esther mashiker
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 616
- 552
BIASHARA ya utumiaji wa gesi majumbani (LPG) inazidi kuongezeka nchini kutokana na takwimu za miaka ya hivi karibuni kuonesha ongezeko la wastani wa zaidi ya asilimia 100 kutoka mwaka 2010 hadi kufi kia mwaka 2018.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2018, wastani wa tani 140,000 za gesi hiyo ilikuwa ikiingizwa nchini ikilinganishwa na mwaka 2010 ambapo tani 20,000 pekee za gesi ndiyo ilikuwa ikiingizwa nchini.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina ya siku moja kuhusu taratibu za uombaji leseni za biashara ya gesi ya kupikia na utunzaji salama wa mitungi kwa wauzaji wa gesi hiyo kutoka Kanda ya Mashariki, Meneja wa Kanda hiyo, Nyirabu Musira alisema hatua hiyo pamoja na mambo mengine ndiyo sababu iliyoifanya Ewura kufanya mabadiliko ya kanuni zinazohusu biashara ya gesi hiyo ili kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza.
“Kuanzia kipindi hicho cha mwaka 2018, Ewura iliamua kufanya marekebisho ya kanuni zake ili kuendana na kasi ya maendeleo ya biashara hiyo hapa nchini, na hadi sasa tayari kanuni hizo zimeanza kutumika baada ya kuwa sheria tunayoitaka wafanyabiashara wote wa gesi kuitekeleza,” alisema Musira.
Kwa mujibu wa Musira, kutokana na uwepo wa matumizi makubwa ya gesi inayoendana na kukua kwa biashara ya gesi nchini, iliwalazimu kuangalia namna ambavyo wanaweza kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza katika biashara hiyo ikiwemo kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika vituo vinavyouza na kusambaza gesi.
“Kimsingi pamoja na kuongezeka kwa ubora wa gesi inayotumika majumbani siku hadi siku, wataalamu wetu wamekuwa wakifanya ukaguzi huo ili kuona kama sheria iliyowekwa inazingatiwa wakati huu ambao bado tunaendelea na mikakati mingine ya kuona namna gani tutakavyoweza kudhibiti bei ya gesi huko mitaani,” alisema.
Chanzo: HabariLeo