JokaKuu
Platinum Member
- Jul 31, 2006
- 30,441
- 55,018
..makala ya Mihangwa wa raia mwema akiwachambua Mawaziri Wakuu wa Tanzania kuanzia wakati wa Uhuru.
KUTOKA NYERERE HADI PINDA, YUPI MAHIRI??
Waliotia fora kwa umahiri ? Kawawa, Sokoine
Sumaye, Lowassa waliboronga
Mizengo Pinda apiga jaramba
KAMA ungeulizwa swali hili la kushitukiza: Nitajie majina ya mawaziri wakuu wawili wa kwanza tangu Uhuru; na wawili wa mwisho; ungejibuje?
Bila shaka jibu sahihi lingekuwa ni Mwalimu Julius Nyerere (1961 1962); Rashidi Kawawa; Edward Lowassa (2005 - 2009) na Mizengo Pinda (2009 -).
Katikati ya kipindi cha mawaziri wakuu wawili wa kwanza, na wawili wa mwisho; mawaziri wakuu wengine sita walishika madaraka kwa vipindi mbali mbali; nao ni Edward Sokoine, Cleopa Msuya, Salim Ahmed Salim, Joseph Warioba, John Malecela na Frederick Sumaye.
Waziri Mkuu ndiye mtendaji na msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali na sera. Rais wa nchi si lolote kama waziri mkuu wake ni dhaifu, mapepe na asiyewajibika. Kwa hiyo, ubora wa Serikali unategemea Baraza la Mawaziri makini na mahiri (Mkapa aliwaita Askari wa miavuli), likiongozwa na Waziri Mkuu.
Katika kipindi cha nusu karne cha Uhuru, mawaziri wakuu 10 wamepanda na kutoka juu ya jukwaa la uongozi ambalo William Shakespeare, katika tamthiliya yake Merchant of Venice, yaani Mabepari wa Venisi, analifananisha na jukwaa ambalo juu yake kila mtu hucheza sehemu yake.
Kati ya mawaziri wakuu hao 10 waliopata kupanda juu ya jukwaa, Watanzania hawatawasahau wawili - Rashidi Kawawa na Edward Sokoine, ambao walipanda jukwaani kwa kupokezana kijiti. Nitaeleza sababu za kuvuma kwao hivi punde.
Lakini kabla ya kufanya hivyo, hebu tuwaangalie kwa kifupi tu mawaziri wakuu waliosalia, kisha tujikite kwa hao wawili tunaowalenga.
Mwalimu Nyerere ndiye aliyekuwa Waziri Mkuu wa kwanza baada tu ya Tanganyika kupata Uhuru, Desemba 9, 1961; akichukua nafasi ya Gavana Sir Richard Turnbull.
Lakini Nyerere alitumikia cheo hicho kwa mwezi mmoja tu, kabla ya kujiuzulu Januari 1962, akikabidhi mikoba kwa Rashidi Kawawa.
Sababu nyingi za kujiuzulu kwake zinatolewa. Kubwa inayovuma ni kwamba alifanya hivyo ili kurejea kwa wananchi kukijenga upya na kukiimarisha chama tawala, Tanganyika African National Union (TANU), kabla ya kurejea tena Desemba 1962, kama Rais asiyeambilika (Imperial President) wa Jamhuri ya Tanganyika.
Lakini kuna sababu nyingine inayotolewa, tofauti na ile ya kwanza; kwamba Nyerere alilazimika kujiuzulu kutokana na ugomvi mkubwa kati yake na baadhi ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya TANU, waliotaka Wahindi wote (wakiwaita nyoka) na Wazungu (wakiwaita Manabii wa ukoloni), wafukuzwe nchini; jambo ambalo Nyerere alilipinga vikali, akiliita ni la Kibaguzi, na ambalo kusema kweli, lilileta mvurugano mkubwa ndani ya chama.
