana kukubalika na watu mbalimbali. Wanasiasa na wasio wana siasa wengi inaonekana wameikubali kazi ya Tume ya Jaji wa Warioba ambayo ilipewa jukumu la kusikiliza maoni ya wananchi kuhusiana na Katiba Mpya. Matokeo ya kazi hiyo yameonekana katika rasimu (draft) ya Katiba Mpya ambayo sasa inaenda kwenye mchakato wa pili wa kutolewa maoni kupitia majukwaa ya Katiba. Baadaye mchakato huu utaenda kwenye kuundwa kwa baraza la kutunga Katiba ambapo rasimu itapatikana na hatimaye kutangazwa kuwa ndio rasimu rasmi ambayo wananchi watatakiwa kuipigia kura ya kuikubali au kuikataa.


Rasimu ambayo imeshabikiwa na kukubaliwa na watu wengi na kuzinduliwa haina uzito wowote zaidi ya kuwa ni mapendekezo tu. Vipengele vyake vyote vinaweza kufutwa au kubadilishwa kutokana na mchakato unavyoelekea. Mpaka pale itakapopatikana rasimu ya Katiba ambayo itaenda kupigiwa kura ni muhimu kuzingatia kuwa kilichopo sasa ni mapendekezo tu ya Tume ya Katiba Mpya. Hii siyo rasimu ambayo wananchi wataipigia kura na vipengele vyake siyo lazima viwe ndivyo vipengele vitakavyokuwepo kwenye Katiba Mpya.

Pamoja na hayo, tangu kuzinduliwa kwa rasimu hii baadhi ya watu mbalimbali wameniuliza msimamo wangu kama umebadilika kuhusiana na mchakato wa Katiba Mpya. Kwa wanaokumbuka ni kuwa mimi ni miongoni mwa watu wachache ambao tuliukataa mchakato huu tangu ulipotangazwa na Rais Kikwete, tuliipinga sheria ya kupitia mchakato huu (hata ilipowekwa vipodozi vya mabadiliko) na zaidi kukataa kutambua tume hii iliyoundwa. Baadhi ya marafiki zangu wamenirushia maswali mengi ambayo kumjibu mmoja mmoja imekuwa ni kazi kubwa na hivyo nimeonelea badala ya kuendelea na ile Barua ya Wazi niliyowahidi wiki kadhaa sasa nitumie nafasi hii kujibu baadhi ya maswali hayo.

SWALI: Je, baada ya kutolewa rasimu hii ya Katiba na Tume ya Jaji Warioba na hasa kutokana na mwitikio wa watu mbalimbali ambao wameonesha kuikubali je na wewe umebadili msimamo wako?

JIBU: Msimamo wangu haujabadilika; mchakato haramu matokeo haramu! Kwamba mchakato umetoa "rasimu nzuri" haibadilishi ukweli kuwa ni mchakato haramu. Baadhi ya watu ambao walikuwa na tatizo na mchakato huu sasa hivi –baada ya kusoma rasimu – wamekubali kuwa ni rasimu nzuri na hivyo hawana tena tatizo na mchakato! Hii inashangaza.

SWALI: Lakini kama kilichopatikana ni kitu kizuri na kinakubalika na wananchi wengi kwanini tusikiunge mkono si ndicho ambacho watu wamekuwa wakitaka kwa muda mrefu?

JIBU: Tukikubali kuwa tunaweza kutumia njia (means) mbaya kufikia lengo zuri (ends) na hivyo kwa vile kilichofikiwa ni kizuri basi tutakuwa tunatengeneza mazoea mapya kabisa. Kwamba, tutaruhusu watawala watumie mifumo mibaya kwa kisingizio cha kuishia kwenye mazuri. Kwenye demokrasia na kwenye nchi inayojaribu kujenga utawala wa sheria njia mbaya haziwezi kuruhusiwa kutumika kufikia malengo mazuri. Ili kufikia malengo mazuri tunayoyataka ni lazima tuweke mchakato ambao unakubalika, ni wa wazi na ambao unakubaliana na Katiba au sheria zilizopo.

SWALI: Umekuwa ukisema kuwa mchakato huu – japo umezaa kitu kizuri – lakini ni haramu. Kwanini unasema mchakato huu wa kuandika Katiba Mpya ni haramu?

JIBU: Hapa itabidi niende kwa kina kidogo kwani baadhi ya mambo nitakayoyasema nilishaandika hapa na kuyaandika mara tu mchakato huu ulipotangazwa na Rais Kikwete mwishoni mwa mwaka 2010. Kwanza ni vizuri kutofautisha kufanyia marekebisho Katiba iliyopo na Kuandika Katiba Mpya. Kufanyia marekebisho Katiba iliyopo ni jambo ambalo limewekewa taratibu katika Katiba. Lengo la kufanya marekebisho ni kujaribu kuingiza au kuondoa vipengele fulani fulani kwenye Katiba bila kulazimika kuandika Katiba Mpya.

Mchakato wa kufanya marekebisho ndio ambao umekuwa ukitumika kufanyia marekebisho Katiba yetu tangu 1977. Tangu 1977 hadi hivi sasa kumekuwepo na marekebisho ya vipengele mbalimbali vya Katiba huku vingine vikibadili hata mfumo wa utawala. Marekebisho ya mwisho ya Katiba ya sasa ni yale ya 2005 ambapo pamoja na mambo mengine yalimuingiza Waziri Mkuu kama mtu wa tatu kukaimu kiti cha Urais na kumuondoa Spika wa Bunge kama ilivyokuwa huko awali.

Ibara ya 98 ya Katiba yetu ya sasa inaanza kwa kusema hivi;
Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii kwa kufuata Kanuni zifuatazo:-

Kwamba, kanuni zitakazoelezwa chini zinahusiana na kufanya mabadiliko ‘yoyote' ya Katiba hii ya sasa. Sasa kanuni hizo ambazo zimekuwa zikitumika hadi hivi sasa kufanyia marekebisho vifungu mbalimbali vya Katiba ya sasa ni hizi:

1. Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Katiba ni lazima uungwe mkono na theluthi mbili (2/3) ya Wabunge wote. Hii ni kwa maswala yote yaliyoko kwenye orodha ya kwanza kwenye nyongeza ya pili ya Katiba. Baadhi ya mambo hayo ni: Sheria ya kuthibitisha Tanganyika ni Jamhuri, Sheria ya Utumishi wa Mahakama, Sheria ya Utumishi Serikalini, Sheria ya Uraia, na Sheria ya Mapatano ya Muungano.

2. Muswada wa mabadiliko ya Katiba ambayo yatagusa mambo yaliyoko kwenye orodha ya pili ya nyongeza ya pili ya Katiba ni lazima uungwe mkono na theluthi mbili ya Wabunge wa Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge wa Zanzibar. Mambo yaliyoko kwenye orodha ya pili ni yale yanayojulikana kama "mambo ya Muungano". Haiwezekani kubadilisha mambo ya Muungano bila theluthi mbili ya Wawakilishi wa wananchi kila upande wa Muungano kuridhia.

Sasa Katiba hii inaelezea kama sehemu ya ufafanuzi kuwa kanuni hizo hapo juu zinahusika hata katika kufanyia marekebisho masharti haya.

Kimsingi utaona kuwa Katiba ya sasa haina kifungu kinachoweka utaratibu wa kuiweka pembeni Katiba hii na kuandika Katiba nyingine. Kwa hiyo uharamu wa mchakato huu unaanzia hapa.

SWALI: Hapa sijaelewa; una maana kwamba Katiba ya sasa inaweza tu kufanyiwa vipengele vyake kwa utaratibu huo lakini haiwezi kufutwa na kuandikwa Katiba nyingine?

JIBU: Naam! Siyo Rais Kikwete, wala Tume ya Warioba walio na mamlaka ya kuanzisha au kusimamia mchakato wa Katiba nyingine wakati Katiba ya sasa ipo na inafanya kazi na haijasimamishwa (suspension). Kikwete na viongozi wengine wanakiri kuwa Katiba ya sasa ni halali na inafanya kazi. Sasa kama ni halali na inafanya kazi basi ni lazima izingatiwe.

