Status
Not open for further replies.

FaizaFoxy

Platinum Member
Apr 13, 2011
92,143
107,654
Pres_Magufuli_bigpic.jpg
Hii thread iwe Maalum kwa Maoni, Ushauri na Mapendekezo mbalimbali kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Mimi namuomba, Mheshimiwa Rais mteuliwa, kwa heshima na taadhima hili ni ombi binafsi kwako.

Nnaomba uhakikishe huyu mrembo wa ACT Bi Anna Mghwira unamuingiza bungeni na unampa wadhifa anaostahiki, huyu mama ni kichwa adhyim na adim kabisa.

Nimemfatilia mikutano yake mingi sana ya kampeni, anatoa vitu kichwani utafikiri ana word processor inayopanga na kuchuja anachokizungumza kutoka kichwani bila kusoma.

Halikadhalika leo kanifurahisha sana alipostukizwa na kutoa hotuba pale Diamond, ilikuwa fupi na imelenga points zote nzuri na ameeleweka vyema kabisa.

Anna heko sana na nitakuunga mkono katika siasa zako.

Ili kuipa hadhi na kuitangaza lugha yetu ya taifa, nashauri rais wetu mpya atumie Kiswahili katika shughuli zote rasmi za kitaifa na kimataifa. Cha msingi ni kuwa na wakalimani mahiri katika shughuli za kimataifa. Hii itainua hadhi na heshima ya nchi yetu badala ya kuendelea kuthamini lugha za kigeni. Tumekuwa watumwa mno wa lugha ya kiingereza mpaka kufikia hatua kudhani kuwa mtu anayeongea kiingereza vizuri ndiye aliye elimika wakati si kweli. Elimu ni uwezo siyo kuongea kiingereza. Hiki kiingereza cha "izi, wozi, wea, kongrugesheni, ameizingi, wati?, yu no, no problemu hakitusaidii kitu. Na kwa ujinga wetu tunafundishana kwa lugha tusiyoijua vizuri matokeo yake watoto wanafeli halafu tunawaona wajinga kumbe sera zetu ndio mbovu. Wachina, wakorea, wajerumani, wareno, wafaransa mbona wanatumia lugha zao na wanapiga hatua kubwa sana katika uchumi na sayansi. Sisi na kiingereza chetu cha kuombea maji tumefika wapi zaidi ya kutudhalilisha?

Maoni yangu haya hayana maana kuwa sitambui uwezo mkubwa wa kiingereza alio nao dr. Nataka aendeleze pale mwenzake alipoachia mwenzake, kwani alianza kwa kuhutubia kwa kiswahili kwenye mkutano wa AU lakini baadaye akaacha. Mimi nashauri Dr. sasa ajikite pamoja na mambo mengi kuitangaza lugha ya kiswahili kimataifa kwa yeye mwenyewe kuitumia badala ya kiingereza. Huwa naona viongozi wa nchi nyingine kama za kiarabu pamoja na kuwa wanajua kiingereza lakini utakuta wanazaunguza kiarabu na kisha wasiojua kutafsiriwa. Wakalimani sasa hivi tunao wengi, ni vizuri wakatumika vizuri kuikuza lugha yetu ya taifa. Ukweli ni kuwa unapotumia lugha mama au lugha ya taifa una kuwa na uhuru na uwezo mkubwa sana wa kujieleza na kuelezea kuliko unapotumia lugha za kigeni. Kwa watanzania wengi lugha yetu ya mama ni kiswahili.

Jambo moja ambalo Magufuli aliliona wazi katika kampeni zake ni kwamba Watanzania wanataka mabadiliko, na kwamba wengi walihisi mabadiliko haya yangeletwa na UKAWA. Magufuli akaahidi kwamba yeye ataleta madadiliko Watanzania wanayotaka.

Ushauri wangu kwa Magufuli ni kwamba kama kweli kweli anataka kuwaletea Watanzania mabadiliko - basi asiwe mtu wa kutafuta ushari kwa Kikwete na Mkapa. Wao walikuwa na nafasi ya kuletea Watanzania mabadiliko, na wengi waliona kuwa kwa sehemu kubwa walishindwa kuleta mabadiliko yaliyotakiwa, japo kulikuwa a mafanikio kataka sehemu chache.

Magufuli be your own man and master - Personality yako, kufikiri kwako na kule kwa kwa Kikwete na Mkapa ni tofauti kabisa na Watanzania wanategemea hilo litaleta mabadiliko wanayotarajia. Kuendelea kupokea ushauri toka kwa Kikwete na Mkapa ni kuwapa Watanzania mvinyo ule ule wa zamani katika glasi mpya; hilo ni hatari sana, na linaweza kukufanya uongoze kwa miaka mitano tu na kushindwa uchaguzi ujao.

Tunajua Kikwete a Mkapa walikuwa na mchango kukufanya uwe Raisi wa Tanzania - washukuru yaishie hapo. Waambie wakapumzike sasa, kazi yao imekwisha. Kuendelea kupokea ushauri wao kila wakati utajikuta unafanya kazi ili kuwaridhisha wao na sio Watanzania waliokuchagua. Pia epuka sana kupokea ushauri wao kwa mambo ambayo hujawaomba ushauri.

Lakini kuwa na washauri ni jambo nzuri tu - ila sasa tafuta washauri wako mwenyewe, watu wasio rafiki zako ambao wanaeleweka kuwa na busara na uzoefu katika uongozi, bila kuwa na haja ya kukufurahisha wewe kibinafsi, kutafuta urafiki na wewe au kujipendekeza kwako
Uchaguzi ulisha kwisha good enough tuna katiba ambayo inasema mtu akishatangazwa basi ndiyo rais na huna uwezo wa kupinga matokeo hayo popote its good when it is your turn but mind you atakuja tokea chizi mmoja me or ke ambaye ataamua kumuingiza mkewe au mmewe kwa kujua siku ya siku yeye ndiye mwenye mamlaka ya kutangaza matokeo ya urais atamtangaza spouse wake kutakucha, tuyaache hayo.
Binafsi kama ningepata wasaa wa kuongea na Magufuli ningemshauri haya yafuatayo

1. Hali ya hudumu ya afya ya Tanzania ni mbaya mbaya mbaya hakuna daktari aliye na moyo wa kufanya kazi kwa moyo ule uliokuwapo mwanzo. Mfano, hospitali yetu ya taifa ambayo ni tegemeo ya maskini wote wa Tanzania na daraja la viongozi kupita kwenda India huduma ni hovyo hovyo.

Hivi unajua kuwa huduma za CT Scan na MRI Muhimbili zimesimama Zaidi ya miezi minne na hakuna anayejali. Watu wa wizara ya afya naona hawajali kabisa.

Mimi nashauri wizara ya afya isihusike moja kwa moja na Muhimbili kama mtafuta habari nilienda pale, hakuna mwenye nia za dhati wa kuikomboa sekta ya afya.Wao wanachotaka serikali iendelee kupeleka watu India ili waendelee kupata pesa wanazopata wanajua namna wanavyopata, si watu hawa tunakufaa maskini.

2.Taasisi ya mifupa MOI tunaomba ijipambanue kama ni taasisi ya umma au ni kama Agha Khan kwani huduma zinazotolewa hapa afadhali malipo yake yangekuwa na risiti basi ni ujanja ujanja tu.

Heri na feri kwenye soko la samaki kuliko hapo, elimu yao haifanani na huduma wanazotoa.

Mimi naomba kama kama una power hiyo hizi taasisi ziwe chini yako kwani afya ya watu unaowaongoza ni muhimu saaana tena sana elimu ifuate.
Tanzania sasa tumempata Rais mpya wa awamu ya 5, ambaye watanzania wengi tuna matumaini atatekeleza ahadi zake kwa asimilia zaidi ya 90, katika ahadi zake aliahidi kufufua viwanda , katika kufufua viwanda asisahau zao la mkonge , zao hili kwa sasa limekuwa na soko kubwa sana ukilinganisha na kipindi cha nyuma mkonge kwa sasa grade ya SS kwa tani 1 ni takribani US dollar 2500- 3000 katika soko la dunia na local market ni makadirio ya Tsh 2,500,000 kwa tani , na SSUG ni takribani US dollar 1900-2200 kwa tani

Hivyo basi katika mashamba ya mkonge ajira nyingi zinaweza zalishwa na vijana wengi kuajiriwa wasomi na wasio wasomi na kulipwa vizuri , mashamba mengi yamebinafsishwa kwa wawekezaji ambao wanapunja maslahi ya wafanyakazi hasa unskilled labor kwa kuwapa ujira wa 4950 kwa siku ambayo ni ndogo kulinganisha na kinachozalishwa pia chama cha wafanyakazi mashambani TPAWU wakupe ushirikiano kurekebisha mishahara ya mashambani itakayokidhi maisha ya sasa

Mashamba mengi yamekufa na machache yanauhai , hivyo juhudi zifanyike kurudisha zao la mkonge katika ubora na kupunguza tatizo la ajira kwani mahitaji kwa mkonge duniani ni makubwa sana kulipo hapo awali

Nawasilisha, nikiwa nimefanya research ya kutosha kuhusu zao la mkonge Tanzania
Pamoja na kwamba sina imani na chama chako, ila naomba unishawishi wewe binafsi katika serikali yako.
Kama ulivyojinaji kuwa serikali yako, yani Tanzania ya Magufuli itakuwa KAZI TU, basi naomba udhihirishe hivyo katika baraza lako la mawaziri.

Kabla hata sijataka kujua waziri mkuu ambaye ataendana na sura ya kauli mbiu yako, lakini nataka usituletee watu hawa ambao walikuwa mzigo kwa taifa na waliolifikisha nchi hapa ilipo chini ya aliyekutangulia pamoja na waziri mkuu wake.

1. Sopteter Muhongo.
Huyu pamoja na kwamba tunaambiwa hakuhusika moja kwa moja kwenye kashfa xa escrow lakini alikuwa kinara wa utetezi katika sakata hili. Pia ni miongoni mwa waziri wenye elimu kubwa lkn hakuwa na mkakati bunifu wa kutatua tatizo la umeme nchini zaidi ya kuiacha tanesco kwenye deni kubwa. Pia ni miongoni mwa viongozi ambao hawathamini wawekezaji wa ndani, anaamini nchi itajengwa na wazungu au wachina.

2. Lazaro Nyalandu.
Huyu ni miongoni mwa mawaziri ambao tumeshuhudia tembo wakiuliwa kwa wingi, na twiga wetu wakisafirishwa kwenda nje, hafai katika serikali yako, kwani atafanya kazi ya mazoeaa ya serikali ya awamu ya 4.

3. Mwigulu Nchemba.
Pamoja na kwamba hakukaa kwenye wizara ya fedha kwa mda mrefu, lkn ni miongoni mwa vijana ambao hawana adabu katika taifa hili. Ni mmoja wa wanasiasa wachanga ambao hajali matamshi yake mbele ya umma, haangalii baada ya hapa athari zake zitanipeleka wapi, sio mstaarabu.

4. Willium Lukuvi.
Huyu kwa mwendo wa kasi inayohitajika nchini hatufai, utendaji wake hauto tofautiana na wa awamu ya 4, hana jipya ndani ya serikali yako.

5. Shukuru Kawambwa
Huyu ni moja ya mawaziri walioshusha thamani ya elimu yetu. Sio mbunifu. Fedha za fidia za rada mpaka leo hatujui matumizi yake yalienda wapi, hatufai kabisaa.

6.Hawa Ghasia.
Huyu mama bado uchama umemkaa kichwani kuliko maslai ya taifa. Hayupo active katika utendaji wake.

7. Jumanne Maghembe.
Huyu ni moja ya mawaziri ambao ndio chanzo cha huduma mbovu za elimu na maji. Elimu yake ni kubwa lkn haina msaada kwetu.

8.Harrison Mwakyembe.
Huyu kinachompa sifa ni lile sakata la richmond ambalo tunamwona kama shujaa. Lakini kiukweli hafai hata kuwa mwenyekiti wa kijiji. Sijaona mafanikio yake katika wizara alizozisimamia, ni mzigo ana asili ya mtandao ambao ni chanzo cha utendaji mbovu nchini. Ni mafya wa kisiasa

9. Magreth Sitta
Mama huyu tangu zamani ni outdated, haendani na kasi ya dunia, yupo nyuma na mda, hafai katika serikali yako.

10. Sofia Simba
Hana tofauti na Mama sitta, tena huyu uchama na mtandao wa uongozi umemjaa kichwani, hafai katika serikali yako.

11. Andwer Chenge
Najua huyu unamfahamu vema

12. Anna Tibaijuka
Najua unamfahamu vizur

13. Willium Ngeleja
Najua wamfahamu vzr

NB.
1. Mheshimiwa Rais kuna vijana wengi ambao naamini katika utendaji wao lkn siamini kundi lake, na mmoja wao ni Januari Makamba. Huyu binafsi namwamini kiutendaji, ubunifu lakini kinachomsumbua ni kutaka madaraka makubwa, kundi lake lililo nyuma yake, Huyu badala ya kuchapa kazi atakuwa anawaza urais baada yako kustaafu. Kwa mtazamo wangu ungemweka kando kwa mda baada ya miaka miwili ndo uumpe majukumu.

2. Kwa kukusaidia mh Rais ni vema ukachagua mawaziri wachache ambao wengi wao hawakuwa mawaziri, sio viongozi katika chama, vijana, wenye elimu isiyo na shaka. Hawa ndio wataileta tanzania mpya ya HAPA KAZI TU.

Mh Rais ukikosea kwenye baraza la mawaziri basi jua umeuwa nchi, na hapo tutadhibitisha kuwa hakuna cha Magufuli 4 change itakuwa ccm ni ile ile.

Asantee.
Hali ya Kisiasa
Mgogoro wa Zanzibar ni jukumu lako kwa sasa halikwepeki. Tafuta wasuluhishi wawili (kutoka Bara na Visiwani) wakusaidie kulishughulikia hili
2. Katiba mpya ya JMT ? pengine si ajenda ya chama chako kwa sasa lakini linahitaji dhamira yako? chonde chonde litendee haki taifa hili.

Mfumo na Uendeshaji wa Serikali
Uza mashangingi ya Serikali na ubakize machache tu kwa shughuli muhimu. Watumishi wa Serikali wakopeshwe magari na wapewe mafuta ili kuokoa fedha nyingi mno zinazopotea kiholela.[/FONT]

Rejesha nyumba za Serikali kwani wananchi wengi hatuna imani kuhusu dhamira, mantiki na umuhimu wa kuziuza nyumba za Serikali

Punguza sana idadi ya Wizara na Mawaziri ili kupunguza gharama

Boresha kipato cha Watumishi serikalini ili kuwaongezea morali

Toa fursa katika vipindi tofauti mikoani ukutane na wananchi wenye matatizo uwasikilize ana kwa ana, mmoja mmoja (uwe rais wa wananchi)

Misamaha ya kodi ni donda ndugu linalohujumu Taifa mapato, dhibiti hili kwa nguvu zako zote.

Panua wigo wa vyanzo vya mapato ya Serikali ? hili ni muhimu sana

Dhibiti safari za nje zisizo za lazima kwa Viongozi waandamizi wa Serikali

Rushwa na Ufisadi

Mahakama ya Rushwa na Ufisadi ianzishwe kama ulivyoahidi

TAKUKURU ipewe mamlaka ya kuwafikisha watuhumiwa mahakamani bila kibali cha DPP

Afya, Maji na Mazingira

Karabati hospitali za umma (Taifa, Mikoa, Wilaya) ziko katika hali mbaya (Zahanati kwa kila kijiji inawezekana!)

Imarisha Hospitali ya Muhimbili ikidhi viwango vya kimataifa ili kupunguza gharama za matibabu nje ya nchi

Panua wigo wa Mfuko wa Bima ya Afya ili ijumuishe wananchi wote (Rwanda wameweza hili) watakaochangia kiwango nafuu

Miji na Majiji ni machafu mno (taka ngumu na maji taka), imeshindikana kubadili hali na inaelekea hakuna suluhisho, inabidi tuzoe uchafu ? tunaomba wahusika wageukie taka

Huduma ya Afya ya Mama na Mtoto iboreshwe kwa nguvu zote

Serikal igharimie magonjwa hatarishi ikiwemo saratani na UKIMWI

Matumizi ya mifuko ya plastiki yapigwe marufuku (Rwanda, Zanzibar imewezekana)

Anzisha Mfuko wa Maji Vijijini ili kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji katika maeneo yote

Elimu
Wanafuzi wengi wa elimu ya juu hawakupata mikopo kwa mwaka2015/2016? litatue hili kwani ni aibu

Elimu ya bure hadi kidato cha nne iwe kweli na yenye ubora

Shule ziimarishwe kwa kupatiwa madarasa, maabara, vitabu, walimu na lishe muafaka?
One Computer, One Pupil? ? tujenge taifa la kisasa na linaloendana na mabadiliko ya nyakati kimaendeleo
Anzisha Kamisheni ya Taifa ya Ushauri kuhusu elimu

Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Viwanda

Fufua kilimo cha mazao asilia (mkonge, kahawa)

Anzisha Mfuko wa Taifa wa Kilimona Mifugo utakaotoa mikopo kwa wakulima, wafugaji na wavuvi

Imarisha na jenga miradi ya umwagiliaji na majosho ya mifugo

Imarisha vyama vya ushirika na viwezeshe kujitafutia masoko

Futa kodi zote kandamizi kwa wakulima, wafugaji na wavuvi

Anzisha viwanda vya kusindika mazao ya kilimo, ufugaji na uvuvi

Weka kodi nafuu na shindani kuhamasisha wawekezaji

Miundombinu na Uchukuzi

Punguza gharama za vifaa vya ujenzi ili wananchi wengi wamudu kujenga nyumba bora

Fufua Shirika la Ndege la Taifa (ATC)

Imarisha miundombinu ili kuondosha misongamano katika majiji na miji mikubwa (Dar, Mwanza, Mbeya, Arusha)
    1. Usikubali kofia mbili; wewe ni Raisi, uenyekiti wa CCM muachie mwingine ili chama kibaki chama na serikali ibaki serikali.
    2. Washauri Wabunge wa CCM, watangulize maslahi ya taifa mbele ya maslahi ya chama.
    3. Washauri Wabunge wa CCM kama itawezekana wamchague Spika wa Bunge asiyeegemea upande wowote.
    4. Pokea ushauri kutoka kwa vyama vya siasa lakini uwe huru kufanya maamuzi kulingana na matakwa ya Katiba ukizingatia maslahi ya wananchi.
    5. Usiruhusu Ikulu kutumika kwa maslahi ya CCM, vikao vya chama vifanyike nje ya Ikulu.
    6. Washauri CCM waachie mali za wananchi kwa kuzirudisha mikononi mwa wananchi kupitia serikali.
    7. Agiza vyombo vya dola vitoe haki sawa kwa wananchi bila upendeleo.
    8. Futa sheria zote kandamizi zinazozuia uhuru wa kutafuta, kupokea na kutoa habari. Vyombo vyote vya habari viwe huru.
    9. Hakikisha mikataba yote tunayoingia inawekwa wazi ili vijadiliwe na kupitishwa na Bunge.
    10. Vikumbushe vyombo vya dola kwamba jukumu lao la kwanza ni kuwalinda Watanzania na mali zao na si kupambana nao.
Watu wengi wanaishi wilayani na mahitaji yao mengi yanatatuliwa wilayani hukohuko, hivyo kuweka watendaji mahili na wabunifu kwenye ngazi ya wilaya ndio mtihani wa kwanza wa rais Magufuli. Wakuu wa wilaya na watendaji wengine wa JK sio kabisa, na huwenda ndio chanzo cha migogoro mingi ya wananchi dhidi ya serikali yao. JPM hana namna nyingine zaidi ya kuwaweka pembeni watendaji wote wavivu na wabadhilifu wilayani na mikoani ambao wengi wao wameshachukiwa tayari na wananchi wao.

Mtihani wa pili ni namna atakavyo atakavyotumia uwezo wake kupambana wa watu wajanjawajanja kama vile akina Lyatonga, Chenge, Tibaijuka, Manji, Aziz, Nazir, Harison, Samuel na wengine. Kwa muonekano wao ni wapenda sifa binafsi na kujali maslahi yao tu.

Mtihani wa tatu ni namna atakavyoweza kukaa mbali na kundi la mzee Mkapa waliohusika na kuuza viwanda, migodi, mabenki, mashamba, nyumba za serikali na hata waliotajwa kwenye kashifa ya EPA, meremeta, rada, ndege ya rais, n.k, ambao ni chanzo kikubwa leo cha ukosefu wa ajira kwa vijana na ongezeko kubwa la deni la taifa.

Mtihani wa Nne ni namna ya atakavyopambana na wimbi la watoto na wajukuu wa viongozi wa wakuu wa CCM wanaotaka kupewa nafasi serikalini kwa upendeleo kutumia nafasi za wazazi wao.

Mtihani wa Tano ni namna atakavyoweza kupambana na udini, ukabila, na ukanda katika kutoa nafasi za ajira nchini. Hali ilivyo hivi sasa ni mbaya sana, ajira wizarani, kwenye vitengo mbalimbali, mialiko kwenye mikutano, semina na nafasi za mafunzo inatolewa kwa ukanda, ukabila, udugu na udini.

Asipozingatia haya atahesabika kuwa ameanza na mguu mbaya sana utakaomgarimu sana uchaguzi wa 2020.
Secta ya bunge kitengo cha huduma na haki za mbunge kilichokuwa chini ya Chenge kilipangia bunge masulufu makubwa mno na bado wabunge kwa makusudi au kwa utovu wa adabu walikuwa wanaona haziwatoshi.

Mfano posho za kuhudhuria bunge ni shs 300.000 bado wabunge walikuwa wanaona hazitoshi ziongezwe chini ya Chenge

Mh. Rais kubana matumizi ya serikali iangalie sana secta hii ya bunge

Pia ninakuomba usitishe mikopo ya mashangingi, waheshimiwa wabunge wanunue RAV 4 au NOA kwa hela zao kwa sababu majimbo yamegawanywa na kuwa madogo yanayoweza kufikika kilaisi na usafiri huo.

Mh Rais fanya kazi ya ubunge iwe ngumu lli uchaguzi ujao wanachi wasiikimbilie

Ushauri huu pia nimekutumia kwa e.mail tafadhari naomba unijibu kama kutakuwa na ugumu katika utekelezaji wake

KIFUPI: Bunge linamega sehemu kubwa sana ya keki ya Taifa, serikali ya awamu ya tano liipunguze keki hiyo.
"Hapa Kazi tu", ndio msemo unaotawala sasa katika eneo la siasa. Siku chache zilizopita msemo wa 'mabadilikooo' Lowasaaa, Lowassaa mabadilikoo' ndio ulitamba. Wakati huo vijana, wazee na watoto walitamani mabadiliko aliyotangaza Mh. Edward Ngoyai Lowassa. Lowassa aliwajengea wafuasi wake Imani kubwa hasa pale alipowaambia wampigie kura kwa wingi na suala la kumtangaza mshindi tumuachie yeye. Wananchi wakampigia kura kwa wingi na hadi leo, suala la kutangaza mshindi wamemuachia Lowassa.

Vyovyote vile, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ni John Pombe Magufuli. Anaweza asiwe mioyoni mwa raia wengi zaidi, nikiwemo mimi, lakini ndio Rais. Tukitaka kujadili mambo Makubwa ya Taifa letu, hakuna budi kumtambua Magufuli kwamba ndiye Rais, kwa sasa.

Rais Magufuli ameanza kazi kwa staili ya JK alipoingia mwaka 2005. Magufuli amekuwa akivamia taisisi nyeti za umma, kukagua, kujionea hali halisi, kutoa maagizo na pengine kujifunza. Ni vema na haki kuona tuna Kiongozi anayeonesha kuyajali majukumu ya wengine kiasi cha kufanya ziara za kustukiza kwa lengo la kuona uhalisia wa mambo. Kama Magufuli angekuwa anatoa taarifa za ziara zake, labda pangefanyika maandalizi yanayoweza kuziba sura halisi ya utoaji huduma katika taasisi husika.

Wapo wanaobeza, kukejeli na kupuuza na hata kuita ziara hizi kuwa ni maigizo tu au Nguvu ya soda tu. Wengine wanasema hayo kwa sababu wao wannamini hivyo kutokana na sababu zao wanazoona kuwa ni za msingi, na wengine wanatamani iwe hivyo ili Magufuli akishindwa wajigambe mbele ya 'wapinzani' wao wa kisiasa. Watu hawa hawajui kuwa kushindwa kwa Magufuli ni kushindwa kwa Taifa. Na Taifa ni letu wote, kwa hiyo na sisi sote tutakuwa tumeshindwa.

Mimi binafsi naziona ziara za ghafla za Magufuli kama michezo ya mtoto mdogo anayejifunza kutembea. Mtoto mdogo anapocheza ni ishara ya maendeleo mazuri kiafya. Ni ishara kuwa mtoto hana tatizo. Ni matumaini. Hutokea hata mzazi kushikwa na wasiwasi mtoto wake anapoacha kucheza na wenzake, na hali ilkizidi humpeleka kituo cha afya.

Magufuli anacheza, na hiyo ni ishara nzuri kwa mtoto. Na hapo ndipo inapokuja hamu ya kutaka kuona maendeleo chanya ya Rais wangu Magufuli. Atakapoanza kutembea, atembelee maeneo haya.

1. MADAWA YA KULEVYA
Jeshi la wananchi la Tanzania JWTZ, lina wanajeshi wapatao 30,000 na kuongeza au kupunguza kidogo (around 30,000). Takwimu za vijana walioathirika kwa madawa ya kulevya ni around 700,000 (laki saba) kwa mwaka 2013. Kwa hiyo ukichukua 700,000 ? 30,000 = 23 (aprox).

Hii ni sawa na kusema ukichukua vijana waliathiriwa na madawa ya kulevya unapata ndani yake majeshi 23 ya Tanzania (kwa idadi ya watu). Hili ni kundi ambalo kwa kiasi kikubwa halizalishi, halilipi kodi, ni tegemezi na wengi wao ni wahalifu ingawa uhalifu zaidi ni matokeo ya uathirika wao.

Vijana ni nguvu kazi ya taifa, ndio nguzo ya taifa. Nguzo hii ikiliwa na mchwa taifa litaanguka.

Kwa hiyo kila mtanzania atapenda zaidi kuona Mh. Magufuli anapigana vita kufa kupona dhidi ya madawa ya kulevya ili kuokoa afya za vijana wetu kabla hajawatembelea kwa kushtukiza huko mahospitalini.

Wananchi wangependa kuona madawa ya kulevya yanakamatwa, na kuchomwa moto ili kudiscourage biashara hii ya kuhuisha. Na zaidi amuombe JK majina aliyodai kuwa nayo (kama haukuwa mkwara) ili aanze nayo.

Angalizo: Kila mtu anaweza kuwa mwathirika wa madawa ya kulevya.

2. UJANGILI
Sasa hivi Kilo moja ya meno ya Tembo ina thamani ya Tsh. 200,000. Siku chache zilizopita tumeambiwa Tanzania iliizuia Malawi kuteketeza Meno na pembe za Ndovu zilizokamatwa nchini huko zikitokea Tz. Ripoti zaidi kuhusu ujangili huo hazileti furaha kwa wazalendo.

Al Jazeera wameiita Tanzania 'Point of extinction'. Kwa maana eneo la kuondoa uhai Duniani, au eneo la maangamizi, wakiakisi hali ya ujangili katika Tanzania inayoonesha kuwa Tembo wamepungua kutoka 109,051 mwaka 2009 na kufikia 43,330 mwaka 2014.

Tembo 85181 wameuawa kwa kipindi cha miaka 5. Sawa na tembo 17,016 kila mwaka. Maana yake kwa tembo 43,330 waliobaki ukigawa kwa 17,016 ni sawa na miaka chini ya mi3, tembo watakuwa wamekwisha ikiwa hali haitadhibitiwa. Hiyo ni kwa Tembo tu. Magufuli aguse na hapo.

3. UFISADI
Escrow, Epa, Richmond, Meremeta, Mabilioni ya Uswis, Ufisadi katika uchaguzi, na madudu mengine kibao. Magufuli akitaka kujenga imani kwa wananchi asiache kushughulikia mafisadi kama alivyoahidi. Lakini akiendelea ku'deal' na wanataaluma (mf. Madaktari Muhimbili) lakini akaacha wanasiasa wafanye wanavyotaka, wafanyakazi watapoteza imani naye. Na hapo kazi zitafanyika siku akivamia maofisini na siku mbili tatu baadae halafu 'business as usual'. Itapendeza kama atagusa na Mafisadi.

4. MIKATABA YA MADINI, MAFUTA NA GESI
Tumeshuhudia ugeni mkubwa nchini petu mara baada ya ugunduzi wa mafuta na gesi. Lakini hata sasa watanzania wana wasiwasi kuhusu mikataba 35 ya siri iliyofanywa na Rais wa awamu ya nne na wageni wake Rais Obama wa Marekani na Xi Ji Ping wa China.

Magufuli atakapoacha michezo ya ziara za kustukiza, tungependa aweke mikataba hii wazi, kisha wananchi washuhudie, na kama kuna harufu ya maslahi binafsi ya viongozi waliotia saini mikataba hiyo kwa siri, hatua mahususi zichukuliwe.

Tumeonewa sana kwenye Madini. Wamiliki wa migodi hii sio tu ni watu Matajiri bali pia ni watu wenye ushawishi mkubwa kwenye serikali za mataifa yalipoasisiwa makampuni hayo. Magufuli atapata sifa akituokoa na dhuluma hii iliyofanywa kwa miaka mingi. Haina maana 'neno hapa kazi tu' halafu rasilimali zetu zinakombwa kwa ridhaa yetu wenyewe. Badala ya hapa kazi tu inakuwa 'Hapa ubwege tu'.

5. KATIBA MPYA
Katiba yenye tija, tumaini jipya na mwanzo mpya wa Utanzania tunaotamani. Inafahamika wazi kuwa Magufuli ni miongoni mwa wanaCCM waliouteka na kuubaka mchakato wa katiba mpya. Mh. Sitta akajiandikia kijitabu chake akakiita 'katiba pendekezwa' huku akishadidiwa na wanaCCM, wakapiga makelele ndani ya bunge letu 'tukufu' kama mazuzu waliokosa kunywa dawa siku hiyo. Magufuli alikuwa miongoni mwao.

Sasa Mh. Rais Magufuli ana nafasi ya kuwa huru na kuacha kufuata mihemko ya siasa za vyama kwenye jambo la msingi ka Katiba. Pindi apatapo wasaa, aurejeshe mchakato wa katiba mpya ili kurudisha matumaini yaliyopotezwa. Na hili halihitaji kuvamia wizara ya katiba na sheria.

Maeneo ya msingi ni mengi na muda wa miaka mitano ni mchache sana. Naomba itokee kuwa 'drama' hizi za Mh. Rais iwe mwanzo wa safari ya kuelekea huko nilipoeleza. Haitapendeza kama lengo la hizi 'drama' ni kutafuta kukubalika tu halafu business as usual (cheap popularity).

Pia, ifahamike kuwa kutekeleza mambo hayo ni kama kuingia vitani. Kwa hiyo Mh. Rais Magufuli anapaswa kuwa mtu anayehitaji msaada katika vita hii kuliko mtu mwengine yeyote. Kwa hiyo itakuwa vizuri zaidi endapo 'drama' hizi za ziara za kustukiza zikawa mbinu za kutafuta 'kupendwa na wananchi' na hivyo kupata support kubwa pale atakapoanzisha hiyo vita.

Au kama sivyo, basi ni vema Mh. Rais Magufuri akawa na malengo ya msingi kuliko maeneo niliyogusia. Kumbe sasa endapo hatagusia hayo atagusa wapi? Mh. Rais Utakapomaliza Michezo yako, Naomba uguse na hayo.

Asante.

0713933736
Rais magufuli komesha tatizo la watu kukaimu nafasi kwa mida mrefu

Nafahamu Rais JPM anafahamu kuwa serikalini kuna tatizo la baadhi ya watu kukaimu nafasi za madaraka kwa muda mrefu bila huku wakiwa hawana sifa za kushika madaraka hayo. Wenye sifa wamekuwa wakinyimwa gursa hiyo na hivyo kuwakatisha tamaa na kuzorotesha utendaji kazini.

Watu hao mara nyingi wamekuwa wakisaidiwa na baadhi ya wakubwa walioko wizarani kwa kile kinachoonekana ni ukabila, undugu na urafiki.

Nimetembelea maeneo mengi mfano Singida, Bunda, Shinyanga manispaa na kukuta tatizo hilo hasa kwenye idara za afya, manunuzi na uhasibu.

Naomba serikali hii ishughulikie hili ili wenye sifa wapewe nafasi hizo na hii itaongeza tija ya utendaji serikalini.
Mimi miongoni mwa watanzania zaidi ya milioni hamsini natumia fursa hii kutuma hoja tano kwend kwa JPM kama sehemu yangu ya kumshauri kiongozi wangu wa nchi tuweze kufikia kile wengi tunachokitamani.

1. Nguvu kazi iliyopo utumiwe ipasavyo na kuwa na mkakati kfanikisha wazalishaji mali (producers) wazidi walaji(consumers). Hapa serikali ufungue kilimo na shughuli zingine asilia ambazo ndiyo zinabeba idadi kubwa ya watu. Serikali na secta binafsi nunueni tractors na kutenga maeneo kwa ajili ya kilimo cha mazao mbalimbali na vijina wawekwe ktk mashamba hayo kwa ajili ya kuzalisha. Irrigation schemes ziwepo kwa wingi na serikali iweke utaratibu wa upatikanaji masoko.

2. Tuwe na viwanda vinavyoa aksi malighafi yetu tunayoizalisha sisi ili tukuze hizo shughuli zinazotoa malighafi. Si lazima kuwa na viwanda vikubwa sasa hivi bali tuanze na viwanda vyetu vidogovidogo vinavyoaksi uchumi wetu badala ya kupokea viwanda toka nje hii hataisaidia kwa mda mrefu kwani badae tutajikuta hatumiliki uchumi sisi.

3. Fedha inayopatikana asilimia kubwa yake ifanye maendeleo ya jamii kkt huduma za jamii km afya na miradi ya maendeleo kuliko kuendesha serikali kwani ni wazi kuna bilioni nyingi zinatumika kuendesha serikali pasipo na ulazima . Mfano idadi kubwa ya magari ya kifahari kutokana na vyeo vvyingi km vile idadi kubwa ya wabunge,wakuuu wa mikoa na wilaya,RPCs,wakurugenzi,mawaziri na utitili mwingi ambao wote wanatumia pesa nyingi.

4. Mabadiliko na utungaji wa sheria mpya na hata katiba mpya ili kuiweka Tanzania ktk nafasi salama zaidi yenye maslahi mapana ya nchi.

5. Yapo mambo makubwa yanalitafuna taifa na bado hayajaguswa wala kuzungumziwa mfano mikataba mibovu ya madini. Rais sasa ahame toka kwenye kupapasa ili akajikite na mambo hayo mazito ambayo ni shida kwa taifa.

Asante
By GGM.
 
Ungemuomba atumie nguvu yake kusimamia haki

Mbagala wameporwa mbunge wao.

Kuna uchaguzi wa mameya wa majiji, asimamie haki walioshinda ndo wapewe.

yasije rudia ya manispaa ya Arusha mjini kuhusu uchaguzi wa meya hasa hapa Dar.
 
Kila chama kilikuwa na ilani yake, sasa kusema ampe ubunge then cheo anachostahili Serikalini una maana gani? Je akiwa serikalini atakuwa anatekeleza ilani ipi kati ya ile ya ACT ya kwake na hii yenu ya CCM?
 
Kitufe cha like hakipo....nalazimika nikunukuu.

Ukumbi wa diamond jubilee ulikuwa kimya pale mama Mghwira aliposema tunataka katiba mpya kama kichocheo halali cha kuleta mabadiliko.

Hakika zile ndio siasa.......siasa mpya.....Huyu mama ametokea kupendwa ghafla.

Kama nilivyompenda ghafla FaizaFoxy !!
 
Last edited by a moderator:
Kila chama kilikuwa na ilani yake, sasa kusema ampe ubunge then cheo anachostahili Serikalini una maana gani? Je akiwa serikalini atakuwa anatekeleza ilani ipi kati ya ile ya ACT ya kwake na hii yenu ya CCM?

Mbatia alipewa ubunge na mwenyekiti wa CCM alikuwa anatekeleza ilani ipi?
 
Kila chama kilikuwa na ilani yake, sasa kusema ampe ubunge then cheo anachostahili Serikalini una maana gani? Je akiwa serikalini atakuwa anatekeleza ilani ipi kati ya ile ya ACT ya kwake na hii yenu ya CCM?
Ilani zote zipo kwa ajili ya kumletea mtanzania maendeleo, hakuna zaidi ya hilo.
 
Kila chama kilikuwa na ilani yake, sasa kusema ampe ubunge then cheo anachostahili Serikalini una maana gani? Je akiwa serikalini atakuwa anatekeleza ilani ipi kati ya ile ya ACT ya kwake na hii yenu ya CCM?

Kwani Maalim Seif anatekeleza ilani ipi kama Makamu wa Rais wa Zanzibar?
 
Status
Not open for further replies.
26 Reactions
Reply
Back
Top Bottom