Hoja hii inathibitishwa na gazeti la New York Times la Februari 3, 1962 lilipoandika: Inaonekana kana kwamba, Bwana Nyerere amekumbana na mkasa unaowapata viongozi wengi wa Kiafrika wenye siasa baridi. Jinsi alivyobanwa upesi upesi na mawazo ya wanamapinduzi zaidi kuliko yeye (ndani ya NEC), mpaka akangolewa katika kiti, inatisha.
Naye Gavana Richard Turnbull, alinukuliwa akisema hivi kuhusu hilo: Nilijua mwezi mzima kabla (kutokana na dalili za mvurugano katika chama) kwamba (Bw. Nyerere) angeweza kujiuzulu; lakini nilidhani ya kwamba alikuwa anakata tamaa bure tu.
Kabla ya kujiuzulu siku hiyo, Nyerere aliunda upya Baraza lake la Mawaziri na kumteua Rashidi Kawawa, ambaye wakati huo alikuwa Waziri asiye na Wizara Maalumu, kuwa Waziri Mkuu: Tazama Rashidi; wewe ndiwe Waziri Mkuu, kuanzia sasa hivi. Shika kiti, aliagiza.
Amir Jamal, Waziri mwingine katika Kabineti hiyo, alinukuliwa baadaye akielezea hali ilivyokuwa: Alikuwa mkali sana; alikuwa amekwishavuka ugumu wa kuamua kujiuzulu.
Kutokana na matukio hayo ya mwanzo wa Uhuru, ni dhahiri kwamba Julius Nyerere, kama Waziri Mkuu wa kwanza, hakuweza kuonyesha ushupavu, ujasiri, wala umahiri wowote katika kukabiliana na changamoto za Tanganyika, hususani, katika nyanja za kuimarisha uzalendo, uzawa na suala zima la Watanzania kushika hatamu za uongozi wa nchi katika ngazi zote za Serikali, kwa hofu ya kutojua matokeo ya mabadiliko ya ghafla. Na pale aliposhindwa kuelewana na wanamapinduzi wenzake ndani ya NEC juu ya Africanization, na juu ya Wazungu na Wahindi kutoruhusiwa kujiunga na TANU, na kukiita kitendo hicho kuwa ni cha kibaguzi; akajiuzulu Uwaziri Mkuu kwa hasira na kuamua kurejea kwa wananchi, kukusanya nguvu kwa njia ya kukiimarisha Chama (TANU), kabla hajarejea kwa wadhifa mpya wa Rais Mtendaji, mwenye mamlaka makubwa, yakiwamo yale ya kuweka watu, kizuizini, hasa wale wenye kupinga au kuhoji Serikali na utendaji wa Rais.
Katika kipindi kilichofuata, Mwalimu aliwahi kuulizwa maswali mawili magumu kuhusiana na tukio hili; kwamba alikuonaje kujiuzulu kwake uwaziri mkuu, kisha kurejea madarakani?; na aliyaonaje madaraka yake ya Rais wa Jamhuri ya Tanganyika?
Naye alijibu kwamba, kosa kubwa alilofanya ni kukubali kurejea madarakani; hatua ambayo alisema, inaweza kutafsiriwa kwa usahihi kabisa, kama ishara ya uchu wa madaraka.
Na kuhusu nafasi mpya ya Urais Mtendaji, alisema, Katiba ilimpa madaraka makubwa mno kustahili kuitwa dikteta.
Tutaona baadaye kidogo, ni kwa nini alimteua Rashidi Kawawa kushika (kushikilia?) nafasi ya Waziri Mkuu alipojiuzulu; na kwa nini Kawawa aliwasilisha Bungeni muswada kuanzisha nafasi ya Rais Mtendaji, nafasi ambayo imepata changamoto kutoka kwa wanaharakati wa demokrasia, tangu mwanzo hadi sasa.
Mambo mengi makubwa yalifanyika haraka haraka na kwa kasi ya kutisha chini ya Kawawa kama Waziri Mkuu, ambayo pengine yasingefanyika kama Nyerere angekuwa Waziri Mkuu.
La kwanza, lilikuwa ni kuondolewa haraka sana kwa Wazungu katika nafasi zote za juu za utumishi wa Umma, na kuchukuliwa na Waafrika (Africanisation) wasio na ujuzi katika medani za utawala.
Na kama isingekuwa Nyerere kusitisha zoezi hili aliporejea madarakani kama Rais, pasingebakia Mzungu wala Mhindi nchini katika kipindi chini ya mwaka mmoja wa uongozi wa Kawawa.
Lakini kwa Nyerere kusitisha zoezi hilo, kulimletea matata makubwa; kwani, wakati ngazi za juu za utumishi wa kiraia tayari zilishikwa na Waafrika, nafasi za juu Jeshini bado ziliendelea kushikwa na Wazungu. Na pale Waafrika Jeshini walipoanza kupoteza matumaini ya kupewa madaraka ya juu kutokana na kitendo hicho cha Nyerere cha kusitisha Africanisation, Jeshi liliasi dhidi ya Nyerere na Serikali yake, Januari 20, 1964.
Katika tafrani hiyo, nchi ilikuwa mikononi mwa Jeshi kwa siku mbili mfululizo, wakati huo Nyerere na Kawawa wamejificha kusikojulikana.
Hatua nyingine iliyochukuliwa na Kawawa, ilikuwa ni kubadili utaratibu wa kumiliki ardhi, kwa kukomesha mtu mmoja kupewa kabisa ardhi na uwezo wa kuuza; badala yake ardhi ikafanywa kuwa ya kukodisha: Utaratibu wa kumkabidhi mtu ardhi moja kwa moja ikawa yake kabisa bila ya masharti, unawajengea watu tamaa ya fedha na unyonyaji, na hivyo lazima ukomeshwe, alisema bungeni lilipokutana Februari 1962.
Jambo jingine lililofanyika chini ya Waziri Mkuu Kawawa, ni kutungwa na kutangazwa kwa Katiba ya (Tanganyika kuwa) Jamhuri (the Republican Constitution), kuchukua nafasi ya Katiba ya Uhuru (the Independence Constitution) ya mwaka 1961, kwa kuanzisha nafasi ya Rais Mtendaji (Executive/Imperial Presidency), ambayo hatimaye iligombewa na Mwalimu Nyerere katika uchaguzi wa Novemba 1962; akashinda na kuwa Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Tanganyika.
Chini ya Nyerere, Kawawa aliendelea kuwa Waziri Mkuu na baadaye kuongezewa Cheo cha Makamu wa Pili wa Rais, baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana kuunda Tanzania, mwaka 1964. Tutaona hivi punde ubora au udhaifu wa Kawawa kama Waziri Mkuu chini ya Nyerere.
Nafasi ya Kawawa ilichukuliwa na Sokoine mwaka 1980, kama tutakavyoona; na baadaye, Sokoine alijiuzulu, na nafasi hiyo kushikwa na Msuya, kabla ya kurejea tena 1983.
Msuya alikuwa Waziri Mkuu baridi, asiye na msukumo lakini mwenye kujiamini. Hakuwa mwanasiasa, bali alikuwa mtendaji makini wa kazi za mezani, na mgumu wa kuchanganyika. Na kwa sababu hii, Msuya alipwaya kama Waziri Mkuu mwenye dhamana ya kusimamia maendeleo na sera za nchi.
Salim Ahmed Salim, kama alivyokuwa Joseph Sinde Warioba, alikuwa mwanaharakati wa sera za maendeleo za mrengo wa Ujamaa, lakini alikuwa mgumu wa kuthubutu, tofauti na walivyokuwa Kawawa na Sokoine. Na kwa sababu hii, hakuweza kuacha nyayo katika jukwaa la maendeleo ambapo mkazo ulikuwa juu ya maendeleo vijijini.
Isitoshe, Warioba alishika Uwaziri Mkuu katika kipindi cha Serikali ya awamu ya Pili ya Rais Ali Hassan Mwinyi, ambapo msingi wa maendeleo kwa wote ulikuwa umebomoka kwa njia ya Ruksa kwa kila jambo, bila kujali maslahi ya nchi na ya walio wengi.
Malecela, kama ilivyokuwa kwa Sumaye, alishika madaraka wakati nchi ikiwa imenaswa katika mtego wa Sera za Kibepari za Benki ya Dunia (WB), Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na wafadhili, ambamo miradi na ubinafsishaji, badala ya mipango ya maendeleo yenye kulenga watu, vilichukua kiti cha mbele katika Sera za nchi za uchumi, na hivyo kuwasahau walio chini.
Ukichanganya Ruksa ya Rais Mwinyi na Uwazi na Ukweli wa Rais aliyefuata, Benjamin Mkapa, walifungua na kuacha mlango wazi kwa wageni na wawekezaji kupora sera na rasilimali za Taifa wapendavyo, na kwa nchi kugeuzwa shamba la Bibi. Malecela na Sumaye hawakuwa na ubavu wa kuonyesha weledi wao, wakaamua kufunika kombe mwana haramu apite, wakitazama uzalendo, maadili ya Taifa na uchumi wa nchi vikiangamia. Kwa hiyo, historia yao si ya kujivunia sana. Ni Mawaziri Wakuu walioachia nchi iingie katika wawekezaji na ukoloni mamboleo.
Ilipoingia madarakani Serikali ya awamu ya nne, ya Rais Jakaya Kikwete,
Watanzania walio wengi, walipumua kwa matumaini kwamba hatimaye ukombozi umefika; na baadhi kumwita Rais huyu Chaguo la Mungu, Nyerere kazaliwa upya au Kimbilio la wanyonge. Na alipomteua Edward Lowassa kuwa Waziri wake, naye akaahidi kufanyakazi kwa umakini na umahiri mkubwa; wengi walidhani Sokoine kazaliwa upya bila kuelewa kwamba Lowassa tayari alikuwa majeruhi wa Sera za Ruksa na za Uwazi na Ukweli; tena majeruhi mahututi zaidi aliyevunjika miguu kwa kufukuzia vinavyongara.
Tuhuma lukuki zinazoelekezwa kwake, likiwamo sakata la Richmond/Dowans hata akalazimika kuachia ngazi, ni ushahidi tosha kwamba hawezi kuvaa viatu vya Kawawa na Sokoine.
Kupanda jukwaani kwa Mizengo Pinda, mtu aliyekulia Ikulu, tena mbele ya macho ya kila siku ya Mwalimu Nyerere, kumeliwaza kwa kiasi fulani mioyo ya baadhi ya Watanzania; kwamba huenda, Waziri Mkuu huyu, ambaye tangu mwanzo amejitambulisha na wanyonge wa nchi hii, anaweza kuwa Mussa wa Watanzania kuwapeleka nchi ya ahadi, baada ya miaka 49 jangwani.
Akijitofautisha na akina Sumaye na Lowassa, wakati akitangaza ukwasi wake kiduchu hivi karibuni, Pinda amesema, haoni sababu ya kulimbikiza mali; wala hataki kuishi kwa tamaa zaidi, kwani wadhifa alio nao, endapo atastaafu, atahudumiwa na Serikali: Serikali imeweka utaratibu mzuri, ninapewa nyumba, chakula, magari; kwa hiyo mapato yangu nafanya saving (naweka akiba), najiona mwenye bahati, Mungu amenifikisha hapa ili niwatumikie wananchi.
Hapana shaka kwamba kauli hii ya Pinda ni ya dhati, katikati ya mfumo unaonuka rushwa na ufisadi, toka utosini hadi unyayoni. Bila shaka, kwa ishara hii, ni dhahiri Pinda ameanza kupiga jaramba kujiandaa kwa Serikali ya awamu ijayo. Lakini, nani mahiri kuwashinda Kawawa na Sokoine?
Itaendelea Toleo lijalo.