Mbunge Chadema rumande

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
VITA ya madaraka ya Umeya na Uenyekiti wa Halmashauri nchini, umezua balaa baada ya jana Mbunge wa Arusha Mjini, Gobless Lema wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kujikuta akiswekwa rumande akidaiwa kuchochea vurugu wakati wa uchaguzi wa
Meya wa Jiji la Arusha.

Lema alikutwa na balaa hilo baada ya kurejea kwenye ukumbi wa Manispaa ambako wanaCCM walikuwa wanaendelea na uchaguzi, baada ya awali Chadema kususa na
kwenda mbali na ukumbi huo.

Kutokana na Chadema kususa uchaguzi huo, madiwani wa CCM na TLP waliendelea na
uchaguzi na kumchagua diwani wa Kata ya Olerien, Gaudence Lyimo kuwa Meya wa Jiji la
Arusha wakati nafasi ya Naibu Meya ikienda kwa Diwani wa kata ya Sokoni One, Michael
Kivuyo wa TLP aliyeshinda baada ya pinzani wake, Julius Ole Sekeyani wa CCM kujiengua
katika dakika za mwisho kabla ya uchaguzi.

Kabla ya uchaguzi wa jana, awali uchaguzi huo uliokuwa ufanyike juzi uliwekwa kiporo
baada ya madiwani wa Chadema kususa kupiga kura kwa madai ya kuwa mbunge wa viti
maalumu wa mkoa wa Tanga, Mary Chatanda hapaswi kupiga kura ya kumchagua Meya wa
Jiji hilo.

Mbali ya madai hayo, madiwani wa Chadema pia walimtaka Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la
Arusha, Estomy Changah kumruhusu kwa maandishi diwani wa viti maalumu wa TLP,
Mwanvua Mwahanza kuruhusiwa kupiga kura katika uchaguzi huo baada ya kupata baraka za
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Thobias Andengenye alithibitisha kutokea kwa tukio
hilo la kukamatwa kwa Mbunge huyo na kusema alikuwa anashikiliwa katika Kituo Kikuu
cha Polisi mjini hapa.

Hata hivyo, habari ambazo baadaye zilizifikia gazeti hili zinasema kwamba, Lema aliachiwa
kwa dhamana na kwamba alipokelewa kwa maandamano na umati wa wafuasi wake waliokuwa wamekizingira kituo hicho.

Juhudi za kumpata Lema kuzungumzia tukio hilo hazikuzaa matunda, kwani kila alipotafutwa kwa simu yake ya mkononi iliita bila ya kupokewa.

Lakini mapema asubuhi, diwani wa Elerai, John Bayo akizungumza kwa niaba ya madiwani
wa Chadema, alisema walikubaliana kutoingia kupiga kura hadi sharti lao la kuondolewa
kwa Chatanda litakapotekelezwa.

Alisema kwamba, juzi waliingia katika mkutano huo na kuapishwa, lakini walikataa kujiandikisha katika rejesta ya madiwani baada ya kuelezwa kuwa Mkurugenzi wa Jiji na
madiwani wa Chama Cha Mapinduzi wanataka kumwingiza Chatanda kupiga kura.

Aliendelea kusema kuwa baada ya kugomea hilo, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji Changah
aliamuru kutolewa kwa sanduku la kupiga kura ndipo madiwani wa Chadema
walipolitupa nje sanduku hilo na kupiga ‘’kelele’’ za kutaka Chatanda atoke nje ya ukumbi.

Akizungumzia suala hilo, Changah alisema kuwa Chatanda anaruhusiwa kushiriki uchaguzi
huo, kwani ni mjumbe halali wa mkutano huo kwa sababu ni mkazi wa Jiji la Arusha.

Alisema kuwa Mbunge wa Tanga Viti Maalumu si sababu ya msingi ya kumzuia yeye kupiga kura katika jiji la Arusha, akidai sheria haisemi hivyo na aliwataka madiwani wa Chadema
kutafsiri sheria na kanuni vizuri.

Jana jioni, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa akizungumzia suala hilo kwa njia ya simu alielezea kusikitishwa kwake na taarifa zinazodai kuwa, polisi wamempiga na kumjeruhi Mbunge wa Chadema, Lema kisha kumweka mahabusu badala ya kumpeleka hospitalini kutibiwa majeraha yaliyotokana na kipigo hicho.

Dk. Slaa analaani kitendo hicho kwa kuwa kinakiuka haki za binadamu na kurudisha nyuma
jitihada za Watanzania za kujenga mfumo wa demokrasia.
 
Back
Top Bottom