Elections 2010 Mbio za urais za Bilal zaanzia Ikulu Dar

Zak Malang

JF-Expert Member
Dec 30, 2008
5,404
234
Mbio za urais za Bilal zaanzia Ikulu Dar


Na Patricia Kimelemeta,
Mwananchi


WAZIRI kiongozi wa zamani wa Zanzibar, Dk Mohammed Ghalib Bilal ameweka bayana nia yake ya kuwania tena kiti cha urais wa visiwani hivyo kwenye uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Bilal, ambaye alizua kizaazaa mwaka 2005 wakati alipochukua fomu ya kuwania urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM na kuonekana anapingana na utamaduni wa chama hicho wa kumuachia rais amalizie kipindi cha miaka 10, anaonekana alikuwa ni nia ya dhati ya kuwa rais wa saba wa visiwa hivyo miaka mitano iliyopita.

Wakati huo, rais wa sasa, Amani Abeid Karume ndio kwanza alikuwa amemaliza miaka mitano ya awamu yake ya kwanza, lakini mtoto huyo wa rais wa kwanza wa Zanzibar amemaliza muda wake na tayari homa ya mrithi wake imeshakuwa kubwa.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Mwananchi juzi kwenye hafla ya maadhimisho ya miaka 46 ya Muungano wa Tanzania Bara na Zanzibar, Ikulu jijini Da es Salaam, Dk Bilal alisema pamoja na kuwa na nia hiyo, anasubiri kupata ridhaa ya wananchi wa Zanzibar.

Alisema anatambua kuwa muda wa kutangaza kuwania nafasi hiyo haujafika, lakini aliamua tu kudokeza nia hiyo.

“Nasubiri tamko kutoka kwa wananchi wangu ambao wameonyesha nia ya kunitaka niwanie kiti hicho, hivyo basi usiwe na haraka sana juu ya jambo hilo kwa sababu muda bado kidogo sana toka sasa, na muda ukifika nitatangaza na utajua yote hayo,” alisema Bilal, ambaye kwa sasa ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma.

Alisema wananchi ndio wenye uamuzi wa mwisho juu ya kuwania kiti hicho kwa sababu wanahitaji kiongozi anayefaa, kwa ajili ya maendeleo yao na taifa kwa ujumla na kwamba ni imani yake kuwa uamuzi wao ndio utakaowasaidia kupata kiongozi bora.

Kwa mujibu wa Dk Bilal, wanachohitaji wananchi wa Zanzibar kwa sasa ni maendeleo na hivyo uamuzi wao utakuwa sahihi iwapo watamchagua kiongozi wanayeona anaweza kuwaletea maendeleo kwa kura yao aliyosema ni ya thamani.

Bilal, ambaye aliwahi kuwa katibu mkuu Wizara ya Sayansi na Teknolojia wakati wa Benjamin Mkapa akiongoza wizara hiyo kabla ya kwenda kuwa Waziri Kiongozi, amekuwa akitumiwa na CCM kwenye mambo kadhaa ya kitaalamu na hivi karibuni aliongoza kamati iliyopewa jukumu la kukusanya maoni ya jinsi ya kuwa na mfumo bora wa kupata viongozi kuanzia ndani ya CCM.

Kwa sasa Bilal ni mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dodoma ambako pia anafundisha fizikia.

Wakati huohuo, Makongoro Nyerere, mtoto wa Baba wa Taifa, amesema kuna uwezekano mdogo kwa vyama vya upinzani kuchukua madaraka kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Makongoro alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam akilinganisha hali ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita na kipindi cha sasa ambacho kimeshuhudia waliogombea urais wakihamishia nguvu zao kwenye kuwania ubunge.

Alisema vyama vya upinzani vimepoteza mwelekeo na kusababisha kupoteza hali ya kukubalika kwa wananchi na hivyo wapinzani wanahitaji nguvu za ziada ili waweze kukabiliana na CCM katika uchaguzi uliopangwa kufanyika Oktoba 31.

“Upinzani siku hizi hakuna, ndio maana baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa wanaamua kukimbilia kwenye majimbo kwa ajili ya kuongeza nguvu. Hata hivyo, wanahitaji nguvu sana ili waweze kufanikiwa kwa sababu CCM imejipanga sana kwenye maeneo yake,” alisema Makongoro, ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Arusha Mjini kwa tiketi ya NCCR Mageuzi kabla ya kurejea CCM.

Aliongeza CCM ina mtandao nchi nzima, jambo ambalo limesaidia kutambulika na kuweka nguzo imara kwenye maeneo yake.

Alisema kwa hali hiyo wanaotaka kushindana nayo lazima wajipange kikamilifu ili waweze kufanikiwa, vinginevyo hawatapata mwanya kutamba kisiasa.

Alivisihi vyama vya siasa kupendana na kutafuta mbinu za kuwasaidia kuleta upinzani wa kweli kwa wananchi ili kuhakikisha kuwa wanakusanya nguvu ambayo itaweza kukiong’oa chama tawala.
Kwa mujibu wa Makongoro, bila ya upinzani wa kweli wataishia kupiga kelele.

Naye Jaji Joseph Sinde Warioba amewataka wananchi kushiriki uchaguzi mkuu ujao kwa amani na utulivu ili waweze kupata viongozi bora ambao wataleta maendeleo.

Alisema wananchi wanapaswa kuwa makini katika kipindi cha kuelekea uchaguzi kwa kuangalia ni kiongozi gani anayeweza kuwapa maendeleo, ndipo wafanye uamuzi wa kumchagua.

“Nawatakia wananchi uchaguzi wa amani na utulivu, vurugu si nzuri kwa sababu zinaweza kuhatarisha amani ya nchi na kusababisha maafa. Hivyo ninawaomba wawe makini hasa katika kipindi cha uchaguzi kwa kumchagua kiongozi mnayeona anafaa kwa maendeleo yenu na taifa kwa ujumla,” alisema Warioba.
 
Huyu alionekana tangu mapema sana...Anyway namsifu kwamba yuko bold, na hataki kusemea mambo yake kichinichini wala kwa fitna!..
Nadhani nia ya ke kuu ni kutawala Jamkhuri ya Muungano wa TZ!
 
Kila la kheri.Afadhali huyu anayetumia haki yake ya demokrasia bila kutuletea mizengwe au kelele. Kama mtu anaona anafaa kuongoza basi akachukue fomu agombanie kama anavyotaka kufanya Dr Bilali.
 
Back
Top Bottom