Tumaini Makene
JF-Expert Member
- Jan 6, 2012
- 2,642
- 6,071
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinatoa ufafanuzi kwa umma kwamba pamoja na kauli ya Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya kusudio la kuwasilisha ripoti tatu zilizotolewa kuhusu mauaji ya Mwanahabari Daudi Mwangosi kwenye Baraza Kivuli la Mawaziri kwa ajili ya hatua za kibunge kuchukuliwa na Kambi Rasmi ya Upinzani; CHADEMA kitaendelea kuchukua hatua zingine nje ya Bunge kwa kuzingatia maamuzi ya Kamati Kuu ya kutaka hatua kuchukuliwa na Rais Jakaya Kikwete kwa mujibu wa barua aliyoandikiwa.
Iwapo Rais kwa niaba ya Serikali hatazingatia, CHADEMA kiliamua kwamba kitachukua hatua ya ziada ya kuwaongoza wananchi kwa njia za kidemokrasia ikiwemo maandamano ya amani kushinikiza hatua za haraka kuchukuliwa kwa maslahi ya taifa.
Itakumbukwa kwamba tarehe 9 Septemba 2012 Kamati Kuu ya CHADEMA ilifanya kikao maalum cha kujadili hali ya siasa nchini kufuatia mfululizo wa mauaji yanayofanywa na Jeshi la Polisi katika shughuli za kisiasa za CHADEMA na mipango ya baadhi ya viongozi wa Serikali ya kudhibiti vuguvugu la mabadiliko (M4C) kwa mbinu haramu.
Kamati Kuu ilizingatia masuala mbalimbali na kupitisha maazimio nane na kuamua kumuandikia barua Rais kwa lengo la kumtaka achukue hatua za utekelezaji kwa mujibu wa mamlaka yake na kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo, CHADEMA bado kinamtaka Rais Jakaya Kikwete kueleza hatua alizochukua na kujibu barua ya CHADEMA.
Itakumbukwa kwamba baada ya kuwasilisha barua hiyo ya tarehe 10 Septemba 2012 iliyoandikwa na Mwenyekiti wa Taifa, Freeman Mbowe (Mb) ambayo pamoja na hatua nyingine CHADEMA ilitaka Rais achukue hatua ya kuwafukuza kazi Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Ndugu Emmanuel Nchimbi, IGP Said Mwema, Kamanda Mkuu wa Operesheni Paul Chagonja, RPC wa Mkoa wa Morogoro Faustine Shigolile, RPC wa Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda na Mkuu wa FFU Mkoa wa Morogoro, kwa kutowajibika kufuatia mauaji yaliyotokea mkoani Morogoro na Iringa; ikulu ilinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari ikieleza kuwa majibu yatatolewa baada ya Kamati iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani kutoa ripoti yake.
Rais Kikwete anapaswa kuchukua hatua kwa kuzingatia barua ya CHADEMA na kwa kurejea pia Ripoti ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ambayo imeeleza uvunjwaji wa haki za binadamu, ukiukaji wa sheria na uvunjaji wa misingi ya utawala bora uliofanywa na wahusika wakuu ambao tayari CHADEMA iliwataja kwenye barua yake kwa Rais na kutaka wafukuzwe kazi.
Hata hivyo, Rais Kikwete na umma uzingatie kuwa barua ya CHADEMA haikuhusu mauaji ya Mwangosi pekee bali mfululizo wa mauaji yaliyotokea katika mazingira ya kisiasa na pia ifahamike kwamba pamoja na Ripoti ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kueleza uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukaji wa sheria na misingi ya utawala bora uliofanywa katika matukio ya Iringa; muktasari wa ripoti unaashiria tume haikufanya uchunguzi mpana wa mtandao mzima uliohusika kupanga operesheni haramu na kusababisha mauaji na kupendekeza hatua kali kwa wahusika wote ikiwemo za kisheria.
Hivyo, CHADEMA bado kinasubiri kauli ya Rais na majibu kuhusu barua ambayo pamoja na hatua zingine ilitaka aunde tume ya Kijaji/ Kimahakama ya uchunguzi wa vifo vilivyotokea katika mikusanyiko, mikutano, maandamano au mazingira ya kisiasa yaliyohusisha CHADEMA. Vifo hivi ni vile vilivyotokea Arusha (05/01/2011), Igunga (Novemba 2011), Arumeru Mashariki (Aprili 2012), Iramba (Julai 2012), Morogoro (27/08/2012) na Iringa (02/09/2012).
Itakumbukwa kuwa katika maandamano yaliyoitishwa na CHADEMA tarehe 05/01/2012 watu watatu walipoteza maisha baada ya Jeshi la Polisi kutumia nguvu na risasi za moto kutawanya waandamanaji.
Katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Igunga pamoja na matukio mengine yaliyojitokeza na yaliyohusisha vurugu kinyume cha Sheria, Ndugu Mbwana Masoud mwanachama wa CHADEMA aliteswa na kunyongwa katika mazingira ya kutatanisha. Mpaka sasa hakuna hatua stahiki zilizochukuliwa kufanya uchunguzi kuhusu kifo hicho.
