Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,295
- 33,079
*AAHIDI KUMPIGIA DEBE DK SLAA NCHI NZIMA
Ramadhan Semtawa
WAKILI na mwanasiasa mwanzilishi wa mageuzi, Mabere Marando, amejitoa NCCR- Mageuzi na kujiunga Chadema huku akieleza kuwa atakata mbuga nchi nzima kuhakikisha Dk Willibrod Slaa anashinda urais mwezi Oktoba.
Marando amejiunga na Chadema katika kipindi ambacho Dk Slaa, amechanganya hisia za watu huku baadhi wakiuona uamuzi wa kukubali kuingia mbio za urais ni sahihi na wengine kuuona uamuzi huo kuwa sawa na kujimaliza kisiasa.
Akizungumza na wahariri na wawakilishi wao jijini Dar es Salaam jana, Marando alisema: Nimejiunga Chadema ili nishiriki kuiondoa CCM madarakani.
Chadema ni chama ambacho kimefanya kazi kubwa ya siasa ikiwemo Operesheni Sangara. Niliwahi kumwambia Dk Slaa akiingia katika kuwania urais, nitakata mbuga nchi nzima kuhakikisha anashinda. Dk Slaa ana uwezo mkubwa.
Marando alifafanua, yeye na waasisi wenzake wa mageuzi wamekuwa na malengo mawili makuu, ambayo kwanza ni wananchi kufahamu umuhimu wa mfumo wa vyama vingi na pili, kuanzisha vyama kwa lengo la kuingoa CCM madarakani.
Aliongeza kwamba:, Kwa hiyo kuhamia Chadema sijapotea njia, Chadema ni wapambanaji na mimi mapambano ni asili yangu.
Kwa mujibu wa Marando ambaye aliwahi kuwa Katibu Mkuu na mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi kabla na baada ya kupigwa na dhoruba ya kisiasa, alisema Chadema ni chama ambacho kimeweza kujiimarisha kisiasa, kutoa mwamko kwa wananchi na kuinua nguvu za mageuzi nchini.
Kwa hiyo, wanaosema Dk Slaa kugombea urais ni kujimaliza, hawako sahihi. Dk Slaa anahitajika zaidi ya Karatu, anahitajika nchi nzima, alisema na kuongeza:,
Hao ni waoga, wanaogopa wanajua kuna Challenge (changamoto) kubwa ambayo rais Kikwete atakabiliana nayo kutoka kwa Dk Slaa.
Marando alisema ni kweli Dk Slaa ameweza kutoa mchango mkubwa bungeni, ameweza kuibua mambo mazito, anajua kuchambua mambo kwa kina, lakini alisema mchango wake (Slaa) sasa unahitajika kwa nchi nzima.
Kwa sababu Tanzania ni kubwa kuliko Karatu, hata leo (jana) pale ofisini kwangu nimekuta watu wanasema hivyo Dk Slaa kakosea. Ilibidi nitulie nikachukua muda kuwaelimisha kidogo.
Marando alikisifia Chadema kuwa kimetoa mchango mkubwa bungeni na ni chama chenye mawazo mazuri, wabunge wake wachache wameweza kuibua mambo mengi bungeni.
"Hata hizi ajenda za ufisadi ni za akina Dk Slaa na akina Zitto, alisisitiza Marando na kuongeza:
Nani angejua mambo ya EPA kama si akina Dk Slaa? Nani angeweza kujua haya mambo ya madini kama si Zitto? Hata CCM wamedandia hoja hii, kwa hiyo utaona mchango wa Chadema ni mkubwa.
Alisema kwa kifupi, ni wabunge wachache wa upinzani hasa wa Chadema ndiyo wameonyesha na kuamsha watanzania kuhusu nchi yao inavyoliwa na iilivyokosa uongozi makini.
Wakili huyo alisema kwamba, nafasi ya chama cha upinzani si kukosoa na kushauri chama tawala, bali ni kuhakikisha wanaingoa CCM madarakani.
Kuhusu yeye kama ataogombea Rorya, alisema hatagombea nafasi yoyote si ubunge wala udiwani isipokuwa ameamua kujiunga Chadema kuongeza nguvu ili waweze kuingoa CCM.
Alipoulizwa haoni kuingia Chadema ni kudandia mafanikio wakati aliacha kuimarisha chama chake cha NCCR, alijibu:, Ni kweli kabisa nimedandia mafanikio. Ila hilo neno la kudandia kidogo linanipa tabu.
Lakini, siku zote watu wenye malengo ya kisiasa wanaangalia sehemu ambazo kazi ya siasa imefanyika kama chama ambacho kina matawi, ndiyo maana unaona maprofesa kutoka vyuo vikuu wanakwenda CCM wanajua tayari kina matawi kila sehemu huku kwetu wanaogopa. Mimi nimeamua kuunganisha nguvu na wenzangu wa mageuzi.
Juzi, Kamati Kuu Chadema ilimpendekeza Dk Slaa kupeperusha bendera ya chama hicho katika mbio za urais wa Oktoba, hatua ambayo imebua mgawanyiko wa mawazo miongongoni mwa watanzania.
Wananchi wa Karatu juzi waliandamana kupinga Dk Slaa kuwania kiti hicho cha urais wakimataka aendelee kutetea kiti chake jimboni humo.
Chanzo ni http://www.mwananchi.co.tz/habari/4-habari-za-kitaifa/3414-marando-sasa-apaa-na-helikopta-ya-chadema
Hongera Mzee Marando ningeomba na viongozi wengine waige mfano wa Mzee Marando. Ili kuweza kukishinda Chama Tawala CCM.