Rais Kikwete alijipa madaraka ambayo hana; kutangaza kwa taifa kuwa ataanzisha mchakato wa kuandika upya Katiba. Tena ingekuwa ni nchi ambayo inajua kweli nguvu ya Katiba Kikwete alitakiwa aondolewe madarakani kwa mujibu wa Ibara ya 46A(2b) ambacho kinasema Bunge linaweza kumshtaki Rais kwa sababu kadhaa ya kwanza kati ya hizo ni "ametenda vitendo ambavyo kwa jumla vinaivunja Katiba au Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma"

Ninaamini Rais Kikwete kwa kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya – japo kwa nia njema kabisa – amevunja Katiba ya sasa kwani hana madaraka ya kufanya hivyo.

SWALI: Lakini Kikwete ndiyo Rais anaweza kufanya hivyo; maana kama yeye hawezi kufanya hivyo nani anaweza?

JIBU: Mojawapo ya mambo ambayo yananishangaza sana ni imani kuwa Rais anaweza kufanya lolote, popote, kwa lolote na yeyote. Kwamba kwa vile yeye ni Rais basi anaweza kufanya jambo lolote bila kuulizwa na yeyote. Nakumbuka wakati mmoja Rais Kikwete akizungumza na wabunge Dodoma alisema katika hotuba yake kuwa alikuwa na madaraka makubwa kiasi kwamba anaweza kuagiza Dr. Slaa akamatwe "na akakamatwa". Baadhi ya watu – kama siyo wengi – walikubali pendekezo hilo la Rais. Naamini nilikuwa peke yangu kupinga hadharani kuwa Rais hana mamlaka hayo. Nilisema wakati ule – kwenye gazeti hili hili – kuwa Rais ana madaraka yale tu ambayo Katiba imempa; hana madaraka nje ya Katiba na Sheria. Hawezi kukurupuka asubuhi na kuagiza polisi waende kumkamata muuza mafenesi sokoni ati kwa vile kaoteshwa kuwa muuza mafenesi huyo hampendi!

Unaweza kuuliza wanasheria wakuambie Rais Kikwete alipata wapi madaraka ya kuanzisha mchakato mpya wa Katiba uone watakavyohangaika kuhalalisha uharamu wa mchakato huu!

SWALI: Ni hilo tu linalofanya mchakato huu kuwa haramu?

JIBU: Hapana, kutokana na hilo hapo juu kuna tatizo jingine la msingi sana. Rais Kikwete na wabunge waliopitisha sheria ya kuanzisha mchakato huu waliapa mbele ya umma kuwa "watailinda, kuitetea, na kuihifadhi Katiba ya Jamhuri ya Muungano". Maneno haya kwa baadhi ya watu wanayatamka kama mazoea tu bila kuelewa maana yake. Kiapo ni kitu ambacho kinamfunga mtu aliyekula kukitimiza. Watu hawali viapo ili wapate au kuingia madarakani bali wanakula viapo wakimaanisha kuwa wanavitimiza.

Rais na Wabunge wote walikula kiapo cha kuwa watetezi wa Katiba na walinzi wake. Sasa Katiba inapovunjwa au kuonekana kuvunjwa nani anaweza kuitetea? Mimi sijala kiapo cha kuilinda, kuitetea au kuihifadhi Katiba wao ndio wamekula; kwanini hawaitetei na badala yake wanashikiri kwenye mchakato huu haramu? Kwa hiyo uharamu wa mchakato na rasimu iliyotolewa pia unatokana na ukweli kuwa walioapa kuilinda hii Katiba ambao wengi waliishika mikononi mwao kwa furaha hawasimami kuilinda lakini kwa ajabu kabisa wakapiga kura kukubali sheria ya "mapitio ya Katiba" ambayo ilikuwa na lengo la kuifuta Katiba ya sasa na kuleta Katiba Mpya!

SWALI: Sasa, watu wengine watasema Mwanakijiji umeshachelewa meli imeshaondoka bandarini; mchakato umeiva, rasimu imepatikana na watu wanajiandaa kutoa maoni kwenye mabaraza ya Katiba. Kujaribu kurudi nyuma haiwezekani. Utasemaje?

JIBU: Ukweli haugeuki uongo kwa sababu watu wengi wanaupinga; na uongo hauwi ukweli kwa sababu watu wengi wanauunga mkono. Mchakato wa kuandika Katiba ambao unasimamiwa na Tume ya Warioba na baadaya Bunge la Katiba haupati uhalali wake kwa sababu unaungwa mkono na watu wengi. Kama kuunga mkono kunatoa uhalali basi kusingekuwa na haja ya kuwa na Katiba ya sasa!

Lengo langu ni kuonesha tu kuwa wale wanaoishiriki mchakato huu kwa kiwango chochote kile wanashiriki kwenye kitu haramu na kuwa huko mbeleni wakija watu ambao watataka kuandika Katiba Mpya kwa mchakato halali watakuwa na haki kabisa ya kufanya hivyo. Lengo likiwa ni kusahihisha makosa haya ambayo tumeyaona. Kama hawa sasa hivi wamejipa madaraka ya kuandika Katiba upya miaka si mingi ijayo watakuja Watanzania wengine ambao watataka kuandika Upya katiba. Tutawakatalia?

SWALI: Umesema kwa kirefu juu ya kukiukwa kwa Katiba ya sasa; je kama Katiba ya sasa ingefuatwa na mswada wa sheria ungeendelea kuwa kama ulivyo mchakato ungekuwa halali?

JIBU: Bado ungekosa uhalali kutokana na sheria yenyewe ilivyoandikwa. Ikumbukwe kuwa watu wanaandika Katiba Mpya kwa sababu moja kubwa tu – kuanza kwa taifa jipya. Taifa ambalo tayari limekuwepo na ambalo tayari lina Katiba yake haliamui kuandika Katiba yake upya kwa sababu tu wameona ni kazi kufanyia marekebisho vipengele vilivyopo.

Hata hivyo, wakati mwingine mataifa yanalazimika kuandika upya kabisa katiba yao kwa sababu nyingine kubwa yaani kukidhi mahitaji ya wananchi na jamii husika. Sasa, inapotokea kuwa Taifa linaamua kuandika upya Katiba yake ni lazima Ukuu wa Wananchi (supremacy of the people) uongoze mchakato huo. Sasa, katika kufanya hivyo wananchi hawapaswi kuzuiwa kuzungumzia nchi yao au taifa lao.

Hiki ndicho kilichofanyika katika mchakato huu. Rais Kikwete alituambia mapema tu kuwa mchakato wa Katiba Mpya hautaruhusu mambo fulani kuzungumzwa na wananchi – yaani wenye nchi. Yaani ni sawasawa na CEO wa kampuni alete ajenda kwa wana hisa halafu awaambie wana hisa kuwa hawapaswi kuzungumzia mambo yanayohusiana na kampuni – uendeshaji wake, uwepo wake, au faida na hasara zinazopatikana.

Sheria waliyoipitisha ambayo iliwapa wananchi kiinimacho kuwa wanaandika Katiba Mpya iliweka wazi kuwa mambo kadha wa kadha hawaruhusiwi kuzungumza au kuyajadili. Na kama wanataka kuyajadili basi wajadili kwa vipi. Sasa nani aliwapa madaraka ya kuwakataza wananchi kuzungumzia mambo yanayowahusu wao kama wananchi?

Hapo juu nimeonesha kuwa Ibara ya 98 imeweka utaratibu wa jinsi ambavyo mambo ya Muungano yanavyoweza kubadilishwa. Kwamba Zanzibar hawawezi kubadilisha mambo ya Muungano wenyewe na Bunge la Muungano haliwezi kubadili mambo ya Muungano bila kuhusisha Zanzibar. Sasa kama hili ni kweli na liko kwenye Katiba; hawa wenzetu kuamua mambo fulani yasizungumzwe na wananchi madaraka hayo wanayapata wapi?

SWALI: Lakini Mwanakijiji wapo watu ambao wataona kuwa unajifanya unajua sana na unawapotosha wananchi na kuwa kupinga rasmi hii ni kukosa uzalendo na dalili ya kutoitakia Tanzania mema?

JIBU: Mimi ni miongoni mwa watu ambao tunaamini kuwa uzalendo siyo kukubaliana na upuuzi unaofanywa kwa jina la nchi au kwa migongo ya wananchi. Kwamba, kwa vile aliyefanya jambo fulani ni Rais au kiongozi wan chi basi wananchi tunatakiwa tuunge mkono ni nadharia inayotokana na uzalendo uliopotoka.

Nakumbuka wakati wa sakata la "Mapanki" ambalo liliwafanya watu wakubaliane na Rais Kikwete hadi kuliingiza Bunge kutoa tamko la kumuunga mkono sisi wengine tulisimama upande wa ukweli. Tulikataa kuutetea uongo kwa sababu unafanywa kwa jina la nchi. Wakati mwingine uzalendo ni pamoja na kupinga mambo ambayo yanatishia utawala wa demokrasia au yanaonekana kuvunja Katiba hata kama yanafanywa kwa jina la wananchi au "kwa nia njema".

Mchakato huu wa Katiba ni haramu; hoja ni hiyo. Mwanakijiji siyo hoja kwani hoja hujibiwa kwa hoja siyo viroja. Kwamba mchakato umeanzishwa kinyume na Katiba ya sasa sio maoni yangu ni ukweli usiopingika; kwamba Rais hana madaraka ya kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba mpya kwa matakwa yake tu siyo maoni yangu ni ukweli; Kwamba mchakato mzima umetengezwa ili kuhakikisha CCM inajaza wanachama na mashabiki wake ni ukweli nao sio maoni yangu; kwamba mwisho wa siku Katiba Mpya italetwa kwetu "kwa hisani ya wana CCM" ni ukweli usiopingika vile vile.

SWALI: Sasa unasema nini kuhusu wapinzani ambao wameonekana kuikubali; miongoni mwao ni CHADEMA. Si mambo ambayo wapinzani walikuwa wanayalilia kwa muda mrefu yameingizwa kwenye rasimu huoni hilo ni jambo zuri na wapinzani washukuru?

JIBU: Kwani nani alisema tunataka katiba mpya ya Upinzani? Kwani tulipokuwa tunalilia nafasi ya kuandika Katiba Mpya tulikuwa tunataka Katiba Mpya ya CHADEMA? Katiba Mpya siyo ya chama au itikadi fulani ya watu; inatakiwa kuwa Katiba ya nchi inayotokana na wenye nchi – Wananchi. Siyo Katiba ya kikundi cha wasomi waliobobea au ya wanaharakati wa haki za binadamu; la hasha ni Katiba ya wananchi wa Tanzania. Sasa kama wapinzani wanafurahia kuwa rasimu hii imesikiliza maoni yao na wao wanafurahia inashangaza.

Hivi, hawajui kuwa mchakato huu utakapoenda kwenye mabaraza ya Katiba (ambayo yamejaa wana CCM) na badala kwenye Bunge la Katiba ambalo limenaa karibu theluthi mbili wana CCM rasimu hii haitakuwa ilivyo sasa? Kwamba CCM itachukua msimamo ambao utahakikisha kuwa Katiba inaendana na maoni yake na hivyo mwisho wa siku wao ndio wataamua nini kilichomo. Na kwa vile kupitisha katiba kunahitaji asilimia 50 ya wapiga kura ya maoni CCM haitakuwa na kazi ngumu. Sasa tusije kushangaa hawa hawa ndugu zangu wapinzani wanaoshabikia rasimu hii wakageuka na kuanza kulalamika mbeleni.

Hawatakuwa na haki ya kufanya hivyo; kwa kukubali uhalali wa mchakato huu na kushindwa kujitoa mapema wapinzani wanajifunga kukubali matokeo yake. Nitawashangaa wakija mbeleni na kuanza kulalamika mambo yakianza kwenda kombo. Nitawauliza kama nilivyowauliza huko nyuma – kwani hawakujua?

SWALI: Sasa unasemaje kama neno la mwisho katika hili?

JIBU: Niseme kwamba ni kweli meli imeshaondoka bandarini. Wananchi wa Tanzania wawe tayari kuletewa Katiba Mpya ambayo dalili zote zinaonesha kuwa itatoka kwa kikundi cha wasomi na watu wachache. Wakae wakijua kuwa malalamiko juu ya Katiba hiyo mpya yatakuja tena na miaka michache huko mbeleni tutalazimika kuandika Katiba mpya ya wananchi na labda tutafanyahivyo baada ya kuuvunja huu muungano ambao mchakato huu umeanza kuuvunja.

