Sema Tanzania
JF-Expert Member
- May 18, 2016
- 251
- 465
Ukatili wa kingono unaofanywa dhidi ya watoto bado ni tatizo kubwa hapa nchini. Hii ni kutokana na ukweli kwamba tatizo hili hujitokeza katika sura tofauti na kwa nyakati zisizotarajiwa. Jambo la kusikitisha zaidi ni kuwa idadi kubwa ya watoto wanaoathiriwa na vitendo hivi hukosa ujasiri wa kuzungumza wazi juu ya masuala haya na huenda jambo hili ndiyo hasa husababisha uwepo wa ufinyu wa takwimu mahsusi zinazohusu matukio ya kikatili wanayokumbana nayo watoto.
Utafiti uliofanywa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) kupitia vyombo vya habari kuanzia Januari mpaka Juni mwaka 2019 ulionyesha kuwa asilimia 66 ya matukio ya ukatili dhidi ya watoto yalikuwa ni ya kingono, hasa ubakaji na ulawiti. Wahanga wengi walikuwa ni watoto wa shule za msingi wenye miaka kati ya 7 hadi 14. Takwimu hizi zinaiwashia taa nyekundu jamii kwa kuikumbusha kwamba inahitaji kufanya jambo ili kukomesha ukatili kwani huenda hali ikawa mbaya zaidi huko mbeleni.
Ukatili wa kingono dhidi ya watoto ni jambo la kutisha na kwakuwa mtoto anapofanyiwa kitendo hiki hupitia kipindi kigumu katika maisha yake, sisi kama wazazi, walezi, walimu mashuleni pamoja na watu wote wenye nia thabiti ya kukabiliana na janga hili, hatuna budi kujifunza viashiria vya mtoto aliyefanyiwa kitendo hicho. Kwa hakika, njia hii huweza kutusaidia kumsaidia mtoto anapopatwa na janga hili.
Chuki zisizo na sababu kwa baadhi ya watu, mabadiliko ya tabia yanayoambatana na kujitenga na wenzake, upweke, kufedheheka, kupata mshtuko na uoga usio wa kawaida katika baadhi ya maeneo, vitu ama watu, kujichukia na kukosa ujasiri pindi anapokuwa na watu wengine ni baadhi ya dalili za mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono.
Mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono hupoteza imani na watu. Hujihisi amesalitiwa na jamii pale tu agunduapo kwamba mtu aliyekua akimuamini sana ndiye aliyemuingilia kimwili. Matokeo ya kitendo hicho ndiyo hasa hupelekea mtoto kukosa imani na mtu yeyote. Huwaona wote kama watu wasiofaa, waliojivika ngozi ya Kondoo kumbe ni Mbwa Mwitu.
Kwa minajili hiyo, hatua ya kwanza katika kufanya jitihada za kumuokoa kifikra mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono ni kuirejesha imani yake kwa watu. Hapa, sharti apatikane mtu anayeweza kuyafariji majuto na huzuni ya mtoto ambapo mtoto atajihisi yuko huru kuzungumza nae na kukisikia kilio chake.
Wepesi wa jambo hili utategemea zaidi uharaka wa mtu huyo katika kushughulikia uovu na huzuni ajisikiayo mtoto. Hii si kazi rahisi lakini kwani tulio wengi tusikiapo matukio na simulizi za kusikitisha, muitikio wetu wa awali huhusisha kulaumu na kuhukumu. Tunashindwa kutambua kwamba tunapofanya hivyo, mtoto hujihisi kubebeshwa mzigo wa lawama ulio na hukumu ndani yake na hivyo huona ni bora akaendelea kuitunza yake siri.
Hatupaswi kuzungumza maneno yanayoweza kuleta tafsiri mbaya kwa mtoto na kwamba tunamlaumu. Wakati mwingine hatia anayoihisi mtoto hutokana na fikra kwamba huenda ukatili aliofanyiwa tayari umeharibu maisha yake, jaribu kumuepusha na fikra hizo. Aidha, mdhibitishie kuwa maisha yake hayajaenda kombo kama afikiriavyo, mpe mifano ya watu mashuhuri waliowahi kuwa wahanga wa ukatili wa kingono lakini sasa wana mafanikio makubwa, mifano hiyo huweza kuwa chachu ya kuondoa majuto aliyonayo mtoto, kulirejesha tumaini lake na ujasiri wake.
Hatuna budi kumhakikishia mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji wa kingono kuwa, pamoja na yote yaliyomkumba, yeye ni wa thamani sana na bado ana nafasi ya kufikia ndoto zake. Wajibu wetu ndiyo maisha yake. Tuukatae udhalilishaji wa kingono dhidi ya watoto!
