Marekebisho ya Sheria za uchaguzi yaondoe kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na ut

John Mnyika

JF-Expert Member
Jun 16, 2006
712
1,240
Leo Waziri husika amelitaarifu Bunge kwamba Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi utajadiliwa na kupitishwa katika mkutano wa bunge unaoendelea na tayari kanuni imeshatenguliwa kuruhusu mchakato huo.

Kama sehemu ya kuendeleza mjadala kuhusu sheria husika nawaletea maoni yangu kuhusu hatua nyingine muhimu ya uchaguzi; upigaji kura, kuhesabu na kutangaza matokeo.

.....................Zipo kasoro za moja kwa moja ambazo hujitokeza katika kuhesabu na kutangaza matokeo. Mathalani katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 Jimbo la Ubungo matokeo ya ubunge yalitangazwa kwa shuruti bila kutangaza na kujumlisha kwa pamoja matokeo ya kituo hadi kituo hali iliyoashiria kuwa matokeo ya Ubunge yalikuwa na utata. Kutangaza huku kwa nguvu ilikuwa ni mkakati wa kutaka matokeo hayo yasihojiwe kama ilivyokuwa katika matokeo ya urais ambayo yalichelewa kutangazwa kutokana na kukutwa na mapungufu mengi. Kwa hali iliyodhihirisha wazi kuwa matokeo yalipikwa, waliopiga kura za Ubunge walikuwa 185,684 wakati waliopiga kura za Rais walikuwa 152,525 na hivyo kufanya tofauti ya kura za Ubunge na urais kufikia 33,159. Katika hali ya kawaida na katika uchaguzi uliofanyika kwa wakati mmoja ilikuwa ni vigumu kwa tofauti kubwa ya kura kiasi hiki. Na hata kama wananchi wangekuwa hawapendi kupiga kura za rais kwa kuwa mpiga kura alikuwa akipewa karatasi zote tatu kura hizi zilipaswa kuwepo katika kura zilizoharibika kitu ambacho hakikutokea. Mfano wa Jimbo la Ubungo unaibua hoja ya utofauti mkubwa baina ya jumla ya wapiga kura katika ubunge na urais katika majimbo mbalimbali Tanzania, suala hili linapaswa kujadiliwa. Ufanyike uchambuzi huo kujua utofauti katika kila jimbo ili kuweza kubaini chanzo cha hali hiyo na kukabilina nacho.

Katika kipindi cha mwaka 2006 mpaka 2009, kumeonekana tatizo lingine ambalo nalo linahitaji mjadala wa kina; mwitikio mdogo wa wapiga kura katika chaguzi za marudio. Mathalani chaguzi ndogo za ubunge: Tunduru (48%), Kiteto (47%), Tarime(46%) na Mbeya Vijijini(35%). Kwa upande wa chaguzi ndogo za madiwani hali ilikuwa mbaya zaidi katika baadhi ya kata mathalani: Upanga Mashariki-Dar es salaam (7%) na Sombetini-Arusha(14%) nk. Suala linahitaji kufanyiwa utafiti na chombo zaidi ya kimoja, ili kuwianisha matokeo ya sababu na mazingira yatayoanishwa. Maelezo ya wananchi mbalimbali ni kwamba ‘kadi za kupigia kura zinanunuliwa ama kuchukuliwa kabla ya kwenda kupiga kura'. Uchunguzi wa kina utasaidia kubaini tatizo hili ambalo linaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa misingi ya uhuru na haki katika chaguzi zinazofuata.

Ikumbukwe kuwa Tarehe 11 Disemba 2009 Serikali ilichapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi na kutangaza kupitia vyombo vya habari tarehe 21 Disemba 2009 maudhui ya miswada hiyo. Miswada hiyo imeshajadiliwa na kamati husika za Bunge na inatarajiwa kujadiliwa ndani ya mkutano wa Bunge unaonza mwezi huu.
Hata hivyo, marekebisho hayo yaliyopendekezwa katika miswada hiyo hayajagusa kikamilifu maeneo yenye kasoro yanayohusu upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo. Eneo pekee linaloguswa katika marekebisho ni lile linalohusu zoezi la uandikishaji wapiga kura, ambapo imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Hivyo ni muhimu mjadala ukapunuliwa kuwezesha kasoro kushughulikia likiwemo tatizo la kupungua kwa idadi ya wapiga kura. Zipo nchi ambazo sheria ya uchaguzi inalazimisha wananchi kupiga kura ili kuondokana na tatizo la kupungua kwa idadi ya wananchi wanaojitokeza kupiga kura. Mazingira ya kisheria yanaweza kuweka bayana kwamba uhalali wa kiongozi kutangazwa mshindi unategemea asilimia ya wananchi waliopiga kura. Kiongozi aliyechaguliwa na wananchi ambao hawafiki hata asilimia kumi ya wapiga kura waliojiandikisha uhalali wake uko mashakani.

Maoni yangu zaidi yanapatikana hapa: http://mnyika.blogspot.com/2010/01/marekebisho-ya-sheria-za-uchaguzi.html
 
Back
Top Bottom