Niandikie: mwanakijiji@jamiiforums.com
Nitafute Facebook: "Mzee Mwanakijiji"
Twitter: "Mwanakijiji"
 
Mkuu ngoja kwanza ipite walau hii,ccm wakishapotea ktk duru za siasa itatengenezwa katiba ya wananchi ya tanganyika!
 
mkuu Mzee Mwanakijiji nitatofautiana na wewe kwenye maeneo kadhaa.La kwanza ni hili
mchakato haramu matokeo haramu! Kwamba mchakato umetoa “rasimu nzuri” haibadilishi ukweli kuwa ni mchakato haramu. Baadhi ya watu ambao walikuwa na tatizo na mchakato huu sasa hivi –baada ya kusoma rasimu – wamekubali kuwa ni rasimu nzuri na hivyo hawana tena tatizo na mchakato! Hii inashangaza.
Sio lazma kwa kila mchakato haramu uzae matunda haramu.Hii nadharia sio universaly applied na ukiitumia kama nadharia ya jumla; wakati fulani itakupa hitimisho lenye makosa.Kwa mfano;Tuchukulie wote tuna lengo la kujenga barabara ya Fly Over Tanzara, lengo ni kupunguza msongamano.Tukakubaliana kuwa watahusika watu 50 kujenga.Hatimae kwenye purukushani (kihalali au kiharamu) watu 10 hawakushiriki, lakini hatimae tukajikuta tuna Fly over za uhakika pale TAZARA ambapo wote tunakubaliana kuwa ni za ukweli; je? tutasema kilichopatikana ni haramu kwa kuwa ujenzi ulijenga na watu tofauti na hivyo kupinga uwepo wake; au kwanza tunasherehekea kutatua tatizo la msingi halafu baadae ndo tuseme lakini.......!. Katika mazingira ya dharura, ni sahihi kufanya kitu haramu kwa ajili ya kuleta matunda mema.Kwa mfano kuua mtu ni haramu lakini kama unaendesha gari lenye abiria sabini, halafu akatokea mmoja akaingia barabarani , na ukagundua ukimkwepa utaua wengi zaidi ni bora kumuua.Kwa hiyo hii nadharia ya mchakato haramu=Matunda haramu sio nadharia ya jumla.

Tukikubali kuwa tunaweza kutumia njia (means) mbaya kufikia lengo zuri (ends) na hivyo kwa vile kilichofikiwa ni kizuri basi tutakuwa tunatengeneza mazoea mapya kabisa.
Mkuu kwa hapa si suala la mazoea; ni suala la dharura.Ikumbukwe kuwa miongoni mwa udhaifu wa katiba tuliyonayo ni kutoonesha jinsi tunavyoweza kupata katiba mpya.kwa hiyo kwa kuwa tayari tulikuwa na tatizo (kama ajali) pasi tulichotakiwa kuangalia ni "The way foward".

.

Kimsingi utaona kuwa Katiba ya sasa haina kifungu kinachoweka utaratibu wa kuiweka pembeni Katiba hii na kuandika Katiba nyingine. Kwa hiyo uharamu wa mchakato huu unaanzia hapa.
Hii ni kama ajali;Wewe hapa ungeshauri kwamba tungeanza je(maana napo palikuwa na mjadala mkali).Hata hivyo kwa kuwa sasa tuko kwenye hatua nyengine, Ingekuwa vyema kama tungetazama mbele badala ya kutzama nyuma.

JIBU: Naam! Siyo Rais Kikwete, wala Tume ya Warioba walio na mamlaka ya kuanzisha au kusimamia mchakato wa Katiba nyingine wakati Katiba ya sasa ipo na inafanya kazi na haijasimamishwa (suspension). Kikwete na viongozi wengine wanakiri kuwa Katiba ya sasa ni halali na inafanya kazi. Sasa kama ni halali na inafanya kazi basi ni lazima izingatiwe.
Kwa hiyo wewe kwa maoni yako ungeshauri nani aanzishe operesheni okoa jahazi?
Ninaamini Rais Kikwete kwa kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya – japo kwa nia njema kabisa – amevunja Katiba ya sasa kwani hana madaraka ya kufanya hivyo.
Mkuu nikupe mfano; Katika taasisi zote rasmi,Kila mfanya kazi hupewa mkataba na majukumu yake ya kazi.Jaalia ndio sasa wote mmefika ofisini,ofisi imefunga; mmoja anajua funguo ilipo, anaweza kuichukua na kufungua watu wote wakaingia lakini "Job Description" yake haimuoneshi kama kufungua ofisi ni kazi yake.Je! anatakiwa achukue funguo popote pale afungue watu waingie ili sasa waweze kuweka utaratibu mzuri kwamba kwa siku zijazo ni nani atakuwa na jukumu la kufunga na kufungua; au anatakiwa aache wote waendelee kukaa nje na kwa kukaa nje mwishowe hakutakuwa na mazingira mazuri ya kupanga nani afungue?

Wananchi wa Tanzania wawe tayari kuletewa Katiba Mpya ambayo dalili zote zinaonesha kuwa itatoka kwa kikundi cha wasomi na watu wachache.
Mkuu; mwisho wa siku lazma kitu makini kama Katiba ni lazma itengenezwe na wasomi.Watu wote watatoa maoni ila mwisho wa siku watakaochuja ni wasomi.Hakuna njia zaidi ya hiyo.Nakumbuka Kwenye mjadala mmoja juu ya katiba mpya kuna mama mmoja Alisema serikali inataka kubomoa nyumba yake iliyopo penbezoni mwa bara bara ya morogoro.Akataka katiba mpya izuilie nyumba yake isibomolewe.Hapa unadhani jambo kama hili unaliweka je katika katiba bila kuwapa kazi hii wasomi wachambue?
 
Last edited by a moderator:
MWANAKIjiji
huna lolote mfia dini una ajenda zako za siri na huta fanikiwa,rasimu hiyo ni maoni ya wananchi.Tatizo unajiona una akili za kipekee kuliko wote waliotoa maoni.Hiyo ni dalili ya ujivuni.Mchakato unaendelea na punde tutapata katiba tuitakayo.
 
Last edited by a moderator:
Kwa watu wliomfahamu vyema "mwenye heri" Nyerere, hawawezi kuikubali hii rasimu abadan. Hii rasimu kwa kiasi kikubwa itavunja vunja azma ya moyoni ya nyerere. wachache watanielewa!!!
 
Kama ni uharamu basi muungano wenyewe ndio haramu,zanzibr kwanza.
 
Kuna mambo ya msingi ambayo hata mimi yalinifanya na yananifanya kuona uharamu NA UBATILI wa huu mchakato na tunda lake. Na ndio maana kwenye hili tunashabihiana na MMM na wadau wengine ingawa hatuko wengi.

1) Udhaifu na makosa (yameshajadiliwa mno humu sina haja kurejea) ya sheria iliyounda mchakato huu,
2) Hadidu za rejea (hasa makatazo)
3) "Owner" wake kuwa ni Rais badala ya WANANCHI.

Get real folks; hiki kiini macho kikifika kwenye mabaraza na hatimaye bungeni hakitakuwa hivi! Hapo mmeonjeshwa ndimu iliyopakwa asali kwa juu.....shubiri inafuatia.
 
Wazanzi ari nao hawakupaswa kuukubali mchakato huu. Kwa kuukubali ni lazima wawe tayari kuishi na matokeo yake.
 
Mwanakijiji unaanza kuchuja hizi hoja zimechuja vinginevyo uwe na jambo lingine lakini kwa hoja hizi hauko sawa wala hupaswi kusifiwa.
 
Kinachonishangaza ni kupitisha katiba ya Muungano wakati hatuna katiba ya Tanganyika! Zanzibar wanayo ya kwao waliyoipitisha wenyewe. Ya bara iko wapi? Ndio hizi mbili zitoe ya Muungano? Hapa kwa kweli sijui kama tunaenda sawa.
 
Kwa watu wliomfahamu vyema "mwenye heri" Nyerere, hawawezi kuikubali hii rasimu abadan. Hii rasimu kwa kiasi kikubwa itavunja vunja azma ya moyoni ya nyerere. wachache watanielewa!!!

hatuna ujinga kiasi hicho, yaani tusitumie akili zetu badala yake tuendelee kutumia akili za nyerere, huo ni upumbavu, na wala si ujinga.
 
Mzee mwanakiji nisaidie hata fikra tu manake naona najikosea mimi na familia yangu kushuhudia ujinga mkubwa namna hii kufanyika katika zama hizi tena mbele ya madokta na maprofessor kibao,

wakati wanasoma kuupata udokta na uprofessor mara zote wamemkejeli chief Mangungo, sijui sijui wamelaaniwa na warugaruga kwa kejeli zao.

Mimi siafiki tena sikubali kabisa vyama vishiriki kuandika katiba, kwa kuwa vimeshapewa upper hand NALIPINGAJE HILI LIKATIBA LAOOOOOO!
 
Last edited by a moderator:
mkuu Mzee Mwanakijiji nitatofautiana na wewe kwenye maeneo kadhaa.La kwanza ni hili
Sio lazma kwa kila mchakato haramu uzae matunda haramu.Hii nadharia sio universaly applied na ukiitumia kama nadharia ya jumla; wakati fulani itakupa hitimisho lenye makosa.Kwa mfano;Tuchukulie wote tuna lengo la kujenga barabara ya Fly Over Tanzara, lengo ni kupunguza msongamano.Tukakubaliana kuwa watahusika watu 50 kujenga.Hatimae kwenye purukushani (kihalali au kiharamu) watu 10 hawakushiriki, lakini hatimae tukajikuta tuna Fly over za uhakika pale TAZARA ambapo wote tunakubaliana kuwa ni za ukweli; je? tutasema kilichopatikana ni haramu kwa kuwa ujenzi ulijenga na watu tofauti na hivyo kupinga uwepo wake; au kwanza tunasherehekea kutatua tatizo la msingi halafu baadae ndo tuseme lakini.......!. Katika mazingira ya dharura, ni sahihi kufanya kitu haramu kwa ajili ya kuleta matunda mema.Kwa mfano kuua mtu ni haramu lakini kama unaendesha gari lenye abiria sabini, halafu akatokea mmoja akaingia barabarani , na ukagundua ukimkwepa utaua wengi zaidi ni bora kumuua.Kwa hiyo hii nadharia ya mchakato haramu=Matunda haramu sio nadharia ya jumla.

Mkuu kwa hapa si suala la mazoea; ni suala la dharura.Ikumbukwe kuwa miongoni mwa udhaifu wa katiba tuliyonayo ni kutoonesha jinsi tunavyoweza kupata katiba mpya.kwa hiyo kwa kuwa tayari tulikuwa na tatizo (kama ajali) pasi tulichotakiwa kuangalia ni "The way foward".

.

Hii ni kama ajali;Wewe hapa ungeshauri kwamba tungeanza je(maana napo palikuwa na mjadala mkali).Hata hivyo kwa kuwa sasa tuko kwenye hatua nyengine, Ingekuwa vyema kama tungetazama mbele badala ya kutzama nyuma.

Kwa hiyo wewe kwa maoni yako ungeshauri nani aanzishe operesheni okoa jahazi?
Mkuu nikupe mfano; Katika taasisi zote rasmi,Kila mfanya kazi hupewa mkataba na majukumu yake ya kazi.Jaalia ndio sasa wote mmefika ofisini,ofisi imefunga; mmoja anajua funguo ilipo, anaweza kuichukua na kufungua watu wote wakaingia lakini "Job Description" yake haimuoneshi kama kufungua ofisi ni kazi yake.Je! anatakiwa achukue funguo popote pale afungue watu waingie ili sasa waweze kuweka utaratibu mzuri kwamba kwa siku zijazo ni nani atakuwa na jukumu la kufunga na kufungua; au anatakiwa aache wote waendelee kukaa nje na kwa kukaa nje mwishowe hakutakuwa na mazingira mazuri ya kupanga nani afungue?

Mkuu; mwisho wa siku lazma kitu makini kama Katiba ni lazma itengenezwe na wasomi.Watu wote watatoa maoni ila mwisho wa siku watakaochuja ni wasomi.Hakuna njia zaidi ya hiyo.Nakumbuka Kwenye mjadala mmoja juu ya katiba mpya kuna mama mmoja Alisema serikali inataka kubomoa nyumba yake iliyopo penbezoni mwa bara bara ya morogoro.Akataka katiba mpya izuilie nyumba yake isibomolewe.Hapa unadhani jambo kama hili unaliweka je katika katiba bila kuwapa kazi hii wasomi wachambue?

Hivi hii rasimu ikifika kwenye mabaraza ya katiba na hatimae bunge la katiba, na vipengele vingi vikibadilishwa na vingine kuongezwa, utamlaumu nani?
 
4 Reactions
Reply
Back
Top Bottom