Kwa maoni na ushauri tupigie simu namba 116 ambayo ni maalumu kwa huduma za mtoto nchini. Huduma hii haitozi malipo toka mitandao yote nchini. Vilevile unaweza kutupata kupitia ukurasa wetu wa JamiiForums: Sema Tanzania;
Utafiti uliofanywa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) kupitia vyombo vya habari kuanzia Januari mpaka Juni mwaka 2019 ulionyesha kuwa asilimia 66 ya matukio ya ukatili dhidi ya watoto yalikuwa ni ya kingono, hasa ubakaji na ulawiti. Wahanga wengi walikuwa ni watoto wa shule za msingi wenye miaka kati ya 7 hadi 14. Takwimu hizi zinaiwashia taa nyekundu jamii kwa kuikumbusha kwamba inahitaji kufanya jambo ili kukomesha ukatili kwani huenda hali ikawa mbaya zaidi huko mbeleni.
Ukatili wa kingono dhidi ya watoto ni jambo la kutisha na kwakuwa mtoto anapofanyiwa kitendo hiki hupitia kipindi kigumu katika maisha yake, sisi kama wazazi, walezi, walimu mashuleni pamoja na watu wote wenye nia thabiti ya kukabiliana na janga hili, hatuna budi kujifunza viashiria vya mtoto aliyefanyiwa kitendo hicho. Kwa hakika, njia hii huweza kutusaidia kumsaidia mtoto anapopatwa na janga hili.
Chuki zisizo na sababu kwa baadhi ya watu, mabadiliko ya tabia yanayoambatana na kujitenga na wenzake, upweke, kufedheheka, kupata mshtuko na uoga usio wa kawaida katika baadhi ya maeneo, vitu ama watu, kujichukia na kukosa ujasiri pindi anapokuwa na watu wengine ni baadhi ya dalili za mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono.
Mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono hupoteza imani na watu. Hujihisi amesalitiwa na jamii pale tu agunduapo kwamba mtu aliyekua akimuamini sana ndiye aliyemuingilia kimwili. Matokeo ya kitendo hicho ndiyo hasa hupelekea mtoto kukosa imani na mtu yeyote. Huwaona wote kama watu wasiofaa, waliojivika ngozi ya Kondoo kumbe ni Mbwa Mwitu.
Kwa minajili hiyo, hatua ya kwanza katika kufanya jitihada za kumuokoa kifikra mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kingono ni kuirejesha imani yake kwa watu. Hapa, sharti apatikane mtu anayeweza kuyafariji majuto na huzuni ya mtoto ambapo mtoto atajihisi yuko huru kuzungumza nae na kukisikia kilio chake.
Wepesi wa jambo hili utategemea zaidi uharaka wa mtu huyo katika kushughulikia uovu na huzuni ajisikiayo mtoto. Hii si kazi rahisi lakini kwani tulio wengi tusikiapo matukio na simulizi za kusikitisha, muitikio wetu wa awali huhusisha kulaumu na kuhukumu. Tunashindwa kutambua kwamba tunapofanya hivyo, mtoto hujihisi kubebeshwa mzigo wa lawama ulio na hukumu ndani yake na hivyo huona ni bora akaendelea kuitunza yake siri.
Hatupaswi kuzungumza maneno yanayoweza kuleta tafsiri mbaya kwa mtoto na kwamba tunamlaumu. Wakati mwingine hatia anayoihisi mtoto hutokana na fikra kwamba huenda ukatili aliofanyiwa tayari umeharibu maisha yake, jaribu kumuepusha na fikra hizo. Aidha, mdhibitishie kuwa maisha yake hayajaenda kombo kama afikiriavyo, mpe mifano ya watu mashuhuri waliowahi kuwa wahanga wa ukatili wa kingono lakini sasa wana mafanikio makubwa, mifano hiyo huweza kuwa chachu ya kuondoa majuto aliyonayo mtoto, kulirejesha tumaini lake na ujasiri wake.
Hatuna budi kumhakikishia mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji wa kingono kuwa, pamoja na yote yaliyomkumba, yeye ni wa thamani sana na bado ana nafasi ya kufikia ndoto zake. Wajibu wetu ndiyo maisha yake. Tuukatae udhalilishaji wa kingono dhidi ya watoto!
Kwa maoni na ushauri tupigie simu namba 116 ambayo ni maalumu kwa huduma za mtoto nchini. Huduma hii haitozi malipo toka mitandao yote nchini. Vilevile unaweza kutupata kupitia ukurasa wetu wa JamiiForums: Sema Tanzania;