Mara baada ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kiongozi wa Kata wa CHADEMA Ndugu Msafiri Mbwambo alichinjwa na chanzo chake kudaiwa kusababishwa na masuala ya kisiasa na hivi karibuni baadhi ya watuhumiwa wa mauaji hayo wametoroka
kutoka wakiwa mikononi mwa polisi katika mazingira yenye kuashiria njama za kutoroshwa.
Hivi karibuni yalitokea mauaji katika Kijiji cha Ndago, Wilaya ya Iramba Mkoani Singida ambapo kikundi cha watu kilivamia mkutano wa CHADEMA kwa mawe Polisi wakiwepo bila kuchukua hatua na baada ya mkutano kumalizika na viongozi wa CHADEMA kuondoka eneo la mkutano kijana mmoja anayedaiwa kuwa kiongozi wa Kata wa UVCCM alikutwa katika kijiji hicho akiwa amepoteza maisha.
Tayari taarifa za ziada zimeanza kujitokeza kuhusu maelezo ya baadhi ya vijana wa UVCCM kwamba tukio hilo lilipangwa na kigogo mmoja wa CCM (vyombo vya habari vilivyoandika habari hizo vimeeleza kuhifadhi jina lake kwa sasa) huku polisi wakishindwa kufanya uchunguzi huru na kuchukua hatua.
Hivi karibuni tena katika maandamano ya mapokezi ya viongozi wa CHADEMA Mkoani Morogoro Polisi walimshambulia Ndugu Ally Zona na kupoteza maisha, na baadae Polisi wakatoa taarifa kuwa aligongwa na kitu kizito.
Mkoani Iringa wakati wa kufungua matawi ya Chama kwenye kata ya Nyololo, Polisi walimlipua kwa bomu Mwandishi wa Habari Ndugu Daudi Mwangosi. Pamoja na Polisi kuhusika na mauaji hayo bado Waziri wa Mambo ya Ndani, IGP Said Mwema, Kamanda wa Operesheni wa Jeshi la Polisi Paul Chagonja, RPC wa Mkoa wa Morogoro Faustine Shigolile na RPC wa Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda hawakuchukua hatua yoyote ya kuwajibika kwa kuhusika moja kwa moja na matukio haya au kiutendaji katika Jeshi la Polisi kwa ujumla.
Mauaji yote haya hayajafanyiwa uchunguzi wowote wa Kimahakama/ Kijaji kwa mujibu wa Sheria za nchi yetu kinyume na ahadi ya Waziri Mkuu Bungeni wakati akihitimisha hoja yake katika Bunge la Bajeti la mwaka 2011/2012. Hakuna uchunguzi wa kifo inquest uliofanyika na hakuna Mahakama ya korona coroners court iliyoanzishwa ili kuchunguza vifo hivi.
Irejewe kwamba kufuatia hali hiyo, Kamati Kuu ya CHADEMA ilifanya kikao maalumu siku ya Jumapili Tarehe 09 Septemba 2012 katika Hoteli ya Blue Pearl Jijini Dar es Salaam. Kikao hicho kilijadili hali ya siasa nchini kufuatia mfululizo wa mauaji yanayofanywa na Jeshi la Polisi katika shughuli za kisiasa za CHADEMA na mipango ya baadhi ya viongozi wa Serikali ya kudhibiti vuguvugu la mabadiliko (M4C) kwa mbinu haramu.
Katika majadiliano ya kina kabla ya kufikia maazimio na maamuzi hayo, Kamati Kuu ilizingatia kuwa hali ya siasa nchini ni tete, Serikali inayoongozwa na CCM imeshindwa kusimamia vizuri rasilimali za nchi ikiwemo kudhibiti mfumuko na ongezeko la bei na kuchangia katika ugumu wa maisha kwa wananchi na migogoro ya kijamii na ufisadi nchini.
Taifa limegubikwa na tuhuma za vyombo vya Serikali kutenda kinyume na haki za kikatiba na kutumiwa kudhibiti mabadiliko kwa njia haramu ikiwemo kuteka na kutesa (Mf. Tukio la Dr Ulimboka), kulifungia gazeti la Mwanahalisi na kufanya vurugu na mauaji katika shughuli halali za kisiasa za CHADEMA.
Pamoja na hali hiyo, Kamati Kuu iliazimia kuwa Operesheni ya M4C iendelee na kazi zake kwa kufuata kikamilifu ratiba iliyopitishwa na Baraza Kuu na Kamati Kuu katika vikao vya awali kiwa ni sehemu ya kutimiza dhima yake ya kuleta uongozi bora, sera sahihi, mikakati makini na oganizesheni thabiti kwa maendeleo endelevu ya Tanzania.
Imetolewa tarehe 12 Oktoba 2012 na:
John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi