Maoni ya Taasisi ya Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) kuhusu masuala ya wanafunzi kipindi hiki cha dharura ya ugonjwa wa corona (Covid 19)

Dec 13, 2016
8
5
Mtandao wa wanafunzi Tanzania – TSNP unapenda kutoa maoni juu ya jitihada mbalimbali zinazofanyika ili kuendeleza masomo katika kipindi hiki cha dharura ya ugonjwa wa CORONA:

Kwanza: Kuhusu vipindi vya masomo kwa njia ya Redio na Televisheni vinavyoratibiwa naTaasisi ya Elimu Tanzania (TIE). TSNP inaipongeza sana TIE kwa kuanzisha program hizi ambazo zitawawezesha wanafunzi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha sita kujifunza wanapokua nyumbani.

Tunatoa wito kwa wazazi na walezi kuwasimamia na kuwawekea mazingira wezeshi wanafunzi wanapokuwa nyumbani ili waweze kufuatilia kikamilifu na kuongeza maarifa zaidi.

Pili: Kuhusu jitihada za uanzishaji wa masomo kwa njia ya mtandao (online classes) katika vyuo vikuu mbalimbali nchini. TSNP inatambua kwamba, baadhi ya vyuo vikuu nchini vinafikiria kuanzisha masomo kwa njia ya mtandao (online classes) ili kuendeleza masomo,huku vingine vikienda mbali zaidi kwa kuwataka wanafunzi kulipia ada.

Pamoja na kuthamini jitihada hizi na kwa kutambua mamlaka ya vyuo katika kusimamia taaluma za wanafunzi wa vyuo husika, TSNP tunatoa wito kwa vyuo vinavyoanza jitihada hizi kujiridhisha pasi na shaka kuwa wanafunzi wote popote walipo nchini iwe (vijijini au mijini) wanaweza kushiriki masomo hayo bila kikwazo chochote.

Kinyume na hapo, hekima itumike, kusubiri janga hili lipite na masomo yaendelee kwa utaratibu utakaowekwa na Serikali.

Sanjari na hilo, tunatoa rai kwamba, wanafunzi wasilazimishwe kulipa ada hadi pale Serikali itakapotoa muongozo kuhusu wanafunzi wanaolipiwa ada na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi ya Juu (HESLB) utaratibu wa malipo ya ada zao utafanyikaje.

Aidha, tunatoa wito kwa wanafunzi na watanzania wote kuendelea kuchukua hatua za kujikinga na maambukizi ya virusi vya CORONA kwa kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalamu kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Pia, tunawasihi wanafunzi wote kujilinda na kuripoti vitendo vyote vya unyanyasaji wa kijinsia vinavyojitokeza katika kipindi hiki cha likizo hii ya dharura.

Imetolewa na,

Davis Betram Komba
Mwenyekiti – Mtandao Wa Wanafunzi Tanzania
IMG-20200423-WA0113.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom