Marekani yatenga donge nono kuhamasisha ushoga (makala)

mdau wetu

JF-Expert Member
Apr 20, 2011
548
58
ILI kuonesha kwamba lazima zile nchi za Afrika zinazogoma kukubali kutambua ushoga kisheria zinatii amri hiyo, nchi ya Marekani na washirikika wake zimeamua kutumia kila njia kuhakikisha wanazilazimisha kutambua na kulinda haki za mashoga.
Wamepanga katika majukwaa mbalimbali wanapokuwa wanakutana na viongozi wa mataifa mbalimbali, hasa ya Bara la Afrika, watakuwa wakizungumzia kuhusu haki hizo, ambazo zimebainishwa kuwa kigezo hata cha kupata misaada.
Kwa kuthibitisha hilo, hivi karibuni katika Siku ya Haki za Binadamu Duniani, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Hillary Rodham Clinton, kwenye hotuba yake ametoa wito wa kulinda haki za mashoga, akidai kuwa ‘ndiyo imebaki miongoni mwa changamoto nyingi za haki za binadamu’.
Waziri Clinton amesema kuwa Marekani itatumia mbinu za kidiplomasia na itatoa msaada wa kifedha wa dola milioni tatu (sawa na sh bil. 5.4) kuzindua mfuko wa kusaidia kupanua haki za mashoga duniani kote.
Katika hotuba yake hiyo aliyoitoa Desemba 10, mwaka huu katika maadhimisho hayo, Clinton alizitaka nchi washiriki kulinda haki za mashoga akidai kuwa “kwa sasa ndiyo miongoni mwa changamoto ambazo zimebakia kwa wakati tulio nao” na kuilinganisha hali hiyo na vita dhidi ya haki za kina mama, ubaguzi wa rangi na uhuru wa kuabudu.
Akiwahutubia wajumbe wa mataifa mbalimbali wa bodi ya haki za binadamu mjini, Geneva, Uswisi, alisema kuwa vikwazo vingi vya usawa wa kijinsia duniani zaidi “vinaangukia katika nafsi, siasa, utamaduni na imani za kidini.”
Clinton alisema kuwa haki za binadamu ni lazima zifanyiwe marekebisho ili na zile zinazohusu haki ya kujamiiana ziingizwe.
“Wengine wamekuwa wakishauri kuwa haki za mashoga na binadamu ni vitu tofauti, lakini kwa hakika ni moja na zinafanana,” alisema Clinton. “Haki za mashoga ni haki za binadamu,” aliongeza.
Clinton alikwenda mbali na kukumbusha kwamba tangu mwaka 1948 lilipotolewa tangazo la kimataifa la haki za binadamu hadi sasa kumekuwa na hatua kubwa katika masuala ya haki za binadamu.
Kwa miaka 63 Clinton alikili kwamba mataifa mengi yamepiga hatua kubwa katika kutambua na kujali haki za binadamu lakini si za mashoga.
Clinton katika hotuba yake hiyo alisema kuwa katika maeneo mengi, sheria za ubaguzi wa rangi zimeondolewa, sheria na vitendo vya kijamii ambavyo viliwaweka wanawake katika daraja la pili vimeondolewa, na haki ya kuwapa uhuru wachache kufanya ibada, ikiwa ni ubaguzi imeondolewa pia.
Alisema watu walipigana na kufanya kampeni katika sehemu za wazi na zisizo za wazi kubadilisha si tu sheria, bali na mitazamo ya watu.
“Bado kuna, kama wote mnavyofahamu, mengi ya kufanya ili kufikia malengo yaliyokusudiwa, na maendeleo kwa watu wote.
“Leo nataka kuzungumzia kuhusu kazi ambayo tumeiacha ya kulilinda kundi moja la watu ambao haki zao za binadamu bado zinakandamizwa katika sehemu nyingi duniani.
“Ni kundi la watu wachache wasioonekana, wanakamatwa, kupigwa, kunyanyaswa, hata kuuawa. Wengi wanadharauliwa na kufanyiwa fujo na wananchi wenzao, huku mamlaka zinazotakiwa kuwalinda zikiwa hazijali, na wakati mwingine hushiriki pia katika uonevu huo.
“Wananyimwa haki za kufanya kazi na kijifunza, wanafukuzwa katika nyumba zao na nchini mwao.
“Ninazungumzia kuhusu mashoga, ambao ni binadamu waliozaliwa huru na kupewa haki sawa ya kuishi kama wengine, lakini wanapokonywa haki na heshima yao, ambayo kwa sasa ni miongoni mwa changamoto ambazo tumebaki nazo duniani.
“Wengine wanaonekana kuamini katika dhana ya Kimagharibi, hivyo watu ambao wako nje ya Magharibi wanadhani kuwa wana sababu za kuikataa.
“Sawa, katika uhalisia mashoga wamezaliwa ndani ya jamii na wana uhusiano na kila jamii duniani.” Sehemu ya hotuba hiyo ya Clinton ilieleza.
Alizitaka serikali nyingine kuungana na Marekani katika juhudi dhidi ya ubaguzi wa kijinsia, hasa kuwanyima haki mashoga.
Saa chache baadaye Rais Barack Obama alizielekeza taasisi za Marekani zinazofanya kazi nje ya nchi hiyo kusaidia kupiga vita unyanyasaji katika kujamiiana na kusaidia kuwalinda mashoga.
Kwa kuthibitisha kuwa Marekani imeamua kupiga hatua zaidi katika kutambua haki za mashoga, utawala wa Rais Obama umewakubalia mashoga kujiunga na jeshi la nchi hiyo tofauti na awali.
Makao makuu ya jeshi la Marekani (Pentagon), mwaka huu yamelegeza masharti kwa kuondoa zuio la kuwakataza mashoga kulitumikia jeshi waziwazi, na Obama hivi karibuni amezikataza serikali za majimbo kung’ang’ania sheria inayotambua kuwa ndoa ni kati ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja.
Ndoa ya jinsia moja bado imepigwa marufuku katika majimbo mengi nchini Marekani, na unyanyasaji dhidi ya mashoga umetamalaki katika jamii nyingi nchini humo.
“Ninalisema hili kwa kuwa nafahamu kwamba rekodi ya nchi yangu kuhusu haki za mashoga ni nzuri,” Clinton alisema. “Kwa hiyo nimekuja mbele yenu kwa heshima, uelewa na huruma,” aliongeza Clinton.
Clinton alilinganisha dini na utamaduni katika ukiukwaji wa haki za mashoga kuwa ni kama sababu zinazotolewa na jamii nyingi katika kukeketa wasichana.
“Baadhi ya watu wanatetea vitendo hivyo kuwa ni sehemu ya utamaduni wao,” alisema Clinton. “Lakini ukatili dhidi ya wanawake si utamaduni. Ni uhalifu. Kama ilivyo kwa utumwa, kama ulivyokuwa umehalalishwa kwamba ni mapenzi ya Mungu, lakini sasa umethibitika kuwa ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu,” alisema Clinton.
 
Back
Top Bottom